Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Wengine Watii Mambo Ambayo Biblia Inafundisha

Wasaidie Wengine Watii Mambo Ambayo Biblia Inafundisha

Wasaidie Wengine Watii Mambo Ambayo Biblia Inafundisha

“Na zile zilizo kwenye udongo mzuri, hawa ndio ambao, baada ya kusikia lile neno kwa moyo mzuri na mwema, hulihifadhi na kuzaa matunda kwa uvumilivu.”—LUKA 8:15.

1, 2. (a) Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kimechapishwa kwa kusudi gani? (b) Katika miaka ya karibuni, Yehova amebariki jinsi gani jitihada za watu wake za kufanya wanafunzi?

“NI KITABU kizuri sana. Wanafunzi wangu wanakipenda. Mimi ninakipenda. Kitabu hiki kinatuwezesha kuanzisha mafunzo ya Biblia pamoja na watu milangoni pao.” Hivyo ndivyo alivyosema painia mmoja ambaye ni mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova kuhusu kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? * Mtangazaji mmoja wa Ufalme mwenye umri mkubwa alisema hivi kuhusu kitabu hicho: “Nimepata pendeleo la kuwasaidia watu wengi kumjua Yehova katika muda wa miaka 50 ambayo nimekuwa nikihubiri. Lakini ninaweza kusema kwamba kitabu hiki cha kujifunzia Biblia ni cha pekee sana. Picha na mifano yake yenye kuchochea inapendeza.” Je, unahisi vivyo hivyo kuhusu kitabu Biblia Inafundisha? Kitabu hicho cha kujifunzia Biblia kimekusudiwa kukusaidia kutimiza amri hii ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mathayo 28:19, 20.

2 Bila shaka, moyo wa Yehova unashangilia anapoona Mashahidi wake milioni 6.6 hivi wakitii kwa kupenda amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi. (Methali 27:11) Ni wazi kwamba Yehova anabariki jitihada zao. Kwa mfano, katika mwaka wa 2005, habari njema ilihubiriwa katika nchi 235 na, kwa wastani, mafunzo ya Biblia zaidi ya 6,061,500 yaliongozwa. Hivyo, watu wengi ‘walilisikia neno la Mungu na kulikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.’ (1 Wathesalonike 2:13) Katika miaka miwili hivi iliyopita, wanafunzi wapya zaidi ya nusu milioni wamepatanisha maisha yao na viwango vya Yehova na kujiweka wakfu kwa Mungu.

3. Tutazungumzia maswali gani kuhusu kutumia kitabu Biblia Inafundisha?

3 Je, umepata shangwe ya kujifunza Biblia na mtu fulani hivi karibuni? Ulimwenguni pote, bado kuna watu mmoja-mmoja walio na “moyo mzuri na mwema” ambao wakisikia neno la Mungu ‘watalihifadhi na kuzaa matunda kwa uvumilivu.’ (Luka 8:11-15) Acha tuone jinsi unavyoweza kutumia kitabu Biblia Inafundisha katika kazi ya kufanya wanafunzi. Tutazungumzia maswali matatu: (1) Unaweza kuanzisha funzo la Biblia kwa njia gani? (2) Ni njia gani za kufundisha zenye matokeo zaidi? (3) Unaweza kumsaidia mtu jinsi gani asiwe mwanafunzi tu, bali awe pia mwalimu wa Neno la Mungu lililoandikwa, Biblia?

Jinsi Unavyoweza Kuanzisha Funzo la Biblia

4. Kwa nini huenda watu fulani wakasitasita kujifunza Biblia, na unaweza kuwasaidia kwa njia gani wakubali funzo?

4 Ikiwa ungeambiwa uruke na kuvuka mto mpana, huenda ungekataa kufanya hivyo. Lakini ikiwa mawe ya kukanyagia yangewekwa hatua fupi-fupi, inaelekea ungekubali kuvuka. Vivyo hivyo, mtu mwenye shughuli nyingi anaweza kusitasita kujifunza Biblia. Mwenye nyumba huyo anaweza kufikiri kwamba wakati na jitihada nyingi zinahitajiwa ili kujifunza Biblia. Unaweza kumsaidia kwa njia gani ili akubali kujifunza? Kwa kuwa na mazungumzo mafupi-mafupi ya kawaida yenye kuelimisha, unaweza kutumia kitabu Biblia Inafundisha ili kumwongoza mtu huyo katika funzo la kawaida la Neno la Mungu. Ukijitayarisha vizuri, kila ziara ya kurudia unayofanya itakuwa kama jiwe la kukanyagia ambalo litamwongoza kuwa na urafiki pamoja na Yehova.

5. Kwa nini unahitaji kusoma kitabu Biblia Inafundisha?

5 Hata hivyo, kabla ya kumsaidia mtu mwingine afaidike na kitabu Biblia Inafundisha, unahitaji kukielewa kabisa kitabu hicho. Je, umekisoma kuanzia mwanzo mpaka mwisho? Wenzi fulani wa ndoa walibeba kitabu hicho walipoenda likizo, na wakaanza kukisoma walipokuwa wakistarehe kwenye ufuo wa bahari. Mwanamke mmoja aliyekuwa akiwauzia watalii vitu aliwafikia na kuona kichwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? Akawaambia kwamba saa chache tu zilizopita, alikuwa amesali ili Mungu ampe jibu la swali hilo. Wenzi hao wa ndoa walifurahi kumpa mwanamke huyo kitabu hicho. Je, ‘umejinunulia wakati’ wa kusoma kitabu hicho, labda kwa mara ya pili, unapongoja uhudumiwe au wakati wa mapumziko kazini au shuleni? (Waefeso 5:15, 16) Ukifanya hivyo, utakielewa kitabu hicho cha kujifunzia Biblia na unaweza pia kupata nafasi za kuzungumza na wengine kuhusu mambo yaliyomo.

6, 7. Unaweza kuanzisha mafunzo ya Biblia kwa njia gani ukitumia kitabu Biblia Inafundisha?

6 Unapowatolea watu kitabu hicho katika huduma ya hadharani, tumia vizuri picha, maandiko, na maswali yaliyo kwenye ukurasa wa 4, 5, na 6. Kwa mfano, unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kuuliza, “Kwa kuwa wanadamu wanakabili matatizo mengi leo, unafikiri wanaweza kupata wapi mwongozo unaotegemeka?” Baada ya kusikiliza kwa makini jibu la mtu huyo, soma 2 Timotheo 3:16, 17, na ueleze kwamba Biblia inatoa suluhisho lenye kutegemeka kwa matatizo ya wanadamu. Kisha, mwombe mwenye nyumba atazame ukurasa wa 4 na wa 5, na umuulize: “Ni jambo gani kati ya mambo yanayoonyeshwa kwenye ukurasa huu ambalo linakusononesha zaidi?” Baada ya mwenye nyumba kuchagua jambo moja, mwombe ashike kitabu halafu usome andiko linalohusika katika Biblia yako. Kisha, soma ukurasa wa 6, na umuulize mwenye nyumba hivi: “Kati ya maswali sita yaliyo katika sehemu ya chini ya ukurasa huu, ni swali gani ambalo ungependa kupata jibu lake?” Akichagua swali moja, mwonyeshe sura ambayo inajibu swali hilo, mwachie kitabu, na ufanye mipango kamili ya kumrudia tena ili mzungumzie swali hilo.

7 Utangulizi ambao tumepitia unachukua dakika tano hivi. Lakini katika dakika hizo chache, utakuwa umejua jambo ambalo linamhangaisha mwenye nyumba, utakuwa umesoma na kueleza maandiko mawili, na utakuwa umeweka msingi wa ziara ya kurudia. Huenda mwenye nyumba hajapata kuwa na mazungumzo yenye kutia moyo na yenye kufariji sana hivi karibuni kama mazungumzo hayo mafupi ambayo mmekuwa nayo. Ukifanya hivyo, inaelekea hata mtu mwenye shughuli nyingi atatazamia sana kuzungumza nawe kwa dakika nyingine chache unapomsaidia kuchukua hatua inayofuata ya kutembea katika “barabara inayoongoza kwenye uzima.” (Mathayo 7:14) Baada ya muda, mwenye nyumba anapozidi kupendezwa, mnapaswa kujifunza kwa muda mrefu zaidi. Unaweza kufanya hivyo kwa kumwomba mketi na kujifunza kwa muda fulani hususa ambao ni mrefu zaidi.

Njia za Kufundisha Zenye Matokeo Zaidi

8, 9. (a) Unaweza kumtayarisha kwa njia gani mwanafunzi wako wa Biblia ashinde vipingamizi na majaribu ambayo huenda akapata? (b) Vifaa visivyoshika moto vya kujenga imani yenye nguvu vinaweza kupatikana wapi?

8 Mtu anapoanza kutii yale ambayo Biblia inafundisha, huenda atapata vipingamizi ambavyo vinaweza kumzuia kufanya maendeleo. Mtume Paulo alisema hivi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Paulo alilinganisha majaribu hayo na moto ambao unateketeza vifaa vya ujenzi ambavyo ni hafifu lakini hauwezi kuteketeza vifaa kama vile dhahabu, fedha, na mawe ya thamani. (1 Wakorintho 3:10-13; 1 Petro 1:6, 7) Ili kumsaidia mwanafunzi wako wa Biblia asitawishe sifa zinazohitajiwa ili kushinda majaribu ambayo anaweza kupata, unahitaji kumsaidia kwa kujenga kwa vifaa visivyoshika moto.

9 Mtunga-zaburi analinganisha “maneno ya Yehova” na “fedha iliyosafishwa katika tanuru ya kuyeyushia kwenye udongo, iliyosafishwa mara saba.” (Zaburi 12:6) Bila shaka, Biblia ina vifaa vyote vya thamani ambavyo vinaweza kutumiwa kujenga imani yenye nguvu. (Zaburi 19:7-11; Methali 2:1-6) Na kitabu Biblia Inafundisha kinakuonyesha jinsi unavyoweza kutumia Maandiko kwa ustadi.

10. Unaweza kutumia njia gani kumsaidia mwanafunzi aikazie Biblia fikira?

10 Wakati wa funzo, msaidie mwanafunzi akazie fikira maandiko yaliyo katika kila sura mnayozungumzia. Tumia maswali kumsaidia mwanafunzi kuelewa maandiko ya msingi ya Biblia na kuyatumia maishani mwake. Uwe mwangalifu usimwambie jambo la kufanya. Badala yake, iga mfano wa Yesu. Mtu fulani mwenye ujuzi mwingi wa Sheria alipomuuliza swali, Yesu alimjibu hivi: “Ni mambo gani yameandikwa katika Sheria? Wewe unasomaje?” Mtu huyo alimjibu kwa kutumia Maandiko, na Yesu akamsaidia kuona jinsi ya kutumia kanuni hiyo maishani mwake. Pia, Yesu alitoa mfano ili kumsaidia mtu huyo aone jinsi fundisho hilo linavyomhusu. (Luka 10:25-37) Kitabu Biblia Inafundisha kina mifano mingi rahisi ambayo unaweza kutumia kumsaidia mwanafunzi afuate kanuni za Kimaandiko maishani mwake.

11. Unapaswa kujifunza kiasi gani cha habari katika kila kipindi cha funzo?

11 Kitabu Biblia Inafundisha kinaeleza Neno la Mungu kwa lugha rahisi na ya moja kwa moja kama vile Yesu alivyoeleza mambo magumu kwa maneno rahisi. (Mathayo 7:28, 29) Fuata mfano wa Yesu. Eleza habari kwa njia yenye kueleweka, rahisi, na sahihi. Usipitie habari hiyo haraka-haraka. Badala yake, hali na uwezo wa mwanafunzi unapaswa kukusaidia kuamua idadi ya mafungu mtakayojifunza katika kila kipindi cha funzo. Yesu alijua uwezo wa wanafunzi wake naye hakuwalemea kwa kuwapa habari nyingi ambazo hawakuhitaji wakati huo.—Yohana 16:12.

12. Nyongeza inapasa kutumiwa kwa njia gani?

12 Kitabu Biblia Inafundisha kina nyongeza yenye vichwa 14 vya habari. Ikitegemea mahitaji ya mwanafunzi, wewe ukiwa mwalimu wake unapaswa kuamua njia nzuri ya kutumia nyongeza hiyo. Kwa mfano, ikiwa mwanafunzi anaona habari fulani kuwa ngumu kuelewa au ikiwa ana maswali kuhusu habari fulani kwa sababu ya mambo aliyoamini zamani, huenda ikatosha kumwelekeza kwenye sehemu inayofaa ya nyongeza na kumwomba ajisomee habari hiyo. Kwa upande mwingine, huenda hali ya mwanafunzi ikakulazimu kujifunza habari hiyo pamoja naye. Nyongeza hiyo ina vichwa muhimu vya Kimaandiko, kama vile “Maneno ‘Nafsi’ na ‘Roho’ Yanamaanisha Nini Hasa?” na “Kumtambulisha ‘Babiloni Mkubwa.’” Ukipenda unaweza kuzungumzia vichwa hivyo pamoja na mwanafunzi wako. Kwa kuwa habari iliyo katika nyongeza haina maswali yoyote, utahitaji kuijua vizuri habari hiyo ili uulize maswali yako mwenyewe yanayofaa.

13. Sala inaimarisha imani jinsi gani?

13 Andiko la Zaburi 127:1 linasema, “Yehova mwenyewe asipoijenga nyumba, ni bure kwamba wajenzi wake wameifanyia kazi ngumu.” Kwa hiyo, unapojitayarisha kuongoza funzo la Biblia, sali ili Yehova akusaidie. Acha sala unayotoa mwanzoni na mwishoni mwa kila funzo ionyeshe kwamba una uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova. Mtie moyo mwanafunzi amwombe Yehova hekima ya kuelewa Neno Lake na nguvu za kufuata mashauri yake. (Yakobo 1:5) Mwanafunzi akifanya hivyo, ataimarishwa kuvumilia majaribu naye ataendelea kuimarika katika imani.

Wasaidie Wanafunzi wa Biblia Wawe Walimu

14. Wanafunzi wa Biblia wanahitaji kufanya maendeleo gani?

14 Ikiwa wanafunzi wetu wa Biblia watatii “mambo yote” ambayo Yesu aliwaamuru wanafunzi wake, wanahitaji kufanya maendeleo na kuwa walimu wa Neno la Mungu wala si wanafunzi tu. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:6-8) Unaweza kufanya nini ili kumsaidia mwanafunzi afanye maendeleo hayo ya kiroho?

15. Kwa nini unapaswa kumtia moyo mwanafunzi wako wa Biblia ahudhurie mikutano ya Kikristo?

15 Tangu siku ya kwanza ya funzo, mwalike mwanafunzi ahudhurie mikutano pamoja nawe. Mweleze kwamba unapata mazoezi ya kuwa mwalimu wa Neno la Mungu katika mikutano hiyo. Kwa majuma kadhaa, tumia dakika chache mwishoni mwa kila funzo la Biblia kumweleza kuhusu programu ya mafundisho ya kiroho ambayo unapokea katika mikutano na makusanyiko mbalimbali. Mweleze kwa uchangamfu faida unazopata unapohudhuria. (Waebrania 10:24, 25) Mara tu mwanafunzi anapoanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, inaelekea kwamba atakuwa mwalimu wa Neno la Mungu.

16, 17. Ni miradi gani ambayo mwanafunzi wa Biblia anaweza kujiwekea na kufikia?

16 Msaidie mwanafunzi wa Biblia ajiwekee miradi ambayo anaweza kufikia. Kwa mfano, mtie moyo azungumze na rafiki au mtu wake wa ukoo kuhusu mambo anayojifunza. Pia, mtie moyo ajiwekee mradi wa kusoma Biblia nzima. Ukimsaidia kuwa na zoea zuri la kusoma Biblia kwa ukawaida, zoea hilo litamfaidi hata baada ya kubatizwa. Kwa kuongezea, mbona usipendekeze kwamba mwanafunzi huyo ajiwekee mradi wa kukumbuka angalau andiko moja la Biblia ambalo linajibu swali moja muhimu kutoka katika kila sura ya kitabu Biblia Inafundisha? Akifanya hivyo, atakuwa ‘mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, akilitumia sawasawa neno la kweli.’—2 Timotheo 2:15.

17 Badala ya kumfundisha mwanafunzi kunukuu tu maandiko au kuyaeleza kwa maneno yake tu, mtie moyo atumie mistari fulani ya Biblia kuwajibu wale wanaotaka kujua sababu ya imani yake. Vipindi vifupi vya mazoezi vinaweza kumsaidia. Unaweza kujifanya kuwa mtu wa ukoo au mfanyakazi mwenzake na kisha umwambie mwanafunzi huyo akueleze mambo anayoamini. Mwonyeshe mwanafunzi jinsi ya kujibu kwa “tabia-pole na heshima kubwa.”—1 Petro 3:15.

18. Mwanafunzi wa Biblia anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, unaweza kumsaidia kwa njia gani nyinginezo?

18 Baada ya muda, huenda mwanafunzi akastahili kushiriki katika huduma ya shambani. Kazia kwamba ni pendeleo kuruhusiwa kushiriki katika kazi hii. (2 Wakorintho 4:1, 7) Baada ya wazee kuhakikisha kwamba mwanafunzi anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, msaidie kutayarisha habari rahisi, kisha nenda naye katika utumishi wa shambani. Endelea kuhubiri naye kwa ukawaida katika sehemu nyingine za huduma ya hadharani, na umfundishe jinsi ya kutayarisha na kufanya ziara nzuri za kurudia. Mfano wako mzuri utamchochea.—Luka 6:40.

‘Kujiokoa Wewe Mwenyewe na Wale Wanaokusikiliza Pia’

19, 20. Tunapaswa kuwa na mradi gani, na kwa nini?

19 Bila shaka, kazi nyingi ngumu inahitajiwa ili kumsaidia mtu kupata “ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Hata hivyo, ni mambo machache maishani yanayoweza kuleta furaha kama ile ya kumsaidia mtu fulani kutii yale ambayo Biblia inafundisha. (1 Wathesalonike 2:19, 20) Kwa kweli, tuna pendeleo kubwa sana la kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” katika kazi hii ya kufundisha inayofanywa ulimwenguni pote!—1 Wakorintho 3:9.

20 Kupitia Yesu Kristo na malaika wenye nguvu, hivi karibuni Yehova atawahukumu vikali wale “wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 Wathesalonike 1:6-8) Maisha ya watu yamo hatarini. Je, unaweza kuweka mradi wa kuongoza angalau funzo moja la Biblia kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Unaposhiriki katika kazi hii, una nafasi ya ‘kujiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.’ (1 Timotheo 4:16) Sasa kuliko wakati mwingine wowote, tunapaswa kuwasaidia haraka wengine watii yale ambayo Biblia inafundisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Umejifunza Nini?

• Kitabu Biblia Inafundisha kimechapishwa kwa kusudi gani?

• Unaweza kuanzisha mafunzo ya Biblia kwa njia gani ukitumia kitabu Biblia Inafundisha?

• Ni njia gani za kufundisha zenye matokeo zaidi?

• Unaweza kumsaidia namna gani mwanafunzi awe mwalimu wa Neno la Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je, unakitumia vizuri kitabu hiki?

[Picha katika ukurasa wa 27]

Mazungumzo mafupi yanaweza kumchochea sana mtu atake kupata ujuzi wa Biblia

[Picha katika ukurasa wa 29]

Unaweza kufanya nini ili kumsaidia mwanafunzi aikazie Biblia fikira?

[Picha katika ukurasa wa 30]

Msaidie mwanafunzi wa Biblia afanye maendeleo