Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tuwatazamie Wengine Tu Waseme Ukweli?

Je, Tuwatazamie Wengine Tu Waseme Ukweli?

Je, Tuwatazamie Wengine Tu Waseme Ukweli?

“NINACHUKIA uwongo, na ninachukia kudanganywa!” akasema msichana mwenye umri wa miaka 16. Wengi wetu tunahisi vivyo hivyo. Tunapenda kuamini kwamba habari tunazopata ni za kweli, iwe zinapitishwa kwa mdomo au tunazisoma. Lakini, je, sisi tuna zoea la kusema ukweli tunapowapa wengine habari?

Katika uchunguzi uliofanywa nchini Ujerumani, watu wengi ambao walihojiwa walihisi kwamba “kusema uwongo katika mambo madogo ili kujilinda au kuwalinda wengine wasipatwe na madhara kunaruhusiwa na hata ni kwa lazima ili watu wawe na uhusiano mzuri.” Mwandishi mwingine wa habari aliandika hivi: “Kusema ukweli na ukweli mtupu nyakati zote ni jambo zuri, lakini kunachosha.”

Je, inawezekana kwamba tunataka watu wengine waseme ukweli huku tukihisi kuwa nyakati nyingine sisi tuna sababu nzuri za kutosema ukweli? Je, haidhuru ikiwa tunasema ukweli au uwongo? Kusema uwongo kuna matokeo gani?

Madhara ya Kusema Uwongo

Fikiria madhara ya kusema uwongo. Kusema uwongo kunafanya mume na mke na hata washiriki wa familia wakose kuaminiana. Porojo isiyo na msingi inaweza kumharibia mtu sifa. Gharama za kuendesha biashara zinapanda kwa sababu ya wafanyakazi kudanganya na kusababisha bei ya vitu iongezeke. Ripoti za uwongo kuhusu kodi zinazuia serikali zisipate pesa zinazohitajiwa ili kutoa huduma kwa raia. Habari zilizopotoshwa za watafiti zinaharibu kazi zao nzuri na kuharibu sifa ya mashirika yanayoheshimika. Miradi ya udanganyifu ya kutajirika upesi imewafanya wafanyabiashara wapoteze akiba yao ya maisha au wapate hasara kubwa zaidi. Haishangazi kwamba Biblia inatuambia kuwa mambo ambayo Yehova Mungu anachukia yanatia ndani “ulimi wa uwongo” na “shahidi wa uwongo anayesema uwongo!”—Methali 6:16-19.

Kuzoea kusema uwongo kunaweza kuwadhuru watu mmoja-mmoja na pia jamii kwa ujumla. Watu wengi wanakubaliana na jambo hilo. Basi, kwa nini watu wanazoea kusema uwongo kimakusudi? Je, kila jambo lisilo la kweli ni uwongo? Tutazungumzia majibu ya maswali hayo na mengineyo katika makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Kusema uwongo kunawafanya wenzi wa ndoa wakose kuaminiana