Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Rahisi, Lakini Je, Ni Sahihi?

Ni Rahisi, Lakini Je, Ni Sahihi?

Ni Rahisi, Lakini Je, Ni Sahihi?

MNAMO Septemba 2005, Kanisa la Anglikana lilitoa kwa uchangamfu Biblia ya Dakika 100 (The 100-Minute Bible). Katika Biblia hiyo inayokusudiwa kusomwa kwa dakika 100, Maandiko yote ya Kiebrania yamewekwa kwenye ukurasa mmoja wenye visehemu 17 nayo Maandiko ya Kigiriki katika visehemu 33, na hivyo wameondoa zile sehemu zilizoitwa na msomaji mmoja “sehemu zenye kuchosha.” Ni Biblia rahisi kusoma, lakini je, ni sahihi?

Mwanafunzi wa Biblia aliye makini sana atagundua kwamba haina jina la Mungu, Yehova, na pia ataona mambo mengine ambayo si sahihi. (Zaburi 83:18) Kwa mfano, sehemu ya 1 inasema kwamba Mungu “aliumba mbingu na dunia katika kipindi cha siku sita halisi.” Hata hivyo, kitabu cha Mwanzo 1:1 kinasema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Kisha, simulizi hilo la mwanzo linaeleza matendo zaidi ya uumbaji kuhusiana na dunia, ambayo yalichukua “siku” au vipindi sita vya wakati. Halafu, andiko la Mwanzo 2:4 linajumlisha kipindi chote cha uumbaji na kukiita “siku ambayo Yehova Mungu aliifanya dunia na mbingu.”

Kulingana na Biblia ya Dakika 100, Ayubu, yule mtu mtimilifu, alishambuliwa na “Shetani, mmoja wa watumishi [wa Mungu], . . . ambaye kazi yake ilikuwa kuwashtaki wanadamu.” Je, unaona kasoro iliyopo? Jina “Shetani” linamaanisha “Mpinzani.” Shetani si mtumishi wa Mungu, yeye kwa kweli ni adui mkuu wa Mungu na amechagua mwenyewe kuwa mshtaki wa wanadamu.—Ufunuo 12:7-10.

Namna gani sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Biblia ya Dakika 100? Katika mfano wa kondoo na mbuzi, Biblia hiyo mpya inasema kwamba Yesu anawakubali wale ambao walimsaidia “mtu yeyote, hata awe wa hali ya chini kadiri gani.” Hata hivyo, Yesu alisema kwamba anawabariki wale wanaowatendea mema wafuasi wake wa karibu, yaani, “ndugu” zake. (Mathayo 25:40) Kitabu cha Ufunuo kilichofupishwa kinawajulisha wasomaji kwamba “Rome, ambayo ni Babiloni mkubwa, itaharibiwa kabisa.” Hata hivyo, wanafunzi wa Biblia wanajua kwamba maandishi ya awali hayasemi popote kwamba Roma ni “Babiloni Mkubwa.”—Ufunuo 17:15–18:24.

Kwa wale wanaotaka kumjua Muumba na kuelewa kusudi lake, hakuna kitu kingine kinachoweza kuchukua mahali pa Biblia nzima. Ni kweli kwamba kusoma Biblia kutachukua zaidi ya dakika 100, lakini kufanya hivyo kuleta thawabu isiyo na kifani. (Yohana 17:3) Tafadhali, fanya jitihada hizo nawe utapata thawabu.—2 Timotheo 3:16, 17.