Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kujifunza Nini Kutoka kwa Watoto?

Unaweza Kujifunza Nini Kutoka kwa Watoto?

Unaweza Kujifunza Nini Kutoka kwa Watoto?

“UNATENDA kama mtoto!” Ikiwa tungeambiwa hivyo, inaelekea kwamba tungeudhika. Ingawa watoto wadogo wanapendeza, ni wazi kwamba si wakomavu na hawana uzoefu na hekima ambayo kwa kawaida watu wazima wanakuwa nayo.—Ayubu 12:12.

Hata hivyo, wakati fulani Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Msipogeuka na kuwa kama watoto wachanga, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 18:3) Yesu alimaanisha nini? Watoto wadogo wana sifa gani ambazo watu wazima wanapaswa kuiga?

Kusitawisha Unyenyekevu Kama wa Watoto

Fikiria hali iliyomfanya Yesu aseme maneno hayo. Akiwa amefika Kapernaumu baada ya safari ndefu, Yesu aliwauliza wanafunzi wake: “Mlikuwa mkibishania nini barabarani?” Wanafunzi hao walinyamaza kwa aibu, kwa kuwa walikuwa wamebishana kuhusu ni nani kati yao aliye mkuu zaidi. Mwishowe, walipata ujasiri na kumuuliza Yesu: “Ni nani kwa kweli aliye mkuu zaidi katika ufalme wa mbinguni?”—Marko 9:33, 34; Mathayo 18:1.

Huenda ikashangaza kwamba baada ya kuwa na Yesu kwa miaka mitatu hivi, wanafunzi wangebishana kuhusu cheo. Hata hivyo, walilelewa katika dini ya Kiyahudi iliyokazia sana mambo kama hayo. Kwa wazi, malezi hayo ya kidini pamoja na kutokamilika kwa kibinadamu kuliathiri maoni yao.

Yesu aliketi chini, akawaita wanafunzi wake, na kusema: “Ikiwa mtu yeyote anataka kuwa wa kwanza, lazima awe wa mwisho kati ya wote na mhudumu wa wote.” (Marko 9:35) Inaelekea kwamba maneno hayo yaliwashangaza wanafunzi. Maelezo ya Yesu yalipingana kabisa na maoni ya Kiyahudi kuhusu ukuu! Kisha, Yesu akamwita mtoto mdogo kando yake. Huku akimkumbatia mtoto huyo, Yesu alikazia wazo kuu: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Msipogeuka na kuwa kama watoto wachanga, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni. Basi, yeyote atakayejinyenyekeza mwenyewe kama mtoto huyu mchanga ndiye aliye mkuu zaidi katika ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 18:3, 4.

Alifundisha somo zuri kama nini kuhusu unyenyekevu! Wazia ilivyokuwa. Kikundi cha wanaume wazima waliokomaa ambao walichukua mambo kwa uzito kilimzunguka mtoto mmoja mdogo. Wanaume hao walimkazia macho. Mtoto huyo alikuwa mtulivu na mwenye kuwatumaini sana wengine! Hakuwa na chuki wala uadui wowote! Alikuwa mwenye kujitiisha na mwenye kiasi kama nini! Ndiyo, mtoto huyo mdogo alionyesha kwa njia nzuri sana sifa ya Mungu ya unyenyekevu.

Somo la Yesu liko wazi. Sote tunapaswa kusitawisha unyenyekevu kama wa watoto ikiwa tutarithi Ufalme wa Mungu. Katika mpango wa familia ya Yehova, hakuna nafasi ya kushindana au kuwa na kiburi. (Wagalatia 5:26) Kwa kweli, hizo ndizo sifa mbaya ambazo zilimchochea Shetani Ibilisi amwasi Mungu. Haishangazi kwamba Yehova anachukia sifa hizo!—Methali 8:13.

Wakristo wa kweli wanataka kutumikia wala si kuwa na cheo. Hata tupewe kazi ya chini jinsi gani, au tuwe tunamtumikia mtu wa chini kadiri gani, unyenyekevu wa kweli unatuchochea kuwatumikia wengine. Utumishi kama huo wa unyenyekevu unaleta thawabu kubwa. Yesu anasema: “Yeyote yule anayempokea mmoja wa watoto wachanga kama huyu kwa msingi wa jina langu, ananipokea mimi; na yeyote anayenipokea mimi, anapokea, si mimi tu, bali pia yule aliyenituma.” (Marko 9:37) Kusitawisha ukarimu, unyenyekevu, na roho kama ya watoto kunatufanya tuwe na umoja na Mtu mkuu zaidi katika ulimwengu na pia na Mwana wake. (Yohana 17:20, 21; 1 Petro 5:5) Tutapata furaha inayotokana na kutoa. (Matendo 20:35) Nasi tunaridhika kwa sababu ya kuchangia amani na umoja ulio kati ya watu wa Mungu.—Waefeso 4:1-3.

Wenye Kufundishika na Kutumaini

Kisha, Yesu anakazia somo lingine ambalo watu wazima wanaweza kujifunza kutoka kwa watoto: “Yeyote yule asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mchanga hataingia kamwe ndani yake.” (Marko 10:15) Watoto ni wanyenyekevu na pia wenye kufundishika. “Wanafyonza habari kama sifongo,” anasema mama mmoja.

Kwa hiyo, ili turithi Ufalme wa Mungu, ni lazima tukubali na kutii ujumbe wa Ufalme. (1 Wathesalonike 2:13) Kama watoto wachanga waliozaliwa hivi karibuni, ni lazima ‘tukuze tamaa kwa ajili ya maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni ya lile neno, ili kupitia hayo tukue kufikia wokovu.’ (1 Petro 2:2) Namna gani ikiwa fundisho fulani la Biblia linaonekana kuwa gumu kueleweka? “Watoto wanaendelea kuuliza ‘Kwa nini?’ mpaka wanapopata majibu yenye kuridhisha kwa maswali yao,” anasema mfanyakazi mmoja anayewatunza watoto. Tunapaswa kuiga mfano wao. Basi endelea kujifunza. Zungumza na Wakristo wenye uzoefu. Mwombe Yehova hekima. (Yakobo 1:5) Bila shaka, mwishowe utapata thawabu ukiendelea kusali bila kuacha.—Mathayo 7:7-11.

Hata hivyo, huenda wengine wakajiuliza, ‘Watu wenye kufundishika wanaweza kudanganywa kwa urahisi, sivyo?’ Hawawezi ikiwa wana mwongozo unaotegemeka. Kwa mfano, kwa kawaida watoto wanatafuta mwongozo wa wazazi wao. “Wazazi wanathibitisha kwamba wanaweza kutumainiwa kwa kuwalinda na kuwatunza watoto wao kila siku,” anasema baba mmoja. Bila shaka, tunapaswa kumtumaini Baba yetu wa kimbingu, Yehova, kwa sababu hizohizo. (Yakobo 1:17; 1 Yohana 4:9, 10) Yehova anatupa mwongozo wenye kutegemeka kupitia Neno lake lililoandikwa. Roho yake takatifu na tengenezo lake linatufariji na kututegemeza. (Mathayo 24:45-47; Yohana 14:26) Kutumia maandalizi hayo kutatulinda ili tusipate madhara ya kiroho.—Zaburi 91:1-16.

Kama watoto, tunapositawisha sifa ya kumtumaini Mungu tunakuwa na amani ya akili. Msomi mmoja wa Biblia anasema hivi: “Tunapokuwa watoto tunaanza safari bila nauli na bila kujua jinsi tutakavyofika tuendako, lakini hatuwi na mashaka yoyote kwamba wazazi wetu watatufikisha huko salama.” Je, tunamtumaini Yehova vivyo hivyo katika safari yetu maishani?—Isaya 41:10.

Kumtumaini Mungu kwa moyo wote kunatusaidia kuepuka mtazamo na matendo yanayoweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho. Badala yake, tunaamini kabisa maneno ya Yesu ya kwamba Baba yetu wa mbinguni anajua matendo yetu na kwamba tukiendelea kutafuta Ufalme kwanza na uadilifu wa Mungu, Mungu atatutunza. Na hilo litatuwezesha kushinda vishawishi vya kufuatia mambo ya kimwili na kupuuza wajibu wetu wa kiroho.—Mathayo 6:19-34.

“Watoto Kuhusiana na Ubaya”

Ingawa watoto hawazaliwi wakiwa wakamilifu, wao wana akili na mioyo safi. Kwa sababu hiyo, Biblia inawahimiza Wakristo hivi: “Iweni watoto kuhusiana na ubaya.”—1 Wakorintho 14:20.

Mfikirie Monique mwenye umri wa miaka mitano, ambaye alimwambia mama yake hivi kwa msisimko: “Rafiki yangu mpya Sarah, ana nywele zilizojipinda-pinda tu kama zangu!” Monique hakusema kuhusu rangi ya ngozi au jamii ya akina Sarah. Mzazi mmoja anasema: “Watoto wadogo hawajali rangi. Hawana ukabila wala ubaguzi.” Kuhusiana na hilo, watoto wanaonyesha kwa njia bora maoni ya Mungu wetu asiye na ubaguzi, ambaye anawapenda watu wa mataifa yote.—Matendo 10:34, 35.

Pia, watoto wana uwezo mkubwa sana wa kusamehe. Mzazi mmoja anasema hivi: “Jack na Levi wanapopigana, tunawaambia waombane msamaha, na muda si muda wanaanza tena kucheza kwa furaha. Hawanuni, hawakumbuki yaliyopita, au kutoa masharti kabla ya kusameheana. Wanaendelea tu na maisha.” Ni mfano mzuri kama nini kwa watu wazima!—Wakolosai 3:13.

Zaidi ya hilo, watoto wadogo wanakubali kwa urahisi kwamba kuna Mungu. (Waebrania 11:6) Mara nyingi, unyoofu wao unawachochea kuwatolea wengine ushahidi kwa ujasiri. (2 Wafalme 5:2, 3) Sala zao rahisi na zinazotoka moyoni zinaweza kugusa moyo ulio mgumu sana. Na wanaposhawishiwa, wanaweza kuwa imara sana. Watoto wadogo ni zawadi zenye thamani kama nini!—Zaburi 127:3, 4.

Kuwa Tena na Sifa Nzuri

Huenda ukajiuliza, ‘Je, inawezekana watu wazima kuwa tena na sifa nzuri kama za watoto?’ Jibu rahisi na lenye kutia moyo ni ndiyo! Kwa kweli, amri ya Yesu ya “kuwa kama watoto wachanga” inathibitisha kwamba hilo linawezekana.—Mathayo 18:3.

Kwa mfano: Kikundi cha wasanii kinaweza kurekebisha mchoro wenye thamani kubwa. Wanafanya hivyo kwa kuondoa uchafu na kurekebisha makosa yaliyofanywa na wengine. Baada ya subira na jitihada nyingi za wasanii hao, watu wote wanaweza tena kuona mchoro wa awali ulio maridadi na wenye rangi za kuvutia. Vivyo hivyo, tukijitahidi bila kuacha, na kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova, na utegemezo wenye upendo wa kutaniko la Kikristo, tunaweza tena kuwa na sifa nzuri ambazo tulionyesha tulipokuwa watoto.—Waefeso 5:1.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kiasili watoto ni wanyenyekevu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watoto wadogo hawana ubaguzi, wanasamehe na kusahau haraka