Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usiache Kamwe Kukuza Uthamini Wako

Usiache Kamwe Kukuza Uthamini Wako

Usiache Kamwe Kukuza Uthamini Wako

“Jinsi mawazo yako yalivyo yenye thamani kwangu! Ee Mungu, jinsi jumla yake yote ilivyo kuu!”—ZABURI 139:17.

1, 2. Kwa nini tuthamini Neno la Mungu, na mtunga-zaburi alisema nini kuhusu jinsi alivyolithamini?

ULIKUWA ugunduzi wa ajabu. Hekalu la Yehova huko Yerusalemu lilipokuwa likirekebishwa, Kuhani Mkuu Hilkia alipata “kitabu cha sheria ya Yehova kupitia mkono wa Musa.” Bila shaka, kitabu hicho kilikuwa nakala ya awali iliyoandikwa karibu miaka 800 mapema! Je, unaweza kuwazia jinsi Mfalme Yosia mwenye kumwogopa Mungu alivyohisi alipopewa kitabu hicho? Kwa kweli, alikithamini sana, na mara moja akamwagiza Shafani, mwandishi, akisome kwa sauti.—2 Mambo ya Nyakati 34:14-18.

2 Leo, Neno la Mungu, likiwa zima au sehemu, linaweza kusomwa na mabilioni ya watu. Lakini je, hilo linapunguza thamani au umuhimu wa Maandiko? Bila shaka hapana! Kwa kweli, maandiko yana mawazo ya Mweza-Yote, yaliyoandikwa kwa faida yetu. (2 Timotheo 3:16) Akieleza jinsi alivyohisi kuhusu Neno la Mungu, mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Jinsi mawazo yako yalivyo yenye thamani kwangu! Ee Mungu, jinsi jumla yake yote ilivyo kuu!”—Zaburi 139:17.

3. Ni nini kinachoonyesha kwamba Daudi alielewa kindani mambo ya kiroho?

3 Uthamini wa Daudi kwa ajili ya Yehova, Neno lake, na mpango wake wa ibada ya kweli haukupungua kamwe. Zaburi nyingi zenye kupendeza ambazo zilitungwa na Daudi zilionyesha jinsi alivyohisi. Kwa mfano, aliandika hivi katika Zaburi 27:4: “Nimemwomba Yehova jambo moja ndilo nitakalolitafuta, kwamba nipate kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yangu, ili kuuona uzuri wa Yehova na kulitazama kwa uthamini hekalu lake.” Katika Kiebrania cha awali, maneno ‘kutazama kwa uthamini’ yanamaanisha kuendelea kutafakari, kuchunguza, kutazama kwa furaha, kwa upendezi, na kuvutiwa. Ni wazi kwamba Daudi alielewa kindani mambo ya kiroho, alithamini kikweli maandalizi ya kiroho ya Yehova, na alikula kwa hamu chakula cha kweli ya kiroho ambayo Mungu alifunua. Tunapaswa kuiga sifa yake nzuri ya kuthamini.—Zaburi 19:7-11.

Thamini Pendeleo la Kujua Kweli ya Biblia

4. Ni nini kilichomfanya Yesu awe na “shangwe sana katika roho takatifu”?

4 Kuelewa kindani Neno la Mungu hakutegemei uwezo wa kiakili au elimu ya kilimwengu ambayo inaleta kiburi. Badala yake, kunategemea fadhili zisizostahiliwa za Yehova ambazo anawaonyesha watu wanyenyekevu wenye mioyo minyoofu ambao wanatambua uhitaji wao wa kiroho. (Mathayo 5:3; 1 Yohana 5:20) Yesu alipotafakari kuhusu wanadamu fulani wasio wakamilifu ambao majina yao yalikuwa yanaandikwa mbinguni, ‘alikuwa na shangwe sana katika roho takatifu, akasema: “Ninakusifu hadharani wewe, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha kwa uangalifu wenye hekima na walio na akili mambo hayo, nawe umeyafunua kwa watoto.”’—Luka 10:17-21.

5. Kwa nini wanafunzi wa Yesu hawakupaswa kupuuza kweli za Ufalme ambazo walifunuliwa?

5 Baada ya kutoa sala hiyo ya kutoka moyoni, Yesu aliwageukia wanafunzi wake na kusema: “Yenye furaha ni macho yanayoona mambo ambayo ninyi mnayaona. Kwa maana ninawaambia ninyi, Manabii na wafalme wengi walitamani kuyaona mambo ambayo ninyi mnayaona lakini hawakuyaona, na kuyasikia mambo ambayo ninyi mnayasikia lakini hawakuyasikia.” Ndiyo, Yesu aliwatia moyo wafuasi wake waaminifu wasipuuze kweli za Ufalme zenye thamani ambazo walikuwa wakifunuliwa. Kweli hizo hazikuwa zimefunuliwa kwa vizazi vilivyotangulia vya watumishi wa Mungu, na bila shaka, hazikuwa zimefunuliwa kwa “wenye hekima na walio na akili” wa siku za Yesu!—Luka 10:23, 24.

6, 7. (a) Tuna sababu gani za kuthamini kweli kutoka kwa Mungu? (b) Leo kuna tofauti gani kati ya dini ya kweli na dini ya uwongo?

6 Leo, tuna sababu nyingi hata zaidi za kuthamini kweli kutoka kwa Mungu, kwa kuwa Yehova, kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” amewapa watu wake uelewaji wenye kina zaidi wa Neno lake. (Mathayo 24:45; Danieli 12:10) Kuhusu wakati wa mwisho, nabii Danieli aliandika hivi: “Wengi watakwenda huku na huku, na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.” (Danieli 12:4) Je, hukubali kwamba leo ujuzi juu ya Mungu ‘umekuwa mwingi’ na kwamba watumishi wa Yehova wanalishwa vizuri kiroho?

7 Tunaona tofauti kubwa kati ya ufanisi wa kiroho wa watu wa Mungu na mvurugo wa kidini wa Babiloni Mkubwa! Kwa sababu hiyo, watu wengi ambao wamekatishwa tamaa au kuchukizwa na dini ya uwongo wanaingia katika ibada ya kweli. Watu hao walio mfano wa kondoo ‘hawataki kushiriki pamoja na Babiloni Mkubwa dhambi zake’ au “kupokea sehemu ya mapigo yake.” Yehova na watumishi wake wanawakaribisha watu wote kama hao kwenye kutaniko la kweli la Kikristo.—Ufunuo 18:2-4; 22:17.

Watu Wenye Uthamini Wanamiminika kwa Mungu

8, 9. Maneno ya Hagai 2:7 yanatimizwa namna gani leo?

8 Yehova alitabiri hivi kuhusu nyumba yake ya kiroho ya ibada: “Nitayatikisa mataifa yote, navyo vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote vitaingia; nami nitaijaza nyumba hii utukufu.” (Hagai 2:7) Unabii huo wa ajabu ulitimia katika siku za Hagai wakati mabaki ya watu wa Mungu walipojenga upya hekalu la Yerusalemu. Leo, maneno ya Hagai yanatimia zaidi kuhusiana na hekalu kubwa la kiroho la Yehova.

9 Tayari mamilioni wamemiminika kwenye hekalu la mfano ili kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli,” na kila mwaka mamia ya maelfu ya “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote” yanaendelea kumiminika kwenye hekalu hilo. (Yohana 4:23, 24) Kwa mfano, ripoti ya ulimwenguni pote ya mwaka wa utumishi wa 2006 inaonyesha kwamba watu 248,327 walibatizwa ili kuonyesha kuwa walijiweka wakfu kwa Yehova. Huo ni wastani wa watu wapya 680 kila siku! Upendo wao kuelekea kweli na tamaa yao ya kumtumikia Yehova wakiwa watangazaji wa Ufalme inaonyesha wazi kwamba kwa kweli walivutwa na Mungu.—Yohana 6:44, 65.

10, 11. Simulia jambo lilioonwa linaloonyesha jinsi ambavyo watu wamepata kuithamini kweli ya Biblia.

10 Watu wengi wenye mioyo minyoofu walivutwa kwenye kweli kwa sababu waliona tofauti kati ya “mwadilifu na mwovu, kati ya mtu anayemtumikia Mungu na mtu ambaye hajamtumikia.” (Malaki 3:18) Fikiria kisa cha Wayne na Virginia wenzi wa ndoa ambao walikuwa waumini wa Kanisa la Kiprotestanti lakini hawakuwa wamepata majibu yenye kuridhisha kwa maswali yao mengi. Walichukia vita na walitatizika na kusumbuka walipoona viongozi wa kidini wakibariki askari-jeshi na silaha. Wenzi hao walipokuwa wakizeeka, walihisi kwamba walipuuzwa na washiriki wengine wa kanisa, hata ingawa Virginia alikuwa amefundisha shule ya Jumapili (Siku ya Yenga) kwa miaka kadhaa. Walisema hivi: “Hakuna aliyetutembelea wala kujali hali yetu ya kiroho. Kanisa lilitaka tu pesa zetu. Tulikata tamaa sana.” Walikata tamaa hata zaidi kanisa lilipokubali ngono kati ya watu wa jinsia moja.

11 Wakati huohuo, mjukuu wa Wayne na Virginia na baadaye binti yao wakawa Mashahidi wa Yehova. Ingawa mwanzoni Wayne na Virginia hawakufurahia jambo hilo, baadaye walibadili maoni yao na kukubali funzo la Biblia. Wayne alisema hivi: “Kwa miezi mitatu tu tulijifunza mambo mengi zaidi kuhusu Biblia kuliko yale tuliyojifunza katika miaka 70 iliyotangulia! Hatukujua kamwe kwamba jina la Mungu ni Yehova, wala hatukujua kuhusu Ufalme na Paradiso duniani.” Punde si punde, wenzi hao wanyoofu walianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki katika huduma. Virginia alisema hivi: “Tunataka kumwambia kila mtu kuhusu kweli.” Wenzi hao walibatizwa mwaka wa 2005 wakiwa na umri wa miaka zaidi ya 80. Walisema: “Tumepata familia ya Wakristo wa kweli.”

Thamini Kuwa na “Vifaa Kamili kwa Ajili ya Kila Kazi Njema”

12. Nyakati zote Yehova anawapa nini watumishi wake, na tunapaswa kufanya nini ili tufaidike?

12 Nyakati zote Yehova anawasaidia watumishi wake kufanya mapenzi yake. Kwa mfano, Noa alipewa maagizo hususa yaliyo wazi kuhusu ujenzi wa safina. Ingawa ilikuwa ni mara ya kwanza, Safina ilipaswa kujengwa kwa usahihi kabisa. Na ilijengwa hivyo. Kwa nini? Kwa sababu Noa ‘alifanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.” (Mwanzo 6:14-22) Leo pia, Yehova anawapa watumishi wake vifaa kamili ili wafanye mapenzi yake. Bila shaka, kazi yetu kuu ni kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa na kuwasaidia wale wanaostahili wawe wanafunzi wa Yesu Kristo. Na kama ilivyokuwa katika kisa cha Noa, mafanikio yetu yanategemea utii. Ni lazima tutii na kufuata mwelekezo ambao Yehova anatoa kupitia Neno na tengenezo lake.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

13. Yehova anatuzoeza kupitia nini?

13 Ili tutimize kazi hiyo, ni lazima tujifunze ‘kutumia sawasawa’ kifaa chetu kikuu—Neno la Mungu—ambalo “ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 2:15; 3:16, 17) Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, Yehova anatupa mazoezi yenye thamani kupitia kutaniko la Kikristo. Leo, katika makutaniko 99,770 ulimwenguni pote, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi unafanywa kila juma ili kutusaidia katika huduma. Je, unaonyesha kwamba unathamini mikutano hiyo muhimu kwa kuihudhuria kwa ukawaida na kutumia mambo unayojifunza?—Waebrania 10:24, 25.

14. Watumishi wa Yehova wanaonyesha jinsi gani kwamba wanathamini pendeleo la kumtumikia Mungu? (Tia ndani maelezo kuhusu chati iliyo kwenye ukurasa wa 27 mpaka 30.)

14 Mamilioni ya watu wa Mungu duniani pote wanaonyesha wanathamini mazoezi ambayo wanapata kwa kushiriki kwa bidii katika huduma. Kwa mfano, katika mwaka wa utumishi wa 2006, wahubiri wa Ufalme 6,741,444 walitumia saa 1,333,966,199 katika sehemu zote za huduma, kutia ndani kuongoza mafunzo ya Biblia 6,286,618. Hizo ni habari chache tu kati ya habari nyingi zenye kutia moyo zilizo katika ripoti ya ulimwenguni pote. Tunakuomba uchunguze kwa uangalifu ripoti hiyo na kupata kitia moyo kutokana nayo, kama vile tu ndugu zetu wa karne ya kwanza walivyotiwa moyo sana na ripoti za kupanuka kwa kazi ya kuhubiri wakati wao.—Matendo 1:15; 2:5-11, 41, 47; 4:4; 6:7.

15. Kwa nini yeyote hapaswi kuvunjika moyo kuhusu utumishi wake wa nafsi yote anaomtolea Yehova?

15 Sauti kubwa sana ya sifa inayotolewa kwa Mungu kila mwaka inaonyesha kwamba watumishi wa Yehova wanathamini sana pendeleo la kumjua Yehova na kutoa ushahidi kumhusu. (Isaya 43:10) Ni kweli kwamba dhabihu za sifa ambazo ndugu na dada zetu waliozeeka, wagonjwa au walio dhaifu wanatoa zinaweza kulinganishwa na sarafu ndogo mbili za mjane. Lakini tusisahau kwamba Yehova na Mwana wake wanawathamini sana wale wanaomtumikia Mungu kwa nafsi yote, huku wakifanya yote wanayoweza.—Luka 21:1-4; Wagalatia 6:4.

16. Katika nyakati za karibuni, Mungu ametupa vitabu gani vya kufundishia?

16 Zaidi ya kutuzoeza kwa ajili ya huduma, Yehova, kupitia tengenezo lake, ametupa vifaa bora vya kufundishia. Katika makumi ya miaka ya karibuni, vifaa hivyo vimetia ndani kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele na hivi sasa, kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Wale ambao kwa kweli wanathamini maandalizi hayo wanatumia vizuri vitabu hivyo katika huduma.

Tumia Vizuri Kitabu Biblia Inafundisha

17, 18. (a) Unapenda kutumia sehemu gani za kitabu Biblia Inafundisha katika huduma yako? (b) Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema nini kuhusu kitabu Biblia Inafundisha?

17 Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ambacho kina sura 19 na nyongeza yenye habari nyingi, na ambacho kimeandikwa kwa lugha rahisi na iliyo wazi, ni zawadi katika huduma. Kwa mfano, sura ya 12 inazungumzia kichwa “Kuishi Maisha Yanayompendeza Mungu.” Habari hiyo inamweleza mwanafunzi jinsi anavyoweza kuwa rafiki ya Mungu, jambo ambalo watu wengi hawajawahi kamwe kufikiria au wanafikiri haliwezekani. (Yakobo 2:23) Watu wana maoni gani kuhusu kitabu hicho cha kujifunzia Biblia?

18 Mwangalizi mmoja wa mzunguko huko Australia anaripoti kwamba kitabu Biblia Inafundisha “kinawavutia watu mara moja na kuwaingiza haraka wenye nyumba katika mazungumzo.” Anaongezea kwamba ni rahisi sana kukitumia hivi kwamba “kimewasaidia wahubiri wengi wa Ufalme kuwa tena na uhakika na shangwe katika huduma. Haishangazi kwamba wengine wanakiita kitabu hicho, Hazina ya Dhahabu!”

19-21. Simulia mambo kadhaa yaliyoonwa ambayo yanaonyesha thamani ya kitabu Biblia Inafundisha.

19 Mwanamke mmoja huku Guyana alimwambia hivi painia aliyefika mlangoni pake: “Bila shaka Mungu amekutuma.” Muda mfupi uliotangulia, mwenzi wake alikuwa amemwacha pamoja na watoto wao wawili wadogo. Painia huyo alifungua sura ya 1 ya kitabu Biblia Inafundisha na kusoma kwa sauti fungu la 11, chini ya kichwa “Mungu Anahisije Kuhusu Ukosefu wa Haki?” “Habari hiyo ilimgusa moyo sana,” akasema painia huyo. “Kwa kweli, ilimbidi mama huyo kusimama, kwenda nyuma ya duka lake, na kulia sana.” Mwanamke huyo alikubali kujifunza Biblia kwa ukawaida na dada fulani, na sasa anafanya maendeleo.

20 José, anaishi Hispania, na mke wake alikufa katika msiba wa barabarani. José alitumia dawa za kulevya ili kupata kitulizo, na pia alipata msaada wa madaktari. Hata hivyo, madaktari hao hawangeweza kujibu swali ambalo lilikuwa likimsumbua zaidi José: “Kwa nini Mungu alimwacha mke wangu afe?” Siku moja José alikutana na Francesc, ambaye walifanya kazi pamoja katika kampuni fulani. Francesc alipendekeza wazungumzie sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha. Sura hiyo ina kichwa “Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?” Maelezo ya Kimaandiko na mfano wa mwalimu na mwanafunzi ulimgusa moyo sana José. Alianza kujifunza kwa bidii, akahudhuria kusanyiko la mzunguko, na sasa anahudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme la kwao.

21 Roman, mfanyabiashara mwenye umri wa miaka 40 huko Poland, amekuwa akiheshimu Neno la Mungu sikuzote. Lakini alijishughulisha sana na kazi yake na hakufanya maendeleo sana katika kujifunza Biblia. Hata hivyo, alihudhuria kusanyiko la wilaya na akapokea kitabu Biblia Inafundisha. Baada ya hapo, alifanya mabadiliko makubwa. “Kupitia kitabu hiki,” anasema, “mafundisho yote ya msingi ya Biblia yanapatana kikamilifu.” Sasa Roman anajifunza Biblia kwa ukawaida na anafanya maendeleo mazuri.

Endelea Kukuza Uthamini Wako

22, 23. Tunaweza kuendelea kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini tumaini lililowekwa mbele yetu?

22 Kama ilivyoelezwa katika Kusanyiko la Wilaya lenye kusisimua la “Ukombozi Unakaribia!” Wakristo wa kweli wanatamani sana “ukombozi wa milele” ulioahidiwa na Mungu na ambao unawezekana kupitia damu iliyomwagwa ya Yesu Kristo. Hakuna njia bora ya kuonyesha uthamini wetu wa kutoka moyoni kwa ajili ya tumaini hilo lenye thamani kuliko kuendelea kusafishwa “kutoka katika matendo yaliyokufa ili tutoe utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai.”—Waebrania 9:12, 14.

23 Ndiyo, kwa kweli ni muujiza kuona watangazaji wa Ufalme zaidi ya milioni sita wakivumilia kwa uaminifu katika utumishi wa Mungu ingawa wanachochewa kuliko wakati mwingine wowote wafuatie tamaa zao za kichoyo. Jambo hilo linathibitisha pia kwamba watumishi wa Yehova wanathamini sana pendeleo la kumtumikia Mungu wakijua kwamba ‘kazi yao si ya bure kuhusiana na Bwana.’ Tusiache kamwe kukuza uthamini huo!—1 Wakorintho 15:58; Zaburi 110:3.

Ungetoa Jibu Gani?

• Mtunga-zaburi anatufundisha nini kuhusu kumthamini Mungu na maandalizi yake ya kiroho?

• Maneno ya Hagai 2:7 yanatimizwa namna gani leo?

• Ni vifaa gani ambavyo Yehova amewapa watumishi wake ili wamtumikie kwa matokeo?

• Unaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba unathamini wema wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Chati katika ukurasa wa 27-30]

RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 2006 YA MASHAHIDI WA YEHOVA

(Ona buku lililojadiliwa)

[Picha katika ukurasa wa 25]

Yehova anatupa vifaa kamili ili tufanye mapenzi yake