Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mungu Anayethamini

Yehova Ni Mungu Anayethamini

Yehova Ni Mungu Anayethamini

“Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—WAEBRANIA 6:10.

1. Yehova alionyesha jinsi gani kwamba alimthamini Ruthu Mmoabu?

YEHOVA anathamini sana jitahidi za wale ambao kwa kweli wanataka kufanya mapenzi yake, naye anawapa thawabu kubwa. (Waebrania 11:6) Boazi, mwanamume mwaminifu, alijua sifa hiyo nzuri ya utu wa Mungu, kwa kuwa alimwambia hivi Ruthu Mmoabu, ambaye alimtunza kwa upendo mama mkwe wake aliyekuwa mjane: “Yehova na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda, na upate malipo kamili kutoka kwa Yehova.” (Ruthu 2:12) Je, Ruthu alibarikiwa na Mungu? Alibarikiwa sana, na hata kisa chake kimeandikwa katika Biblia! Zaidi ya hilo, Ruthu aliolewa na Boazi naye akawa nyanya ya Mfalme Daudi na ya Yesu Kristo. (Ruthu 4:13, 17; Mathayo 1:5, 6, 16) Huo ni mfano mmoja kati ya mifano mingi iliyo katika Biblia inayoonyesha kwamba Yehova anawathamini watumishi wake.

2, 3. (a) Ni nini kinachofanya uthamini wa Yehova uwe wa pekee? (b) Kwa nini Yehova anaweza kuonyesha uthamini wa kweli? Toa mfano.

2 Yehova angejiona kuwa asiye mwadilifu ikiwa angekosa uthamini. Andiko la Waebrania 6:10 linasema hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.” Maneno hayo ni ya pekee sana kwa sababu yanaonyesha kwamba Mungu anawathamini watu waliojitoa kwake hata ingawa ni watenda-dhambi na wanapungukiwa na utukufu wake.—Waroma 3:23.

3 Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, huenda tukahisi kwamba matendo yetu ya ujitoaji-kimungu ni duni sana na hivyo hatustahili baraka za Mungu. Hata hivyo, Yehova anaelewa kabisa nia na hali zetu, naye anathamini kikweli utumishi wetu wa nafsi yote. (Mathayo 22:37) Fikiria mfano huu: Mama fulani anapata zawadi ya mkufu wa bei ya chini kwenye meza yake. Anaweza kuiona zawadi hiyo kuwa yenye thamani ndogo na kuipuuza. Lakini, kadi iliyoambatanishwa na zawadi hiyo inaonyesha kwamba zawadi hiyo imetoka kwa binti yake mdogo ambaye alitumia pesa zake zote alizohifadhi ili kuinunua. Sasa mama huyo anakuwa na maoni tofauti kuhusu zawadi hiyo. Pengine akilengwa-lengwa na machozi, anamkumbatia mtoto wake na kuonyesha uthamini wake wa kutoka moyoni.

4, 5. Yesu alimwiga Yehova jinsi gani katika kuonyesha uthamini?

4 Kwa sababu anajua kabisa nia na udhaifu wetu, Yehova anathamini tunapompa kile kilicho bora, iwe ni kidogo au kikubwa. Kuhusiana na hilo, Yesu alimwiga kabisa Baba yake. Kumbuka simulizi la Biblia kuhusu mjane aliyetoa sarafu ndogo mbili. “[Yesu] alipotazama juu aliwaona matajiri wakitumbukiza zawadi zao ndani ya masanduku ya hazina. Ndipo akaona mjane fulani mwenye uhitaji akitumbukiza humo sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana, naye akasema: ‘Ninawaambia ninyi kwa kweli, Mjane huyu, ijapokuwa ni maskini, ametumbukiza ndani zaidi kuliko hao wote. Kwa maana wote hawa walitumbukiza zawadi kutokana na ziada yao, lakini mwanamke huyu kutokana na uhitaji wake alitumbukiza ndani riziki yote aliyokuwa nayo.’”—Luka 21:1-4.

5 Ndiyo, akijua hali za mwanamke huyo—kwamba alikuwa mjane na maskini—Yesu alielewa thamani kamili ya zawadi yake, naye aliithamini sana. Tunaweza kusema vivyo hivyo kumhusu Yehova. (Yohana 14:9) Je, haitii moyo kujua kwamba haidhuru hali zako, unaweza kupata kibali machoni pa Mungu wetu anayethamini na pa Mwana wake?

Yehova Amthawabisha Mwethiopia Mwenye Kumwogopa Mungu

6, 7. Kwa nini Yehova alionyesha uthamini wake kumwelekea Ebed-meleki, naye alifanya hivyo jinsi gani?

6 Maandiko yanaonyesha tena na tena kwamba Yehova anawathamini wale wanaofanya mapenzi yake. Fikiria jinsi alivyoshughulika na Ebed-meleki, Mwethiopia mwenye kumwogopa Mungu. Ebed-meleki aliishi siku za Yeremia na alikuwa mtumishi katika nyumba ya Mfalme Sedekia wa Yuda, ambaye hakuwa mwaminifu. Ebed-meleki alipata habari kuwa wakuu wa Yuda walikuwa wamemshtaki isivyo haki nabii Yeremia kwamba alikuwa mchochezi na wakamtupa ndani ya tangi ili afe njaa humo. (Yeremia 38:1-7) Akijua kwamba Yeremia alichukiwa sana kwa sababu ya ujumbe aliohubiri, Ebed-meleki alihatarisha uhai wake mwenyewe na kuzungumza na mfalme. Kwa ujasiri, Mwethiopia huyo alisema: “Ee bwana wangu mfalme, watu hawa wametenda mabaya kwa yote ambayo wamemtendea Yeremia nabii, ambaye wamemtupa ndani ya tangi la maji, hivi kwamba atakufa hapo alipo kwa sababu ya njaa.” Ndipo mfalme akamwamuru Ebed-meleki achukue wanaume 30 na kumwokoa nabii wa Mungu.—Yeremia 38:8-13.

7 Yehova aliona kwamba Ebed-meleki alikuwa na imani, ambayo ilimsaidia kushinda woga wowote ambao huenda alikuwa nao. Hivyo, Yehova alionyesha uthamini wake na akamwambia Ebed-meleki hivi kupitia Yeremia: “Ninayatimiza maneno yangu juu ya jiji hili kuwe msiba wala si mema . . . Nami nitakukomboa wewe katika siku ile, . . . nawe hutatiwa mkononi mwa watu ambao unawaogopa. Kwa maana bila shaka nitakuokoa . . . ; na hakika nafsi yako itakuwa kama nyara kwako kwa sababu umenitegemea mimi.” (Yeremia 39:16-18) Ndiyo, Yehova alimwokoa Ebed-meleki, na pia Yeremia, kutoka kwa wakuu waovu wa Yuda na baadaye kutoka kwa Wababiloni, ambao waliteketeza Yerusalemu. Zaburi 97:10 inasema kwamba, “[Yehova] anazilinda nafsi za washikamanifu wake; huwakomboa kutoka katika mkono wa waovu.”

“Baba Yako Anayetazama Akiwa Mahali pa Siri Atakulipa”

8, 9. Kama Yesu alivyoonyesha, Yehova anathamini sala za namna gani?

8 Jambo lingine linalothibitisha kwamba Yehova anathamini sana matendo yetu ya ujitoaji-kimungu linaweza kuonekana katika yale ambayo Biblia inasema kuhusu sala. “Sala ya wanyoofu ni furaha kwake [Mungu],” akasema mwenye hekima. (Methali 15:8) Katika siku za Yesu viongozi wengi wa kidini walisali hadharani ili kuwapendeza watu wala si kwa sababu ya unyoofu wa kutoka moyoni. “Wanapata thawabu yao kwa ukamili,” akasema Yesu. “Lakini wewe unaposali,” akawaagiza wafuasi wake, “ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye mahali pa siri; ndipo Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa.”—Mathayo 6:5, 6.

9 Bila shaka, Yesu hakuwa akishutumu sala za hadharani, kwa sababu yeye mwenyewe alisali hadharani pindi fulani. (Luka 9:16) Yehova anathamini sana tunaposali kwake kwa moyo mnyoofu, bila kuwa na nia ya kuwapendeza wengine. Kwa kweli, sala zetu za faraghani, zinaonyesha waziwazi kina cha upendo wetu kwa Mungu na jinsi tunavyomtumaini. Hivyo, haishangazi kwamba mara kadhaa Yesu alisali mahali pasipo na watu. Pindi moja, alifanya hivyo “asubuhi na mapema, kulipokuwa bado kuna giza.” Pindi nyingine, ‘alipanda mlimani akiwa peke yake ili kusali.’ Na kabla ya kuwachagua mitume wake 12, Yesu alisali usiku wote akiwa peke yake.—Marko 1:35; Mathayo 14:23; Luka 6:12, 13.

10. Sala zetu zinapoonyesha unyoofu na hisia za ndani, tunaweza kuwa na uhakika gani?

10 Wazia jinsi Yehova alivyosikiliza kwa makini sala za kutoka moyoni za Mwana wake! Ni kweli kwamba nyakati nyingine Yesu alisali “pamoja na vilio vyenye nguvu na machozi, naye akasikiwa vizuri kwa sababu ya kumwogopa Mungu.” (Waebrania 5:7; Luka 22:41-44) Sala zetu zinapoonyesha unyoofu na hisia za ndani kama hizo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yetu wa mbinguni anasikiliza kwa makini na kwa uthamini. Ndiyo, “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, . . . wote wanaomwitia yeye katika ukweli.”—Zaburi 145:18.

11. Yehova anahisi namna gani kuhusu yale tunayofanya mahali pa siri?

11 Ikiwa Yehova anathamini tunaposali kwake tukiwa mahali pa siri, bila shaka anathamini sana tunapomtii mahali pa siri! Ndiyo, Yehova anajua yale tunayofanya katika siri. (1 Petro 3:12) Kwa kweli, kuwa waaminifu na watiifu tukiwa peke yetu kunaonyesha vizuri kwamba tuna “moyo kamili” kumwelekea Yehova, yaani, moyo wenye nia nzuri ambao unashikamana na yaliyo sawa. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Mwenendo kama huo unafanya moyo wa Yehova ushangilie kama nini!—Methali 27:11; 1 Yohana 3:22.

12, 13. Tunaweza kulinda akili na moyo wetu jinsi gani na kuwa kama mwanafunzi mwaminifu Nathanaeli?

12 Hivyo, Wakristo waaminifu wanajilinda wasitende dhambi za siri ambazo zinachafua akili na moyo, kama kutazama ponografia (picha au habari za ngono) na jeuri. Ingawa dhambi fulani zinaweza kufichwa kwa wanadamu, tunatambua kwamba “vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13; Luka 8:17) Tunapojitahidi kuepuka mambo yasiyompendeza Yehova, tunakuwa na dhamiri safi na tunafurahi kujua kwamba tuna kibali cha Mungu. Ndiyo, hapana shaka kwamba Yehova anathamini sana mtu “anayetembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wake.”—Zaburi 15:1, 2.

13 Hata hivyo, tunaweza kulinda jinsi gani akili na moyo wetu katika ulimwengu huu ambao umejaa uovu? (Methali 4:23; Waefeso 2:2) Zaidi ya kufaidika kabisa na maandalizi yote ya kiroho, ni lazima tujitahidi kadiri tunavyoweza kukataa mambo mabaya na kufanya yaliyo mema, na kuchukua hatua ya haraka ili tamaa zisizofaa zisichukue mimba na kuzaa dhambi. (Yakobo 1:14, 15) Hebu wazia furaha ambayo ungekuwa nayo ikiwa Yesu angesema hivi juu yako kama alivyosema kumhusu Nathanaeli: “Ona, [mtu] ambaye hamna udanganyifu ndani yake.” (Yohana 1:47) Baadaye Nathanaeli, ambaye pia aliitwa Bartholomayo, alipata pendeleo la kuwa mmoja wa mitume 12 wa Yesu.—Marko 3:16-19.

“Kuhani Mkuu Mwenye Rehema na Mwaminifu”

14. Maoni ya Yesu kuhusu tendo la Maria yalitofautiana jinsi gani na ya wengine?

14 Yesu akiwa “mfano wa Mungu asiyeonekana,” Yehova, sikuzote anamwiga kikamili Baba yake katika kuwathamini wale wanaomtumikia Mungu kwa moyo safi. (Wakolosai 1:15) Kwa mfano, siku tano kabla ya kutoa uhai wake, Yesu na wanafunzi wake kadhaa walialikwa nyumbani kwa Simoni wa Bethania. Jioni hiyo, Maria, dada ya Lazaro na Martha, alichukua “ratili moja ya mafuta yenye marashi, nardo halisi, ghali sana” (yenye thamani ya karibu mshahara wa mwaka mmoja), na kuyamwaga juu ya kichwa na miguu ya Yesu. (Yohana 12:3) “Hasara hii ni ya nini?” wengine wakauliza. Hata hivyo, Yesu alikuwa na maoni tofauti kabisa kuhusu tendo la Maria. Yesu aliliona kuwa tendo la ukarimu na umuhimu mkubwa kwa sababu alikuwa akikaribia kufa na kuzikwa. Hivyo, badala ya kumchambua Maria, Yesu alimsifu. “Kokote ambako hii habari njema itahubiriwa katika ulimwengu wote,” akasema, “jambo ambalo mwanamke huyu ametenda litasimuliwa pia kuwa kumbukumbu lake.”—Mathayo 26:6-13.

15, 16. Tunafaidika jinsi gani kwa sababu ya Yesu kuishi akiwa mwanadamu na kumtumikia Mungu?

15 Tuna pendeleo kubwa kama nini kuwa na Kiongozi mwenye kuthamini sana, yaani, Yesu! Kwa hakika, maisha ya Yesu akiwa mwanadamu yalimtayarisha kwa ajili ya kazi ambayo Yehova alitaka afanye, yaani, kuwa Kuhani Mkuu na Mfalme, kwanza kwa ajili ya kutaniko la watiwa-mafuta na baadaye kwa ajili ya ulimwengu.—Wakolosai 1:13; Waebrania 7:26; Ufunuo 11:15.

16 Hata kabla hajaja duniani, Yesu aliwathamini sana na kuwapenda wanadamu kwa njia ya pekee. (Methali 8:31) Kwa kuishi akiwa mwanadamu, Yesu alipata kuelewa zaidi majaribu tunayopata tunapomtumikia Mungu. “[Yesu] alipaswa kuwa kama ‘ndugu’ zake katika mambo yote,” akaandika mtume Paulo, “ili awe kuhani mkuu mwenye rehema na mwaminifu . . . Kwa kuwa yeye mwenyewe ameteseka alipokuwa akijaribiwa, anaweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.” Yesu anaweza “kuusikitikia udhaifu wetu” kwa sababu “amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na dhambi.”—Waebrania 2:17, 18; 4:15, 16.

17, 18. (a) Barua kwa makutaniko saba ya Asia Ndogo zinaonyesha nini kuhusu kina cha uthamini wa Yesu? (b) Wakristo hao watiwa-mafuta walikuwa wakitayarishwa kwa ajili ya nini?

17 Baada ya kufufuliwa ilikuwa wazi kwamba Yesu alielewa zaidi majaribu yaliyowapata wafuasi wake. Fikiria barua zake kwa makutaniko saba huko Asia Ndogo, ambazo ziliandikwa na mtume Yohana. Yesu aliliambia hivi kutaniko la Smirna: “Ninajua dhiki na umaskini wako.” Ni kana kwamba Yesu alikuwa akisema, ‘Ninaelewa kabisa matatizo yako; Ninajua kwelikweli mambo unayokabili.’ Kisha, akiwa mwenye huruma na mamlaka aliyopata kwa kuteseka mpaka kifo, Yesu aliongeza hivi: “Uwe mwaminifu hata kufikia kifo, nami nitakupa taji la uzima.”—Ufunuo 2:8-10.

18 Barua hizo kwa makutaniko saba zina maneno mengi yanayoonyesha kuwa Yesu alielewa vizuri hali ngumu ya wanafunzi wake na kwamba alithamini sana maisha yao ya utimilifu. (Ufunuo 2:1–3:22) Kumbuka kwamba Yesu aliwaambia maneno hayo Wakristo watiwa-mafuta walio na tumaini la kutawala pamoja naye mbinguni. Kama Bwana wao, walikuwa tayari kutimiza daraka kubwa la kuwasaidia kwa huruma nyingi wanadamu wagonjwa wafaidike na dhabihu ya fidia ya Kristo.—Ufunuo 5:9, 10; 22:1-5.

19, 20. Wale wanaofanyiza “umati mkubwa” wanaonyesha uthamini wao kwa Yehova na Mwana wake jinsi gani?

19 Bila shaka, upendo wa Yesu kwa wafuasi wake watiwa-mafuta unaonyeshwa pia kuelekea ‘kondoo wake wengine’ washikamanifu. Mamilioni ya kondoo hao sasa wanafanyiza “umati mkubwa . . . kutoka mataifa yote,” ambao utaokoka ile “dhiki kuu” inayokuja. (Yohana 10:16; Ufunuo 7:9, 14) Kondoo hao wanamiminika upande wa Yesu kwa sababu wanathamini dhabihu yake ya fidia na tumaini lao la uzima wa milele. Wanaonyesha uthamini wao kwa njia gani? Wanafanya hivyo kwa ‘kumtolea Mungu utumishi mtakatifu mchana na usiku.’—Ufunuo 7:15-17.

20 Ripoti ya ulimwenguni pote ya mwaka wa utumishi wa 2006, iliyo kwenye ukurasa wa 27 mpaka 30, inaonyesha wazi kwamba kwa kweli wahudumu hao waaminifu wanamtolea Yehova “utumishi mtakatifu mchana na usiku.” Kwa kweli, katika mwaka huo mmoja tu, wao pamoja na mabaki wachache wa Wakristo watiwa-mafuta walitumia jumla ya saa 1,333,966,199 katika huduma ya hadharani—muda unaolingana na miaka 150,000!

Endelea Kuonyesha Uthamini!

21, 22. (a) Inapohusu kuonyesha uthamini, kwa nini Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu leo? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika habari inayofuata?

21 Katika kushughulika na wanadamu wasio wakamilifu, Yehova na Mwana wake wameonyesha uthamini mkubwa sana. Hata hivyo, kwa kusikitisha, wanadamu wengi hawamjali Mungu, wanakazia tu fikira mambo yao wenyewe. Akieleza kuhusu sifa za watu wanaoishi katika “siku za mwisho,” Paulo aliandika hivi: “Watu watakuwa wenye kujifikiria wenyewe tu, wenye pupa ya pesa . . . Watakuwa wasio na shukrani hata kidogo.” (2 Timotheo 3:1-5, Phillips) Wakristo wa kweli wako tofauti kabisa na watu hao, kwa sababu kupitia sala na utii wao wa kutoka moyoni, na utumishi wao wa nafsi yote wanaonyesha kwamba wanathamini yote ambayo Mungu amewafanyia!—Zaburi 62:8; Marko 12:30; 1 Yohana 5:3.

22 Katika habari inayofuata, tutazungumzia machache kati ya maandalizi mengi ya kiroho ambayo Yehova ametupa kwa upendo. Acheni tukuze hata zaidi uthamini wetu tunapotafakari kuhusu ‘zawadi hizo njema.’—Yakobo 1:17.

Ungetoa Jibu Gani?

• Yehova ameonyesha jinsi gani kwamba yeye ni Mungu anayethamini?

• Tunapokuwa mahali pa siri, tunaweza jinsi gani kufanya moyo wa Yehova ushangilie?

• Yesu alionyesha uthamini kwa njia gani?

• Kuishi akiwa mwanadamu kulimsaidia Yesu namna gani kuwa mtawala mwenye huruma na anayethamini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kama mzazi anavyothamini zawadi ya mtoto wake, Yehova anathamini tunapompa kilicho bora