Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Furahia Dunia Yetu Maridadi

Furahia Dunia Yetu Maridadi

Furahia Dunia Yetu Maridadi

WATAALAMU WA NYOTA wameona kwamba makao ya wanadamu ni doa dogo tu katika ulimwengu mkubwa sana. Uhai haujapatikana mahali pengine popote katika ulimwengu. Dunia ndiyo sayari ya pekee ambayo ina hali zinazofaa kabisa kwa ajili ya uhai.

Zaidi ya hayo, tunaweza kufurahia maisha katika sayari hii maridadi. Inafurahisha kama nini kufurahia joto la jua siku yenye baridi! Ni nani kati yetu asiyevutiwa kuona rangi maridadi jua linapochomoza au kushuka? Bila shaka, jua letu linafanya mengi zaidi ya kutupendeza tu. Uhai wetu unategemea sana jua.

Kwa mamilioni yasiyohesabika ya miaka, nguvu za uvutano za jua zimeshikilia dunia yetu na sayari nyingine katika mizunguko iliyo imara. Na kama wanafunzi wanavyojifunza shuleni, mfumo mzima wa jua unazunguka katikati ya kikundi chetu cha nyota kinachoitwa Kilimia. Lakini katika kikundi chetu cha nyota, jua ni moja tu kati ya nyota zaidi ya bilioni 100 zinazozunguka pamoja.

Nguvu za uvutano zinashikilia kikundi chetu cha nyota pamoja na vikundi vingine 35 hivi vya nyota. Makundi makubwa zaidi ya nyota yana maelfu ya vikundi vya nyota. Inaelekea kwamba mfumo wetu wa jua haungekuwa imara sana ikiwa ungekuwa katika kundi kubwa zaidi lenye vikundi vingi sana vya nyota. Lakini, kama ilivyo, ni maeneo machache katika ulimwengu mzima “yanayofaa kwa ajili ya uhai tata kama wetu,” wanasema Guillermo Gonzalez na Jay W. Richards katika kitabu chao (The Privileged Planet).

Je, uhai ulijitokeza wenyewe tu duniani kutokana na “mlipuko mkubwa” uliotukia kwa aksidenti? Au je, kuna kusudi muhimu zaidi la uhai katika Dunia hii maridadi?

Watu wengi wamekata kauli kwamba dunia ambayo ni makao yetu ilibuniwa hasa ili kutegemeza uhai. * Karne nyingi zilizopita, mtungaji wa mashairi Mwebrania alizungumza kuhusu dunia na mbingu. Aliandika hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini?” (Zaburi 8:3, 4) Mtungaji huyo wa mashairi aliamini kwamba lazima kuna Muumba. Je, kauli hiyo inapatana na akili katika kizazi hiki cha kisayansi?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona kitabu cha Zaburi, hasa Zaburi ya 8.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 3]

“Kutoka mbali, Dunia inang’aa kama kito cha bluu katika anga lenye giza,” kinasema kitabu kimoja (The Illustrated Science Encyclopedia—Amazing Planet Earth).

[Hisani]

Globe: U.S. Fish & Wildlife Service, Washington, D.C./NASA