Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wake, Waheshimuni Sana Waume Zenu

Wake, Waheshimuni Sana Waume Zenu

Wake, Waheshimuni Sana Waume Zenu

‘Wake, na mjitiishe kwa waume zenu.’—WAEFESO 5:22.

1. Kwa nini mara nyingi inakuwa vigumu kumheshimu mume?

KATIKA nchi nyingi watu wanapofunga ndoa, bibi-arusi anafanya nadhiri, akiahidi kwamba atamheshimu sana mume wake. Lakini, inaweza kuwa rahisi au vigumu kutimiza nadhiri hiyo ikitegemea jinsi waume wengi wanavyowatendea wake zao. Hata hivyo, ndoa ilikuwa na mwanzo mzuri sana. Mungu alichukua ubavu kutoka kwa mwanamume wa kwanza, Adamu, na kufanya mwanamke. Adamu alisema hivi: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu.”—Mwanzo 2:19-23.

2. Ni mambo gani yametukia kuhusiana na wanawake na ndoa katika nyakati za karibuni?

2 Ingawa ndoa ilikuwa na mwanzo mzuri, harakati inayoitwa ukombozi wa wanawake, ilianza nchini Marekani mapema katika miaka ya 1960. Harakati hiyo ilijaribu kuwaweka wanawake huru ili wasitawaliwe na wanaume. Wakati huo, kwa kila waume 300 hivi walioacha familia zao, ni mke mmoja tu aliyefanya hivyo. Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1960, hali ilibadilika ikawa waume 100 hivi kwa kila mke 1. Sasa, inaonekana wanawake wanatumia matusi, wanakunywa, wanavuta sigara, na kujiendesha kwa njia isiyo ya adili kama wanaume. Lakini je, wanawake wamepata furaha zaidi? Hapana. Katika nchi fulani, karibu nusu ya watu wanaofunga ndoa mwishowe wanatalikiana. Je, jitihada za wanawake fulani za kuboresha ndoa zao zimefanya hali iwe nzuri au mbaya zaidi?—2 Timotheo 3:1-5.

3. Ni tatizo gani kuu linaloharibu ndoa?

3 Tatizo kuu ni nini? Kwa kadiri fulani, tatizo hilo limekuwapo tangu Hawa aliposhawishiwa na yule malaika mwasi, “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani.” (Ufunuo 12:9; 1 Timotheo 2:13, 14) Shetani amedharau yale ambayo Mungu anafundisha. Kwa mfano, Ibilisi amefanya ndoa ionekane kuwa ngumu sana na kwamba inawanyima watu uhuru. Habari za uwongo ambazo anaeneza kupitia vyombo vya habari vya ulimwengu huu ambao anautawala, zinakusudiwa kufanya maagizo ya Mungu yaonekana yasiyo ya haki na yaliyopitwa na wakati. (2 Wakorintho 4:3, 4) Hata hivyo, tukichunguza kwa unyoofu maagizo ya Mungu kuhusu wajibu wa mke katika ndoa, tutaona jinsi Neno la Mungu lilivyo yenye hekima na lenye faida.

Onyo kwa Wale Wanaofunga Ndoa

4, 5. (a) Kwa nini mwanamke anapaswa kuwa mwangalifu anapofikiria kufunga ndoa? (b) Mwanamke anapaswa kufanya nini kabla ya kukubali kufunga ndoa?

4 Biblia inatoa onyo. Inasema kwamba katika ulimwengu huu unaotawaliwa na Ibilisi, hata wale walio na ndoa zenye mafanikio watakuwa na “dhiki.” Kwa hiyo, ingawa ndoa ni mpango wa Mungu, Biblia inawaonya wale wanaoingia katika mpango huo. Mwandikaji mmoja wa Biblia aliyeongozwa na roho alisema hivi kuhusu mwanamke ambaye mume wake amekufa na hivyo yuko huru kuolewa tena: “Ni mwenye furaha zaidi akibaki kama alivyo.” Yesu pia alipendekeza useja kwa ajili ya wale ‘wanaoweza kuupa nafasi.’ Hata hivyo, mtu yeyote akiamua kufunga ndoa, anapaswa kufanya hivyo na yule aliye “katika Bwana,” yaani, mtu aliyejiweka wakfu na kubatizwa na ambaye anamwabudu Mungu.—1 Wakorintho 7:28, 36-40; Mathayo 19:10-12.

5 Onyo hili la Biblia linaonyesha kwa nini hasa mwanamke anapaswa kuwa mwangalifu kuhusu yule ambaye anataka kufunga ndoa naye: “Mwanamke aliyeolewa amefungwa na sheria kwa mume wake.” “Yuko huru kutoka katika sheria ya mume” wakati tu mume anapokufa au anapofanya uzinzi na wenzi hao wanatalikiana kwa sababu hiyo. (Waroma 7:2, 3) Hisia ya kuvutiwa kimapenzi na mtu unapomwona kwa mara ya kwanza ni ya kimahaba tu, si msingi imara wa kuwa na ndoa yenye furaha. Kwa hiyo, mwanamke mseja anahitaji kujiuliza, ‘Je, niko tayari kuingia katika mpango ambao utanifanya niwe chini ya sheria ya mwanamume huyu?’ Swali hilo linapaswa kufikiriwa kabla ya kufunga ndoa, wala si baada ya kufunga ndoa.

6. Wanawake wengi leo wanaweza kufanya uamuzi gani, na kwa nini hilo ni jambo la maana sana?

6 Katika sehemu nyingi leo, mwanamke anaweza kuamua kukubali au kutokubali uchumba. Hata hivyo, huenda kufanya uamuzi wenye hekima kukawa jambo gumu zaidi ambalo mwanamke amewahi kufanya, kwa kuwa tamaa yake ya urafiki na ya kupendwa katika ndoa inaweza kuwa yenye nguvu sana. Mwandishi mmoja alisema hivi: “Kadiri tunavyotaka sana kufanya jambo fulani, iwe ni kufunga ndoa au kupanda mlima fulani, ndivyo tunavyowazia kwamba hali ni nzuri na hivyo kukubali tu habari ambayo tunataka kusikia.” Uamuzi usio wa busara unaweza kumfanya mtu anayepanda mlima apoteze uhai wake; na kuchagua mwenzi wa ndoa bila hekima kunaweza kusababisha hasara kubwa sana.

7. Ni mashauri gani yenye hekima ambayo yametolewa kuhusu kumtafuta mwenzi wa ndoa?

7 Mwanamke anapaswa kufikiria kwa uzito mambo yanayohusika katika kuwa chini ya sheria ya mwanamume ambaye anataka kumuoa. Miaka kadhaa iliyopita, msichana mmoja Mhindi alikubali hivi kwa unyenyekevu: “Wazazi wetu wana umri mkubwa na hekima zaidi, nao hawawezi kudanganywa kwa urahisi kama sisi. . . . Ni rahisi kwangu kukosea.” Wazazi na watu wengine wanaweza kutoa msaada muhimu. Kwa miaka mingi mshauri mmoja mwenye hekima aliwatia moyo vijana wafahamiane na wazazi wa yule ambaye wanatarajia awe mwenzi wao wa ndoa na pia wachunguze kwa uangalifu jinsi anavyoshughulika na wazazi wake na washiriki wengine wa familia yao.

Jinsi Yesu Alivyojitiisha

8, 9. (a) Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu kujitiisha kwa Mungu? (b) Kujitiisha kunaleta faida gani?

8 Ingawa inaweza kuwa vigumu kujitiisha, wanawake wanaweza kuona kujitiisha kuwa jambo la heshima, kama Yesu alivyoliona. Hata ingawa aliteseka na kuuawa kwenye mti wa mateso kwa sababu ya kujitiisha kwa Mungu, Yesu alipata shangwe katika kujitiisha kwa Mungu. (Luka 22:41-44; Waebrania 5:7, 8; 12:3) Wanawake wanaweza kuiga mfano wa Yesu, kwa kuwa Biblia inasema hivi: “Kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Wakorintho 11:3) Hata hivyo, wanawake hawawi chini ya ukichwa wa wanaume wakati tu wanapoolewa.

9 Biblia inaeleza kwamba wanawake, iwe wameolewa au ni waseja, wanapaswa kujitiisha kwa ukichwa wa wanaume wenye sifa za kustahili kiroho ambao ni waangalizi katika kutaniko la Kikristo. (1 Timotheo 2:12, 13; Waebrania 13:17) Wanawake wanapofuata mwongozo wa Mungu kuhusu kujitiisha, wanakuwa vielelezo kwa malaika katika mpango wa kitengenezo wa Mungu. (1 Wakorintho 11:8-10) Kwa kuongezea, kupitia mfano wao mzuri na mashauri yao yenye faida, wanawake wenye umri mkubwa ambao wameolewa wanawafundisha wanawake vijana ‘wajitiishe kwa waume zao wenyewe.’—Tito 2:3-5.

10. Ni kwa njia gani Yesu aliweka mfano katika kujitiisha?

10 Yesu alielewa umuhimu wa kujitiisha inavyofaa. Pindi moja, alimwagiza mtume Petro alipe kodi kwa ajili yao wawili kwa mamlaka za kibinadamu, hata alimpa Petro pesa za kulipa. Baadaye, Petro aliandika hivi: “Kwa ajili ya Bwana jitiisheni wenyewe kwa kila kitu kilichofanywa na binadamu.” (1 Petro 2:13; Mathayo 17:24-27) Tunasoma hivi kuhusu mfano bora sana wa Yesu wa kujitiisha: “Alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu. Zaidi ya hayo, alipojikuta katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo.”—Wafilipi 2:5-8.

11. Kwa nini Petro aliwahimiza wake wajitiishe hata kwa waume wasioamini?

11 Akiwahimiza Wakristo wajitiishe hata kwa mamlaka za ulimwengu huu ambazo ni kali na zisizofuata haki, Petro alieleza hivi: “Kwa kweli, mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Baada ya kueleza jinsi Yesu alivyoteseka sana na jinsi alivyovumilia kwa ujitiisho, Petro aliwahimiza hivi wake walio na waume wasioamini: “Vivyo hivyo, ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”—1 Petro 3:1, 2.

12. Mwenendo wa Yesu wa kujitiisha ulikuwa na faida gani?

12 Kujitiisha unapodhihakiwa na kutendewa vibaya kunaweza kuonwa kuwa ishara ya udhaifu. Hata hivyo, Yesu hakuwa na maoni hayo. Petro aliandika hivi: “Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho.” (1 Petro 2:23) Watu fulani waliomwona Yesu akiteseka walipata kuwa waamini, angalau kwa kiasi fulani, kama yule mnyang’anyi aliyetundikwa kando yake na yule ofisa-jeshi aliyekuwa akitazama Yesu alipokuwa akiuawa. (Mathayo 27:38-44, 54; Marko 15:39; Luka 23:39-43) Vivyo hivyo, Petro alionyesha kwamba waume fulani wasioamini, hata wale wanaowatendea vibaya wake zao, watakuwa Wakristo baada ya kushuhudia mwenendo wa kujitiisha wa wake zao. Tumeona hilo likitukia leo.

Jinsi Wake Wanavyoweza Kupata Kibali

13, 14. Wake wanaojitiisha kwa waume wasioamini wamepata matokeo gani mazuri?

13 Wake ambao wamekuwa waamini wamewavuta waume zao kupitia mwenendo wao ambao ni kama wa Kristo. Katika kusanyiko la wilaya la hivi karibuni la Mashahidi wa Yehova, mume mmoja alisema hivi kuhusu mke wake Mkristo: “Ninafikiri nilimtendea kijeuri. Lakini, aliniheshimu sana. Hakunishushia heshima hata siku moja. Hakujaribu kunilazimisha nifuate imani yake. Alinitunza kwa njia ya upendo. Alipokwenda kwenye kusanyiko, alijitahidi kunitayarishia chakula mapema na kumaliza kazi za nyumbani. Nilianza kupendezwa na Biblia kwa sababu ya mtazamo wake. Na sasa, mimi ni Shahidi!” Ndiyo, kwa kweli alikuwa ‘amevutwa bila neno’ kupitia mwenendo wa mke wake.

14 Kama Petro alivyokazia, matokeo mazuri hayategemei sana yale ambayo mke anasema lakini yale ambayo anafanya. Hilo lilionyeshwa na mfano wa mke fulani ambaye alijifunza kweli za Biblia na aliazimia kuhudhuria mikutano ya Kikristo. “Agnes, ukitoka nje ya mlango huo, usirudi tena!” mume akapaaza sauti. Badala ya kutokea “mlango huo” alitokea mlango mwingine. Wakati wa mkutano uliofuata, mume alimtisha hivi: “Hutanikuta hapa utakaporudi.” Na kwa kweli hakumkuta, alienda kwa muda wa siku tatu. Aliporudi, mke alimuuliza hivi kwa fadhili: “Je, nikutayarishie chakula?” Agnes hakukengeuka kamwe katika ujitoaji wake kwa Yehova. Mwishowe, mume wake alikubali funzo la Biblia, akajiweka wakfu kwa Mungu, na baadaye akawa mwangalizi mwenye mapendeleo mengi.

15. Ni “mapambo” gani yanayopendekezwa kwa ajili ya wake Wakristo?

15 Mtume Petro alipendekeza jambo ambalo wake waliozungumziwa katika mafungu yaliyotangulia wameonyesha, yaani, “mapambo,” lakini si mapambo yanayopita kiasi ya “kusuka nywele” au “kuvaa mavazi ya nje.” Badala yake, Petro alisema: “[Kujipamba kwenu] kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.” Roho hiyo inaonyeshwa kupitia sauti na mwenendo mzuri badala ya kuwa mwenye kushutumu au mwenye kudai mengi. Kwa njia hiyo, mke Mkristo anaonyesha kwamba anamheshimu sana mume wake.—1 Petro 3:3, 4.

Mifano ya Kuiga

16. Sara ni mfano mzuri kwa wake Wakristo katika njia gani?

16 Petro aliandika hivi: “Ndivyo walivyokuwa wakijipamba wale wanawake watakatifu hapo zamani, waliokuwa wakimtumaini Mungu, wakijitiisha kwa waume zao wenyewe.” (1 Petro 3:5) Wanawake hao walitambua kwamba kumpendeza Yehova kwa kutii mashauri yake mwishowe kungeleta furaha katika familia na thawabu ya uzima wa milele. Petro anamtaja Sara, mke mrembo wa Abrahamu, naye anasema ‘alikuwa akimtii Abrahamu, akimwita “bwana.”’ Sara alimuunga mkono mume wake aliyemwogopa Mungu, ambaye aliagizwa na Mungu aende katika nchi ya mbali. Sara aliacha maisha ya starehe na hata akahatarisha uhai wake. (Mwanzo 12:1, 10-13) Petro alimsifu Sara kwa sababu ya mfano wake wa ujasiri, akisema: “Mmekuwa watoto wake, mradi tu mnaendelea kutenda mema na kutokuwa na woga kwa sababu ya kitisho chochote.”—1 Petro 3:6.

17. Kwa nini huenda Petro alikuwa akimfikiria Abigaili kuwa mfano kwa wake Wakristo?

17 Pia, Abigaili alikuwa mwanamke asiyeogopa ambaye alimtumaini Mungu, na huenda Petro alikuwa akimfikiria pia. Abigaili “alikuwa mwenye busara njema,” lakini mume wake Nabali “alikuwa mkali na mwenye matendo mabaya.” Nabali alipokataa kumsaidia Daudi na wanaume wake, walijitayarisha kumwangamiza Nabali na watu wote wa nyumbani mwake. Lakini Abigaili alichukua hatua ili kuwaokoa watu wa nyumbani mwake. Alipakia chakula juu ya punda na kwenda kukutana na Daudi aliyekuwa akija pamoja na wanaume wake wenye silaha. Alipomwona Daudi, Abigaili alishuka kutoka juu ya punda, akaanguka miguuni pa Daudi, na kumsihi asitende kwa haraka. Daudi aliguswa moyo sana. Alisema hivi: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee! Busara yako na ibarikiwe.”—1 Samweli 25:2-33.

18. Wake wanaweza kutafakari kuhusu mfano wa nani wanaposhawishiwa kimapenzi na mwanamume mwingine, na kwa nini?

18 Mfano mwingine mzuri kwa wake ni ule wa msichana Mshulami ambaye alibaki akiwa mshikamanifu kwa mchumba wake ambaye alikuwa mchungaji tu. Aliendelea kumpenda sana hata ingawa alishawishiwa kimapenzi na mtawala tajiri. Akichochewa kuonyesha upendo wake kwa yule kijana mchungaji, msichana huyo alisema hivi: “Nitie kama muhuri juu ya moyo wako, kama muhuri juu ya mkono wako; kwa maana upendo una nguvu kama kifo . . . Maji mengi hayawezi kuuzima upendo, wala mito haiwezi kuufagilia mbali.” (Wimbo wa Sulemani 8:6, 7) Wanawake wote wanaokubali kuolewa na waazimie vivyo hivyo kubaki washikamanifu kwa waume zao na kuwaheshimu sana.

Mashauri Mengine Kutoka kwa Mungu

19, 20. (a) Wake wanapaswa kujitiisha kwa waume zao kwa sababu gani? (b) Wake wamewekewa mfano gani mzuri?

19 Mwishowe, fikiria mistari mingine inayofuata andiko letu la msingi: ‘Wake na mjitiishe kwa waume zenu.’ (Waefeso 5:22) Kwa nini ni lazima wajitiishe? “Kwa sababu,” mstari unaofuata unasema “mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko.” Kwa hiyo, wake wanahimizwa hivi: “Kama kutaniko linavyojitiisha kwa Kristo, vivyo hivyo wanawake pia na wajitiishe kwa waume zao katika mambo yote.”—Waefeso 5:23, 24, 33.

20 Ili kutii amri hiyo, wake wanahitaji kujifunza na kisha kuiga mfano wa kutaniko la Kristo la wafuasi watiwa-mafuta. Tafadhali soma 2 Wakorintho 11:23-28 ili uone yale ambayo mtume Paulo, aliyekuwa mshiriki wa kutaniko hilo alivumilia ili kubaki mwaminifu kwa Kichwa chake, Yesu Kristo. Kama Paulo, wake na vilevile washiriki wengine wa kutaniko wanapaswa kuendelea kujitiisha kwa ushikamanifu kwa Yesu. Wake wanafanya hivyo kwa kuendelea kujitiisha kwa waume zao.

21. Ni nini kinachoweza kuwachochea wake waendelee kujitiisha kwa waume zao?

21 Ingawa huenda wake wengi hawapendi kujitiisha, mwanamke mwenye hekima atafikiria faida za kufanya hivyo. Kwa mfano, ikiwa mume si mwamini, mke akijitiisha kwa ukichwa katika mambo yote ambayo hayavunji sheria au kanuni za Mungu, anaweza kupata thawabu nzuri sana ya ‘kumwokoa mume wake.’ (1 Wakorintho 7:13, 16) Zaidi ya hayo, mke anaweza kuridhika akijua kwamba Yehova Mungu anapendezwa na mwenendo wake naye atamthawabisha sana kwa sababu ya kuiga mfano wa Mwana wake mpendwa.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini huenda ikawa vigumu kwa mke kumheshimu mume wake?

• Kwa nini kukubali uchumba ni jambo zito?

• Yesu aliwawekea wake mfano gani, na wanaweza kupata faida gani wakifuata mfano wake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kwa nini uamuzi wa kukubali au kukataa uchumba ni mzito sana?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wake wanaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya watu wanaotajwa katika Biblia kama vile Abigaili?