Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Watoto, Watiini Wazazi Wenu”

“Watoto, Watiini Wazazi Wenu”

“Watoto, Watiini Wazazi Wenu”

“Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hilo ni jambo la uadilifu.”—WAEFESO 6:1.

1. Kutii kunaweza kukulinda jinsi gani?

HUENDA tuko hai leo kwa sababu tulitii, lakini wengine wamekufa kwa sababu hawakutii. Kutii nini? Kutii maonyo, kama yale yanayotolewa na miili yetu ‘iliyoumbwa kwa njia ya ajabu.’ (Zaburi 139:14) Macho yetu yanaona mawingu meusi na masikio yetu yanasikia mingurumo ya radi. Halafu, nguvu za umeme zilizo hewani zinafanya nywele zetu zisimame. Kwa wale ambao wanajua hatari zinazoweza kuwapata, ishara hizo ni onyo kwamba wanapaswa kutafuta mahali salama pa kujikinga kutokana na dhoruba inayokuja yenye radi na mawe ya mvua ambayo ni hatari kwa uhai.

2. Kwa nini watoto wanahitaji maonyo, na kwa nini wanapaswa kuwatii wazazi wao?

2 Ninyi watoto mnahitaji maonyo kuhusu hatari zinazoweza kuwapata, na wazazi wenu wana wajibu wa kutoa maonyo hayo. Huenda unakumbuka umewahi kuambiwa: “Usiguse jiko lenye moto. Utaungua.” “Usikaribie bwawa la maji. Ni hatari.” “Kabla ya kuvuka barabara, tazama kushoto na kulia.” Kwa kuhuzunisha, watoto wameumia au hata kufa kwa sababu ya kutotii. Kuwatii wazazi wako “ni jambo la uadilifu,” jambo zuri na linalofaa. Ni jambo la hekima pia. (Methali 8:33) Andiko lingine la Biblia linasema kwamba jambo hilo “linapendeza vema” kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Kwa kweli, Mungu anawaamuru mtii wazazi wenu.—Wakolosai 3:20; 1 Wakorintho 8:6.

Thawabu za Kudumu za Kutii

3. “Uzima ulio wa kweli” ni nini kwa wengi wetu, na watoto wanaweza kufanya nini ili waupate?

3 Kuwatii wazazi wenu kunalinda “uzima [wenu] wa sasa,” lakini pia kutii kutawawezesha kufurahia uzima “utakaokuja,” ambao unaitwa “uzima ulio wa kweli.” (1 Timotheo 4:8; 6:19) Kwa wengi wetu, uzima ulio wa kweli ni uzima wa milele duniani katika ulimwengu mpya wa Mungu ambao anaahidi kuwapa wale wanaotii kwa uaminifu amri zake. Amri moja muhimu kati ya amri hizo inasema hivi: “‘Mheshimu baba yako na mama yako’; ambayo ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi: ‘Ili mambo yakuendee vema nawe ukae muda mrefu duniani.’” Kwa hiyo, ukiwatii wazazi wako, utakuwa na furaha. Wakati wako ujao utakuwa salama, na huenda ukapata uzima wa milele katika paradiso duniani!—Waefeso 6:2, 3.

4. Watoto wanaweza kumheshimu Mungu jinsi gani na hivyo kufaidika?

4 Unapowaheshimu wazazi wako kwa kuwatii, unamheshimu pia Mungu kwa sababu yeye ndiye anayekuamuru uwatii wazazi. Wakati huohuo, unafaidika. Biblia inasema: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.” (Isaya 48:17; 1 Yohana 5:3) Unapata faida gani kwa kutii? Unapotii unamfurahisha mama na baba yako, na bila shaka wataonyesha furaha yao katika njia ambazo zitafanya maisha yako yawe yenye furaha zaidi. (Methali 23:22-25) Lakini jambo muhimu zaidi ni kwamba unapotii unamfanya Baba yako wa mbinguni afurahi, naye atakuthawabisha kwa njia nzuri ajabu! Acheni tuone jinsi Yehova alivyombariki na kumlinda Yesu, ambaye alisema hivi kujihusu: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.”—Yohana 8:29.

Yesu—Mfanyakazi Stadi

5. Tuna sababu gani za kuamini kwamba Yesu alikuwa mfanyakazi stadi?

5 Yesu alikuwa mzaliwa wa kwanza wa mama yake, Maria. Yosefu, baba yake mlezi, alikuwa seremala. Yesu pia alikuwa seremala, na inaelekea Yosefu ndiye aliyemfundisha kazi hiyo. (Mathayo 13:55; Marko 6:3; Luka 1:26-31) Unafikiri Yesu alikuwa seremala wa aina gani? Alipokuwa mbinguni, kabla ya kuzaliwa kimuujiza na mama yake bikira na akiwa hekima inayofananishwa na mtu, alisema hivi: ‘Nilikuwa kando yake [Mungu] nikiwa stadi wa kazi, nami nikawa yule ambaye yeye alimpenda sana kwa njia ya pekee siku baada ya siku.’ Mungu alipendezwa na Yesu ambaye alikuwa mfanyakazi stadi huko mbinguni. Je, hufikiri kwamba alipokuwa mtoto hapa duniani alijitahidi kabisa kuwa mfanyakazi stadi, seremala stadi?—Methali 8:30; Wakolosai 1:15, 16.

6. (a) Unafikiri ni kwa nini huenda Yesu alifanya kazi za nyumbani akiwa mtoto? (b) Watoto wanaweza kumwiga Yesu katika njia gani?

6 Hapana shaka kwamba Yesu alipokuwa mtoto, nyakati nyingine alicheza michezo, kama vile Biblia inavyosema kwamba watoto walicheza nyakati hizo. (Zekaria 8:5; Mathayo 11:16, 17) Hata hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba akiwa mtoto wa kwanza katika familia kubwa iliyo maskini, alikuwa na kazi nyingine za kufanya nyumbani zaidi ya kuzoezwa useremala na Yosefu. Baadaye, Yesu akawa mhubiri na akajitoa sana katika huduma hivi kwamba alidhabihu maisha ya starehe. (Luka 9:58; Yohana 5:17) Je, unaona njia ambazo unaweza kumwiga Yesu? Je, wazazi wako wanakuomba usafishe chumba chako au ufanye kazi nyingine za nyumbani? Je, wanakutia moyo ushiriki katika ibada ya Mungu kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuwajulisha wengine kuhusu imani yako? Unafikiri Yesu akiwa mtoto angeitikia namna gani maombi hayo?

Mwanafunzi na Mwalimu wa Biblia Mwenye Bidii

7. (a) Inaelekea Yesu alisafiri pamoja na nani kwenda kwenye Pasaka? (b) Yesu alikuwa wapi wengine walipoanza safari ya kurudi nyumbani, na alikuwa akifanya nini huko?

7 Washiriki wote wa kiume katika familia ya Mwisraeli waliamriwa waende kumwabudu Yehova hekaluni wakati wa zile sherehe tatu za Kiyahudi. (Kumbukumbu la Torati 16:16) Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, huenda familia yao yote ilisafiri kwenda Yerusalemu kwa ajili ya Pasaka. Inaelekea kwamba hata ndugu na dada zake wa kambo walienda pia. Hata hivyo, wale waliosafiri pamoja na familia hiyo ya Yesu huenda walitia ndani Salome, ambaye labda alikuwa dada ya Maria, pamoja na mume wake Zebedayo na wana wao Yakobo na Yohana, ambao baadaye walikuwa mitume. * (Mathayo 4:20, 21; 13:54-56; 27:56; Marko 15:40; Yohana 19:25) Walipokuwa wakirudi, huenda Yosefu na Maria walidhani kwamba Yesu alikuwa na watu wao wa ukoo, kwa hiyo mwanzoni hawakugundua kwamba hakuwapo. Maria na Yosefu walipompata Yesu siku tatu baadaye, alikuwa hekaluni, “ameketi katikati ya walimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali.”—Luka 2:44-46.

8. Yesu alifanya nini hekaluni, na kwa nini watu walishangaa?

8 Ni katika njia gani Yesu alikuwa ‘akiwauliza’ walimu maswali? Huenda maswali yake hayakuwa tu ya udadisi au ya kutaka kupata habari. Neno la Kigiriki ambalo limetumiwa hapa linaweza kumaanisha maswali kama yale yanayotumiwa katika uchunguzi wa kihukumu na hivyo yanaweza kutia ndani mahojiano. Ndiyo, hata akiwa mtoto, Yesu alikuwa amekomaa na kuwa mwanafunzi wa Biblia ambaye aliwashangaza walimu wa kidini wenye elimu ya juu! Biblia inasema: “Wale wote waliokuwa wakimsikiliza walikuwa wakishangazwa daima na uelewaji wake na majibu yake.”—Luka 2:47.

9. Unaweza kuiga mfano wa Yesu jinsi gani katika kujifunza Biblia?

9 Unafikiri ni kwa nini Yesu akiwa na umri mdogo aliwashangaza hata walimu stadi kwa ujuzi wake wa Biblia? Bila shaka, alibarikiwa kwa kuwa na wazazi waliomwogopa Mungu ambao walimfundisha tangu utotoni maagizo ya Mungu. (Kutoka 12:24-27; Kumbukumbu la Torati 6:6-9; Mathayo 1:18-20) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yosefu alienda na Yesu akiwa mtoto kwenye sinagogi ili asikilize Maandiko yakisomwa na kuzungumziwa. Je, wewe pia umebarikiwa kuwa na wazazi ambao wanajifunza Biblia pamoja nawe na kwenda nawe kwenye mikutano ya Kikristo? Je, unathamini jitihada zao, kama Yesu alivyothamini jitihada za wazazi wake? Je, unawaambia wengine mambo unayojifunza, kama Yesu alivyofanya?

Yesu Alijitiisha

10. (a) Kwa nini wazazi wa Yesu walipaswa kujua mahali ambapo wangempata? (b) Yesu aliwawekea watoto mfano gani mzuri?

10 Unafikiri Maria na Yosefu walihisi namna gani wakati walipompata Yesu hekaluni baada ya siku tatu? Bila shaka, walifurahi sana! Hata hivyo, Yesu alishangaa kwamba wazazi wake hawakujua alikokuwa. Wote wawili walijua kwamba Yesu alizaliwa kimuujiza. Zaidi ya hilo, ingawa hawakuwa na habari zote, haikosi walijua mambo fulani kuhusu daraka lake la wakati ujao akiwa Mwokozi na Mtawala wa Ufalme wa Mungu. (Mathayo 1:21; Luka 1:32-35; 2:11) Kwa hiyo, Yesu aliwauliza: “Kwa nini mlilazimika kunitafuta? Je, hamkujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?” Hata hivyo, kwa utii, Yesu aliondoka pamoja na wazazi wake na kurudi nyumbani kwao huko Nazareti. Biblia inasema hivi: “Akaendelea kujitiisha kwao.” Kwa kuongezea, “mama yake akaweka kwa uangalifu maneno yote hayo moyoni mwake.”—Luka 2:48-51.

11. Unaweza kujifunza somo gani kuhusu utii kutokana na Yesu?

11 Je, unaona ni rahisi kumwiga Yesu, na kuwatii wazazi wako sikuzote? Au unaona kwamba mara nyingi hawaelewi ulimwengu wa leo na kwamba unajua mengi kuliko wao? Ni kweli kwamba huenda unajua mambo mengi kuhusu vitu fulani kama vile simu za mkononi, kompyuta, au vifaa vingine vya kisasa. Lakini mfikirie Yesu, ambaye aliwashangaza walimu stadi kwa “uelewaji wake na majibu yake.” Huenda ukakubali kwamba unajua machache ukilinganishwa na Yesu. Hata hivyo, Yesu alijitiisha kwa wazazi wake. Hilo halimaanishi kwamba sikuzote alikubaliana na maamuzi yao. Lakini, ‘aliendelea kujitiisha kwao,’ katika miaka yake yote ya ujana. Unafikiri unaweza kujifunza somo gani kutokana na mfano wake?—Kumbukumbu la Torati 5:16, 29.

Si Rahisi Kutii

12. Utii unaweza kuokoa uhai wako jinsi gani?

12 Sikuzote si rahisi kutii, kama ilivyotokea miaka michache iliyopita wakati wasichana wawili wadogo walipotaka kukimbia na kuvuka barabara kuu iliyo pana sana badala ya kupita kwenye daraja. Walimsihi hivi mvulana ambaye aliandamana nao aliyekuwa akienda kupanda daraja, “Njoo John, hutaki kuvuka pamoja nasi?” Alipositasita, mmoja wa wasichana hao alimdhihaki hivi, “Wewe ni mwoga tu kama kuku!” Ingawa hakuwa mwoga, John alisema hivi: “Ni lazima nimtii mama yangu.” Punde si punde, alisikia mlio wa magurudumu ya gari kisha akatazama chini na kuona wasichana hao wakigongwa. Msichana mmoja alikufa, na mwenzake aliumia vibaya sana hivi kwamba mguu wake ulihitaji kukatwa. Mama ya wasichana hao, ambaye alikuwa amewaonya kwamba wawe wakivuka kwa daraja, baadaye alimwambia hivi mama ya John, “Laiti wangekuwa watiifu kama mwana wako.”—Waefeso 6:1.

13. (a) Kwa nini unapaswa kuwatii wazazi wako? (b) Ni wakati gani mtoto hapaswi kufanya yale ambayo mzazi anamwambia afanye?

13 Kwa nini Mungu anasema: “Watoto, watiini wazazi wenu”? Unapowatii wazazi wako, unamtii Mungu. Zaidi ya hilo, wazazi wako wana uzoefu zaidi kuliko wewe. Kwa mfano, miaka mitano tu kabla ya msiba uliosimuliwa hapo juu kutokea, mama ya John alikuwa na rafiki ambaye mtoto wake aligongwa na kufa alipojaribu kuvuka barabara hiyohiyo! Kwa kweli, si rahisi nyakati zote kuwatii wazazi wako, lakini Mungu anasema kwamba unapaswa kuwatii. Kwa upande mwingine, wazazi wako au watu wengine wakikwambia useme uwongo, uibe, au ufanye jambo lisilompendeza Mungu, unapaswa ‘kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’ Kwa sababu hiyo, baada ya kusema “watiini wazazi wenu,” Biblia inaongezea, “katika muungano na Bwana.” Hilo linatia ndani kuwatii wazazi wako katika mambo yote yanayopatana na sheria ya Mungu.—Matendo 5:29.

14. Kwa nini ni rahisi kwa mtu mkamilifu kutii, na kwa nini angehitaji kujifunza utii?

14 Je, unafikiri kwamba kama ungekuwa mkamilifu, yaani, mtu “asiye na unajisi, aliyetengwa kutoka kwa watenda-dhambi,” kama Yesu, sikuzote ingekuwa rahisi kwako kuwatii wazazi wako? (Waebrania 7:26) Kama ungekuwa mkamilifu, hungekuwa na mwelekeo ulio nao sasa wa kufanya yaliyo mabaya. (Mwanzo 8:21; Zaburi 51:5) Lakini, hata Yesu, alijifunza mambo fulani kuhusu utii. Biblia inasema: “Ijapokuwa [Yesu] alikuwa Mwana, alijifunza kutii kutokana na mambo aliyoteseka.” (Waebrania 5:8) Mateso yalimsaidia Yesu jinsi gani kujifunza utii, jambo ambalo hakuhitaji kujifunza huko mbinguni?

15, 16. Yesu alijifunza utii kwa njia gani?

15 Chini ya mwongozo wa Yehova, Yosefu na Maria walimlinda Yesu asipate madhara alipokuwa mtoto. (Mathayo 2:7-23) Hata hivyo, mwishowe Mungu aliondoa ulinzi unaozidi wa kibinadamu ambao Yesu alikuwa nao. Yesu aliteseka sana kiakili na kimwili hivi kwamba Biblia inasema kuwa “alitoa dua na pia maombi . . . pamoja na vilio vyenye nguvu na machozi.” (Waebrania 5:7) Hilo lilitukia wakati gani?

16 Lilitukia hasa katika saa za mwisho za maisha ya Yesu hapa duniani wakati Shetani alipojitahidi kufa na kupona kuvunja utimilifu wa Yesu. Ni wazi kwamba Yesu alipofikiria jinsi kuuawa kwake kama mtu aliyedhaniwa kuwa mtenda-dhambi kungeharibu sifa ya Baba yake, aliteseka sana kimawazo hivi kwamba ‘alipoendelea kusali katika bustani ya Gethsemane jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka chini.’ Saa chache baadaye, kifo chake kwenye mti wa mateso kilikuwa chenye maumivu makali sana hivi kwamba Yesu alitoa “vilio vyenye nguvu na machozi.” (Luka 22:42-44; Marko 15:34) Kwa njia hiyo, “alijifunza kutii kutokana na mambo aliyoteseka” na hivyo akaufanya moyo wa Baba yake ushangilie. Sasa akiwa mbinguni, Yesu anahisi maumivu yetu tunapoendelea kupambana ili kuwa watiifu.—Methali 27:11; Waebrania 2:18; 4:15.

Kujifunza Somo la Utii

17. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kutiwa nidhamu?

17 Wakati mama na baba yako wanapokutia nidhamu, hilo linaonyesha kwamba wanataka uwe na maisha mazuri na wanakupenda. Biblia inauliza hivi: “Ni mwana gani ambaye baba hamtii nidhamu?” Je, halingekuwa jambo la kusikitisha ikiwa wazazi wako hawangekupenda vya kutosha kwa kutumia wakati na kujitahidi kukurekebisha? Vivyo hivyo, Yehova anakurekebisha kwa sababu anakupenda. “Ni kweli, hakuna nidhamu inayoonekana kwa sasa kuwa yenye shangwe, bali ni yenye kuhuzunisha; lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo huzaa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.”—Waebrania 12:7-11.

18. (a) Nidhamu inayotolewa kwa upendo inaonyesha nini? (b) Umeona nidhamu ikiwafinyanga watu kwa njia gani nzuri?

18 Mfalme mmoja wa Israeli la kale ambaye Yesu alimtaja kwa sababu ya hekima yake nyingi, alisema kuhusu uhitaji wa kurekebishwa kwa upendo na wazazi. Sulemani aliandika hivi: “Anayezuia fimbo yake anamchukia mwana wake, lakini anayempenda ni yule anayemwangalia kwa nidhamu.” Sulemani hata alisema kwamba nafsi ya mtu anayerekebishwa kwa upendo inaweza kukombolewa na kifo. (Methali 13:24; 23:13, 14; Mathayo 12:42) Mwanamke mmoja Mkristo anakumbuka kwamba alipokuwa mtoto, baba yake alimwambia kwamba angemwadhibu wakirudi nyumbani kwa sababu ya kucheza katika mikutano ya Kikristo. Sasa anamkumbuka na kumpenda baba yake kwa sababu alimtia nidhamu kwa upendo na kumfinyanga kwa njia nzuri.

19. Kwa nini hasa unapaswa kuwatii wazazi wako?

19 Unapaswa kushukuru ikiwa una wazazi ambao wanakupenda sana hivi kwamba wanatumia wakati na kujitahidi kukutia nidhamu kwa upendo. Watii kama Bwana wetu Yesu Kristo alivyowatii wazazi wake, Yosefu na Maria. Lakini watii hasa kwa sababu Baba yako wa mbinguni, Yehova Mungu, anakuambia ufanye hivyo. Ukifanya hivyo utajifaidi mwenyewe, na ‘mambo yatakuendea vema nawe utakaa muda mrefu duniani.’—Waefeso 6:2, 3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona kitabu Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 841 au Étude Perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 869, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungetoa Jibu Gani?

• Watoto wanaweza kupata faida gani wakiwatii wazazi wao?

• Akiwa mtoto, Yesu aliweka mfano gani katika kuwatii wazazi wake?

• Yesu alijifunza utii jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yesu aliyekuwa mwenye umri wa miaka 12 alijua sana Maandiko

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yesu alijifunza jinsi gani utii kutokana na mateso?