Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Furahia Maisha Katika Kumwogopa Yehova

Furahia Maisha Katika Kumwogopa Yehova

Furahia Maisha Katika Kumwogopa Yehova

“Mwogopeni Yehova, enyi watakatifu wake, kwa maana wale wanaomwogopa hawakosi chochote.”—ZABURI 34:9.

1, 2. (a) Dini zinazodai kuwa za Kikristo zina maoni gani tofauti kuhusu kumwogopa Mungu? (b) Tutazungumzia maswali gani?

WAHUBIRI wa dini zinazodai kuwa za Kikristo ambao wanafundisha kuhusu kumwogopa Mungu, mara nyingi wanafanya hivyo kwa msingi wa fundisho lisilo la kimaandiko la kwamba Mungu anawaadhibu watenda-dhambi katika moto wa milele. Fundisho kama hilo linapingana na yale ambayo Biblia inafundisha kumhusu Yehova akiwa Mungu wa upendo na haki. (Mwanzo 3:19; Kumbukumbu la Torati 32:4; Waroma 6:23; 1 Yohana 4:8) Wahudumu wengine wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wanafundisha jambo tofauti. Hawataji kamwe kumwogopa Mungu. Badala yake, wanafundisha kwamba Mungu anawaendekeza watu na kukubali karibu kila mtu haidhuru anaishi maisha ya aina gani. Biblia haifundishi hilo pia.—Wagalatia 5:19-21.

2 Kwa kweli, Biblia inatutia moyo tumwogope Mungu. (Ufunuo 14:7) Fundisho hilo la Biblia linatokeza maswali fulani. Kwa nini Mungu mwenye upendo anataka tumwogope? Mungu anataka tumwogope kwa njia gani? Kumwogopa Mungu kunaweza kutufaidi jinsi gani? Tutazungumzia maswali hayo tunapoendelea na mazungumzo yetu kuhusu Zaburi ya 34.

Kwa Nini Tumwogope Mungu?

3. (a) Una maoni gani kuhusu amri ya kumwogopa Mungu? (b) Kwa nini watu wanaomwogopa Mungu ni wenye furaha?

3 Akiwa Muumba na Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, Yehova anastahili kuogopwa. (1 Petro 2:17) Hata hivyo, woga huo si hofu inayopita kiasi ya mungu mkatili. Ni kumcha Yehova na kumheshimu sana kwa sababu ya cheo chake. Pia kunamaanisha kuogopa kutompendeza. Kumwogopa Mungu ni sifa bora inayofanya maisha ya mtu yawe mazuri, haimfanyi mtu ashuke moyo au atetemeke. Yehova, “Mungu mwenye furaha,” anataka viumbe wake wa kibinadamu wafurahie maisha. (1 Timotheo 1:11) Hata hivyo, ili tufurahie maisha ni lazima tuishi kulingana na matakwa ya Mungu. Kwa watu wengi, hilo linamaanisha kubadili mtindo wao wa maisha. Wote wanaofanya mabadiliko yanayohitajika wanaona ukweli wa maneno haya ya mtunga-zaburi Daudi: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mwanamume ambaye humkimbilia. Mwogopeni Yehova, enyi watakatifu wake, kwa maana wale wanaomwogopa hawakosi chochote.” (Zaburi 34:8, 9) Wote wanaomwogopa Yehova hawakosi chochote chenye thamani ya kudumu kwa sababu wana uhusiano mzuri na Mungu.

4. Daudi na Yesu walitoa uhakikisho gani?

4 Ona kwamba kama ilivyokuwa katika siku zake, Daudi aliwaheshimu wanaume wake kwa kuwaita “watakatifu.” Walikuwa sehemu ya taifa takatifu la Mungu. Pia, walikuwa wakihatarisha maisha yao ili kumfuata Daudi. Ingawa walikuwa wakimkimbia Mfalme Sauli, Daudi alikuwa na uhakika kwamba Yehova angeendelea kuwatimizia mahitaji yao ya lazima. Daudi aliandika hivi: “Wana-simba wenye manyoya shingoni wamekuwa na vichache na kukaa njaa; lakini kwa wale wanaomtafuta Yehova, hawatakosa chochote chema.” (Zaburi 34:10) Yesu aliwapa wafuasi wake uhakikisho kama huo.—Mathayo 6:33.

5. (a) Wafuasi wengi wa Yesu walikuwa watu wa hali gani? (b) Yesu alitoa shauri gani kuhusu kuogopa?

5 Wengi kati ya watu waliomsikiliza Yesu walikuwa maskini, Wayahudi wa hali ya chini. Hivyo, Yesu “akawasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Je, watu hao wa hali ya chini wangekuwa na ujasiri wa kumfuata Yesu? Ili wafanye hivyo, walihitaji kusitawisha woga kumwelekea Yehova, badala ya kuwaogopa wanadamu. Yesu alisema: “Msiwaogope wale wanaouua mwili na baada ya hilo hawawezi kufanya jambo lolote zaidi. Lakini nitawaonyesha ninyi yule mnayepaswa kumwogopa: Mwogopeni yule ambaye baada ya kuua ana mamlaka ya kutupa ndani ya Gehena. Ndiyo, ninawaambia ninyi, Mwogopeni Huyo. Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado hakuna hata mmoja wao husahaulika mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.”—Luka 12:4-7.

6. (a) Wakristo wameimarishwa na maneno gani ya Yesu? (b) Kwa nini Yesu ni mfano bora zaidi wa kumwogopa Mungu?

6 Wale wanaomwogopa Yehova wanaposukumwa na maadui wao waache kumtumikia Mungu, wanaweza kukumbuka shauri hili la Yesu: “Kila mtu anayekiri kuwa pamoja nami mbele ya wanadamu, Mwana wa binadamu atakiri pia kuwa pamoja naye mbele ya malaika za Mungu. Lakini yule anayenikana mbele ya wanadamu atakanwa mbele ya malaika za Mungu.” (Luka 12:8, 9) Maneno hayo yamewaimarisha Wakristo, hasa katika nchi ambako ibada ya kweli imepigwa marufuku. Watu kama hao wanaendelea kumsifu Yehova kwa busara kwenye mikutano ya Kikristo na katika huduma yao ya hadharani. (Matendo 5:29) Yesu anaweka mfano bora wa “kumwogopa Mungu.” (Waebrania 5:7) Neno la kinabii lilitabiri hivi kumhusu: “Roho ya Yehova itatua juu yake, roho . . . ya kumwogopa Yehova; naye atakuwa na shangwe katika kumwogopa Yehova.” (Isaya 11:2, 3) Hivyo, Yesu ndiye anayestahili zaidi kutufundisha faida za kumwogopa Mungu.

7. (a) Wakristo wanakubali jinsi gani mwaliko kama ule uliotolewa na Daudi? (b) Wazazi wanaweza kufuata mfano mzuri wa Daudi jinsi gani?

7 Kwa kweli, wote wanaofuata mfano wa Yesu na kutii mafundisho yake, wanakubali mwaliko kama ule uliotolewa na Daudi: “Njooni, enyi wana, nisikilizeni; nitawafundisha kumwogopa Yehova.” (Zaburi 34:11) Kwa kawaida, Daudi aliwaita wanaume wake “wana” kwa sababu walimheshimu akiwa kiongozi wao. Kwa upande wake, Daudi aliwasaidia kiroho wafuasi wake ili wawe na umoja na kupata kibali cha Mungu. Huo ni mfano mzuri kama nini kwa wazazi Wakristo! Yehova amewapa mamlaka juu ya wana na binti zao ili ‘waendelee kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.’ (Waefeso 6:4) Kwa kuzungumzia mambo ya kiroho kila siku pamoja na watoto wao na kwa kujifunza Biblia pamoja nao kwa ukawaida, wazazi wanawasaidia watoto wao kufurahia maisha katika kumwogopa Yehova.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Jinsi Tunavyoonyesha Kwamba Tunamwogopa Mungu

8, 9. (a) Ni nini kinachofanya maisha ya kumwogopa Mungu yapendeze sana? (b) Kuulinda ulimi wetu kunahusisha nini?

8 Kama ilivyotajwa mapema, kumwogopa Yehova hakumaanishi kujinyima shangwe. Daudi aliuliza hivi: “Ni nani mtu yule anayependezwa na uhai, ambaye anapenda siku za kutosha ili kuona mema?” (Zaburi 34:12) Kwa wazi, kumwogopa Yehova ni jambo muhimu ili kuwa na maisha marefu na kuona mema. Hata hivyo, ni rahisi kudai hivi: “Ninamwogopa Mungu.” Lakini ni jambo tofauti kabisa kuthibitisha hilo kwa mwenendo wetu. Hivyo, Daudi anaeleza jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunamwogopa Mungu.

9 “Linda ulimi wako na yaliyo mabaya, na midomo yako isiseme udanganyifu.” (Zaburi 34:13) Mtume Petro aliongozwa na roho ya Mungu kunukuu sehemu hii ya Zaburi ya 34 baada ya kuwashauri Wakristo watendeane kwa upendo wa kindugu. (1 Petro 3:8-12) Kuulinda ulimi wetu na yaliyo mabaya kunamaanisha kwamba tutaepuka kueneza porojo yenye kudhuru. Badala yake, sikuzote tutajitahidi kuwa wenye kujenga tunapozungumza na wengine. Zaidi ya hayo, tutajitahidi kuwa wajasiri na kusema kweli.—Waefeso 4:25, 29, 31; Yakobo 5:16.

10. (a) Eleza maana ya kugeuka kutoka katika yaliyo mabaya. (b) Kufanya yaliyo mema kunahusisha nini?

10 “Geuka kutoka katika yaliyo mabaya, na kufanya yaliyo mema; utafute amani, na kuifuatia.” (Zaburi 34:14) Tunaepuka mambo ambayo Mungu anashutumu kama vile ukosefu wa adili katika ngono, ponografia (picha au habari za ngono), wizi, kuwasiliana na pepo, jeuri, ulevi, na matumizi ya dawa za kulevya. Tunakataa pia burudani ambazo zinakazia mambo kama hayo yenye kuchukiza. (Waefeso 5:10-12) Badala yake, tunatumia wakati wetu kufanya yaliyo mema. Jambo zuri zaidi ambalo tunaweza kufanya ni kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi ili kuwasaidia wengine wapate wokovu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kufanya yaliyo mema kunatia ndani pia kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kutoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, kutunza Jumba letu la Ufalme, na kuwasaidia Wakristo wenye uhitaji.

11. (a) Daudi alionyesha jinsi gani kwa matendo mambo aliyohubiri kuhusu amani? (b) Unaweza kufanya nini ili ‘kufuatia amani’ kutanikoni?

11 Daudi aliweka mfano mzuri katika kufuatia amani. Mara mbili alipata nafasi ya kumuua Sauli. Katika pindi zote mbili, alijizuia asitende kwa ujeuri na baadaye alizungumza na mfalme huyo kwa heshima, huku akitumaini kwamba angerudisha amani. (1 Samweli 24:8-11; 26:17-20) Tunaweza kufanya nini leo wakati hali fulani inapotisha kuvuruga amani ya kutaniko? Tunapaswa ‘kutafuta amani, na kuifuatia.’ Hivyo, tunapohisi kwamba kuna matatizo katika uhusiano wetu pamoja na mwamini mwenzetu, tunatii shauri hili la Yesu: “Kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako.” Halafu tuendelee na shughuli nyingine za ibada ya kweli.—Mathayo 5:23, 24; Waefeso 4:26.

Kumwogopa Mungu Kunaleta Thawabu Kubwa

12, 13. (a) Watu wanaomwogopa Mungu wanapata faida gani sasa? (b) Waabudu waaminifu watapata thawabu gani kubwa hivi karibuni?

12 “Macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.” (Zaburi 34:15) Masimulizi ya shughuli za Mungu pamoja na Daudi yanathibitisha kwamba maneno hayo ni ya kweli. Leo, tunapata shangwe nyingi na amani ya moyoni kwa sababu tunajua kwamba Yehova anatulinda. Tuna hakika kwamba ataendelea kutimiza mahitaji yetu hata tukiwa chini ya hali zenye kufadhaisha sana. Tunajua kwamba hivi karibuni waabudu wote wa kweli watakabili shambulizi lililotabiriwa la Gogu wa Magogu nao wataiona ‘siku ya Yehova yenye kuogopesha.’ (Yoeli 2:11, 31; Ezekieli 38:14-18, 21-23) Haidhuru hali tutakayokabili, maneno haya ya Daudi yatatimia: “Wao walilia kwa sauti, naye Yehova mwenyewe akasikia, naye akawakomboa kutoka katika taabu zao zote.”Zaburi 34:17.

13 Wakati huo, tutasisimka kama nini kuona Yehova akilitukuza jina lake kuu! Kuliko wakati mwingine wowote, mioyo yetu itajawa na heshima nyingi zaidi, na wapinzani wote watapata uharibifu wenye kuaibisha. “Uso wa Yehova uko dhidi ya wale wanaotenda yaliyo mabaya, ili kumbukumbu lao liondolewe mbali duniani.” (Zaburi 34:16) Itakuwa thawabu kubwa kama nini kupata ukombozi huo mkubwa na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu!

Ahadi Ambazo Zinatusaidia Kuvumilia

14. Ni nini kitakachotusaidia kuvumilia tujapokabili misiba?

14 Kwa sasa tunahitaji uvumilivu ili tuendelee kumtii Yehova katika ulimwengu huu uliopotoka na wenye chuki. Kumwogopa Mungu kutatusaidia sana kuwa watiifu. Kwa sababu tunaishi katika nyakati za hatari, watumishi fulani wa Yehova wanakabili hali ngumu sana ambazo zinawavunja moyo na kuponda roho zao. Hata hivyo, wanaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba wakimtegemea Yehova, atawasaidia kuvumilia. Maneno haya ya Daudi yanatoa faraja ya kweli: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” (Zaburi 34:18) Inatia moyo kwamba Daudi aliendelea kusema hivi: “Mwadilifu ana misiba mingi, lakini Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo.” (Zaburi 34:19) Hata tukikabili misiba mingi kadiri gani, Yehova ana nguvu za kutosha kutukomboa.

15, 16. (a) Daudi alipata habari kuhusu msiba gani baada ya kutunga Zaburi ya 34? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuvumilia majaribu?

15 Muda mfupi baada ya kutunga Zaburi ya 34, Daudi alisikia kuhusu msiba uliowapata wakaaji wa Nobu, Sauli alipowaua wakaaji hao na wengi kati ya makuhani. Ni wazi kwamba Daudi alifadhaika sana alipokumbuka kuwa Sauli alikasirika kwa sababu alikuwa ametembelea jiji la Nobu! (1 Samweli 22:13, 18-21) Hapana shaka kwamba Daudi alimwomba Yehova msaada, na bila shaka alifarijika kujua kwamba kutakuwa na ufufuo wa “waadilifu” wakati ujao.—Matendo 24:15.

16 Leo, tumaini la ufufuo linatuimarisha pia. Tunajua kwamba jambo lolote ambalo maadui wetu wanaweza kufanya haliwezi kutuletea madhara ya kudumu. (Mathayo 10:28) Daudi alionyesha usadikisho kama huo kwa maneno haya: “Yeye anailinda mifupa yote ya mtu huyo [mwadilifu]; hakuna hata mmoja uliovunjwa.” (Zaburi 34:20) Andiko hilo lilitimia kihalisi kuhusiana na Yesu. Ingawa Yesu aliuawa kikatili, hakuna mfupa wake hata mmoja ‘uliovunjwa.’ (Yohana 19:36) Kanuni ya Zaburi 34:20 inatuhakikishia kwamba hata wakabili majaribu gani, Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao, “kondoo wengine,” hawatapata kamwe madhara ya kudumu. Kwa njia ya mfano, mifupa yao haitavunjwa kamwe.—Yohana 10:16.

17. Ni msiba gani unaowangoja watu wasiotubu ambao wanawachukia watu wa Yehova?

17 Hali ya waovu ni tofauti. Hivi karibuni watavuna mabaya ambayo wamepanda. “Msiba utamuua mwovu; na wale wanaomchukia mwadilifu watahesabiwa kuwa na hatia.” (Zaburi 34:21) Wote wanaoendelea kuwapinga watu wa Mungu wanakabili msiba mbaya sana. Wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo, “watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele.”—2 Wathesalonike 1:9.

18. Ni katika maana gani “umati mkubwa” umekombolewa leo, na wataona nini wakati ujao?

18 Zaburi ya Daudi inamalizia kwa uhakikisho huu: “Yehova anaikomboa nafsi ya watumishi wake; wala hakuna yeyote kati ya wale wanaomkimbilia atakayehesabiwa kuwa na hatia.” (Zaburi 34:22) Karibu mwisho wa utawala wake wa miaka 40, Mfalme Daudi alisema: ‘Mungu aliikomboa nafsi yangu kutoka katika taabu zote.’ (1 Wafalme 1:29) Kama Daudi, hivi karibuni wale wanaomwogopa Yehova watashangilia watakapokumbuka jinsi walivyokombolewa kutokana na hatia yoyote waliyokuwa nayo kwa sababu ya dhambi na kuokolewa kutoka katika majaribu yao yote. Tayari, Wakristo wengi watiwa-mafuta wamepokea thawabu yao ya kimbingu. Sasa, “umati mkubwa” kutoka katika mataifa yote unajiunga na mabaki ya ndugu za Yesu katika kumtumikia Mungu na hivyo wanakuwa na msimamo safi mbele za Yehova. Hiyo ni kwa sababu wanaonyesha imani katika nguvu za kukomboa za damu iliyomwagwa ya Yesu. Katika Utawala wa Miaka Elfu Moja unaokuja wa Kristo, faida kamili za dhabihu ya fidia zitatumiwa kwa ajili yao na kuwasaidia wawe wanadamu wakamilifu.—Ufunuo 7:9, 14, 17; 21:3-5.

19. Washiriki wa “umati mkubwa” wameazimia kufanya nini?

19 Kwa nini “umati mkubwa” wa waabudu wa Mungu utapata baraka hizo zote? Kwa sababu wameazimia kuendelea kumwogopa Yehova, kumtumikia kwa heshima na woga, na kumtii sana. Kwa kweli, kumwogopa Yehova kunafanya maisha yafurahishe sasa na kunatusaidia ‘tushike imara ule uzima ulio wa kweli,’ yaani, uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu.—1 Timotheo 6:12, 18, 19; Ufunuo 15:3, 4.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunapaswa kumwogopa Mungu, na kumwogopa Mungu kunamaanisha nini?

• Kumwogopa Mungu kunapaswa kutufanya tujiendeshe jinsi gani?

• Kumwogopa Mungu kunaleta thawabu gani?

• Ni ahadi gani zinazotusaidia kuvumilia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wale wanaomwogopa Yehova wanatenda kwa busara chini ya marufuku

[Picha katika ukurasa wa 28]

Jambo zuri zaidi tunaloweza kuwafanyia majirani wetu ni kuwahubiria habari njema ya Ufalme