Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Haidhuru Unachagua Dini Gani?

Je, Haidhuru Unachagua Dini Gani?

Je, Haidhuru Unachagua Dini Gani?

TUNAPOENDA dukani, wengi wetu tungependa kupata vitu vingi vya kuchagua. Kunapokuwa matunda na mboga mbalimbali sokoni, tunaweza kuchagua matunda au mboga tunazopenda zaidi na zinazofaa familia yetu. Ikiwa duka la nguo lina nguo za mitindo na rangi mbalimbali, tunaweza kuchagua nguo inayotufaa zaidi. Mambo fulani tunayochagua maishani yanategemea tu mapendezi yetu wenyewe. Hata hivyo, mambo mengine tunayochagua yanahusu hali yetu njema kama vile, uchaguzi wetu kuhusu chakula chenye afya au marafiki wenye hekima. Namna gani dini tunayochagua? Je, njia yetu ya ibada inategemea tu mapendezi yetu wenyewe? Au je, huo ni uchaguzi muhimu unaohusu hali yetu njema?

Kuna dini nyingi sana ambazo tunaweza kuchagua. Nchi nyingi leo zinawapa watu uhuru wa kidini, na watu wanaacha dini ya wazazi wao kwa urahisi zaidi. Uchunguzi fulani uliofanywa nchini Marekani ulionyesha kwamba asilimia 80 ya Wamarekani “wanaamini kwamba kuna dini zaidi ya moja zinazoweza kuongoza kwenye wokovu.” Kulingana na uchunguzi huohuo, “mtu mmoja kati ya watano waliohojiwa alisema kwamba alibadili dini yake alipokuwa mtu mzima.” Uchunguzi uliofanywa Brazili ulionyesha kwamba karibu robo ya Wabrazili wote wamebadili dini yao.

Hapo zamani, watu walijadiliana vikali kuhusu mafundisho tofauti ambayo yanatofautisha dini moja na nyingine. Sasa watu wengi wana maoni ya kwamba ‘Haidhuru unachagua dini gani.’ Lakini hivyo ndivyo ilivyo? Je, dini unayochagua inaweza kuwa na matokeo maishani mwako?

Mnunuzi mwenye hekima ni yule anayeuliza maswali kuhusu chanzo cha bidhaa zinazouzwa. Vivyo hivyo, ni jambo la hekima kuuliza: ‘Dini hizi nyingi zilianza jinsi gani, na kwa nini?’ Biblia inatoa majibu.

Dini Zinaanza Jinsi Gani?

Katika taifa la kale la Israeli, Mfalme Yeroboamu alianzisha dini mpya karibu miaka 1,000 kabla ya Yesu kuja duniani. Yeroboamu alikuwa mfalme wa kwanza wa taifa huru la kaskazini la Israeli. Alikuwa na kazi ngumu ya kuwaunganisha watu ili watimize miradi yake. “Mfalme akafanya shauri, akatengeneza ndama wawili wa dhahabu na kuwaambia watu: ‘Ni vigumu mno kwenu kwenda Yerusalemu. Tazama, huyu ni Mungu wenu, enyi Israeli.’” (1 Wafalme 12:28) Ni wazi kwamba mfalme alitaka kutumia dini kuwazuia watu wasiwe washikamanifu kuelekea jiji la Yerusalemu, ambako walikuwa wakiabudu. Dini ambayo Yeroboamu alianzisha iliendelea kwa karne nyingi na mwishowe ilisababisha vifo vya mamilioni ya watu wakati Mungu alipotekeleza hukumu yake juu ya taifa la Israeli lenye kuasi imani. Yeroboamu alianzisha dini ili kujifaidi kisiasa. Vivyo hivyo, dini fulani za Kitaifa ambazo zipo leo zilianzishwa ili kuimarisha mamlaka za kisiasa.

Mtume Paulo alifunua jambo lingine ambalo linawafanya watu waanzishe dini mpya aliposema hivi: “Ninajua kwamba baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wenye kukandamiza wataingia katikati yenu nao hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:29, 30) Mara nyingi, viongozi wenye kiburi wanaanzisha harakati za kidini ili wasifiwe na watu. Makanisa ambayo yanadai kwa uwongo kuwa ya Kikristo yamegawanyika katika vikundi vingi.

Dini Zinataka Kumpendeza Nani?

Huenda watu fulani wakaanzisha dini mpya kwa sababu watu wengi wanawahimiza wafanye hivyo. Kwa mfano, gazeti moja (Economist) lilitoa ripoti kuhusu yale yanayoitwa eti makanisa makubwa nchini Marekani. Gazeti hilo linasema kwamba makanisa hayo yanakua kwa sababu “yanategemea kanuni ambayo inaongoza biashara zote zenye mafanikio: kanuni ya kuwafurahisha wateja.” Makanisa fulani kati ya hayo “yanachanganya ibada na burudani kama vidio, drama na muziki wa kisasa.” Viongozi fulani wa kidini katika makanisa hayo wanadai kwamba wanawafundisha washiriki wao kuwa “matajiri, kuwa na afya nzuri, na kuishi bila wasiwasi wowote.” Gazeti hilo linasema kwamba ingawa makanisa hayo yanalaumiwa kwa sababu ya kuwa katika biashara ya burudani au katika “biashara ya kujisaidia, yanafanya hivyo kwa sababu waumini wanataka hivyo.” Ripoti hiyo inamalizia hivi: “Muungano wa biashara na dini umefanikiwa kabisa.”

Hata ingawa huenda dini nyingine hazionekani waziwazi kuwa za kibiashara, makanisa ambayo “yanafanya vile waumini wanavyotaka” yanatukumbusha onyo la Paulo. Aliandika hivi: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe; nao watageuza masikio yao kutoka kwenye kweli, nao watageuzwa kando kufuata hadithi za uwongo.”—2 Timotheo 4:3, 4.

Kwa kuwa dini nyingi zilianza kwa sababu ya tamaa ya kupata mamlaka ya kisiasa, sifa, na kukubaliwa na watu badala ya tamaa ya kumpendeza Mungu, haishangazi kwamba dini zinahusika katika mambo mabaya kama vile kuwatendea watoto vibaya, udanganyifu, vita, au ugaidi. Kwa kawaida, dini zinawadanganya watu. Unaweza kuepuka jinsi gani kudanganywa?

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Dini nyingi zilianza kwa sababu ya tamaa ya kupata mamlaka ya kisiasa, sifa, na kukubaliwa na watu badala ya tamaa ya kumpendeza Mungu