Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuitambua Ibada ya Kweli

Jinsi ya Kuitambua Ibada ya Kweli

Jinsi ya Kuitambua Ibada ya Kweli

DINI nyingi zinadai kwamba zinafundisha mambo yanayotoka kwa Mungu. Kwa hiyo, tunahitaji kutii maneno ya Yohana, mtume wa Yesu, aliyeandika hivi: “Wapendwa, msiamini kila neno lililoongozwa na roho, lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu, kwa sababu manabii wengi wa uwongo wameingia ulimwenguni.” (1 Yohana 4:1) Tunaweza kujaribu namna gani jambo fulani ili kuona kama linatokana na Mungu?

Kila jambo linalotokana na Mungu linaonyesha utu wake, hasa sifa yake kuu ya upendo. Kwa mfano, uwezo wetu wa kunusa, ambao unatuwezesha kufurahia harufu nzuri ya mimea, maua, au mkate ambao umetoka kuokwa, unaonyesha upendo wa Mungu. Uwezo wetu wa kuona kutua kwa jua, kipepeo, au tabasamu ya mtoto mdogo unaonyesha kwamba Mungu anatupenda. Uwezo wetu wa kusikia sauti ya ndege, muziki mtamu, au sauti ya mpendwa wetu unaonyesha hivyo pia. Hata mwili wetu wa kibinadamu unaonyesha kwamba Mungu anatupenda hata ingawa sisi si wakamilifu. Ndiyo sababu mara nyingi tunajionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Tunafurahia kuonyesha upendo kwa sababu tumeumbwa “kwa mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:27) Ingawa Yehova ana sifa nyingine nyingi, upendo ndio sifa kuu ya utu wake.

Maandishi yaliyoongozwa na Mungu yanapaswa kuonyesha kwamba anatupenda. Dini za ulimwengu zina maandishi mengi ya zamani. Je, maandishi hayo yanaonyesha wazi kwamba Mungu anatupenda?

Ukweli ni kwamba maandishi mengi ya zamani ya kidini hayaelezi mengi kuhusu jinsi Mungu anavyotupenda au jinsi tunavyoweza kumpenda Mungu. Hivyo, mamilioni ya watu hawapati jibu wanapouliza, “Kwa nini uumbaji unaonyesha kwamba Mungu anatupenda lakini mateso na uovu unaendelea?” Kwa upande mwingine, Biblia ndiyo maandishi pekee ya zamani ya kidini ambayo yanaeleza kikamili upendo wa Mungu. Biblia inatufundisha pia jinsi tunavyoweza kuonyesha upendo kwa matendo.

Kitabu Kinachozungumzia Upendo

Neno la Mungu, Biblia, linaonyesha kwamba Yehova ni “Mungu wa upendo.” (2 Wakorintho 13:11) Biblia inaeleza jinsi upendo ulivyomchochea Yehova kuwapa wanadamu wa kwanza maisha ambayo hayakuwa na magonjwa wala kifo. Lakini wanadamu walianza kuteseka kwa sababu ya kuasi mamlaka ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Waroma 5:12) Yehova alichukua hatua ya kurudisha kile kilichopotezwa. Neno la Mungu linasema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Maandiko Matakatifu yanafunua zaidi upendo wa Mungu yanapoeleza jinsi ambavyo Mungu amesimamisha serikali kamilifu mikononi mwa Yesu ili kuwarudishia amani wanadamu watiifu.—Danieli 7:13, 14; 2 Petro 3:13.

Biblia inaeleza hivi kwa ufupi kuhusu wajibu wa mwanadamu: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.” (Mathayo 22:37-40) Biblia inasema kwamba iliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Kwa kuwa inaonyesha wazi utu wake, tunaweza kuwa na hakika kwamba ilitoka kwa “Mungu wa upendo.”—2 Timotheo 3:16.

Tukitumia kanuni hiyo, tunaweza kutambua maandishi ya zamani ambayo kwa kweli yametokana na Mungu. Upendo unawatambulisha pia waabudu wa kweli, kwa kuwa wanamwiga Mungu katika kuonyesha upendo.

Jinsi ya Kuwatambua Watu Wanaompenda Mungu

Wale ambao wanampenda Mungu kikweli wako tofauti, hasa leo tunapoishi katika zile zinazoitwa na Biblia “siku za mwisho.” Watu wanazidi ‘kujipenda wenyewe, kupenda pesa, na kupenda raha badala ya kumpenda Mungu.’—2 Timotheo 3:1-4.

Unaweza kuwatambua jinsi gani watu wanaompenda Mungu? Biblia inasema: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.” (1 Yohana 5:3) Kumpenda Mungu kunawachochea watu waheshimu viwango vya Biblia vya maadili. Kwa mfano, Neno la Mungu lina sheria kuhusu ngono na ndoa. Mahusiano ya kingono yanaruhusiwa tu katika ndoa, na ndoa inapaswa kudumu. (Mathayo 19:9; Waebrania 13:4) Mwanamke mmoja nchini Hispania ambaye alijifunza theolojia alipohudhuria mkutano ambamo Mashahidi wa Yehova walikuwa wakijifunza kwa hamu sheria za Biblia za maadili, alisema hivi: “Nilipoondoka mkutanoni nilihisi nimejengwa, si tu na hotuba zenye kuelimisha za Kimaandiko lakini pia na umoja ulio kati ya watu hao, viwango vyao vya juu vya maadili, na mwenendo wao mzuri.”

Zaidi ya kumpenda Mungu, Wakristo wa kweli wanatambuliwa kwa urahisi kwa njia ambayo wanawaonyesha majirani wao upendo. Kazi yao muhimu zaidi ni kuzungumza na wengine kuhusu tumaini pekee la wanadamu, Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Hakuna jambo linaloweza kuwafaidi milele majirani wao kuliko kuwasaidia kupata ujuzi juu ya Mungu. (Yohana 17:3) Wakristo wa kweli wanaonyesha upendo wao kwa njia nyingine pia. Wanawasaidia kimwili wale wanaoteseka. Kwa mfano, tetemeko la nchi liliposababisha msiba nchini Italia, gazeti moja la huko liliripoti kwamba Mashahidi wa Yehova “wanachukua hatua zinazofaa, wanawasaidia wale wanaoteseka, bila kujali wao ni wa dini gani.”

Zaidi ya kumpenda Mungu na jirani, Wakristo wa kweli wanapendana wao kwa wao. Yesu alisema: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—Yohana 13:34, 35.

Je, upendo wa Wakristo wa kweli unaonekana kuwa tofauti? Mfanyakazi wa nyumbani anayeitwa Ema alifikiri hivyo. Anafanya kazi huko La Paz, Bolivia, ambako mara nyingi tofauti za kikabila zinawatenganisha matajiri na maskini. Alisema hivi: “Nilipohudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza, nilimwona mwanamume aliyevalia vizuri akiwa ameketi akizungumza na mwanamke Mhindi. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kuona hilo. Papo hapo, nikajua kwamba hawa ni watu wa Mungu.” Vivyo hivyo, mwanamke mmoja Mbrazili anayeitwa Miriam alisema hivi: “Sikujua jinsi ninavyoweza kuwa na furaha, hata katika familia yetu. Mara ya kwanza nilipoona upendo ukionyeshwa kwa matendo ilikuwa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova.” Huko Marekani, mkurugenzi wa habari katika kituo kimoja cha televisheni aliandika hivi: “Ikiwa watu wengi wangeishi kama washiriki wa dini yenu, hali ingekuwa tofauti katika taifa hili. Mimi ni mwana-habari ambaye anajua kwamba msingi wa tengenezo lenu ni upendo na imani yenye nguvu katika Muumba.”

Tafuta Ibada ya Kweli

Upendo ni sifa inayotambulisha ibada ya kweli. Yesu alilinganisha kupata ibada ya kweli na kupata barabara inayofaa na kuamua kuifuata. Hiyo ndiyo barabara ya pekee inayoongoza kwenye uzima wa milele. Yesu alisema: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu barabara inayoongoza kwenye uharibifu ni pana na kubwa, na wengi ndio wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Ni kikundi kimoja tu cha Wakristo wa kweli kinachotembea kwa umoja pamoja na Mungu kwenye barabara ya ibada ya kweli. Kwa hiyo, ni muhimu kufikiria dini unayochagua. Ukipata barabara hiyo na kuchagua kuifuata, utakuwa umepata njia bora ya maisha kwa kuwa ni njia ya upendo.—Waefeso 4:1-4.

Wazia shangwe utakayopata ukitembea kwenye barabara ya ibada ya kweli! Ni kama kutembea pamoja na Mungu. Mungu anaweza kukufundisha hekima na upendo ili uwe na mahusiano mazuri na watu wengine. Anaweza kukufundisha kusudi la maisha, na unaweza kuelewa ahadi za Mungu na kuwa na tumaini la wakati ujao. Hutajuta kamwe kuitafuta ibada ya kweli.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kati ya maandishi ya zamani ya kidini, ni Biblia tu inayofunua upendo wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wakristo wa kweli wanatambuliwa kwa sababu wanaonyesha upendo kwa matendo