Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kungoja Ufalme Ambao Si “Sehemu ya Ulimwengu Huu”

Kungoja Ufalme Ambao Si “Sehemu ya Ulimwengu Huu”

Simulizi la Maisha

Kungoja Ufalme Ambao Si “Sehemu ya Ulimwengu Huu”

Kama lilivyosimuliwa na Nikolai Gutsulyak

Kwa siku 41 mchana na usiku, nilijikuta katikati ya uasi gerezani. Kwa ghafula, niliamshwa kutoka usingizini na milio ya mizinga. Vifaru vya vita na askari-jeshi waliingia kwa ghafula katika kambi ya gereza na kuwashambulia wafungwa. Maisha yangu yalikuwa hatarini.

NILIINGIA katika hali hiyo jinsi gani? Acheni nieleze. Kisa hicho kilitukia mwaka wa 1954. Wakati huo, nilikuwa na umri wa miaka 30. Kama Mashahidi wengi wa Yehova ambao waliishi chini ya utawala wa Sovieti, nilifungwa gerezani kwa sababu ya kutoshiriki mambo ya kisiasa na kwa sababu ya kuwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu. Kikundi chetu cha Mashahidi waliofungwa gerezani kilikuwa na wanaume 46 na wanawake 34. Tulifungiwa katika kambi ya kazi ngumu karibu na kijiji cha Kengir, katikati mwa Kazakhstan. Tuliishi huko pamoja na maelfu ya wafungwa wengine.

Joseph Stalin, kiongozi wa Muungano wa Sovieti, alikuwa amekufa mwaka uliotangulia. Wafungwa wengi walitumaini kwamba huenda serikali mpya huko Moscow ingesikiliza malalamiko yao kuhusu hali mbaya za magereza. Mwishowe, wafungwa walishindwa kuvumilia na wakaanza kuasi waziwazi gerezani. Katika mapambano yaliyotokea, sisi Mashahidi tulilazimika kuwaeleza wazi waasi hao wenye hasira na pia walinzi wa kijeshi msimamo wetu. Tulihitaji imani katika Mungu ili kuchukua msimamo huo wa kutokuwamo.

Uasi Unaanza!

Uasi ulianza gerezani mnamo Mei (Mwezi wa 5), tarehe 16. Siku mbili baadaye, wafungwa zaidi ya 3,200 walikataa kwenda kazini, wakidai hali za gereza ziboreshwe na wafungwa wa kisiasa wapewe haki fulani. Mambo yalibadilika haraka. Kwanza waasi hao waliwafukuza walinzi kutoka kambini. Kisha wakatoboa shimo katika ua uliozingira kambi. Halafu wakabomoa kuta ambazo zilitenganisha gereza la wanawake na la wanaume, hivyo wafungwa wote wakaishi pamoja kama familia. Katika siku zilizofuata zenye kusisimua, wafungwa fulani hata walioana, na arusi zilisimamiwa na makasisi ambao pia walikuwa wamefungwa gerezani. Katika magereza matatu kambini ambamo uasi ulitokea, wengi kati ya wafungwa 14,000 walishiriki katika uasi huo.

Waasi hao walipanga halmashauri ya kambi ya kuzungumza na jeshi. Hata hivyo, muda si muda ubishi ulitokea kati ya washiriki wa halmashauri hiyo, na kambi ikaanza kusimamiwa na wafungwa sugu zaidi. Hali ilizorota hata zaidi. Viongozi wa uasi walipanga idara ya ulinzi, idara ya kijeshi, na idara ya propaganda ili kudumisha “utaratibu.” Viongozi hao walitumia vipaza-sauti ambavyo vilikuwa vimetundikwa kwenye milingoti kutangaza habari motomoto, na kufanya roho ya uasi ipambe moto kambini. Waasi hao waliwazuia wafungwa wengine wasitoroke, wakawaadhibu wale waliowapinga, na kutangaza kwamba walikuwa tayari kumuua mtu yeyote ambaye hawakumtaka. Kulikuwa na uvumi kwamba tayari wafungwa fulani walikuwa wameuawa.

Kwa kuwa waasi hao walitarajia kushambuliwa na askari-jeshi, walijitayarisha kabisa kujilinda. Ili kuhakikisha kwamba wafungwa wengi iwezekanavyo wangekuwa na silaha za kulinda kambi, viongozi waliamuru wafungwa wote wajitafutie silaha. Ili kuwa na silaha, wafungwa waling’oa vyuma vya madirisha na kutengeneza visu na silaha nyingine kutokana na vyuma hivyo. Hata walifaulu kupata bunduki na gruneti.

Mashahidi Walazimishwa Waunge Mkono Uasi

Wakati huo, waasi wawili walinifikia. Mmoja wao alinipa kisu kilichotoka tu kunolewa. “Chukua kisu hiki!” akaniamuru. “Utakihitaji ili kujilinda.” Nilimwomba Yehova kimyakimya anisaidie kubaki mtulivu. Nilimjibu hivi: “Mimi ni Mkristo, Shahidi wa Yehova. Mimi pamoja na Mashahidi wengine tumefungwa gerezani kwa sababu tunapigana, si na watu, bali na majeshi ya roho wasioonekana. Silaha tunazotumia kupigana nao ni imani yetu na tumaini letu katika Ufalme wa Mungu.”—Waefeso 6:12.

Nilishangaa wakati mwanamume huyo alipoonyesha kwa kichwa kwamba anaelewa. Hata hivyo, yule mwasi mwingine alinipiga kwa nguvu. Kisha wakaondoka. Waasi walienda kutoka jengo moja hadi lingine, wakijaribu kuwalazimisha Mashahidi waunge mkono uasi huo. Lakini ndugu na dada zetu Wakristo walikataa wote.

Msimamo wa kutokuwamo wa Mashahidi wa Yehova ulizungumziwa kwenye mkutano wa halmashauri ya waasi. “Washiriki wa dini zote, Wapentekoste, Waadventisti, Wabaptisti, na watu wengine wote wanaunga mkono uasi. Mashahidi wa Yehova tu ndio wamekataa,” wakasema. “Tutawachukulia hatua gani?” Mtu fulani alipendekeza Shahidi mmoja atupwe ndani ya jiko la gereza ili kutuogopesha. Lakini ofisa mmoja wa zamani wa jeshi, mfungwa ambaye aliheshimiwa na wengine, alisimama na kusema hivi: “Hilo si jambo la hekima. Tunapaswa kuwaweka wote katika jengo moja pembeni mwa kambi, karibu na lango. Kwa njia hiyo, ikiwa jeshi litatushambulia kwa vifaru vya vita, Mashahidi watakuwa wa kwanza kukanyagwa na vifaru hivyo. Nasi hatutakuwa na hatia ya kuwaua.” Wengine walikubali pendekezo lake.

Wawekwa Mahali Hatari

Muda si muda, wafungwa walitembea katika kambi yote wakipaaza sauti, “Mashahidi wa Yehova, ondokeni!” Kisha sote 80 tukakusanywa na kupelekwa pembeni mwa kambi. Waliondoa vitanda vya ghorofa vilivyokuwa katika jengo hilo ili kuwe na nafasi zaidi kisha wakatuamuru tuingie humo. Jengo hilo likawa gereza letu ndani ya gereza hilo.

Ili kuwa na faragha, dada Wakristo waliokuwa katika kikundi chetu waliunganisha pamoja shuka, na tulizitumia kugawanya jengo hilo katika sehemu mbili, sehemu moja kwa ajili ya wanaume na nyingine ya wanawake. (Baadaye, Shahidi mmoja wa Urusi alichora majengo hayo. Picha hiyo inaonyeshwa hapo chini.) Tulipokuwa tukiishi katika majengo hayo yaliyosongamana, mara nyingi tulisali pamoja, na kumwomba Yehova atupe hekima na “nguvu zinazopita zile za kawaida.”—2 Wakorintho 4:7.

Wakati huo wote, tulikuwa mahali hatari kati ya waasi na jeshi la Sovieti. Hakuna yeyote kati yetu aliyejua vikundi hivyo vingefanya nini. Ndugu mmoja Mkristo mwaminifu mwenye umri mkubwa zaidi alituhimiza hivi: “Msijaribu kukisia. Yehova hatatuacha.”

Dada zetu Wakristo wapendwa, wadogo kwa wakubwa, walionyesha uvumilivu wa pekee sana. Mmoja alikuwa na umri wa miaka 80 hivi na alihitaji msaada zaidi. Wengine walikuwa wagonjwa na walihitaji matibabu. Wakati huo wote, milango ya jengo letu ilifunguliwa wazi ili waasi waweze kutuchunguza daima. Usiku, wafungwa wenye silaha walikuja kwenye jengo hilo. Nyakati nyingine walisikiwa wakisema, “Ufalme wa Mungu umelala.” Mchana, walipoturuhusu kwenda kwenye jumba la chakula kambini, sikuzote tulikaa pamoja na kusali ili Yehova atulinde kutokana na wanaume wenye jeuri.

Tukiwa kambini, tulijitahidi kutiana moyo kiroho. Kwa mfano, kwa kawaida ndugu alisimulia tukio fulani la Biblia, kwa sauti ambayo sote tungeweza kusikia. Kisha, alionyesha jinsi simulizi hilo lilivyohusiana na hali zetu. Ndugu mmoja mzee kwa umri alipenda hasa kuzungumza kuhusu jeshi la Gideoni. Alitukumbusha hivi: “Katika jina la Yehova, wanaume 300 waliobeba ala za muziki mikono mwao walipigana na askari-jeshi 135,000 wenye silaha. Wote 300 walirudi bila madhara yoyote.” (Waamuzi 7:16, 22; 8:10) Mfano huo na mifano mingine ya Biblia ilitutia nguvu kiroho. Nilikuwa Shahidi mpya tu, lakini nilipoona imani yenye nguvu ya ndugu na dada wenye uzoefu zaidi nilitiwa moyo sana. Nilihisi kwamba kwa kweli Yehova alikuwa pamoja nasi.

Vita Vinaanza

Majuma yalipita, na hali ya wasiwasi iliongezeka kambini. Mazungumzo kati ya waasi na wenye mamlaka yalipamba moto. Viongozi wa waasi walisisitiza kwamba makao makuu ya serikali huko Moscow yatume mwakilishi ili wakutane naye. Wenye mamlaka waliamuru waasi hao wajisalimishe, waweke silaha chini, na kurudi kazini. Kila upande ulikataa makubaliano. Kufikia wakati huo, kambi ilikuwa imezungukwa na askari-jeshi wakingojea amri ya kushambulia. Waasi nao walikuwa tayari kupigana, waliweka vizuizi na walikuwa na rundo la silaha. Kila mtu alitarajia vita kati ya jeshi na wafungwa vingezuka wakati wowote.

Mnamo Juni (Mwezi wa 6), tarehe 26, tuliamshwa na milio mikubwa sana ya mizinga. Vifaru viliangusha ua na kuingia kambini. Kisha, askari-jeshi waliingia na kushambulia kwa bunduki zenye kumimina risasi. Wafungwa, wanaume kwa wanawake walikimbia kuelekea kwenye vifaru vilivyokuwa vikija, wakipaaza sauti “Huree!” na kurusha mawe, mabomu waliyojitengenezea, na kitu chochote ambacho walipata. Vita vikali vilizuka, na sisi Mashahidi tulijikuta katikati ya mapambano hayo. Yehova angejibu jinsi gani sala zetu za kuomba msaada?

Kwa ghafula, askari-jeshi waliingia katika jengo letu. “Tokeni nje, ninyi watakatifu!” wakasema kwa sauti. “Ondokeni haraka nje ya ua!” Ofisa mkuu aliwaagiza askari-jeshi hao wasitupige risasi lakini wakae nasi na kutulinda. Vita vilipokuwa vikiendelea, tuliketi kwenye uwanja wenye nyasi nje ya kambi. Kwa saa nne, tulisikia milipuko, risasi, vilio, na sauti za watu wakiomboleza kutoka kambini. Kisha, kukawa na kimya. Baadaye, asubuhi ilipofika, tuliona askari-jeshi wakibeba maiti kutoka kambini. Tulipata habari kwamba mamia ya watu waliumizwa au kufa.

Baadaye siku hiyo, ofisa ambaye nilimfahamu alikuja mahali tulipokuwa. Akauliza kwa majivuno, “Nikolai, ni nani aliyewaokoa? Ni sisi au ni Yehova?” Tulimshukuru kutoka moyoni kwa sababu ya kuokoa maisha yetu, na tukaongezea, “Tunaamini kwamba Mungu wetu mweza-yote, Yehova, aliwachochea ili msituue, kama alivyowachochea wengine ili wawakomboe watumishi wake katika nyakati za Biblia.”—Ezra 1:1, 2.

Ofisa huyo pia alitueleza jinsi askari-jeshi walivyojua sisi ni nani na tulikuwa wapi. Alisema kwamba wakati wa mazungumzo kati ya jeshi na waasi, askari-jeshi walishutumu waasi kwa sababu ya kuwaua wafungwa ambao hawakuwaunga mkono. Waasi walijitetea kwa kusema kwamba Mashahidi wa Yehova hawakushiriki katika uasi lakini hawakuuawa. Badala yake, kama adhabu, Mashahidi wote walifungiwa katika jengo moja. Maofisa wa jeshi walikumbuka maneno hayo.

Tulisimama Imara kwa Ajili ya Ufalme

Mtungaji maarufu wa vitabu kutoka Urusi Aleksandr Solzhenitsyn anataja katika kitabu chake (The Gulag Archipelago), uasi uliotokea katika gereza letu. Kuhusu tukio hilo, anaandika kwamba uasi ulianza kwa sababu, kama alivyosema, “bila shaka tunataka uhuru, . . . lakini ni nani anayeweza kutupa uhuru?” Sisi Mashahidi wa Yehova tuliokuwa katika gereza hilo, tulitamani pia kupata uhuru. Hata hivyo, si uhuru tu kutoka gerezani bali uhuru ambao unaweza kuletwa tu na Ufalme wa Mungu. Tukiwa gerezani, tulijua kwamba tulihitaji nguvu kutoka kwa Mungu ili kubaki imara upande wa Ufalme wake. Yehova alituandalia kila kitu tulichohitaji. Alitupa ushindi bila kutumia visu wala gruneti.—2 Wakorintho 10:3.

Yesu Kristo alimwambia Pilato hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana.” (Yohana 18:36) Basi, tukiwa wafuasi wa Kristo hatukushiriki kamwe katika mapambano ya kisiasa. Tulifurahi kwamba wakati na baada ya uasi huo, wengine waliona ushikamanifu wetu kwa Ufalme wa Mungu. Solzhenitsyn aliandika hivi kuhusu mwenendo wetu wakati huo: “Mashahidi wa Yehova walijihisi huru kufuata kabisa sheria zao na walikataa kujenga ngome au kulinda kambi.”

Miaka zaidi ya 50 imepita tangu matukio hayo hatari yatokee. Hata hivyo, mara nyingi ninakumbuka nyakati hizo kwa shukrani kwa sababu nilijifunza masomo ya kudumu kuhusu kuvumilia, kama vile kumngoja Yehova na kutegemea kabisa mkono wake wenye uwezo. Ndiyo, kama Mashahidi wengine wengi wapendwa katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, nimeona kwamba kwa kweli Yehova anawapa uhuru, ulinzi, na ukombozi wale wanaongoja Ufalme ambao “si sehemu ya ulimwengu huu.”

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kambi ya kazi ngumu huko Kazakhstan ambako tulikuwa wafungwa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mchoro wa jengo la Mashahidi, sehemu ya wanawake

[Picha katika ukurasa wa 11]

Nikiwa na ndugu Wakristo baada ya kuachiliwa huru