Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Na Tulikweze Jina la Yehova Pamoja

Na Tulikweze Jina la Yehova Pamoja

Na Tulikweze Jina la Yehova Pamoja

“Mtukuzeni Yehova pamoja nami, na tulikweze jina lake pamoja.”—ZABURI 34:3.

1. Yesu aliweka mfano gani mzuri wakati wa huduma yake duniani?

USIKU wa Nisani 14, 33 W.K., Yesu na mitume wake waliimba sifa za Yehova pamoja katika chumba cha juu cha nyumba moja huko Yerusalemu. (Mathayo 26:30) Hiyo ilikuwa mara ya mwisho kwa Yesu kufanya hivyo akiwa pamoja na mitume wake. Hata hivyo, ilifaa kwake kumalizia mkutano huo kwa njia hiyo. Tangu mwanzo hadi mwisho wa huduma yake hapa duniani, Yesu alimsifu Baba yake na kulitangaza jina Lake kwa bidii. (Mathayo 4:10; 6:9; 22:37, 38; Yohana 12:28; 17:6) Kwa kufanya hivyo, alitoa mwaliko huu mchangamfu wa mtunga-zaburi: “Mtukuzeni Yehova pamoja nami, na tulikweze jina lake pamoja.” (Zaburi 34:3) Alituwekea mfano mzuri kama nini wa kufuata!

2, 3. (a) Tunajua jinsi gani kwamba Zaburi ya 34 ina umuhimu wa kinabii? (b) Tutazungumzia nini katika habari hii na ile inayofuata?

2 Saa chache baada ya kuimba sifa pamoja na Yesu, mtume Yohana alishuhudia tukio lingine tofauti kabisa. Aliona Bwana wake na wahalifu wawili wakiuawa juu ya miti ya mateso. Askari-jeshi wa Roma walivunja miguu ya wale wahalifu wawili ili wafe haraka. Hata hivyo, Yohana anaripoti kwamba hawakuvunja miguu ya Yesu. Askari-jeshi hao walipomfikia Yesu, alikuwa tayari amekufa. Katika Injili yake, Yohana alitaja kwamba tukio hilo lilitimiza sehemu nyingine ya Zaburi ya 34: “Hakuna hata mfupa wake mmoja utakaovunjwa.”—Yohana 19:32-36; Zaburi 34:20, Biblia Habari Njema.

3 Zaburi ya 34 ina mambo mengine mengi yanayowapendeza Wakristo. Hivyo, katika habari hii na ile inayofuata, tutazungumzia hali ambazo Daudi alikuwa akikabili alipoandika zaburi hii na kisha tutazungumzia mambo yenye kutia moyo yaliyo katika zaburi hiyo.

Daudi Amkimbia Sauli

4. (a) Kwa nini Daudi alitiwa mafuta awe mfalme wa Israeli ambaye angefuata? (b) Kwa nini Sauli ‘alimpenda sana’ Daudi?

4 Daudi alipokuwa kijana, Sauli alikuwa mfalme wa Israeli. Hata hivyo, Sauli aliacha kutii naye akapoteza kibali cha Yehova. Kwa sababu hiyo, nabii Samweli alimwambia hivi: “Yehova ameurarua utawala wa kifalme wa Israeli kutoka kwako leo, naye hakika atampa mwenzako ambaye ni bora kuliko wewe.” (1 Samweli 15:28) Baadaye, Yehova alimwongoza Samweli amtie mafuta Daudi, mwana mdogo zaidi wa Yese, awe mfalme wa Israeli ambaye angefuata. Wakati huohuo, kwa sababu ya kuondolewa roho ya Mungu, Mfalme Sauli alisumbuka sana kihisia. Daudi, aliyekuwa mwanamuziki stadi, aliletwa Gibea ili amtumikie mfalme, na muziki wa Daudi ulimtuliza Sauli ambaye ‘alimpenda sana’ Daudi. —1 Samweli 16:11, 13, 21, 23.

5. Kwa nini mtazamo wa Sauli kuelekea Daudi ulibadilika, na Daudi alilazimika kufanya nini?

5 Kadiri wakati ulivyopita, Yehova aliendelea kuwa pamoja na Daudi. Yehova alimsaidia Daudi kumshinda Goliathi, lile jitu la Wafilisti, naye alimtegemeza na hivyo Daudi akaheshimiwa katika Israeli kwa ustadi wake wa kijeshi. Hata hivyo, kwa sababu Yehova alimbariki Daudi, Sauli alimwonea wivu, naye akamchukia Daudi. Mara mbili Daudi alipokuwa akipiga kinubi chake mbele za Sauli, mfalme huyo alimrushia Daudi mkuki. Mara zote mbili, Daudi alifaulu kuhepa mkuki. Sauli alipojaribu mara ya tatu kumuua Daudi, mfalme huyo wa Israeli ambaye angefuata alitambua kwamba anapaswa kukimbia ili kuokoa uhai wake. Mwishowe, kwa sababu Sauli aliendelea kumsaka ili amuue, Daudi alilazimika kukimbilia nje ya eneo la Israeli.—1 Samweli 18:11; 19:9, 10.

6. Kwa nini Sauli aliagiza wakaaji wa Nobu wauawe?

6 Alipokuwa akielekea kwenye mpaka wa Israeli, Daudi alisimama katika jiji la Nobu, ambako maskani ya Yehova yalikuwa. Inaelekea kwamba Daudi aliandamana na kikundi cha wanaume vijana alipokuwa akikimbia, naye alitafuta chakula kwa ajili yake na wenzake. Sauli alipata habari kwamba kuhani mkuu alikuwa amempa Daudi na wanaume wake chakula kidogo na ule upanga ambao Daudi alikuwa ameuchukua kutoka kwa Goliathi aliyeuawa. Kwa hasira, Sauli aliagiza kwamba wakaaji wote wa jiji hilo, kutia ndani makuhani 85, wauawe.—1 Samweli 21:1, 2; 22:12, 13, 18, 19; Mathayo 12:3, 4.

Aponea Tena Chupuchupu

7. Kwa nini Gathi hapakuwa mahali salama pa Daudi kujificha?

7 Kutoka Nobu, Daudi alikimbia umbali wa kilomita 40 hivi upande wa magharibi na kuingia katika eneo la Wafilisti. Hatimaye, akafika kwa Akishi, mfalme wa Gathi, mji wa nyumbani kwa Goliathi. Labda Daudi alifikiri kwamba Sauli hangemtafuta huko Gathi. Hata hivyo, muda si muda, watumishi wa mfalme wa Gathi walimtambua Daudi. Daudi aliposikia kwamba alikuwa ametambuliwa, ‘aliogopa sana kwa sababu ya Akishi mfalme wa Gathi.’—1 Samweli 21:10-12.

8. (a) Zaburi ya 56 inatuambia nini kuhusu yale yaliyompata Daudi huko Gathi? (b) Daudi aliponea chupuchupu jinsi gani?

8 Kisha, Wafilisti wakamkamata Daudi. Huenda huo ndio wakati ambapo Daudi alitunga zaburi yenye kugusa moyo ambamo alimwomba Yehova hivi: “Uyaweke machozi yangu katika kiriba chako.” (Zaburi 56:8 na utangulizi) Hivyo, alionyesha uhakika wake kwamba Yehova hangesahau huzuni yake, lakini angemtunza kwa upendo na kumlinda. Daudi alifikiria njia ya kumpumbaza mfalme wa Wafilisti. Alijifanya mwenda-wazimu. Alipoona hivyo, Mfalme Akishi aliwakemea watumishi wake kwa kuleta “mwenda-wazimu” mbele yake. Kwa wazi, Yehova alibariki mbinu ya Daudi. Daudi aliondolewa jijini, na hivyo akaponea tena chupuchupu.—1 Samweli 21:13-15.

9, 10. Kwa nini Daudi aliandika Zaburi ya 34, na huenda alikuwa akiwafikiria nani alipotunga zaburi hiyo?

9 Biblia haisemi ikiwa wale waliomuunga Daudi mkono walikimbilia Gathi pamoja naye au walimlinda katika vijiji vya karibu vya Israeli. Vyovyote vile, lazima walifurahi sana kukutana kwa mara nyingine wakati Daudi alipowasimulia jinsi Yehova alivyomwokoa tena. Zaburi ya 34 inategemea kisa hicho kama utangulizi wake unavyoonyesha. Katika mistari saba ya kwanza ya zaburi hiyo, Daudi anamsifu Mungu kwa kumkomboa naye anawaalika watu wanaomuunga mkono wajiunge naye katika kumkweza Yehova kuwa Mwokoaji Mkuu wa watu Wake.—Zaburi 34:3, 4, 7.

10 Daudi na wanaume wake walijificha katika pango la Adulamu kwenye eneo lenye milima la Israeli, karibu kilomita 15 mashariki ya Gathi. Wakiwa huko, Waisraeli ambao hawakuridhishwa na hali za maisha chini ya utawala wa Mfalme Sauli walianza kuja na kujiunga nao. (1 Samweli 22:1, 2) Daudi alipotunga maneno ya Zaburi 34:8-22, huenda alikuwa akiwafikiria watu hao. Vikumbusho vilivyo katika mistari hiyo ni muhimu pia kwetu leo, na bila shaka tutafaidika tukizungumzia kwa undani zaburi hiyo yenye kupendeza sana.

Je, Hangaiko Lako Kuu Ni Kama la Daudi?

11, 12. Tuna sababu gani za kumsifu Yehova daima?

11 “Nitambariki Yehova nyakati zote; daima sifa yake itakuwa katika kinywa changu.” (Zaburi 34:1) Akiwa mkimbizi, lazima Daudi awe alikuwa na mahangaiko mengi ya kimwili. Lakini kama maneno hayo yanavyoonyesha, hakuacha mahangaiko yake ya kila siku yavunje azimio lake la kumsifu Yehova. Alituwekea mfano mzuri kama nini tunapokabili magumu! Iwe tuko shuleni, kazini, pamoja na Wakristo wenzetu, au katika huduma ya hadharani, tamaa yetu kuu ni kumsifu Yehova. Hebu fikiria sababu nyingi sana tulizo nazo za kufanya hivyo! Kwa mfano, hakuna mwisho wa yale tunayoweza kujifunza na kufurahia kutokana na kazi za ajabu za uumbaji za Yehova. Hebu fikiria yale ambayo ametimiza kupitia sehemu ya kidunia ya tengenezo lake! Ingawa si wakamilifu, Yehova amewatumia wanadamu waaminifu kutimiza mambo mengi sana katika nyakati za kisasa. Kazi za Mungu zinatofautiana jinsi gani na kazi za wanadamu ambao wanaabudiwa na ulimwengu? Je, hukubaliani na Daudi ambaye pia aliandika hivi: “Hakuna yeyote aliye kama wewe katikati ya miungu, Ee Yehova, wala hakuna kazi zozote kama zako.”—Zaburi 86:8.

12 Kama Daudi, tunachochewa kumsifu Yehova daima kwa sababu ya kazi zake zisizo na kifani. Zaidi ya hilo, tunasisimka kujua kwamba Ufalme wa Mungu sasa uko mikononi mwa Mrithi wa kudumu wa Daudi, Yesu Kristo. (Ufunuo 11:15) Hilo linamaanisha kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu. Wakati ujao wa milele wa wanadamu zaidi ya bilioni sita uko hatarini. Hakujawahi kamwe kuwa na uhitaji mkubwa kama sasa wa kuwatangazia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu na yale ambayo utawafanyia wanadamu hivi karibuni na kuwasaidia wamsifu Yehova pamoja nasi. Bila shaka, jambo kuu maishani mwetu linapaswa kuwa kutumia kila nafasi kuwatia wengine moyo wakubali “habari njema” kabla haijawa kuchelewa mno.—Mathayo 24:14.

13. (a) Daudi alijisifu katika nani, na ni watu wa aina gani walioitikia? (b) Wapole wanavutwa kwenye kutaniko la Kikristo leo jinsi gani?

13 “Nafsi yangu itajisifu katika Yehova; wapole watasikia na kushangilia.” (Zaburi 34:2) Daudi hakujisifu kwa yale ambayo alitimiza. Kwa mfano, hakujigamba kuhusu jinsi alivyompumbaza mfalme wa Gathi. Alitambua kwamba Yehova alimlinda alipokuwa huko Gathi na kwamba aliponyoka kwa sababu Yehova alimsaidia. (Methali 21:1) Hivyo, Daudi hakujisifu mwenyewe, lakini alijisifu katika Yehova. Kwa sababu hiyo, wapole walivutwa kwa Yehova. Yesu alitukuza vivyo hivyo jina la Yehova, na hilo liliwavuta watu wanyenyekevu na wenye kufundishika ili wamkaribie Yehova. Leo, watu wapole wa mataifa yote wanavutwa kwenye kutaniko la kimataifa la Wakristo watiwa-mafuta, ambalo Yesu ndiye Kichwa chake. (Wakolosai 1:18) Mioyo ya watu hao wapole inaguswa wanaposikia jina la Mungu likitukuzwa na watumishi wake wanyenyekevu na wanaposikia ujumbe wa Biblia, ambao roho takatifu ya Mungu inawawezesha kuelewa.—Yohana 6:44; Matendo 16:14.

Mikutano Inaimarisha Imani Yetu

14. (a) Je, Daudi alitosheka tu kumsifu Yehova faraghani? (b) Yesu aliweka mfano gani kuhusiana na mikutano ya ibada?

14 “Mtukuzeni Yehova pamoja nami, na tulikweze jina lake pamoja.” (Zaburi 34:3) Daudi hakutosheka tu kumsifu Yehova faraghani. Aliwakaribisha wenzake kwa uchangamfu wajiunge naye katika kulikweza jina la Mungu. Vivyo hivyo, Yesu Kristo, yule Daudi Mkuu Zaidi, alifurahia kumsifu Yehova hadharani, kwenye sinagogi la kwao, kwenye sherehe katika hekalu la Mungu huko Yerusalemu, na akiwa pamoja na wafuasi wake. (Luka 2:49; 4:16-19; 10:21; Yohana 18:20) Ni pendeleo lenye shangwe kama nini kufuata mfano wa Yesu wa kumsifu Yehova katika kila nafasi tunayopata pamoja na waamini wenzetu, hasa sasa kadiri ‘tunavyoona siku ile kuwa inakaribia’!—Waebrania 10:24, 25.

15. (a) Mambo yaliyompata Daudi yalikuwa na matokeo gani juu ya wanaume wake? (b) Tunafaidika jinsi gani tunapohudhuria mikutano yetu?

15 “Nilimuuliza Yehova, naye akanijibu, naye akanikomboa kutoka katika mambo yote yenye kuniogopesha.” (Zaburi 34:4) Mambo hayo yaliyompata Daudi yalikuwa muhimu kwake. Kwa hiyo, aliendelea kusema hivi: “Huyu mwenye kuteseka aliita, na Yehova mwenyewe akasikia. Na Yeye akamwokoa kutoka katika taabu zake zote.” (Zaburi 34:6) Tunaposhirikiana na waamini wenzetu, tuna nafasi nyingi za kusimulia mambo yenye kujenga kuhusu jinsi Yehova ametusaidia kuvumilia hali ngumu. Hilo linaimarisha imani ya waamini wenzetu, kama masimulizi ya Daudi yalivyoimarisha imani ya watu waliomuunga mkono. Katika kisa cha Daudi, watu walioandamana naye “walimtazama [Yehova], wakang’aa, nazo nyuso zao hazingeweza kuona haya kamwe.” (Zaburi 34:5) Ingawa walikuwa wakimkimbia Mfalme Sauli, hawakuona haya. Walikuwa na hakika kwamba Mungu alikuwa akimtegemeza Daudi, na nyuso zao ziling’aa. Vivyo hivyo, wapya wenye kupendezwa na pia wale ambao wamekuwa Wakristo wa kweli kwa muda mrefu wanamtazama Yehova awategemeze. Kwa kuwa wamesaidiwa na Yehova kibinafsi, nyuso zao zenye kung’aa zinaonyesha azimio lao la kubaki waaminifu.

Thamini Msaada wa Malaika

16. Yehova amewatumia malaika wake jinsi gani kutuokoa?

16 “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.” (Zaburi 34:7) Daudi hakuona kwamba ni yeye tu angeweza kuokolewa na Yehova. Ni kweli kwamba Daudi alikuwa mtiwa-mafuta wa Yehova, mfalme wa Israeli ambaye angefuata; lakini alijua kwamba Yehova anatumia malaika wake kuwalinda waabudu wake wote waaminifu, haidhuru ni watu mashuhuri au ni wa hali ya chini. Katika nyakati zetu pia, waabudu wa kweli wamelindwa na Yehova. Katika Ujerumani ya Nazi na pia Angola, Malawi, Msumbiji, na nchi nyingine nyingi, wenye mamlaka wameendesha kampeni ili kuwaangamiza kabisa Mashahidi wa Yehova. Jitihada zao hazijafaulu. Badala yake, watu wa Yehova katika nchi hizo wanaendelea kusitawi huku wakilikweza jina la Mungu pamoja. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anawatumia malaika wake watakatifu kuwalinda na kuwaongoza watu wake.—Waebrania 1:14.

17. Malaika wa Mungu wanatusaidia katika njia gani?

17 Kwa kuongezea, malaika wa Yehova wanaweza kuelekeza mambo ili mtu yeyote anayewakwaza wengine aondolewe miongoni mwa watu wa Yehova. (Mathayo 13:41; 18:6, 10) Hata ingawa huenda hatujui, malaika wanaondoa vitu vinavyokwaza ambavyo vinaweza kutuzuia tusimtumikie Mungu, na wanatulinda kutokana na mambo yanayoweza kuhatarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Jambo muhimu zaidi ni kwamba wanatuongoza katika kazi ya kutangaza “habari njema ya milele” kwa wanadamu wote, kutia ndani maeneo ambako kazi ya kuhubiri inaendeshwa chini ya hali hatari. (Ufunuo 14:6) Visa vinavyothibitisha kwamba malaika wanasaidia vimesimuliwa mara nyingi katika vichapo vya Biblia vinavyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. * Visa hivyo ni vingi sana hivi kwamba hatuwezi kusema kuwa vinatukia vyenyewe tu.

18. (a) Tunapaswa kufanya nini ili tufaidike na msaada wa malaika? (b) Habari inayofuata itazungumzia nini?

18 Ili kuendelea kufaidika na mwongozo na ulinzi wa malaika, tunapaswa kuendelea kulikweza jina la Yehova hata tunapokabili upinzani. Kumbuka kwamba malaika wa Mungu anapiga kambi “kuwazunguka wanaomwogopa [Yehova]” tu. Hilo linamaanisha nini? Kumwogopa Mungu kunamaanisha nini, na tunaweza kusitawisha sifa hiyo jinsi gani? Kwa nini Mungu mwenye upendo anataka tumwogope? Maswali hayo yatazungumziwa katika habari inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Ona Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 550; Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2005, ukurasa wa 53-54; Mnara wa Mlinzi, Machi 1, 2000, ukurasa wa 5-6; Januari 1, 1991, ukurasa wa 27; na Februari 15, 1991, ukurasa wa 26.

Ungetoa Jibu Gani?

• Daudi alivumilia majaribu gani alipokuwa kijana?

• Kama Daudi, hangaiko letu kuu ni nini?

• Tuna maoni gani kuhusu mikutano ya Kikristo?

• Yehova anawatumia malaika wake kwa njia gani ili kutusaidia?

[Maswali ya Funzo]

[Ramani katika ukurasa wa 21]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Rama

Gathi

Siklagi

Gibea

Nobu

Yerusalemu

Bethlehemu

Adulamu

Keila

Hebroni

Zifu

Horeshi

Karmeli

Maoni

En-gedi

Bahari ya Chumvi

[Hisani]

Map: Based on maps copyrighted by Pictorial Archive (Near Eastern History) Est. and Survey of Israel

[Picha katika ukurasa wa 21]

Daudi alilikweza jina la Yehova hata akiwa mkimbizi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Imani yetu inaimarishwa tunaposikiliza mambo yenye kujenga yanayosimuliwa katika makusanyiko yetu ya Kikristo