Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Umpende Yehova . . . kwa Akili Yako Yote”

“Umpende Yehova . . . kwa Akili Yako Yote”

“Umpende Yehova . . . kwa Akili Yako Yote”

YEHOVA alitabiri kufanywa kwa agano jipya na kwamba chini ya agano hilo, roho takatifu ingeongoza kuandikwa kwa sheria za Mungu katika akili na mioyo ya watu wake. (Waebrania 8:10; 10:16) Kwa njia hiyo, wanaweza kutimiza yote ambayo Sheria na Manabii hutegemea, yaani, ‘kumpenda Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kumpenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Mathayo 22:37-40; Luka 10:27, 28) Ni lazima mtu ampende Mungu kwa moyo wake wote (tamaa na hisia za utu wake wa ndani), nafsi yake yote (uhai wake na mwili wake wote), na akili yake yote (uwezo wake wa kufikiri). Maneno hayo ya mwisho yanamaanisha kwamba watumishi wa Mungu hawampendi kwa hisia na nguvu zao tu bali pia wanatumia kwa bidii akili yao ili kupata ujuzi juu ya Mungu na Kristo (Yohana 17:3), kuelewa (Marko 12:33; Waefeso 3:18), kumtumikia Mungu, kutimiza makusudi yake, na kuhubiri habari njema. Wanashauriwa ‘waendelee kukaza akili zao juu ya mambo yaliyo juu’ (Wakolosai 3:2), ‘wakaze akili zao kwa ajili ya utendaji,’ na ‘watunze akili zao kwa ukamili.’ (1 Petro 1:13) Mtume Petro aliona umuhimu wa ‘kuamsha uwezo wao mzuri wa kufikiri’ ili wakumbuke mambo waliyojifunza. (2 Petro 3:1, 2) Ni lazima ‘waweke karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’—2 Petro 3:11, 12.

Akizungumza kuhusu zawadi za kimuujiza za roho katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, Paulo alikazia uhitaji wa kutumia akili. Alisema kwamba ikiwa angesali kwa lugha ambayo hangeweza kuitafsiri, akili yake haingezaa matunda. Pia, ikiwa angeimba sifa kwa lugha, angemsaidia jinsi gani msikilizaji ambaye hakuelewa lugha hiyo? Badala yake, alisema kwamba ingekuwa afadhali aseme maneno matano kwa akili yake, ili awafundishe wengine, kuliko maneno elfu kumi kwa lugha. Aliwahimiza ndugu zake wawe watu wazima katika nguvu za uelewaji.—1 Wakorintho 14:13-20.

Watumishi wa Yehova wanaamriwa ‘waunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.’ (1 Wakorintho 1:10; Wafilipi 2:2; 1 Petro 3:8) Kwa wazi, hilo linamaanisha kuunganishwa inapohusu ibada safi, yaani, mambo yaliyo ya maana, wala si katika mapendezi ya kibinafsi au mambo madogo yanayotatuliwa mtu anapofikia ukomavu. (Waroma 14:2-6, 17) Wanapaswa “wawe na akili moja katika Bwana” (Wafilipi 4:2), wasiwe wakibishana, bali ‘wafikiri kwa upatano.’—2 Wakorintho 13:11.

Wakristo wanapaswa kujitahidi kumjua Mungu vizuri, kwa kadiri ambavyo Mungu amefunua akili yake kuhusu mambo mbalimbali. (Waroma 11:33, 34; 16:25, 26) Wanapaswa pia kuwa na mtazamo wa akilini wa utii na unyenyekevu kama wa Yesu Kristo; hapo ndipo watakapokuwa na “akili ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:15, 16) Petro anashauri hivi: “Kwa kuwa Kristo aliteseka katika mwili, ninyi pia jivikeni silaha ya mwelekeo uleule wa akili.”—1 Petro 4:1.

Kwa sababu Waisraeli waliokuwa kwenye Mlima Sinai hawakuwa wamemgeuzia Yehova mioyo yao kikamili, nguvu zao za akili zilitiwa uzito, na ilikuwa vivyo hivyo kuhusu wale walioendelea kuishi chini ya Sheria baada ya Mungu kuiondoa kupitia Yesu. (2 Wakorintho 3:13, 14) Hawakuona kwamba Yesu ndiye yule aliyetabiriwa na Sheria. (Wakolosai 2:17) Watu ambao hawakukubali kumjua Mungu katika ujuzi sahihi lakini wakaabudu viumbe, “Mungu aliwaacha katika hali ya akili iliyokataliwa”; wamo katika giza kiakili, wakifanya kila namna ya mambo ya ubatili na yasiyo na faida. (Waroma 1:28; Waefeso 4:17, 18) Hata katika siku za Musa, watu waliopotoka kiakili walipinga kweli, na baadaye, watu kama hao walipigana na Ukristo wa kweli, wengine kati yao hata walidai kuwa Wakristo, huku wakijaribu kugawanya na kuvuruga makutaniko. (2 Timotheo 3:8; Wafilipi 3:18, 19; 1 Timotheo 6:4, 5) Wakiwa na akili na dhamiri zilizotiwa unajisi, hakuna kitu ambacho ni safi machoni pao. Hivyo, wanasema mambo yasiyo na faida wakiwa na kusudi la kupotosha akili za Wakristo wa kweli kwa kujaribu kuwafanya wawe watumwa wa mawazo ya wanadamu. (Tito 1:10-16) Kwa sababu hiyo, ni muhimu Wakristo wote, na hasa wale walio na mapendeleo wawe timamu katika akili.Waroma 12:3; 1 Timotheo 3:2; Tito 2:6; 1 Petro 4:7.