Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Hana Alivyopata Amani

Jinsi Hana Alivyopata Amani

Jinsi Hana Alivyopata Amani

MWANAMKE mmoja mwaminifu anamsifu Yehova katika sala kwa sauti. Anahisi kwamba Mungu amemwinua kutoka katika mavumbi na kumkweza na hivyo kumfanya aache kudharauliwa.

Jina la mwanamke huyo ni Hana. Ni nini ambacho kimebadili sana hisia zake? Kwa nini yeye ni mwenye shangwe nyingi sasa? Tunaweza kufaidika kwa njia gani kutokana na mambo yaliyompata? Ili tupate majibu ya maswali hayo, acheni tuchunguze kisa cha Hana.

Familia Yenye Matatizo

Hana ni mmoja wa wake wawili wa Elkana, Mlawi anayeishi katika eneo la Efraimu. (1 Samweli 1:1, 2a; 1 Mambo ya Nyakati 6:33, 34) Ingawa Mungu hakukusudia mume awe na wake wengi, chini ya Sheria ya Musa, ndoa za wake wengi zinaruhusiwa na kanuni za kufuatwa katika ndoa hizo zimetolewa. Familia ya Elkana inamwabudu Yehova, lakini kwa kawaida ndoa za wake wengi zinaleta matatizo, kama hali ya familia ya Elkana inavyoonyesha.

Hana ni mwanamke tasa, lakini Penina, yule mke mwingine wa Elkana, ana watoto kadhaa. Penina anashindana na Hana.—1 Samweli 1:2b.

Mwanamke tasa anadharauliwa miongoni mwa wanawake wa Israeli na hata watu wanaona kwamba kuwa tasa kunaonyesha mtu hastahili machoni pa Mungu. Lakini hakuna jambo linaloonyesha kwamba hali ya Hana ya kutoweza kupata watoto inathibitisha kwamba hana kibali cha Mungu. Hata hivyo, badala ya kujaribu kumfariji Hana, Penina anatumia uwezo wake wa kupata watoto kumuumiza kihisia mke mwenzake.

Safari za Kwenda Patakatifu pa Yehova

Hali hiyo ni yenye kufadhaisha, hata hivyo familia ya Elkana inafunga safari kila mwaka ili kutoa dhabihu katika patakatifu pa Yehova huko Shilo. * Inaelekea kwamba wanasafiri kwa miguu safari hiyo ya kilomita 60 hivi kwenda na kurudi. Haikosi kwamba hizo ni pindi ngumu hasa kwa Hana kwa sababu Penina na watoto wake wanapewa mafungu kadhaa ya dhabihu ya ushirika, lakini Hana anapewa fungu moja tu. Penina anatumia nafasi kama hizo kumsumbua Hana, akimfanya akasirike kwa sababu inaonekana kwamba Yehova “amefunga tumbo lake la uzazi.” Hana anateseka hivyo mwaka baada ya mwaka, na hilo linamfanya Hana alie na asile chakula. Safari ambazo zinapaswa kumletea shangwe zinamhuzunisha sana. Hata hivyo, Hana anafunga safari hizo za kwenda patakatifu pa Yehova.—1 Samweli 1:3-7.

Je, unaona jinsi Hana alivyotuwekea mfano mzuri? Unafanya nini unapovunjika moyo? Je, unajitenga na wengine na kuacha kushirikiana na waamini wenzako? Hana hakufanya hivyo. Alikuwa na desturi ya kuwa kati ya waabudu wa Yehova. Tunapokabili hali ngumu, sisi pia tunapaswa kufanya hivyo.—Zaburi 26:12; 122:1; Methali 18:1; Waebrania 10:24, 25.

Elkana anajaribu kumfariji Hana na kumhimiza afunue yaliyo moyoni mwake. “Hana, kwa nini unalia, na kwa nini huli chakula, na kwa nini moyo wako unahisi vibaya?” anamuuliza. “Je, mimi si bora kwako kuliko wana kumi?” (1 Samweli 1:8) Labda Elkana hajui kwamba Penina anamtendea Hana kwa njia isiyo ya fadhili, na huenda Hana anaona ni afadhali ateseke kimyakimya badala ya kulalamika. Vyovyote vile, Hana ambaye anathamini mambo ya kiroho, anatafuta amani kwa kumwendea Yehova katika sala.

Hana Anaweka Nadhiri

Dhabihu za ushirika zililiwa katika patakatifu pa Yehova. Baada ya kuondoka katika chumba cha kulia chakula, Hana anasali kwa Mungu. (1 Samweli 1:9, 10) “Ee Yehova wa majeshi,” Hana anasihi, “ikiwa hakika utayaona mateso ya kijakazi wako, nawe kwa kweli unikumbuke, na ikiwa hutamsahau kijakazi wako na kwa kweli umpe kijakazi wako uzao wa kiume, mimi nitamtoa kwa Yehova siku zote za maisha yake, wala wembe hautapita juu ya kichwa chake.”—1 Samweli 1:11.

Hana anataja mambo hususa katika sala. Anaomba mtoto wa kiume na kuweka nadhiri kwamba mtoto huyo atawekwa wakfu kwa Yehova na kuwa Mnadhiri maisha yake yote. (Hesabu 6:1-5) Nadhiri kama hiyo inategemea kibali cha mume wake, na mambo ambayo Elkana anafanya baadaye yanaonyesha kwamba anakubali ahadi ya mke wake mpendwa.—Hesabu 30:6-8.

Hana anatoa sala kwa njia ambayo inamfanya Kuhani Mkuu Eli afikiri kwamba Hana amelewa. Midomo yake inatetemeka, lakini Eli hasikii sauti yoyote, kwa kuwa Hana anasali moyoni mwake. Anasali kwa bidii sana. (1 Samweli 1:12-14) Wazia jinsi Hana anavyohisi Eli anapomshtumu kwamba amelewa! Hata hivyo, anamjibu kuhani huyo mkuu kwa heshima. Eli anapotambua kwamba Hana amekuwa akisali “kutokana na wingi wa mahangaiko [yake] na usumbufu [wake],” anasema: “Mungu wa Israeli akupe ombi lako.” (1 Samweli 1:15-17) Baada ya hapo, Hana anaenda zake na kula chakula, na ‘uso wake hauonyeshi tena kuhangaika.’—1 Samweli 1:18.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo hayo yote? Tunaposali kwa Yehova kuhusu mahangaiko yetu, tunaweza kumwambia jinsi tunavyohisi na kusali kutoka moyoni kuhusu kile tunachotaka. Ikiwa hatuwezi kufanya jambo lingine lolote ili kutatua tatizo hilo, tunapaswa kuacha mambo mikononi mwake. Hakuna njia iliyo bora kuliko hiyo.—Methali 3:5, 6.

Baada ya kusali kwa bidii, inaelekea sana kwamba watumishi wa Yehova watakuwa na amani kama ile ya Hana. Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu sala: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Tunapomtupia Yehova mzigo wetu, tunapaswa kumwachia ili auchukue. Kisha, kama Hana, hatuhitaji kuendelea kuhangaika.—Zaburi 55:22.

Yehova Anaazimwa Mwana

Sasa Mungu anamgeuzia Hana fikira; naye anapata mimba na kuzaa mwana. (1 Samweli 1:19, 20) Pindi hii ni moja kati ya pindi chache katika masimulizi ya Biblia ambapo Mungu anasababisha kuzaliwa kwa mtu ambaye atakuwa mtumishi wake. Samweli, mwana wa Elkana na Hana, atakuwa nabii wa Yehova, ambaye atahusika sana katika kusimamisha ufalme wa Israeli.

Hapana shaka kwamba tangu Samweli akiwa mtoto mchanga, Hana anaanza kumfundisha kumhusu Yehova. Lakini je, anasahau nadhiri aliyoweka? Bila shaka hapana! “Mara mvulana huyu atakapoachishwa kunyonya, nitampeleka, naye ataonekana mbele za Yehova na kukaa huko mpaka wakati usio na kipimo,” anasema. Samweli anapoachishwa kunyonya, labda akiwa na miaka mitatu au zaidi, Hana anampeleka ili aishi katika patakatifu pa Yehova, kama tu alivyoahidi katika nadhiri.—1 Samweli 1:21-24; 2 Mambo ya Nyakati 31:16.

Baada ya dhabihu kutolewa kwa Yehova, Hana na mume wake wanampeleka Samweli kwa Eli. Inaelekea sana kwamba Hana anamshika mkono mvulana huyo mdogo huku akimwambia Eli hivi: “Nakuomba radhi, bwana wangu! Kama inavyoishi nafsi yako, bwana wangu, mimi ndiye yule mwanamke aliyekuwa amesimama pamoja nawe mahali hapa ili kusali kwa Yehova. Ilikuwa kuhusu mvulana huyu kwamba nilisali ili Yehova anipe ombi langu nililomwomba. Na mimi nimemwazima Yehova mvulana huyu. Siku zote atakazokuwapo, yeye ni mtu aliyeombwa kwa ajili ya Yehova.” Hivyo ndivyo maisha ya Samweli ya utumishi wa pekee kwa Mungu yanavyoanza.—1 Samweli 1:25-28; 2:11.

Kadiri muda unavyopita, Hana hamsahau Samweli kamwe. Maandiko yanasema: “Mama yake alikuwa akimfanyizia koti dogo lisilo na mikono, na kumletea mwaka baada ya mwaka alipopanda pamoja na mume wake ili kutoa dhabihu ya kila mwaka.” (1 Samweli 2:19) Kwa kweli Hana anaendelea kusali kwa ajili ya Samweli. Bila shaka, kila mwaka anapomtembelea Samweli, Hana anamtia moyo aendelee kuwa mwaminifu katika kumtumikia Mungu.

Pindi moja kama hiyo, Eli anawabariki wazazi wa Samweli na kumwambia Elkana hivi: “Yehova na akupe uzao kutoka kwa mke huyu badala ya kile kitu cha kuazima, ambacho Yehova aliazimwa.” Kupatana na maneno hayo, Hana na Elkana wanabarikiwa kuwa na wana wengine watatu na binti wawili.—1 Samweli 2:20, 21.

Elkana na Hana ni mifano mizuri kama nini kwa wazazi Wakristo! Akina mama na baba wengi wamekuwa tayari kumwazima Yehova wana na binti zao, kwa njia ya mfano, kwa kuwahimiza wafuatilie aina fulani ya utumishi wa wakati wote mbali na nyumbani. Wazazi wenye upendo kama hao wanastahili kupongezwa kwa dhabihu wanazotoa. Na Yehova atawapa thawabu.

Sala Yenye Shangwe ya Hana

Sasa Hana ambaye hapo awali alikuwa tasa, ni mwenye shangwe iliyoje! Ni sala chache zilizotolewa na wanawake ambazo zimeandikwa katika Maandiko. Hata hivyo, tunajulishwa kuhusu sala mbili ambazo Hana alitoa. Ya kwanza inahusu hisia zake aliposumbuliwa na kuteswa, na ya pili ni sala ya shukrani yenye furaha. Hana anaanza hivi: “Moyo wangu unafurahi katika Yehova.” Anashangilia kwamba “hata aliye tasa amezaa,” na anamtukuza Yehova kuwa “Mwenye Kuinua mtu wa hali ya chini kutoka mavumbini.” Kwa kweli, “humwinua maskini kutoka katika shimo la majivu.”—1 Samweli 2:1-10.

Simulizi la Hana ambalo liliongozwa na roho linaonyesha kwamba tunaweza kuumizwa kihisia na udhaifu wa watu wengine au dhihaka zao. Hata hivyo, hatupaswi kuruhusu majaribu kama hayo yatuondolee shangwe yetu ya kumtumikia Yehova. Yeye ndiye Msikiaji mkuu wa sala, ambaye anajibu vilio vya watu wake waaminifu, akiwakomboa kutoka katika mateso na kuwapa amani tele na baraka nyingine nyingi.—Zaburi 22:23-26; 34:6-8; 65:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Biblia inaita kitovu hicho cha ibada ya kweli “hekalu” la Yehova. Lakini katika kipindi hiki cha historia ya Waisraeli, sanduku la agano bado liko katika hema, au maskani. Hekalu la kwanza la kudumu la Yehova litajengwa wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani.—1 Samweli 1:9; 2 Samweli 7:2, 6; 1 Wafalme 7:51; 8:3, 4.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Hana alimwazima Yehova Samweli