Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Malaika Wanavyohusika Katika Maisha ya Wanadamu

Jinsi Malaika Wanavyohusika Katika Maisha ya Wanadamu

Jinsi Malaika Wanavyohusika Katika Maisha ya Wanadamu

“Baada ya mambo haya nikamwona malaika mwingine akishuka kutoka mbinguni, mwenye mamlaka kubwa . . . Naye akapaaza kilio kwa sauti yenye nguvu, akisema: ‘Ameanguka! Babiloni Mkubwa ameanguka!’”—UFUNUO 18:1, 2.

1, 2. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anawatumia malaika kutekeleza mapenzi yake?

AKIWA uhamishoni kwenye kisiwa cha Patmo, mtume Yohana aliyezeeka anapata pendeleo la kuonyeshwa maono ya kinabii. Anaona matukio yenye kusisimua ‘anapoongozwa na roho’ na kuwa katika “siku ya Bwana.” Siku hiyo inaanza Yesu Kristo anapowekwa kuwa mfalme mwaka wa 1914 na inaendelea mpaka mwisho wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja.—Ufunuo 1:10.

2 Yehova Mungu hakumpa Yohana ufunuo huo moja kwa moja. Alitumia njia nyingine. Andiko la Ufunuo 1:1 linasema: “Ufunuo kupitia Yesu Kristo, ambao Mungu alimpa, kuwaonyesha watumwa wake mambo ambayo lazima yatendeke upesi. Naye alimtuma malaika wake na kupitia yeye akautoa kwa njia ya ishara kwa mtumwa wake Yohana.” Yehova, kupitia Yesu, alitumia malaika kumjulisha Yohana mambo ya kustaajabisha kuhusu “siku ya Bwana.” Wakati fulani, Yohana ‘alimwona malaika mwingine akishuka kutoka mbinguni, mwenye mamlaka kubwa.’ Malaika huyo alikuwa na mgawo gani? “Akapaaza kilio kwa sauti yenye nguvu, akisema: ‘Ameanguka! Babiloni Mkubwa ameanguka!’” (Ufunuo 18:1, 2) Malaika huyo mwenye nguvu alikuwa na pendeleo la kutangaza kuhusu kuanguka kwa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Basi, hakuna shaka kwamba Yehova anawatumia malaika kwa njia muhimu ili kutekeleza kusudi lake. Kabla ya kuchunguza kwa undani jukumu la malaika katika kusudi la Mungu na jinsi wanavyohusika katika maisha yetu, acheni tuchunguze jinsi viumbe hao wa roho walivyotokea.

Malaika Walitoka Wapi?

3. Watu wengi wana maoni gani yenye makosa kuhusu malaika?

3 Mamilioni ya watu leo wanaamini kwamba kuna malaika. Lakini wengi wana maoni yenye makosa kuhusu mahali ambapo malaika walitoka. Kwa mfano, watu fulani wa kidini wanafikiri kwamba mpendwa wao anapokufa anaitwa ili ajiunge na Mungu, na hivyo anakuwa malaika. Je, hivyo ndivyo Neno la Mungu linavyofundisha kuhusu kuumbwa, kuwapo, na kusudi la malaika?

4. Maandiko yanatuambia malaika walitoka wapi?

4 Malaika mwenye nguvu na mamlaka nyingi zaidi, aliye mkuu kuliko wote anaitwa Mikaeli, yule malaika mkuu. (Yuda 9) Malaika huyo si mwingine ila ni Yesu Kristo. (1 Wathesalonike 4:16) Miaka mingi sana iliyopita, Yehova alipokusudia kuwa Muumba, alianza uumbaji wake kwa kumuumba Mwana huyo wa kimalaika. (Ufunuo 3:14) Baadaye, kupitia Mwana huyo mzaliwa wa kwanza, Yehova aliumba viumbe wengine wote wa roho. (Wakolosai 1:15-17) Akiwaita viumbe hao wa kimalaika kuwa wanawe, Yehova alimuuliza hivi Ayubu yule mzee wa ukoo: “Ulikuwa wapi nilipoweka msingi wa dunia? Niambie, ikiwa unaelewa. . . . Ni nani aliyeweka jiwe lake la pembeni, nyota za asubuhi zilipopiga vigelegele pamoja kwa shangwe, na wana wote wa Mungu wakaanza kupaaza sauti kwa kushangilia?” (Ayubu 38:4, 6, 7) Ni wazi kwamba malaika waliumbwa na Mungu muda mrefu kabla ya wanadamu kuumbwa.

5. Malaika wamepangwa namna gani?

5 Andiko la 1 Wakorintho 14:33 linasema kwamba “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.” Kwa hiyo, Yehova amewapanga wanawe wa roho katika makundi matatu makuu: (1) maserafi, ambao ni watumishi kwenye kiti cha Ufalme cha Mungu, wanatangaza utakatifu wake, na kuhakikisha kwamba watu wake wako safi kiroho; (2) makerubi, ambao wanategemeza enzi kuu ya Yehova; na (3) malaika wengine ambao wanatenda mapenzi yake. (Zaburi 103:20; Isaya 6:1-3; Ezekieli 10:3-5; Danieli 7:10) Jeshi hilo kubwa la viumbe wa roho linahusika jinsi gani katika maisha ya wanadamu?—Ufunuo 5:11.

Malaika Wana Majukumu Gani?

6. Yehova aliwatumia makerubi jinsi gani katika bustani ya Edeni?

6 Viumbe wa roho wanatajwa kwa mara ya kwanza na kwa njia ya moja kwa moja katika andiko la Mwanzo 3:24, ambalo linasema hivi: “[Yehova] akamfukuza huyo mtu, akaweka upande wa mashariki wa bustani ya Edeni makerubi na upanga unaowaka ambao ulikuwa unajizungusha-zungusha ili kuilinda njia ya kwenda kwenye ule mti wa uzima.” Makerubi hao hawangeruhusu Adamu na Hawa warudi tena katika bustani ambayo ilikuwa makao yao ya kwanza. Hilo lilitukia mwanzoni mwa historia ya wanadamu. Malaika wametimiza majukumu gani tangu wakati huo?

7. Maana ya neno “malaika” katika lugha za awali inaonyesha nini kuhusu moja ya majukumu yao?

7 Malaika wanatajwa karibu mara 400 katika Biblia. Katika Kiebrania na Kigiriki, neno “malaika” linaweza kutafsiriwa kuwa “mjumbe.” Kwa hiyo, Mungu amewatumia malaika kama njia yake ya kuwapasha wanadamu habari. Kama mafungu mawili ya kwanza ya habari hii yanavyosema, Yehova alimtumia malaika kupeleka ujumbe wake kwa mtume Yohana.

8, 9. (a) Manoa na mke wake walihisi namna gani baada ya kutembelewa na malaika? (b) Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Manoa kutembelewa na malaika wa Mungu?

8 Malaika wanatumiwa pia kuwategemeza na kuwatia moyo watumishi wa Mungu duniani. Kwa mfano, nyakati za Waamuzi katika Israeli, Manoa na mke wake aliyekuwa tasa walitamani sana kupata mtoto. Yehova alimtuma malaika wake amjulishe mke wa Manoa kwamba angepata mwana. Simulizi hilo linatuambia hivi: “Tazama! utachukua mimba, nawe utazaa mwana, na wembe wowote usipite juu ya kichwa chake, kwa maana mtoto huyo atakuwa Mnadhiri wa Mungu tangu atakapotoka tumboni; naye ndiye atakayeongoza katika kuokoa Israeli kutoka mkononi mwa Wafilisti.”—Waamuzi 13:1-5.

9 Mwishowe, mke wa Manoa alizaa mwana aliyeitwa Samsoni, ambaye alikuja kujulikana sana katika historia ya Biblia. (Waamuzi 13:24) Kabla mtoto huyo hajazaliwa, Manoa aliomba ili yule malaika arudi na kuwafundisha jinsi ambavyo walipaswa kumlea mvulana huyo. Manoa aliuliza hivi: “Mtoto huyo ataishi maisha ya aina gani, naye atafanya kazi gani?” Malaika wa Yehova alirudia kutaja maagizo ambayo alikuwa amempa mke wa Manoa. (Waamuzi 13:6-14) Hapana shaka kwamba Manoa alitiwa moyo sana! Malaika hawamtembelei mtu mmoja-mmoja kwa njia hiyo leo, lakini kama Manoa, wazazi wanaweza kutafuta maagizo ya Yehova kuhusu kuwazoeza watoto wao.—Waefeso 6:4.

10, 11. (a) Elisha na mtumishi wake walihisi namna gani walipozungukwa na jeshi la Siria? (b) Tunaweza kupata faida gani tukitafakari tukio hilo?

10 Mfano wa utegemezo mkubwa wa kimalaika ulionekana wazi katika siku za nabii Elisha. Elisha alikuwa akikaa katika jiji la Dothani, huko Israeli. Siku moja mtumishi wa Elisha alipoamka asubuhi na mapema na kutazama nje, aliona jiji limezungukwa na farasi na magari ya vita. Mfalme wa Siria alikuwa ametuma jeshi lenye nguvu limkamate Elisha. Mtumishi wa Elisha alifanya nini? Kwa woga, na labda akiwa ameshtuka, alipaaza kilio: “Ole, bwana wangu! Tutafanya nini?” Kwa maoni yake, hakukuwa na tumaini lolote la kuokoka. Lakini Elisha akamjibu hivi: “Usiogope, kwa maana wale walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” Alimaanisha nini?—2 Wafalme 6:11-16.

11 Elisha alijua kwamba majeshi ya malaika yalikuwapo ili yamtegemeze. Hata hivyo, mtumishi wake hakuona chochote. Kwa hiyo, “Elisha akaanza kusali na kusema: ‘Ee Yehova, tafadhali fungua macho yake, ili aone.’ Mara moja Yehova akafungua macho ya yule mtumishi, hivi kwamba akaona; na, tazama! lile eneo lenye milima lilikuwa limejaa farasi na magari ya vita ya moto kumzunguka Elisha pande zote.” (2 Wafalme 6:17) Basi mtumishi huyo angeweza kuona majeshi ya malaika. Kwa macho ya kiroho, sisi pia tunaweza kutambua kwamba malaika, wote wakiwa chini ya mwelekezo wa Yehova na wa Kristo, wanawategemeza na kuwalinda watu wa Yehova.

Utegemezo wa Kimalaika Nyakati za Kristo

12. Malaika Gabrieli alimtegemeza Maria jinsi gani?

12 Fikiria utegemezo ambao bikira Myahudi aliyeitwa Maria alipata alipoambiwa hivi: “Utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu.” Kabla tu ya kumpa ujumbe huo wenye kushangaza, malaika Gabrieli, ambaye alitumwa na Mungu, alimwambia Maria hivi: “Usiogope, Maria, kwa maana umepata kibali cha Mungu.” (Luka 1:26, 27, 30, 31) Bila shaka, Maria alitiwa moyo na kuimarishwa sana na maneno hayo ambayo yalimhakikishia kwamba alikuwa na kibali cha Mungu.

13. Malaika walimtegemeza Yesu jinsi gani?

13 Kisa kingine cha utegemezo wa kimalaika kilitokea baada ya Yesu kushinda majaribu matatu ambayo Shetani alimletea akiwa nyikani. Simulizi hilo linatuambia kwamba baada ya majaribu hayo, ‘Ibilisi alimwacha, na, tazama! malaika wakaja na kuanza kumhudumia.’ (Mathayo 4:1-11) Jambo kama hilo lilitukia usiku ambao Yesu alikufa. Kwa uchungu, Yesu alipiga magoti na kuanza kusali, akisema: “‘Baba, ikiwa unataka, niondolee kikombe hiki. Hata hivyo, acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.’ Ndipo malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.” (Luka 22:42, 43) Lakini malaika wanatutegemeza leo kwa njia gani?

Utegemezo wa Kimalaika Katika Nyakati za Kisasa

14. Mashahidi wa Yehova wamepata mateso gani katika nyakati za kisasa, na matokeo yamekuwa nini?

14 Tunapofikiria historia ya kisasa ya kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova, je, hatuoni uthibitisho unaoonyesha kwamba malaika wamekuwa wakitutegemeza? Kwa mfano, watu wa Yehova waliweza kuvumilia mashambulizi ya Wanazi nchini Ujerumani na huko Ulaya Magharibi kabla na wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu (1939-1945). Wakati wa tawala za Kifashisti za Kikatoliki nchini Italia, Hispania, na Ureno, watu wa Yehova walivumilia mateso kwa muda mrefu hata zaidi. Na kwa makumi ya miaka, walivumilia mateso katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti na mataifa yaliyoshirikiana na muungano huo. Kwa kuongezea, Mashahidi wamevumilia mateso katika nchi fulani za Afrika. * Katika nyakati za karibuni zaidi, watumishi wa Yehova wameteswa kikatili katika nchi ya Georgia. Shetani amefanya yote anayoweza ili kukomesha utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, wakiwa tengenezo, wameokoka upinzani huo nao wamesitawi. Moja ya mambo ambayo yamewasaidia ni ulinzi kutoka kwa malaika.—Zaburi 34:7; Danieli 3:28; 6:22.

15, 16. Malaika wanawategemeza jinsi gani Mashahidi wa Yehova katika huduma yao ya ulimwenguni pote?

15 Mashahidi wa Yehova wanachukua kwa uzito kazi waliyopewa ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote, na kufanya wanafunzi kwa kuwafundisha kweli ya Biblia watu wote wanaopendezwa. (Mathayo 28:19, 20) Hata hivyo, wanajua vizuri kwamba hawawezi kutimiza kazi hiyo bila kutegemezwa na malaika. Kwa hiyo, wametiwa moyo sikuzote na maneno ya Ufunuo 14:6, 7. Andiko hilo linasema hivi: “Nami [mtume Yohana] nikamwona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu, akisema kwa sauti kubwa: ‘Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika, na kwa hiyo mwabuduni Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na chemchemi za maji.’”

16 Maneno hayo yanaonyesha wazi kwamba kazi kubwa ya Mashahidi wa Yehova ya kueneza Injili ulimwenguni pote inategemezwa na kuongozwa na malaika. Yehova anatumia malaika wake kuwaongoza watu wanyoofu kwa Mashahidi wake. Malaika pia wamewaongoza Mashahidi kwa watu wanaostahili. Hilo linaonyesha kwa nini mara nyingi sana kuliko tunavyoweza kutazamia, Shahidi wa Yehova anakutana na mtu kwa wakati unaofaa kabisa mtu huyo anapokuwa na matatizo na anahitaji msaada wa kiroho.

Malaika Watatimiza Jukumu la Pekee Hivi Karibuni

17. Matokeo yalikuwa nini Waashuru waliposhambuliwa na malaika mmoja tu?

17 Malaika wanatimiza kusudi lingine kwa kuongezea jukumu lao wakiwa wajumbe na msaada wenye kutia nguvu kwa waabudu wa Yehova. Katika nyakati zilizopita, walitekeleza hukumu za Mungu. Kwa mfano, huko nyuma katika karne ya nane K.W.K., Yerusalemu lilitishwa na kikosi kikubwa cha askari-jeshi Waashuru. Yehova alifanya nini? Alisema hivi: “Nami hakika nitalilinda jiji hili ili kuliokoa kwa ajili yangu mwenyewe na kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu.” Simulizi hilo la Biblia linatuambia jambo lililotukia: “Ikawa kwamba usiku huo malaika wa Yehova alitoka, akapiga na kuwaua watu 185,000 katika kambi ya Waashuru. Watu walipoamka asubuhi na mapema, tazama, wote walikuwa mizoga iliyokufa.” (2 Wafalme 19:34, 35) Majeshi ya wanadamu yana uwezo mdogo kama nini ukilinganishwa na uwezo wa malaika mmoja tu!

18, 19. Malaika watatimiza jukumu gani la pekee hivi karibuni, na hilo litakuwa na matokeo gani kwa wanadamu?

18 Hivi karibuni malaika watatumika wakiwa jeshi la Mungu la kutekeleza hukumu. Hivi karibuni sana, Yesu atakuja “pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto.” Kusudi lao litakuwa ‘kuleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.’ (2 Wathesalonike 1:7, 8) Hatua hiyo itakuwa na matokeo makubwa kama nini kwa wanadamu! Wale wanaokataa kukubali habari njema ya Ufalme wa Mungu inayotangazwa leo duniani pote wataharibiwa. Ni wale tu ambao wanamtafuta Yehova, wanatafuta uadilifu na upole ndio ‘watakaofichwa katika siku ya hasira ya Yehova.’—Sefania 2:3.

19 Tunaweza kushukuru kwamba Yehova anawatumia malaika wake wenye nguvu kuwategemeza na kuwatia nguvu waabudu wake duniani. Inafariji hasa kujua majukumu ambayo malaika wanatimiza katika kusudi la Mungu, kwa kuwa kuna malaika ambao wamemwasi Yehova na wamekuwa chini ya uongozi wa Shetani. Habari inayofuata itazungumzia hatua ambazo Wakristo wa kweli wanaweza kuchukua ili kujilinda kutokana na uvutano wenye nguvu wa Shetani Ibilisi na roho wake waovu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kwa masimulizi kamili kuhusu mateso hayo, ona Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha Kiingereza au cha Kifaransa cha 1983 (Angola), 1972 (Chekoslovakia), 2000 (Jamhuri ya Cheki), 1992 (Ethiopia), 1974 na 1999 (Ujerumani), 1982 (Italia), 1999 (Malawi), 2004 (Moldova), 1996 (Msumbiji), 1994 (Poland), 1983 (Ureno), 1978 (Hispania), 2002 (Ukrainia), na 2006 (Zambia).

Umejifunza Nini?

• Malaika walitoka wapi?

• Malaika walitumiwa namna gani katika nyakati za Biblia?

• Andiko la Ufunuo 14:6, 7 linafunua nini kuhusu utendaji wa malaika leo?

• Malaika watatimiza jukumu gani la pekee hivi karibuni?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Manoa na mke wake walitiwa moyo na malaika

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Wale walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao”