Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kile Ambacho Kuja Kwa Kristo Kutatimiza

Kile Ambacho Kuja Kwa Kristo Kutatimiza

Kile Ambacho Kuja Kwa Kristo Kutatimiza

“HOFU JIJINI SÃO PAULO.” Hivyo ndivyo gazeti moja (Veja) lilivyosema kuhusu siku nne katika mwezi wa Mei (Mwezi wa 5) 2006 wakati magenge ya uhalifu yalipovuruga kabisa shughuli zote katika jiji kuu na tajiri zaidi huko Brazili. Katika “maasi hayo yaliyochukua zaidi ya saa 100,” maofisa 150 hivi wa kutekeleza sheria, wahalifu, na raia wa kawaida waliuawa.

Visa vya ujeuri vinatangazwa sana katika vyombo vya habari kotekote duniani. Inaonekana kwamba viongozi wa kibinadamu hawawezi kuvikomesha. Ulimwengu wetu unazidi kuwa mahali hatari pa kuishi. Huenda unavunjika moyo kwa sababu kuna habari mbaya kila mahali. Hata hivyo, wakati wa mabadiliko unakaribia.

Yesu aliwafundisha wafuasi wake kusali Ufalme wa Mungu uje ili mapenzi ya Mungu yatendeke “duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Ufalme huo ni serikali ambayo inaongozwa na Kristo Yesu ambaye ndiye Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu. Itatatua matatizo yote ya wanadamu. Hata hivyo, ili Ufalme wa Mungu ulete mabadiliko duniani, ni lazima utawala wa wanadamu uondolewe na mahali pake pachukuliwe na utawala wa Kristo. Hilo hasa ndilo jambo ambalo kuja kwa Kristo kutatimiza.

Je, Mabadiliko Hayo Yatafanywa kwa Amani?

Je, mataifa yatakubali kujitiisha kwa amani chini ya utawala wa Kristo? Mtume Yohana alipewa maono ambayo yanajibu swali hilo. Yohana anasema hivi: “Nami nikamwona yule mnyama-mwitu [mfumo wa kisiasa wa ulimwengu] na wafalme wa dunia na majeshi yao wamekusanyika pamoja ili kupigana vita na [Yesu] anayeketi juu ya farasi na jeshi lake.” (Ufunuo 19:19) Ni nini kitakachotukia kwa wafalme wa dunia katika vita hivyo? Biblia inasema kwamba Mfalme mtiwa-mafuta wa Yehova ‘atawavunja kwa fimbo ya chuma ya enzi, atawavunja vipande-vipande, kama chombo cha mfinyanzi.’ (Zaburi 2:9) Mfumo wa kisiasa utapondwa kabisa. Ufalme wa Mungu “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za kibinadamu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.

Namna gani watu ambao wanapinga Ufalme wa Mungu? “Wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto,” Yesu anaonyeshwa akiwa mtu ‘anayeleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.’ (2 Wathesalonike 1:7, 8) Andiko la Methali 2:22 linasema hivi: “Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.”

Kuhusu kuja kwa Kristo, Biblia inasema hivi: “Tazama! Anakuja na mawingu, na kila jicho litamwona.” (Ufunuo 1:7) Watu hawatamwona kwa macho yao halisi. Tangu alipopanda mbinguni, Yesu ni mtu wa roho “anayekaa katika nuru isiyoweza kufikiwa, ambaye hakuna hata mmoja kati ya wanadamu amemwona au anaweza kumwona.”—1 Timotheo 6:16.

Yesu hahitaji kuja na mwili wa kibinadamu ili ‘aonwe’ na wakaaji wa dunia kama vile Yehova hakuhitaji kuonekana kihalisi alipoleta Mapigo Kumi juu ya Wamisri katika siku za Musa. Watu wa wakati huo hawakuwa na shaka kwamba Yehova ndiye aliyesababisha mapigo hayo na walilazimika kutambua nguvu zake. (Kutoka 12:31) Vivyo hivyo, Kristo anapochukua hatua akiwa Mtekelezaji wa Hukumu wa Mungu, waovu watalazimika ‘kumwona,’ au kutambua, kwamba Yesu anatumiwa na Mungu kuwahukumu. Watajua hilo kwa sababu wanadamu watakuwa wameonywa kimbele. Ndiyo, “kila jicho litamwona [Yesu], na makabila yote ya dunia yatajipiga-piga kwa huzuni kwa sababu yake.”—Ufunuo 1:7.

Kuharibiwa kwa waovu na kuondolewa kwa utawala mwovu ni hatua muhimu zinazohitaji kuchukuliwa kabla amani ya kweli na ufanisi kurudishwa duniani. Kristo atatimiza hayo. Kisha, atakuwa na mamlaka kamili juu ya shughuli zote duniani, na mabadiliko makubwa yatafuata.

Kurudishwa Ambako Kunaleta Faida

Mtume Petro alizungumza kuhusu “kurudishwa kwa mambo yote ambayo Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu wa nyakati za kale.” (Matendo 3:21) Kurudishwa huko kunahusu mabadiliko yatakayotukia duniani wakati wa utawala wa Kristo. Nabii Isaya aliyeishi katika karne ya nane K.W.K., alikuwa mmoja wa manabii ambao Mungu alitumia kusema kuhusu “kurudishwa kwa mambo yote” duniani. Alitabiri kwamba Yesu Kristo, yule “Mkuu wa Amani,” angerudisha amani duniani. Kuhusu utawala wa Kristo, unabii wa Isaya unasema hivi: “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.” (Isaya 9:6, 7) Yesu atawafundisha watu wa dunia njia za amani. Wale wanaokaa duniani “watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

Je, kutakuwa na umaskini na njaa chini ya utawala wa Kristo? Isaya alisema hivi: “Yehova wa majeshi hakika atavifanyia vikundi vyote vya watu, katika mlima huu, karamu ya vyakula vinono vilivyotiwa mafuta, karamu ya divai iliyowekwa kwenye machicha, ya vyakula vinono vilivyotiwa mafuta vilivyojazwa urojorojo, ya divai iliyowekwa kwenye machicha, iliyochujwa.” (Isaya 25:6) Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Zaidi ya hayo, tunasoma hivi kuhusu wakaaji wa dunia: “Na hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale. Kwa maana siku za watu wangu zitakuwa kama siku za mti; na watu wangu waliochaguliwa wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.”—Isaya 65:21, 22.

Isaya alitabiri pia mwisho wa magonjwa na kifo. Mungu alisema hivi kupitia Isaya: “Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.” (Isaya 35:5, 6) Kisha, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Mungu “kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.

Namna gani wafu wote “waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho”? (Yohana 5:28, 29) Isaya alitabiri hivi: “Wafu wako wataishi. . . . Wataamka.” (Isaya 26:19) Ndiyo, wale wanaolala katika kifo watafufuliwa!

“Mungu Ni Kiti Chako cha Ufalme Milele”

Kuja kwa Kristo kutamaanisha kurudishwa kabisa kwa hali nzuri Duniani. Dunia itabadilishwa na kuwa paradiso tukufu, na wanadamu wataunganishwa katika ibada ya Mungu wa kweli. Je, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu Kristo atafaulu kuondoa uovu duniani na kuleta hali za uadilifu?

Fikiria chanzo cha nguvu na mamlaka ambayo Yesu amepewa. Biblia inasema hivi kumhusu Mwana huyo: “Mungu ni kiti chako cha ufalme milele na milele, na fimbo ya enzi ya ufalme wako ni fimbo ya unyoofu. Uliupenda uadilifu, nawe ukauchukia uasi-sheria.” (Waebrania 1:8, 9) Kiti cha ufalme cha Yesu, yaani, cheo au mamlaka yake, kinatoka kwa Yehova. Mungu ndiye Mwanzilishi na Mwenye Kutoa kiti hicho. Hakuna tatizo ambalo Yesu hataweza kutatua.

Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mathayo 28:18) Andiko la 1 Petro 3:22 linasema hivi: “Malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.” Hakuna nguvu wala mamlaka itakayofanikiwa kumpinga Yesu. Hakuna kitu kinachoweza kumzuia asiwaletee wanadamu faida za kudumu.

Jinsi Kuja kwa Kristo Kunavyowahusu Watu

Katika barua yake kwa Wathesalonike, mtume Paulo aliandika hivi: “Daima sisi hukumbuka akilini kazi yenu ya uaminifu na kazi yenu ya jasho yenye upendo na uvumilivu wenu kwa sababu ya tumaini lenu katika Bwana wetu Yesu Kristo mbele za Mungu wetu na Baba.” (1 Wathesalonike 1:3) Paulo alionyesha kwamba tumaini katika Yesu Kristo linatokeza kazi inayozaa matunda na uvumilivu. Tumaini hilo linatia ndani kuamini kuja kwa Kristo na kurudishwa ambako kutafuata. Tumaini kama hilo linaweza kuwategemeza Wakristo wa kweli au kuwasaidia kuvumilia, hata wanapokabili hali ngumu sana.

Kwa mfano, mfikirie Carlos, anayeishi huko São Paulo, Brazili. Mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 2003, Carlos aligundua kwamba ana ugonjwa wa kansa. Tangu hapo, mara nane amefanyiwa upasuaji ambao ulikuwa wenye uchungu na ulimdhoofisha sana. Hata hivyo, ameendelea kuwatia wengine moyo. Kwa mfano, alipokuwa akihubiri barabarani mbele ya hospitali moja kubwa, alikutana na Shahidi mwingine wa Yehova ambaye mume wake alikuwa akitibiwa ugonjwa wa kansa. Kwa kuwa alijua matokeo mabaya ya kansa, Carlos aliweza kumtia moyo na kumfariji dada huyo pamoja na mume wake. Baadaye, walisema kwamba mazungumzo hayo yaliwatia moyo sana. Hivyo, Carlos alijionea ukweli wa maneno haya ya Paulo: “[Mungu] hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tuweze kuwafariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.”—2 Wakorintho 1:4.

Ingawa Carlos ni mgonjwa, ni nini kinachomsaidia kupata nguvu ya kuendelea kuwatia wengine moyo? Tumaini la kuja kwa Kristo na yote ambayo kutatimiza linamchochea Carlos kuendelea “kufanya yaliyo mema.”—Wagalatia 6:9.

Fikiria pia kisa cha Samuel ambaye ndugu yake aliuawa umbali wa mita 50 kutoka nyumbani kwa baba yao. Alipigwa risasi kumi. Maiti yake ilibaki kando ya barabara kwa muda wa saa nane huku polisi wakifanya uchunguzi kuhusu uhalifu huo. Samuel hawezi kusahau yale yaliyotukia siku hiyo. Hata hivyo, anategemezwa na tumaini la kwamba Kristo ataondoa uovu wote duniani na kwamba utawala wenye uadilifu utakaofuata utawaletea wanadamu baraka nyingi. Mara nyingi, Samuel anawazia akimkumbatia ndugu yake atakapofufuliwa katika Paradiso duniani.—Matendo 24:15.

Unapaswa Kufanya Nini?

Tumaini la kuja kwa Kristo na mambo ambayo kutatimiza litakufariji sana. Bila shaka, Yesu Kristo ataondoa visababishi vyote vya matatizo ya wanadamu na uovu unaotukumba.

Unapaswa kufanya nini ili upate baraka hizo ambazo utawala wa Kristo utawaletea wanadamu? Jifunze kwa makini Neno la Mungu, Biblia. Katika sala kwa Baba yake, Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Jiwekee mradi wa kuchunguza yale ambayo Biblia inafundisha. Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu watafurahi kukusaidia kufanya hivyo. Tunakuomba kwa uchangamfu uwasiliane nao au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kuja kwa Kristo kutarudisha kabisa hali nzuri duniani

[Hisani]

Inset, background only: Rhino and Lion Park, Gauteng, South Africa