Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yeremia

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yeremia

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yeremia

YEREMIA aliwatangazia watu wake mwenyewe misiba yenye kushtua kama nini! Hekalu tukufu ambalo lilikuwa kitovu cha ibada kwa zaidi ya karne tatu lingeteketezwa kabisa. Jiji la Yerusalemu na nchi ya Yuda zingeachwa ukiwa, na wakaaji wake kupelekwa uhamishoni. Masimulizi kuhusu matukio hayo na matangazo mengine ya hukumu yamo katika kitabu cha pili kwa ukubwa cha Biblia, yaani, kitabu cha Yeremia. Pia, kinasimulia mambo yaliyompata Yeremia alipokuwa akitimiza kwa uaminifu huduma yake iliyodumu kwa miaka 67. Habari zilizo katika kitabu hicho, hazijapangwa kulingana na tarehe ya matukio, bali kulingana na ujumbe wake.

Kwa nini tunapaswa kupendezwa na kitabu cha Biblia cha Yeremia? Unabii wake uliotimizwa unatia nguvu imani yetu katika Yehova ambaye ni Mtimizaji wa ahadi zake. (Isaya 55:10, 11) Kazi ya Yeremia akiwa nabii na mtazamo wa watu kuelekea ujumbe wake zinafanana na hali katika siku zetu. (1 Wakorintho 10:11) Zaidi ya hayo, masimulizi ya jinsi Yehova alivyoshughulika na watu wake yanakazia sifa zake, na hilo linapaswa kuwa na matokeo makubwa kwetu.—Waebrania 4:12.

“MAMBO MAWILI MABAYA AMBAYO WATU WANGU WAMEFANYA”

(Yeremia 1:1–20:18)

Yeremia anawekwa kuwa nabii katika mwaka wa 13 wa utawala wa Yosia, mfalme wa Yuda, yaani, miaka 40 kabla ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. (Yeremia 1:1, 2) Matangazo yaliyotolewa hasa katika miaka 18 ya mwisho ya utawala wa Yosia yanaonyesha ubaya wa Yuda na kutangaza hukumu za Yehova juu ya Yuda. “Nami nitafanya Yerusalemu kuwa rundo la mawe,” Yehova anasema, “na majiji ya Yuda nitayafanya kuwa mahame yenye ukiwa, bila mkaaji.” (Yeremia 9:11) Kwa nini? “Kwa sababu kuna mambo mawili mabaya ambayo watu wangu wamefanya,” Yehova anasema.—Yeremia 2:13.

Ujumbe huo unahusu pia kurudishwa kwa mabaki wenye kutubu. (Yeremia 3:14-18; 12:14, 15; 16:14-21) Hata hivyo, mjumbe huyo hapokelewi vizuri. “Msimamizi mkuu katika nyumba ya Yehova” anampiga Yeremia na kumtia katika mikatale usiku wote.—Yeremia 20:1-3.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:11, 12—Kwa nini Yehova anaendelea kuwa macho kuhusiana na neno lake juu ya “chipukizi la mlozi”? Chipukizi la mlozi ni mojawapo ya miti inayochipuka kwanza wakati wa masika. Kwa njia ya mfano, Yehova aliendelea ‘kuamka mapema na kuwatuma manabii wake’ ili kuwaonya watu wake kuhusu hukumu zake, naye ‘aliendelea kuwa macho’ hadi utimizo wa hukumu hizo.—Yeremia 7:25.

2:10, 11—Ni nini kilichofanya matendo ya Waisraeli wasio waaminifu yawe yasiyo ya kawaida kabisa? Ingawa huenda mataifa ya kipagani yaliyokuwa magharibi kuelekea Kitimu na mashariki kuelekea Kedari yangeleta miungu ya mataifa mengine na kuiongeza kwenye miungu yao, wazo la kuondoa kabisa miungu yao na kuchukua miungu ya kigeni halikuwazika kamwe. Hata hivyo, Waisraeli walimwacha Yehova, na kuubadili utukufu wa Mungu aliye hai kwa sanamu zisizo na uhai.

3:11-22; 11:10-12, 17—Kwa nini Yeremia alihusisha ufalme wa makabila kumi katika matangazo yake ya hukumu hata ingawa jiji la Samaria lilikuwa tayari limeanguka mwaka wa 740 K.W.K.? Alifanya hivyo kwa sababu uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. ulionyesha hukumu ya Yehova juu ya taifa lote la Israeli, wala si Yuda tu. (Ezekieli 9:9, 10) Kwa kuongezea, baada ya ufalme wa makabila kumi kuanguka, mambo yaliyohusu ufalme huo yaliendelea kushughulikiwa huko Yerusalemu, kwa kuwa ujumbe wa manabii wa Mungu uliendelea kuwahusu Waisraeli.

4:3, 4—Amri hiyo inamaanisha nini? Wayahudi wasio waaminifu walihitaji kutayarisha, kulainisha, na kuondoa uchafu katika udongo wa mioyo yao. Walihitaji kuondoa “magovi” ya mioyo yao, yaani kuondoa kabisa mawazo, nia, na tamaa chafu. (Yeremia 9:25, 26; Matendo 7:51) Walipaswa kubadili mtindo wao wa maisha, yaani, kuacha kufanya mabaya na kufanya mambo yanayoleta baraka za Mungu.

4:10; 15:18—Ni katika maana gani Yehova aliwadanganya watu wake waasi? Katika siku za Yeremia, kulikuwa manabii ambao ‘walitoa unabii kwa uwongo.’ (Yeremia 5:31; 20:6; 23:16, 17, 25-28, 32) Yehova hakuwazuia wasitangaze ujumbe wenye kupotosha.

16:16—Inamaanisha nini Yehova ‘kuwaita wavuvi wengi’ na “wawindaji wengi”? Huenda hilo linahusu kutuma majeshi ya adui kuwatafuta Wayahudi wasio waaminifu ambao Yehova angetekeleza hukumu yake juu yao. Hata hivyo, kulingana na yale ambayo Yeremia 16:15 linasema, mstari huo unaweza pia kumaanisha kuwatafuta Waisraeli wenye kutubu.

20:7—Ni katika njia gani Yehova ‘alitumia nguvu zake’ kumpinga Yeremia na hivyo kumpumbaza? Kwa sababu ya kukabili ubaridi, upinzani, na mateso alipokuwa akitangaza hukumu za Yehova, huenda Yeremia alihisi kwamba hakuwa na nguvu za kuendelea. Hata hivyo, Yehova alitumia nguvu zake kupinga mielekeo kama hiyo, na kumtia Yeremia nguvu ili aendelee. Hivyo, Yehova alimpumbaza Yeremia kwa kumtumia kutimiza yale ambayo nabii huyo mwenyewe alifikiri kwamba hangeweza kufanya.

Mambo Tunayojifunza:

1:8. Nyakati nyingine huenda Yehova akawakomboa watu wake kutoka katika mateso, labda kwa kutokeza mahakimu wasio na ubaguzi, kuondoa maofisa wakali na kuweka wenye usawaziko, au kuwapa waabudu wake nguvu za kuvumilia.—1 Wakorintho 10:13.

2:13, 18. Waisraeli wasio waaminifu walifanya mambo mawili mabaya. Walimwacha Yehova, chanzo hakika cha baraka, mwongozo, na ulinzi. Nao wakajichimbia wenyewe matangi ya mfano kwa kufanya mapatano ya kijeshi pamoja na Misri na Ashuru. Katika nyakati zetu, kumwacha Mungu wa kweli ili kufuata falsafa na nadharia za kibinadamu na siasa za ulimwengu ni kuacha “chemchemi ya maji yaliyo hai” na kugeukia “matangi yaliyovunjika.”

6:16. Yehova anawahimiza watu wake walioasi watue, wajichunguze wenyewe, na kurudi kwenye “barabara” za mababu zao waaminifu. Je, hatupaswi kujichunguza wenyewe mara kwa mara ili kuona ikiwa kwa kweli tunatembea katika njia ambayo Yehova anataka tutembee?

7:1-15. Kulitumaini hekalu, kuliona kuwa aina fulani ya hirizi ya kujilinda, hakukuwaokoa Wayahudi. Tunapaswa kutembea kwa imani wala si kwa kuona.—2 Wakorintho 5:7.

15:16, 17. Kama Yeremia, tunaweza kupambana na hali ya kuvunjika moyo. Tunaweza kufanya hivyo kwa kufurahia kujifunza Biblia kwa bidii, kwa kulikweza jina la Yehova katika huduma, na kuepuka mashirika mabaya.

17:1, 2Dhambi za watu wa Yuda zilifanya dhabihu zao zisimpendeze Yehova. Uchafu wa kiadili unafanya dhabihu zetu za sifa zisikubalike.

17:5-8. Tunaweza kuwategemea wanadamu na mashirika kwa kadiri tu wanavyotenda kupatana na mapenzi na kanuni za Mungu. Inapohusu mambo kama vile wokovu, amani, na usalama wa kweli, ni jambo la hekima tumtegemee Yehova peke yake.—Zaburi 146:3.

20:8-11. Hatupaswi kuruhusu ubaridi, upinzani, au mateso yapunguze bidii yetu katika kazi ya kuhubiri Ufalme.—Yakobo 5:10, 11.

“TIENI SHINGO ZENU CHINI YA NIRA YA MFALME WA BABILONI”

(Yeremia 21:1–51:64)

Yeremia anatangaza hukumu juu ya wafalme wanne wa mwisho wa Yuda na pia juu ya manabii wa uwongo, wachungaji wabaya, na makuhani wapotovu. Akiwataja mabaki waaminifu kuwa tini nzuri, Yehova anasema hivi: “Nitaweka jicho langu juu yao kwa njia nzuri.” (Yeremia 24:5, 6) Unabii wenye sehemu tatu katika sura ya 25 unataja kwa ufupi hukumu zinazozungumziwa kwa urefu katika sura zinazofuata.

Makuhani na manabii wanapanga njama ya kumuua Yeremia. Ujumbe wake ni kwamba wanapaswa kumtumikia mfalme wa Babiloni. Yeremia alimwambia Mfalme Sedekia hivi: “Tieni shingo zenu chini ya nira ya mfalme wa Babiloni.” (Yeremia 27:12) Hata hivyo, “Yeye anayemtawanya Israeli atamkusanya [Israeli] pamoja.” (Yeremia 31:10) Warekabu wanapewa ahadi kwa sababu nzuri. Yeremia anawekwa “kifungoni katika Ua wa Walinzi.” (Yeremia 37:21) Yerusalemu linaharibiwa, na wakaaji wengi wanapelekwa utekwani. Yeremia na mwandishi wake, Baruku, ni kati ya wale wanaobaki. Watu hao wenye woga wanaenda Misri hata ingawa wameonywa na Yeremia wasiende huko. Sura ya 46 mpaka ya 51 zina ujumbe wa Yeremia kwa mataifa.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

22:30—Je, amri hiyo ilifutilia mbali haki ya Kristo ya kuketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi? (Mathayo 1:1, 11) Hapana, haikufanya hivyo. Amri hiyo ilimzuia mzao yeyote wa Yehoyakini ‘asiketi juu ya kiti cha ufalme cha Daudi huko Yuda.’ Yesu angetawala kutoka mbinguni wala si kutoka kwenye kiti cha ufalme huko Yuda.

23:33—“Mzigo wa Yehova” ni nini? Katika siku za Yeremia, matangazo mazito yaliyotolewa na nabii huyo kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu yalikuwa mzigo kwa wananchi wenzake. Nao watu hao wasioitikia walikuwa mzigo kwa Yehova hivi kwamba angewatupilia mbali. Vivyo hivyo, ujumbe wa Kimaandiko kuhusu uharibifu unaokuja wa dini zinazodai kuwa za Kikristo ni mzigo kwa dini hizo, na watu wasiotii ujumbe huo wanamchosha Mungu.

31:33—Sheria ya Mungu imeandikwa katika mioyo jinsi gani? Mtu anapopenda sana sheria ya Mungu hivi kwamba anatamani kwelikweli kufanya mapenzi ya Yehova, inaweza kusemwa kwamba sheria ya Mungu imeandikwa moyoni mwake.

32:10-15—Ni nini lililokuwa kusudi la kuandika hati mbili za makubaliano yaleyale? Hati moja iliachwa wazi ili kuirejelea. Hati iliyotiwa muhuri ilitumiwa kuthibitisha usahihi wa hati iliyoachwa wazi, hilo lilipohitajika. Yeremia alituwekea mfano kwa kufuata utaratibu unaofaa wa kisheria hata aliposhughulika na mtu wa ukoo na mwamini mwenzake.

33:23, 24—“Familia mbili” zinazotajwa hapa ni gani? Moja ni familia ya kifalme ya ukoo wa Mfalme Daudi, na nyingine, ni familia ya kikuhani ya wazao wa Haruni. Baada ya kuharibiwa kwa Yerusalemu na hekalu la Yehova, ilionekana kwamba Yehova alikuwa amezikataa familia hizo mbili na hangekuwa tena na ufalme duniani au kuanzisha tena ibada yake.

46:22—Kwa nini sauti ya Misri inalinganishwa na ile ya nyoka? Huenda hilo linahusu sauti ya nyoka anayekimbia au sauti ya chini ya kunyenyekezwa kwa Misri kwa sababu ya msiba. Ulinganisho huo unaonyesha pia jinsi lilivyokuwa jambo la ubatili kwa mafarao wa Misri kuvaa sanamu ya nyoka mtakatifu kwenye vazi la kichwani ili eti walindwe na mungu wa kike wa nyoka aliyeitwa Uatchit.

Mambo Tunayojifunza:

21:8, 9; 38:19. Hata katika saa ya mwisho, Yehova aliwapa wakaaji wa Yerusalemu wasiotubu, ambao walistahili kufa, nafasi nyingine ya kuamua. Ndiyo, “rehema zake ni nyingi.”—2 Samweli 24:14; Zaburi 119:156.

31:34. Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova hakumbuki dhambi za wale ambao amewasamehe na kuwachukulia hatua wakati ujao.

38:7-13; 39:15-18. Yehova hasahau utumishi wetu wa uaminifu ambao unatia ndani ‘kuwahudumia watakatifu.’—Waebrania 6:10.

45:4, 5Kama siku za mwisho za Yuda, “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo si wakati wa kujitafutia “mambo makuu,” kama vile mali, umashuhuri, au usalama unaotokana na vitu vya kimwili.—2 Timotheo 3:1; 1 Yohana 2:17.

YERUSALEMU LATEKETEA

(Yeremia 52:1-34)

Ni mwaka wa 607 K.W.K. Huo ni mwaka wa 11 wa ufalme wa Sedekia. Mfalme Nebukadneza wa Babiloni amelizingira jiji la Yerusalemu kwa miezi 18 sasa. Katika siku ya saba ya mwezi wa tano ya mwaka wa 19 wa utawala wa Nebukadneza, Nebuzaradani, mkuu wa walinzi, ‘anaingia,’ au kufika Yerusalemu. (2 Wafalme 25:8) Labda kutoka katika kambi yake iliyo nje ya kuta za jiji, Nebuzaradani anachunguza hali na kupanga hatua ya kuchukua. Siku tatu baadaye, katika siku ya kumi ya mwezi huo, ‘anaingia’ Yerusalemu. Naye analiteketeza jiji hilo.—Yeremia 52:12, 13.

Yeremia anaeleza kwa undani jinsi Yerusalemu lilivyoangushwa. Kwa hiyo, maelezo yake yanasababisha maombolezo au vilio. Maombolezo hayo yamo katika kitabu cha Biblia kinachoitwa Maombolezo.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Matangazo ya Yeremia yalitia ndani hukumu ya Yehova juu ya Yerusalemu

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yehova ‘alitumia nguvu zake’ kumpinga Yeremia jinsi gani?

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Kama hizi tini nzuri, ndivyo nitakavyowaona kwa njia nzuri wale wahamishwa wa Yuda.”—Yeremia 24:5