Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Noa aliingiza wanyama safi wangapi ndani ya safina—wanyama saba kati ya kila mnyama safi au vikundi saba vya wanyama wawili wawili?

Noa alipomaliza kujenga safina, Yehova alimwambia hivi: “Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na nyumba yako yote, kwa maana nimekuona wewe kuwa mwadilifu mbele zangu kati ya kizazi hiki. Kati ya kila mnyama aliye safi ujichukulie saba saba, dume na jike lake; na kati ya kila mnyama asiye safi wawili tu, dume na jike lake.” (Mwanzo 7:1, 2) Tafsiri nyingine, kama vile The New English Bible, The New Jerusalem Bible, na Tanakh—The Holy Scriptures, zinatafsiri neno la awali la Kiebrania kuwa “pea saba.”

Katika Kiebrania, neno linalotumiwa linamaanisha kihalisi “saba saba.” (Mwanzo 7:2) Hata hivyo, katika Kiebrania, nyakati nyingine kurudia namba fulani hakumaanishi kwamba tunapaswa kujumlisha namba hizo. Kwa mfano, andiko la 2 Samweli 21:20 linaeleza kuhusu “mtu mwenye ukubwa usio wa kawaida” ambaye alikuwa na “vidole 6 katika kila mmoja wa mikono yake na vidole 6 katika kila mmoja wa miguu yake.” Katika Kiebrania, namba “sita” inarudiwa. Lakini hilo halimaanishi kwamba jitu hilo lilikuwa na pea sita za vidole katika kila mkono (au, 12) na kila mguu. Kurudiwa kwa namba hiyo kunaonyesha tu kwamba jitu hilo lilikuwa na vidole sita katika kila mkono na katika kila mguu.

Kanuni za sarufi ya lugha ya Kiebrania zinasaidia jinsi gani kuelewa kwa nini namba zilirudiwa? Kikizungumzia andiko la Mwanzo 7:2, 9, kitabu cha William R. Harper’s (Introductory Hebrew Method and Manual) kinasema hivi: “Mara nyingi maneno yanarudiwa ili kuonyesha kila kitu kimoja-kimoja katika kikundi wala si vitu vyote kwa ujumla.” Kitabu cha Gesenius (Hebrew Grammar, Toleo la Pili la Kiingereza) kinasema: “Namba zinazohusu kitu kimoja-kimoja zinaonyeshwa . . . kwa kurudia namba inayoonyesha idadi.” Kinatoa mfano wa Mwanzo 7:9, 15 na 2 Samweli 21:20, ambamo maneno “wawili” na “sita” yanarudiwa.

Hivyo, maneno “saba saba” katika Mwanzo 7:2 hayamaanishi pea saba, yaani, 14, kama vile kurudia neno “wawili” katika Mwanzo 7:9, 15 kusivyomaanisha pea mbili, yaani, nne. Kurudiwa kwa maneno hayo katika mistari hiyo kunahusu kitu kimoja-kimoja wala si jumla ya vitu. Hivyo, Noa aliingiza ndani ya safina wanyama safi “saba” kati ya kila mnyama huku akiingiza wanyama “wawili” wasio safi.

Lakini, namna gani maneno “dume na jike lake” ambayo yanafuata maneno “saba saba” katika Mwanzo 7:2? Maneno hayo yamewafanya watu fulani wafikiri kwamba Noa aliagizwa achukue pea saba kati ya kila mnyama safi kwa kusudi la kuzalisha. Hata hivyo, wanyama safi hawakuhifadhiwa tu kwa kusudi la kuzalisha. Mwanzo 8:20 linatuambia baada ya kutoka katika safina, “Noa akamjengea Yehova madhabahu na kuchukua baadhi ya wanyama wote walio safi na baadhi ya viumbe vyote vinavyoruka ambavyo ni safi, akatoa matoleo ya kuteketezwa juu ya ile madhabahu.” Kuwa na mnyama wa saba kati ya kila mnyama safi kulimwezesha Noa kuwa na mnyama ambaye angeweza kumtoa kama dhabihu, na kuacha pea tatu za wanyama kwa kusudi la kuzalisha ili kuongeza idadi ya wanyama hao duniani.