Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaweza Kuwapinga Roho Waovu Jinsi Gani?

Tunaweza Kuwapinga Roho Waovu Jinsi Gani?

Tunaweza Kuwapinga Roho Waovu Jinsi Gani?

“Malaika ambao hawakubaki mahali pao pa kwanza bali wakayaacha makao yao wenyewe yanayofaa [Mungu] amewaweka akiba wakiwa na vifungo vya milele chini ya giza zito kwa ajili ya hukumu ya ile siku kuu.” —YUDA 6.

1, 2. Ni maswali gani yanayoulizwa kuhusu Shetani Ibilisi na roho waovu?

“TUNZENI akili zenu, iweni wenye kulinda,” anaonya mtume Petro. “Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Mtume Paulo anasema hivi kuhusu roho waovu: “Sitaki ninyi muwe washiriki pamoja na roho waovu. Hamwezi kuwa mkinywa kikombe cha Yehova na kikombe cha roho waovu; hamwezi kuwa mkishiriki ‘meza ya Yehova’ na meza ya roho waovu.”—1 Wakorintho 10:20, 21.

2 Lakini, Shetani Ibilisi na roho waovu ni nani? Walitoka wapi na wakati gani? Je, Mungu aliwaumba? Uvutano wao ni wenye nguvu kadiri gani katika maisha ya wanadamu? Je, tuna njia yoyote ya kujilinda nao, na ikiwa ndivyo, ni njia gani hiyo?

Shetani na Roho Waovu Walitoka Wapi?

3. Malaika wa Mungu alipata kuwa Shetani Ibilisi namna gani?

3 Mwanzoni mwa historia ya wanadamu, wakati wanadamu walipowekwa katika bustani ya Edeni, malaika mmoja wa Mungu aliasi. Kwa nini? Kwa sababu hakutosheka na jukumu lake katika mpango wa kimbingu wa Yehova. Adamu na Hawa walipoumbwa, aliona hiyo kuwa nafasi ya kuwakengeusha ili wamtii na kumwabudu yeye badala ya Mungu wa kweli. Kwa kumwasi Mungu na kuwashawishi wanadamu wawili wa kwanza wafuatie mwenendo wa dhambi, malaika huyo alijifanya mwenyewe kuwa Shetani Ibilisi. Baada ya muda, malaika wengine walijiunga naye katika uasi. Jinsi gani?—Mwanzo 3:1-6; Waroma 5:12; Ufunuo 12:9.

4. Malaika fulani waasi walifanya nini kabla ya Gharika ya siku za Noa?

4 Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanatuambia kwamba kabla ya Gharika kubwa ya siku za Noa, malaika fulani walianza kupendezwa isivyo kawaida na wanawake duniani. Wakiwa na kusudi baya, “wana [wa kimbingu] wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza,” inasema Biblia, “nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.” Mahusiano hayo hayakuwa ya kiasili, na yalitokeza wazao wa malaika na wanadamu ambao waliitwa Wanefili. (Mwanzo 6:2-4) Viumbe wa roho ambao hawakumtii Mungu walijiunga na Shetani kumwasi Yehova.

5. Ni nini kilichowapata waasi wakati Yehova alipoleta uharibifu kupitia ile Gharika kubwa?

5 Yehova alipoleta Gharika juu ya wanadamu, Wanefili na mama zao wa kibinadamu waliangamia. Malaika waasi walilazimika kubadili miili yao ya kibinadamu na kuvaa miili ya roho kisha wakarudi katika makao ya roho. Hata hivyo, hawangeweza kurudi tena “mahali pao pa kwanza,” pamoja na Mungu. Badala yake, walitiwa katika “giza zito [la kiroho],” linaloitwa Tartaro.—Yuda 6; 2 Petro 2:4.

6. Roho waovu wanawadanganya watu jinsi gani?

6 Tangu malaika waovu walipopoteza “mahali pao pa kwanza,” wamekuwa roho waovu wanaoshirikiana na Shetani na wamemuunga mkono katika kutimiza makusudi yake maovu. Kuanzia wakati huo na kuendelea, roho waovu hawana uwezo wa kuvaa miili ya kibinadamu. Hata hivyo, wanaweza kuwashawishi wanaume na wanawake washiriki katika matendo mbalimbali yaliyopotoka kingono. Roho waovu wanawadanganya wanadamu wengi kupitia zoea la kuwasiliana na pepo, ambalo linatia ndani mambo kama vile mizungu, uchawi, na watu wanaowasiliana na pepo. (Kumbukumbu la Torati 18:10-13; 2 Mambo ya Nyakati 33:6) Malaika waovu wataharibiwa milele kama Ibilisi. (Mathayo 25:41; Ufunuo 20:10) Hata hivyo, tunahitaji kusimama imara na kuwapinga kabla ya wakati huo. Ni jambo la hekima kuchunguza Shetani ana nguvu nyingi kadiri gani na jinsi tunavyoweza kufaulu kumpinga yeye pamoja na roho wake waovu.

Shetani Ana Nguvu Nyingi Kadiri Gani?

7. Shetani ana nguvu gani juu ya ulimwengu?

7 Kwa muda wote, Shetani amekuwa akisema uwongo kumhusu Yehova. (Methali 27:11) Naye amewapotosha wanadamu wengi. Andiko la 1 Yohana 5:19 linasema hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Ndiyo sababu Ibilisi alijaribu kumshawishi Yesu kwa kumtolea mamlaka na utukufu wa “falme zote za dunia inayokaliwa.” (Luka 4:5-7) Mtume Paulo anasema hivi kuhusu Shetani: “Basi, ikiwa kwa kweli habari njema tunayotangaza imefunikwa utaji, imefunikwa utaji katikati ya wale wanaoangamia, ambao katikati yao mungu wa mfumo huu wa mambo amezipofusha akili za wasioamini, ili nuru ya habari njema yenye utukufu juu ya Kristo, aliye mfano wa Mungu, isipenyeze mwangaza.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Shetani ni “mwongo na ndiye baba ya uwongo,” hata hivyo, anajifanya kuwa “malaika wa nuru.” (Yohana 8:44; 2 Wakorintho 11:14) Ana nguvu na mbinu zinazohitajiwa ili kupofusha akili za watawala wa ulimwengu na raia wao. Amewadanganya wanadamu akitumia propaganda, hadithi na uwongo wa kidini.

8. Biblia inasema nini kuhusu uvutano wa Shetani?

8 Nguvu na uvutano wa Shetani ulionekana wakati wa nabii Danieli, karne tano hivi kabla ya Wakati Wetu wa Kawaida. Yehova alipomtuma malaika mmoja apeleke ujumbe wa kumtia moyo Danieli, malaika huyo alipingwa na “[roho] mkuu wa ufalme wa Uajemi.” Malaika huyo mwaminifu alizuiwa kwa siku 21 mpaka “Mikaeli, aliye mmoja wa hao wakuu wa mbele,” alipokuja kumsaidia. Simulizi hilo linamtaja pia “[roho mwovu] mkuu wa Ugiriki.” (Danieli 10:12, 13, 20) Na katika andiko la Ufunuo 13:1, 2, Shetani anaonyeshwa kuwa “joka mkubwa” ambaye anampa yule mnyama-mwitu wa kisiasa “nguvu zake na kile kiti chake cha ufalme na mamlaka kubwa.”

9. Wakristo wanapigana na nani?

9 Haishangazi kwamba mtume Paulo aliandika hivi: “Tuna kushindana mweleka, si juu ya damu na mwili, bali juu ya serikali, juu ya mamlaka, juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Hata leo, majeshi yasiyoonekana ya roho waovu ambayo yanaongozwa na Shetani Ibilisi yanawachochea watawala wa kibinadamu na wanadamu kwa ujumla, na kuwasukuma watende matendo yasiyoelezeka kama vile maangamizi ya jamii nzima-nzima, ugaidi, na mauaji ya watu. Acheni sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kufaulu kuyapinga majeshi hayo yenye nguvu ya roho.

Tunaweza Kujilinda kwa Njia Gani?

10, 11. Tunaweza kumpinga Shetani na malaika wake waovu kwa njia gani?

10 Hatuwezi kumpinga Shetani na malaika wake waovu kwa nguvu zetu wenyewe, ziwe za kimwili au za kiakili. Paulo anatushauri hivi: “Endeleeni kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake.” Tunahitaji kumtegemea Mungu ili atulinde. Paulo anaongezea: “Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi . . . Chukueni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu, ili mweze kupinga katika ile siku ya uovu, baada ya ninyi kufanya mambo yote kwa ukamili, mweze kusimama imara.”—Waefeso 6:10, 11, 13.

11 Mara mbili Paulo anawahimiza Wakristo wenzake wavae “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.” Neno “kamili” linamaanisha kwamba hatuwezi kushinda mashambulizi ya roho waovu tukiwa na moyo nusunusu. Hivyo basi, mavazi ya kiroho ambayo Wakristo leo wanahitaji kuvaa kwa uharaka ili wapinge roho waovu yana sehemu gani muhimu?

‘Tusimame Imara’ Jinsi Gani?

12. Wakristo wanaweza kujifunga kweli kwenye viuno vyao jinsi gani?

12 Paulo anaeleza hivi: “Kwa hiyo, simameni imara, viuno vyenu vikiwa vimefungwa kwa ile kweli, na mkiwa mmevaa bamba la kifuani la uadilifu.” (Waefeso 6:14) Sehemu mbili za mavazi hayo zinazotajwa hapo ni mshipi na bamba la kifuani. Askari-jeshi alihitaji kufunga mshipi wake kwa nguvu ili kulinda viuno vyake (mapaja, kinena, na sehemu ya chini ya tumbo) na ili kubeba upanga wake mzito. Vivyo hivyo, tunahitaji kujifunga kwa njia ya mfano kweli ya Biblia kwa nguvu ili tuishi kupatana nayo. Je, tuna programu ya kusoma Biblia kila siku? Je, familia yote inashiriki kufanya hivyo? Je, tuna zoea la kuchunguza andiko la siku tukiwa familia? Zaidi ya hayo, je, tunaenda sambamba na maelezo yaliyo katika vichapo vinavyotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (Mathayo 24:45) Ikiwa ndivyo, tunajitahidi kufuata shauri la Paulo. Pia, tuna video na DVD ambazo zinaweza kutupa mwongozo wa Kimaandiko. Kushika kweli kwa nguvu kunaweza kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima na kutulinda tusifuate mwenendo usiofaa.

13. Tunaweza kuulinda namna gani moyo wetu wa mfano?

13 Bamba halisi la kifuani lililinda kifua, moyo, na viungo vingine muhimu vya askari-jeshi. Mkristo anaweza kuulinda moyo wake wa mfano, yaani, mtu wa ndani, kwa kusitawisha upendo kuelekea uadilifu wa Mungu na kufuata viwango vya Yehova vya uadilifu. Bamba la kifuani la mfano linatulinda ili tusipunguze uzito wa Neno la Mungu. ‘Tunapochukia yaliyo mabaya, na kupenda yaliyo mema,’ tunaizuilia mbali miguu yetu “kutoka katika kila pito baya.”—Amosi 5:15; Zaburi 119:101.

14. Ni nini maana ya ‘kuvaa miguuni mwetu viatu vya habari njema ya amani’?

14 Kwa kawaida, askari-jeshi Waroma walivaa viatu miguuni ili kutembea umbali wa mamia ya kilomita kwenye barabara za Roma zilizoenea katika milki hiyo yote. Maneno ‘mmevaa miguuni viatu vya habari njema ya amani,’ yanamaanisha nini kwa Wakristo? (Waefeso 6:15) Yanamaanisha kwamba tuko tayari kwa utendaji. Tuko tayari kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu katika kila nafasi inayofaa. (Waroma 10:13-15) Kuwa na bidii katika huduma ya Kikristo kunatulinda na “hila” za Shetani.—Waefeso 6:11.

15. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba ngao kubwa ya imani ni muhimu sana? (b) Imani yetu inaweza kuharibiwa na ‘mishale gani inayowaka moto’?

15 Paulo anaendelea kusema hivi: “Zaidi ya mambo yote, ichukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwa kuitumia mtaweza kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.” (Waefeso 6:16) Kabla ya kutoa shauri kuhusu kuchukua ngao kubwa ya imani, Biblia inasema “zaidi ya mambo yote,” ili kuonyesha kwamba sehemu hiyo ya mavazi ya silaha ni muhimu sana. Imani yetu haipaswi kuwa na kasoro yoyote. Kama ngao kubwa yenye kulinda, imani yetu inatulinda kutokana na ‘mishale inayowaka moto’ ya Shetani. Mishale hiyo inaweza kufananisha nini leo? Inaweza kufananisha matusi yenye kuumiza, uwongo, na kweli nusu-nusu zinazotolewa na maadui na waasi-imani wanaojaribu kudhoofisha imani yetu. “Mishale” hiyo inaweza pia kuwa vishawishi vya kufuatia vitu vya kimwili, vinavyoweza kutuchochea tujishughulishe sana na kununua vitu vingi na hata kutuchochea tushindane na wale ambao wametumbukia katika mtego wa maisha ya kujionyesha. Huenda wamepata magari na nyumba zilizo kubwa na nzuri zaidi au wanajionyesha kuwa na vito vya thamani kubwa na mitindo ya kisasa ya mavazi. Haidhuru wengine wanafanya nini, tunapaswa kuwa na imani yenye nguvu sana ambayo inaweza kuzuia mishale hiyo inayowaka moto. Tunaweza kujenga na kudumisha imani yenye nguvu kwa njia gani?—1 Petro 3:3-5; 1 Yohana 2:15-17.

16. Ni nini kinachoweza kutusaidia kujenga imani yenye nguvu?

16 Tunaweza kumkaribia Mungu kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida na kusali kwa bidii. Tunaweza kumsihi Yehova aimarishe imani yetu, halafu tutende kupatana na sala zetu. Kwa mfano, je, tunatayarisha kwa uangalifu Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma tukiwa na nia ya kutoa maelezo? Imani yetu itakuwa na nguvu tukijifunza Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia.—Waebrania 10:38, 39; 11:6.

17. Tunaweza ‘kupokea kofia ya chuma ya wokovu’ jinsi gani?

17 Paulo anamalizia maelezo yake kuhusu mavazi ya silaha za kiroho kwa kutoa shauri hili: “Ipokeeni kofia ya chuma ya wokovu, na upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.” (Waefeso 6:17) Kofia ya chuma ililinda kichwa na ubongo wa askari-jeshi, yaani, kiungo cha kufanya maamuzi. Vivyo hivyo, tumaini letu la Kikristo linalinda uwezo wetu wa kufikiri. (1 Wathesalonike 5:8) Badala ya kujaza akili zetu na miradi ya kilimwengu au tamaa ya kuwa na vitu vya kimwili, tunapaswa kukazia fikira zetu tumaini tulilopewa na Mungu, kama Yesu alivyofanya.—Waebrania 12:2.

18. Kwa nini hatupaswi kupuuza programu yetu ya kusoma Biblia kwa ukawaida?

18 Mwishowe, Neno la Mungu, au ujumbe ulioandikwa katika Biblia unaweza kutulinda kutokana na uvutano wa Shetani na roho wake waovu. Hiyo ni sababu nyingine inayoonyesha umuhimu wa kutopuuza programu yetu ya kusoma Biblia kwa ukawaida. Ujuzi mwingi na ulio sahihi wa Neno la Mungu unaweza kutulinda kutokana na uwongo wa Shetani na propaganda za roho waovu na pia kutokana na habari zenye kuumiza za waasi-imani.

‘Endeleza Sala Kila Wakati’

19, 20. (a) Ni nini kitakachompata Shetani na roho wake waovu? (b) Ni nini kinachoweza kutuimarisha kiroho?

19 Hivi karibuni, Shetani, roho wake waovu, na ulimwengu huu mbovu utaondolewa. Shetani anajua kwamba ana “kipindi kifupi cha wakati.” Ana ghadhabu na anapigana vita na wale “wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 12:12, 17) Ni muhimu tumpinge Shetani na roho wake waovu.

20 Tunaweza kushukuru kama nini kwa sababu ya himizo la kuvaa mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu! Paulo anamalizia mazungumzo yake kuhusu silaha za kiroho kwa kutoa shauri hili: “Kwa kila namna ya sala na dua mkiendeleza sala kila wakati katika roho. Na kwa kusudi hilo endeleeni kukaa macho daima na kuomba dua kwa ajili ya watakatifu wote.” (Waefeso 6:18) Sala inaweza kutuimarisha kiroho na kutusaidia tuendelee kukaa macho. Acheni tuchukue kwa uzito maneno ya Paulo na tuendelee kusali, kwa sababu kufanya hivyo kutatusaidia kumpinga Shetani na roho wake waovu.

Umejifunza Nini?

• Shetani na roho wake waovu walitoka wapi?

• Ibilisi ana nguvu nyingi kadiri gani?

• Ni nini kinachoweza kutulinda kutokana na Shetani na roho wake waovu?

• Tunaweza kuvaa namna gani mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Wana wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu”

[Picha katika ukurasa wa 28]

Je, unaweza kutaja sehemu sita za mavazi yetu ya silaha za kiroho?

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kufanya mambo haya kunatulinda jinsi gani kutokana na Shetani na roho wake waovu?