Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Katika Unabii wa Biblia Inaokoa Uhai

Imani Katika Unabii wa Biblia Inaokoa Uhai

Imani Katika Unabii wa Biblia Inaokoa Uhai

YESU anaondoka katika hekalu la Yerusalemu kwa mara ya mwisho wakati mwanafunzi wake mmoja anaposema hivi kwa mshangao: “Mwalimu, ona! jinsi yalivyo mawe haya na majengo haya!” Hekalu hilo linaleta fahari na utukufu kwa taifa hilo la Kiyahudi. Hata hivyo, Yesu anajibu hivi: “Unayaona majengo haya makubwa? Hakuna jiwe litakaloachwa hapa juu ya jiwe nalo lisiangushwe chini.”—Marko 13:1, 2.

Hilo ni wazo lisiloaminika! Mawe fulani ya hekalu hilo ni makubwa sana. Zaidi ya hayo, maneno ya Yesu kuhusu hekalu yanamaanisha kwamba jiji la Yerusalemu litaharibiwa na huenda taifa hilo la Kiyahudi ambalo linatumia hekalu kama kituo cha ibada likaharibiwa pia. Basi, wanafunzi wa Yesu wanamuuliza maswali zaidi: “Tuambie, mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya wakati ambapo mambo yote haya yanakusudiwa kufikia mwisho?”—Marko 13:3, 4.

Yesu anawaonya hivi: “Ule mwisho bado.” Kwanza, wanafunzi hao watasikia juu ya vita, matetemeko ya nchi, njaa kali, na tauni mahali pamoja baada ya pengine. Kisha, matukio yenye kutisha yatalitumbukiza taifa hilo la Kiyahudi katika msiba mkubwa ambao haujawahi kutokea kamwe, yaani, “dhiki kuu.” Hata hivyo, Mungu ataingilia kati ili kuwaokoa “wale waliochaguliwa,” yaani, Wakristo waaminifu. Jinsi gani?—Marko 13:7; Mathayo 24:7, 21, 22; Luka 21:10, 11.

Wanaasi Roma

Miaka 28 inapita, na Wakristo walio Yerusalemu bado wanangojea mwisho. Milki ya Roma inakumbwa na vita, matetemeko ya nchi, njaa kali, na tauni. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 9.) Mapambano mengi ya kijamii na ya kikabila yanatokea huko Yudea. Hata hivyo, kuna usalama wa kadiri ndani ya jiji la Yerusalemu linalozungukwa na kuta. Watu wanakula, wanafanya kazi, wanaoa na kuolewa, na wanazaa watoto, kama kawaida. Watu wanahisi kwamba jiji lao liko salama na imara kwa sababu ya hekalu hilo kubwa sana.

Karibu mwaka wa 61 W.K., Wakristo walio Yerusalemu wanapokea barua kutoka kwa mtume Paulo. Anawapongeza kwa sababu ya uvumilivu wao lakini anaeleza wasiwasi wake kwamba watu fulani kutanikoni hawaoni hatari inayowakabili. Wakristo fulani wanapeperuka kiroho au hawana ukomavu wa Kikristo. (Waebrania 2:1; 5:11, 12) Paulo anawahimiza hivi: “Kwa hiyo, msiutupilie mbali uhuru wenu wa kusema . . . Kwa maana bado ‘muda kidogo sana,’ na ‘yeye anayekuja atafika naye hatakawia.’ ‘Lakini mwadilifu wangu ataishi kwa sababu ya imani,’ na, ‘akirudi nyuma kwa kutetemeka, nafsi yangu haipendezwi naye.’” (Waebrania 10:35-38) Anatoa shauri la wakati unaofaa kabisa! Lakini je, Wakristo watakuwa na imani na kuendelea kuwa macho kuhusu kutimizwa kwa unabii wa Yesu? Je, mwisho wa Yerusalemu uko karibu kweli?

Katika miaka mitano inayofuata, hali zinazidi kuwa mbaya katika Yerusalemu. Mwishowe, katika mwaka wa 66 W.K., Florus, Gavana Mroma aliye mpotovu anachukua talanta 17 za “deni la kodi” kutoka katika hazina takatifu ya hekalu. Wayahudi wanakasirika na kuanza kuasi serikali. Wayahudi waasi wanamiminika Yerusalemu na kuwachinja askari-jeshi Waroma jijini humo. Kisha, wanatangaza kwa ujasiri kwamba Yudea haiko tena chini ya Roma. Sasa vita vinazuka kati ya Roma na Yudea!

Katika muda wa miezi mitatu, gavana Mroma wa Siria, Sesho Galo, anashuka kusini akiwa na askari-jeshi 30,000 ili kuzima uasi wa Wayahudi. Jeshi lake linafika Yerusalemu wakati wa Sherehe ya Vibanda na kuingia moja kwa moja vijijini. Wayahudi waasi ambao ni wachache wanakimbilia katika ngome ya hekalu. Muda si muda, askari-jeshi Waroma wanaanza kuuharibu ukuta wa hekalu. Wayahudi wanaudhika, kwa sababu, askari-jeshi wapagani sasa wanatia unajisi mahali patakatifu zaidi pa dini ya Kiyahudi! Hata hivyo, Wakristo walio jijini wanakumbuka maneno haya ya Yesu: ‘Mtakapoona lile chukizo, likiwa limesimama katika mahali patakatifu, wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani.’ (Mathayo 24:15, 16) Je, wangeonyesha imani katika maneno ya Yesu ya kinabii na hivyo kuchukua hatua inayofaa? Kama ilivyotukia, uhai wao ulitegemea kufanya hivyo. Lakini wangekimbia jinsi gani?

Kwa ghafula na bila sababu yoyote nzuri, Sesho Galo anawaondoa askari-jeshi wake na kuelekea pwani huku wakikimbizwa mbio na Wayahudi waasi. Kwa kushangaza, dhiki juu ya jiji hilo ilikuwa imefupishwa! Wakristo wanaonyesha imani yao katika onyo la kinabii la Yesu na kutoka Yerusalemu na kukimbilia Pela, jiji lisilomilikiwa na yeyote lililo milimani ng’ambo ya Mto Yordani. Wanakimbia kwa wakati unaofaa kabisa. Punde si punde, Wayahudi hao waasi wanarudi Yerusalemu na kuwalazimisha watu waliobaki jijini kuunga mkono uasi wao. * Wakristo wakiwa salama huko Pela, wanangojea matukio mengine.

Hali Inazorota

Baada ya miezi michache, jeshi lingine la Roma linaelekea Yerusalemu. Mnamo mwaka wa 67 W.K., Jenerali Vespasian na mwana wake Tito wanakusanya pamoja jeshi kubwa sana lenye askari 60,000. Kwa miaka miwili inayofuata, jeshi hilo lenye kuharibu linaelekea Yerusalemu, likiponda wapinzani wote njiani. Wakati huo, ndani ya Yerusalemu, vikundi vinavyopingana vya Wayahudi vinapambana vikali. Majengo ya kuhifadhi mbegu jijini yanaharibiwa, eneo linalozunguka hekalu linaharibiwa kabisa, na Wayahudi zaidi ya 20,000 wanauawa. Vespasian anasita kushambulia Yerusalemu, huku akisema: ‘Mungu anatenda kama jenerali Mroma kwa njia bora kuliko mimi; maadui wetu wanaangamizana wenyewe.’

Wakati Maliki Nero wa Roma anapokufa, Vespasian anaenda Roma kuchukua kiti cha ufalme, anamwacha Tito amalize kampeni ya kushambulia Yudea. Tito anashambulia Yerusalemu karibu Pasaka ya mwaka wa 70 W.K., akiwanasa jijini humo wakaaji na wasafiri waliotoka maeneo mengine. Majeshi yake yanakata miti katika maeneo ya mashambani ya Yudea ili kujenga ukuta wenye miti iliyochongoka. Wanajenga ukuta huo umbali wa kilomita 7 kuzunguka jiji hilo. Ni kama tu Yesu alivyotabiri: ‘Adui zako watajenga kukuzunguka ngome yenye miti iliyochongoka nao watakuzunguka na kukutaabisha kutoka kila upande.’—Luka 19:43.

Punde si punde, kunakuwa na njaa kali jijini. Vikundi vyenye silaha vinapora nyumba za watu waliouawa na za wale wanaokufa. Angalau mwanamke mmoja mwenye njaa kali anamuua na kumla mtoto wake mchanga, na hivyo anatimiza unabii uliosema: “Utalazimika kula uzao wa tumbo lako, nyama ya wana wako na binti zako . . . kwa sababu ya mbano na mkazo ambao adui yako atakusonga nao.”—Kumbukumbu la Torati 28:53-57.

Mwishowe, baada ya kuzingirwa kwa miezi mitano, Yerusalemu linaanguka. Jiji hilo na hekalu lake kubwa linaporwa na kuteketezwa kisha, linabomolewa jiwe kwa jiwe. (Danieli 9:26) Jumla ya watu 1,100,000 hivi wanakufa; na wengine 97,000 wanauzwa utumwani. * (Kumbukumbu la Torati 28:68) Yudea linabaki karibu ukiwa bila Wayahudi. Kwa kweli, huo ni msiba wa kitaifa ambao hauna kifani. Maisha ya kisiasa, kidini, na ya kitamaduni ya Wayahudi yanabadilika kabisa. *

Wakati huo, Wakristo walio Pela wanamshukuru Mungu sana kwa sababu ya kuwakomboa. Imani yao katika unabii wa Biblia imeokoa uhai wao!

Tunapofikiria matukio hayo, inafaa kila mmoja wetu leo ajiulize hivi: ‘Je, nina imani ambayo itaokoa uhai wangu wakati wa dhiki kuu inayokuja? Je, mimi ni “namna ya [mtu aliye] na imani ya kuihifadhi hai nafsi”?’—Waebrania 10:39; Ufunuo 7:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Mwanahistoria Myahudi Yosefo anaripoti kwamba Wayahudi waasi waliwafuata Waroma kwa siku saba kabla ya kurudi Yerusalemu.

^ fu. 15 Kulingana na kadirio moja, zaidi ya Myahudi mmoja kwa kila Wayahudi 7 aliuawa katika Milki ya Roma.

^ fu. 15 Alfred Edersheim, msomi wa Biblia Myahudi aliandika hivi: “Dhiki [hiyo] iliyokumba Israeli [haikuwa] na kifani katika historia yake ya matukio mabaya sana, na haingelinganishwa kamwe na misiba iliyotukia baadaye.”

[Chati katika ukurasa wa 9]

Sehemu za Ishara Zilizotimizwa Katika Karne ya Kwanza

VITA:

Gaul (39-40 W.K.)

Afrika Kaskazini (41 W.K.)

Uingereza (43, 60 W.K.)

Armenia (58-62 W.K.)

Mapambano ya kijamii na ya kikabila huko Yudea (50-66 W.K.)

MATETEMEKO YA NCHI:

Roma (54 W.K.)

Pompeii (62 W.K.)

Asia Ndogo (53, 62 W.K.)

Krete (62 W.K.)

NJAA KALI:

Roma, Ugiriki, Misri (karibu 42 W.K.)

Yudea (karibu 46 W.K.)

TAUNI:

Babilonia (40 W.K.)

Roma (60, 65 W.K.)

MANABII WA UWONGO:

Yudea (karibu 56 W.K.)

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 10]

 

Kampeni ya Waroma huko Palestina, mwaka wa 67-70 W.K.

Tolemai

Bahari ya Galilaya

Pela

PEREA

SAMARIA

Yerusalemu

Bahari ya Chumvi

YUDEA

Kaisaria

[Hisani]

Map only: Based on maps copyrighted by Pictorial Archive (Near Eastern History) Est. and Survey of Israel

[Picha katika ukurasa wa 11]

‘Maadui wetu wanaangamizana wenyewe.’—Vespasian

[Picha katika ukurasa wa 11]

Mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yaliharibu Yerusalemu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 11]

Relief: Soprintendenza Archeologica di Roma; Vespasian: Bildarchiv Preussischer Kulturbesitz/Art Resource, NY