Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kazi ya Kufanya Wanafunzi Imefinyanga Maisha Yangu

Kazi ya Kufanya Wanafunzi Imefinyanga Maisha Yangu

Simulizi la Maisha

Kazi ya Kufanya Wanafunzi Imefinyanga Maisha Yangu

Kama lilivyosimuliwa na Lynette Peters

Walikuwa wamekuja kutuhamisha. Mlenga-shabaha mwenye bunduki alikuwa amesimama juu ya nyumba yetu. Askari-jeshi walilala kwenye nyasi, wakiwa tayari kufyatua risasi. Tulipokuwa tukikimbia kuelekea kwenye helikopta iliyokuwa ikitungoja Jumapili (Siku ya Yenga) hiyo asubuhi, mimi pamoja na wamishonari wenzangu tulijitahidi sana kutulia. Muda si muda, helikopta ikapaa hewani. Baada ya dakika kumi hivi, tulifika salama kwenye meli ya kijeshi ambayo ilikuwa imetia nanga karibu na pwani.

ASUBUHI iliyofuata, tulipata habari kwamba waasi walipiga bomu hoteli ambamo tulikuwa tumejificha usiku uliotangulia. Vita vya wenyewe kwa wenyewe vya miaka mingi nchini Sierra Leone vilibadilika na kuwa vita vikubwa sana. Wageni wote, pamoja nasi, tulilazimika kukimbia ghafula kutoka nchini. Acha nisimulie tangu mwanzoni jinsi nilivyojikuta katika hali hiyo.

Nililelewa huko British Guiana, nchi ambayo tangu 1966, imekuwa ikiitwa Guyana. Maisha yangu ya mapema katika miaka ya 1950 yalikuwa mazuri na yenye kufurahisha. Wazazi wengi walithamini sana elimu, na vijana walitazamiwa kufanya vyema shuleni. Ninakumbuka siku moja karani fulani wa benki alimuuliza baba yangu hivi: “Kwa nini unalipa pesa nyingi sana za shule ili kuwaelimisha watoto wako?” Baba akamjibu: “Watafanikiwa tu ikiwa watapata elimu bora kabisa.” Wakati huo, alifikiri kwamba elimu bora ingepatikana tu katika shule maarufu. Baada ya muda, maoni yake yangebadilika.

Nilipokuwa na umri wa miaka 11, mama yangu alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alienda kwenye Jumba la Ufalme pamoja na jirani mmoja. Mambo ambayo walisikia usiku huo yaliwasadikisha wote wawili kwamba walikuwa wamepata kweli. Baadaye, mama yangu alimwambia jirani mwingine mambo ambayo yalizungumzwa huko. Baada ya muda, wote watatu walikuwa wakijifunza pamoja na Daphne Harry (baadaye aliitwa Baird) na Rose Cuffie ambao walikuwa wamishonari. Baada ya muda usiozidi mwaka mmoja, Mama na rafiki zake wawili walibatizwa. Miaka mitano baadaye, baba yangu aliachana na Kanisa la Seventh-Day Adventist na kubatizwa akiwa Shahidi wa Yehova.

Tukiwa watoto, mimi na dada zangu wawili, watoto wakubwa katika familia yenye watoto kumi, tulifurahia kukaa kwa saa nyingi sana katika makao ya wamishonari ambako Daphne na Rose waliishi. Pindi kama hizo, tulisikia mambo yaliyoonwa katika utumishi wa shambani yakisimuliwa. Wamishonari hao walikuwa na shangwe nyingi kwa sababu ya kujitahidi sana kuwasaidia wengine kiroho. Nilichochewa na mfano wao nikaanza kutamani kuwa mmishonari.

Lakini ni nini kilichonisaidia kukazia fikira huduma ya wakati wote ingawa watu wangu wa ukoo na wanashule wenzangu walikazia sana kupata elimu zaidi na kazi nzuri? Kulikuwa na nafasi nyingi zenye kuvutia za kufuatia elimu ya sheria, muziki, udaktari, au taaluma nyingine yoyote. Mfano mzuri wa wazazi wangu ulinipa mwongozo ambao nilihitaji. Waliishi kupatana na kweli, walijifunza Biblia kwa bidii, na kujitoa wenyewe kuwasaidia wengine wajifunze juu ya Yehova. * Zaidi ya hayo, waliwakaribisha kwa ukawaida wahudumu wa wakati wote nyumbani mwetu. Shangwe na uradhi ambao ndugu na dada hao walionyesha ulizidisha tamaa yangu ya kuruhusu kazi ya kufanya wanafunzi ifinyange maisha yangu.

Nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 15. Kisha, baada tu ya kumaliza shule ya sekondari, nilianza utumishi wa wakati wote wa upainia. Mtu wa kwanza ambaye nilimsaidia kufanya maendeleo kufikia wakfu na ubatizo alikuwa mfanyakazi wa hospitali anayeitwa Philomena. Shangwe niliyopata nilipomwona akimpenda Yehova ilizidisha tamaa yangu ya kuendelea na huduma ya wakati wote. Muda mfupi baadaye, nilipewa kazi bora katika idara ya serikali ambamo nilikuwa mwandishi. Nilikataa kazi hiyo, badala yake nikaamua kuendelea na upainia.

Nilikuwa bado nikiishi nyumbani, na wamishonari waliendelea kututembelea. Nilifurahia sana kuwasikiliza wakisimulia mambo waliyoona! Mambo hayo yote yalizidisha tamaa yangu ya kuwa mmishonari, hata ingawa nilifikiri haiwezekani. Siku hizo wamishonari walikuwa wakitumwa Guyana na bado wanatumwa nchini humo. Siku moja mnamo 1969, nilishangaa lakini nilifurahi kupokea mwaliko wa kuhudhuria Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) huko Brooklyn, New York.

Mgawo Ambao Sikutarajia

Darasa la 48 la Gileadi lilikuwa na wanafunzi 54 kutoka katika nchi 21. Wanafunzi 17 kati yetu tulikuwa dada waseja. Ingawa miaka 37 imepita sasa, bado ninakumbuka vizuri miezi hiyo mitano ya shule. Tulijifunza mambo mengi sana, kweli za Kimaandiko na pia mapendekezo na mashauri ya kutusaidia katika maisha yetu ya baadaye tukiwa wamishonari. Kwa mfano, nilijifunza kufuata mwongozo, kuwa na usawaziko kuhusiana na mitindo, na kustahimili hali zisizofaa.

Sikuzote wazazi wangu walikazia umuhimu wa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Mtoto yeyote aliyejifanya mgonjwa na hivyo kukataa kuhudhuria mikutano siku ya Jumapili hakuruhusiwa kuhudhuria mazoezi ya kupiga piano au maonyesho ya muziki usiku uliofuata. Hata hivyo, sikuhudhuria mikutano yote kwa muda fulani wakati wa Shule ya Gileadi. Ijumaa moja (Siku ya 5) jioni, nilimpa Don na Dolores Adams kisingizio cha kutohudhuria mikutano. Hao walikuwa wenzi wa ndoa Wanabetheli ambao walinibeba kwa gari lao kwenda mikutanoni. Ah, nina kazi nyingi ya shule, na mambo mengi ya kuandika! Sina wakati wa kuhudhuria Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi! Baada ya kujaribu kunisadikisha kwa muda, Ndugu Adams alisema: “Dhamiri yako na ikuongoze.” Nilifuata shauri lake na sikukosa mikutano usiku huo wala siku nyingine yoyote. Kwa miaka yote, isipokuwa hali zikiwa mbaya sana, sijaruhusu chochote kinizuie kuhudhuria mikutano ya Kikristo.

Karibu katikati ya kipindi cha shule, kulikuwa na uvumi kwamba tutapewa migawo yetu. Sikuzote nilifikiri kwamba ningetumwa Guyana, ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa sana katika kazi ya kuhubiri. Wazia jinsi nilivyoshangaa nilipopata habari kwamba singerudi huko. Badala yake, nilitumwa Sierra Leone, huko Afrika Magharibi. Nilimshukuru sana Yehova kwamba tamaa yangu ya kuwa mmishonari mbali na nyumbani ilitoshelezwa mwishowe!

Mambo Mengi ya Kujifunza

Nilipoiona nchi ya Sierra Leone kwa mara ya kwanza ilikuwa maridadi sana. Ilikuwa na vilima na milima mingi, ghuba na fuo. Hata hivyo, umaridadi mkubwa zaidi wa nchi hiyo ya Afrika Magharibi ni watu wake. Upendo na fadhili yao inawafanya hata wageni wastarehe. Roho hiyo inawasaidia wamishonari kutotamani kurudi nyumbani kwao. Watu wa Sierra Leone wanapenda kuongea kuhusu utamaduni na desturi zao na wanapenda hasa kuwasaidia wageni kujua lugha ya Krio, ambayo ni lugha kuu ya nchi hiyo.

Watu wanaozungumza lugha ya Krio wana methali nyingi zenye kuvutia. Kwa mfano, Tumbili anafanya kazi naye nyani anakula, ni methali inayomaanisha kwamba sikuzote mkulima si mvunaji. Inaeleza vizuri kama nini ukosefu wa haki ambao umeenea ulimwenguni!—Isaya 65:22.

Kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ilifurahisha. Haikuwa rahisi kumkuta mtu ambaye hakupendezwa na Biblia. Kwa miaka mingi, wamishonari na wale ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu wamewasaidia watu, vijana kwa wazee, kutoka malezi na makabila mbalimbali kuikubali kweli.

Erla St. Hill, mmishonari wa kwanza niliyetumika naye, alikuwa mfanyakazi mwenye bidii sana. Alikuwa na bidii nyingi sana katika huduma na pia alitimiza kwa bidii migawo yake katika makao ya wamishonari. Alinisaidia kuelewa umuhimu wa mambo mengi, kama vile kuwafahamu majirani, kuwatembelea Mashahidi na watu wanaopendezwa ambao ni wagonjwa, na kuunga mkono mipango ya mazishi inapowezekana. Pia alinifundisha umuhimu wa kuwatembelea akina ndugu na dada wanaoishi katika eneo hata kama ni kwa muda mfupi sana na kuwasalimu baada ya utumishi wa shambani. Kwa kufanya hivyo, baada ya muda mfupi nilipata akina mama, ndugu, dada, na marafiki, na mgawo wangu ukawa kama nyumbani.—Marko 10:29, 30.

Pia, nilijenga urafiki wa karibu sana na wamishonari wazuri ambao tulitumika pamoja. Kati ya wamishonari hao ni Adna Byrd, ambaye alitumika nchini Sierra Leone kati ya mwaka wa 1978 na 1981, na Cheryl Ferguson, ambaye nimeishi naye katika chumba kimoja kwa miaka 24 ambayo imepita.

Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe Vyaleta Majaribu

Mwaka wa 1997, mwezi mmoja hivi baada ya kuwekwa wakfu kwa majengo mapya ya ofisi ya tawi nchini Sierra Leone, tulilazimika kuhama nchini kwa sababu ya vita, kama nilivyotaja mapema. Miaka sita kabla ya hapo, tulivutiwa na imani ya Mashahidi wa Liberia ambao walikuwa wamekimbilia Sierra Leone kwa sababu ya vita huko Liberia. Wengine wao hawakuja na chochote. Ingawa walikabili hali ngumu, walishiriki katika huduma kila siku. Tuliguswa moyo sana kuona jinsi walivyompenda Yehova na watu.

Kwa kuwa sasa tulikuwa wakimbizi katika nchi ya Guinea, tulifuata mfano wa ndugu hao wa Liberia na kuendelea kumtegemea Yehova na kuutanguliza Ufalme. Baada ya mwaka mmoja, tulirudi Sierra Leone, lakini baada ya miezi saba, vita vilizuka tena na tukalazimika kuhamia Guinea tena.

Punde si punde, tuliambiwa kwamba wapiganaji wa kikundi kimoja walikuwa wanakaa katika makao yetu ya wamishonari huko Kissy na kwamba vitu vyetu vyote vilikuwa vimeporwa au kuharibiwa. Badala ya kushuka moyo, tulishukuru kwa sababu ya kuwa hai. Tulibaki na vitu vichache sana vya kimwili, lakini tulikabiliana na hali hiyo ngumu.

Baada ya kuhamishwa kwa mara ya pili, mimi na mwenzangu Cheryl tulibaki Guinea. Tulihitaji kujifunza Kifaransa. Baadhi ya wamishonari wenzangu walianza mara moja kuongea Kifaransa walichojifunza bila kujali sana kukosea. Lakini mimi, nilichukia kuongea lugha vibaya, kwa hiyo niliongea Kifaransa wakati tu ilipokuwa lazima. Nilifadhaika sana. Nilihitaji kujikumbusha kila siku kusudi langu la kuwa Guinea, yaani, kuwasaidia wengine wamjue Yehova.

Pole kwa pole, nilifanya maendeleo kwa kujifunza, kwa kuwasikiliza wale waliozungumza lugha hiyo vizuri, na kwa msaada wa watoto kutanikoni, kwa sababu watoto wanakuambia waziwazi unapokosea. Kisha, bila kutarajia, msaada ulikuja kwa wakati wake kutoka kwa tengenezo la Yehova. Kuanzia Septemba (Mwezi wa 9) 2001, Huduma Yetu ya Ufalme imekuwa na mapendekezo ya kuwatolea watu wa dini mbalimbali magazeti, vitabu na broshua. Sasa ninahisi nina uhakika zaidi ninaposhiriki katika huduma, hata ingawa siongei Kifaransa kwa usahihi kabisa kama lugha ya mama yangu.

Kulelewa katika familia kubwa bila shaka kumenisaidia kufaulu kuishi na watu wengi. Pindi fulani niliishi na watu 17. Katika miaka 37 ambayo nimekuwa mmishonari, nimeishi na wamishonari wengine zaidi ya 100. Ni pendeleo kubwa kama nini kuwafahamu watu wengi sana wenye nyutu tofauti lakini wote wanatumika wakiwa na kusudi lilelile! Na ni shangwe iliyoje kuwa mfanyakazi mwenzi wa Mungu na kuona watu wakikubali kweli ya Biblia!—1 Wakorintho 3:9.

Katika miaka ambayo nimekuwa mmishonari, nimekosa matukio mengi muhimu katika maisha ya washiriki wa familia yangu, kama vile arusi za wengi wa ndugu na dada zangu. Pia, sijawa na wakati wa kutosha kuwa pamoja na wapwa zangu. Nimejidhabihu kama washiriki wa familia yangu ambao wamenitia moyo bila ubinafsi niendelee na umishonari.

Lakini mambo ambayo nimekosa kwa kutokuwa nyumbani, nimeyapata pindi kwa pindi katika utumishi wangu wa umishonari. Hata ingawa niliamua kubaki mseja, nina watoto wengi wa kiroho, si wale tu ambao nimejifunza nao Biblia bali pia wengine ambao wamekuwa marafiki wangu. Zaidi ya hayo, nimewaona watoto wao wakikua, wakioa na kuolewa, na kuwalea watoto wao wenyewe katika kweli. Sawa na mimi, wengine wao pia wameruhusu kazi ya kufanya wanafunzi ifinyange maisha yao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Mama yangu alifanya upainia kwa miaka zaidi ya 25, na baba yangu alifanya upainia msaidizi baada ya kustaafu.

[Ramani katika ukurasa wa 15]

 

Nilitumwa Sierra Leone, Afrika Magharibi

GUINEA

SIERRA LEONE

[Picha katika ukurasa wa 13]

Katika miaka ya 1950, mimi na dada zangu hawa wawili tulifurahia kukaa pamoja na wamishonari kwa saa nyingi

[Picha katika ukurasa wa 14]

Nikiwa na wanafunzi wenzangu wa darasa la 48 la Gileadi

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kuwekwa wakfu kwa ofisi mpya ya tawi nchini Sierra Leone