Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujitiisha kwa Unyenyekevu Chini ya Wachungaji Wenye Upendo

Kujitiisha kwa Unyenyekevu Chini ya Wachungaji Wenye Upendo

Kujitiisha kwa Unyenyekevu Chini ya Wachungaji Wenye Upendo

“Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee.”—WAEBRANIA 13:17.

1, 2. Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba Yehova na Yesu ni Wachungaji wenye upendo?

YEHOVA MUNGU na Mwana wake, Yesu Kristo, ni Wachungaji wenye upendo. Isaya alitabiri hivi: “Tazama! Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atakuja kama mtu mwenye nguvu, na mkono wake utakuwa ukitawala kwa ajili yake. . . . Atalichunga kundi lake mwenyewe kama mchungaji. Atawakusanya pamoja wana-kondoo kwa mkono wake; naye atawabeba katika kifua chake. Wale wanaonyonya atawaongoza kwa uangalifu.”—Isaya 40:10, 11.

2 Unabii huo unaohusu kurudishwa kwa ibada ya kweli ulitimizwa mara ya kwanza wakati mabaki ya Wayahudi waliporudi Yuda mwaka wa 537 K.W.K. (2 Mambo ya Nyakati 36:22, 23) Ulitimizwa tena wakati Koreshi Mkuu, Yesu Kristo, alipowakomboa mabaki watiwa-mafuta kutoka “Babiloni Mkubwa” mwaka wa 1919. (Ufunuo 18:2; Isaya 44:28) Yeye ni “mkono” wa Yehova wa kutawala. Anawakusanya pamoja kondoo na kuwachunga kwa wororo. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mimi ndiye mchungaji mwema, nami ninawajua kondoo wangu na kondoo wangu wananijua.”—Yohana 10:14.

3. Yehova anaonyesha namna gani kwamba anahangaikia kwa upendo jinsi kondoo wake wanavyotendewa?

3 Unabii wa Isaya 40:10, 11 unakazia wororo ambao Yehova anaonyesha anapowachunga watu wake. (Zaburi 23:1-6) Wakati wa huduma yake duniani, Yesu pia alionyesha kwamba aliwajali kwa wororo wanafunzi wake na watu kwa ujumla. (Mathayo 11:28-30; Marko 6:34) Yehova na Yesu walishutumu ukosefu wa huruma wa wachungaji, au viongozi wa Israeli ambao bila aibu waliyapuuza na kuyatumia vibaya makundi yao ili kujifaidi. (Ezekieli 34:2-10; Mathayo 23:3, 4, 15) Yehova aliahidi hivi: “Nitawaokoa kondoo zangu, nao hawataendelea kuwa tena kitu cha kuporwa; nami nitahukumu kati ya kondoo na kondoo. Nami nitasimamisha juu yao mchungaji mmoja, naye atawalisha, naam, mtumishi wangu Daudi. Yeye mwenyewe atawalisha, na yeye mwenyewe atakuwa mchungaji wao.” (Ezekieli 34:22, 23) Wakati huu wa mwisho, Yesu Kristo, yule Daudi Mkuu, ndiye “mchungaji mmoja” ambaye Yehova amemweka rasmi juu ya watumishi Wake wote duniani, Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine.”—Yohana 10:16.

Kutaniko Lapewa Zawadi Kutoka Mbinguni

4, 5. (a) Yehova amewapa watu duniani zawadi gani yenye thamani? (b) Yesu ametoa zawadi gani kwa kutaniko lake?

4 Yehova alitoa zawadi yenye thamani kwa kutaniko la Kikristo alipomweka Yesu Kristo yule mchungaji mmoja,” juu ya watumishi Wake duniani. Zawadi hiyo ya Kiongozi kutoka mbinguni ilitabiriwa kwenye Isaya 55:4: “Tazama! Nimemtoa kuwa shahidi kwa vikundi vya mataifa, kuwa kiongozi na kamanda kwa vikundi vya mataifa.” Wakristo watiwa-mafuta na washiriki wa “umati mkubwa” wamekusanywa kutoka katika vikundi vyote vya mataifa, makabila, watu, na lugha. (Ufunuo 5:9, 10; 7:9) Wanakuwa kutaniko la kimataifa, “kundi moja,” chini ya uongozi wa “mchungaji mmoja,” Kristo Yesu.

5 Yesu pia ametoa zawadi yenye thamani kwa kutaniko lake duniani. Ametoa wachungaji wadogo walio waaminifu ambao wanamwiga Yehova na Yesu kwa kulichunga kundi kwa wororo. Mtume Paulo alizungumzia zawadi hiyo yenye upendo katika barua yake kwa Wakristo huko Efeso. Aliandika hivi: “‘Alipopanda juu alichukua mateka; alitoa zawadi katika wanadamu.’ . . . Alitoa wengine kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kuwa waeneza-injili, wengine kuwa wachungaji na walimu, kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo.”—Waefeso 4:8, 11, 12.

6. Waangalizi watiwa-mafuta waliotumika katika mabaraza ya wazee wanafananishwa na nini katika Ufunuo 1:16, 20, na tunaweza kusema nini kuhusu wazee waliowekwa rasmi ambao ni sehemu ya kondoo wengine?

6 Hizo “zawadi katika wanadamu” ni waangalizi, au wazee, ambao wamewekwa rasmi na Yehova na Mwana wake, kupitia roho takatifu ili wachunge kondoo kwa wororo. (Matendo 20:28, 29) Mwanzoni, waangalizi hao wote walikuwa wanaume Wakristo waliotiwa mafuta. Katika andiko la Ufunuo 1:16, 20, wale waliotumika katika mabaraza ya wazee katika makutaniko ya watiwa-mafuta walifananishwa na “nyota” au “malaika” katika mkono wa kuume wa Kristo, yaani, wako chini ya mwelekezo wake. Hata hivyo, wakati huu wa mwisho, makutaniko yana idadi kubwa ya wazee Wakristo ambao ni sehemu ya kondoo wengine kwa sababu waangalizi watiwa-mafuta wanazidi kupungua duniani. Kwa kuwa wanawekwa rasmi na wawakilishi wa Baraza Linaloongoza chini ya mwongozo wa roho takatifu, tunaweza kusema kwamba wao pia wako chini ya mkono wa kuume (au, chini ya mwelekezo) wa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo. (Isaya 61:5, 6) Kwa kuwa wazee wa makutaniko yetu wanajinyenyekeza kwa Kristo, Kichwa cha kutaniko, tunapaswa kushirikiana nao kikamili.—Wakolosai 1:18.

Kutii na Kunyenyekea

7. Mtume Paulo alitoa shauri gani kuhusu mtazamo wetu kuelekea waangalizi Wakristo?

7 Wachungaji wetu wa kimbingu, Yehova Mungu na Yesu Kristo, wanatutazamia tutii na kunyenyekea wachungaji hao wadogo ambao wamepewa majukumu kutanikoni. (1 Petro 5:5) Akiongozwa na roho ya Mungu, mtume Paulo aliandika hivi: “Wakumbukeni wale ambao wanaongoza katikati yenu, ambao wamelisema neno la Mungu kwenu, nanyi mnapotafakari jinsi mwisho wa mwenendo wao unavyokuwa, igeni imani yao. Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.”—Waebrania 13:7, 17.

8. Paulo anatuomba ‘tutafakari’ nini, na tunapaswa ‘kutii’ tukiwa na mtazamo gani?

8 Ona kwamba Paulo anatuomba ‘tutafakari,’ au kuchunguza kwa uangalifu, mwisho wa mwenendo wa uaminifu wa wazee na kuiga mifano hiyo ya imani. Kwa kuongezea, anatushauri tunyenyekee na kutii mwelekezo wa wanaume hao waliowekwa rasmi. Msomi mmoja wa Biblia anayeitwa R. T. France anaeleza kwamba katika Kigiriki cha awali, neno ambalo limetafsiriwa “watiini” si “neno la kawaida linalotumiwa kuhusiana na utii, lakini linamaanisha kihalisi ‘kusadiki,’ na linaonyesha kukubali uongozi wao kwa kupenda.” Tunawatii wazee si kwa sababu tu tunaagizwa tufanye hivyo katika Neno la Mungu, lakini pia kwa sababu tunasadiki kwamba wanahangaikia kabisa mambo ya Ufalme na hali yetu njema. Bila shaka, tutakuwa wenye furaha tukikubali uongozi wao kwa kupenda.

9. Mbali na kutii, kwa nini ni muhimu kwetu ‘kunyenyekea’?

9 Namna gani ikiwa hatusadiki kwamba njia ambayo wazee wanatuelekeza tufanye jambo fulani ndiyo njia bora ya kufanya jambo hilo? Huo ndio wakati hasa tunapohitaji kunyenyekea. Ni rahisi kutii wakati kila jambo linaeleweka nasi tunakubaliana na uamuzi wao, lakini je, tutaonyesha kwamba kwa kweli sisi tunanyenyekea na kutii hata wakati ambapo sisi binafsi hatuelewi mwelekezo uliotolewa? Petro, ambaye alikuja kuwa mtume baadaye, alionyesha unyenyekevu wa aina hiyo.—Luka 5:4, 5.

Sababu Nne za Kushirikiana na Waangalizi Wakristo kwa Kupenda

10, 11. Waangalizi “wamelisema neno la Mungu” jinsi gani kwa Wakristo wenzao katika karne ya kwanza na leo?

10 Katika andiko la Waebrania 13:7, 17 linalotajwa hapo juu, mtume Paulo anatoa sababu nne zinazoonyesha kwa nini tunapaswa kunyenyekea na kuwatii waangalizi Wakristo. Sababu ya kwanza ni kwamba “wamelisema neno la Mungu” kwetu. Kumbuka kwamba Yesu anatoa kwa kutaniko “zawadi katika wanadamu” kwa kusudi la “kuwarekebisha upya watakatifu.” (Waefeso 4:11, 12) Alirekebisha upya fikira na mwenendo wa Wakristo wa karne ya kwanza kupitia wachungaji waaminifu walio chini yake. Wengine wao waliongozwa na roho ya Mungu kuandika barua kwa makutaniko. Aliwatumia waangalizi hao waliowekwa rasmi na roho kuwaongoza na kuwajenga Wakristo wa mapema.—1 Wakorintho 16:15-18; 2 Timotheo 2:2; Tito 1:5.

11 Leo, Yesu anatuelekeza kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” anayewakilishwa na Baraza lake Linaloongoza na wazee waliowekwa rasmi. (Mathayo 24:45) Tunatii shauri hili la Paulo kwa kuwa tunamheshimu “mchungaji mkuu,” Yesu Kristo: “Mwatilie maanani wale wanaofanya kazi kwa bidii kati yenu na kuwasimamia ninyi katika Bwana na kuwaonya ninyi.”—1 Petro 5:4; 1 Wathesalonike 5:12; 1 Timotheo 5:17.

12. Waangalizi “wanaendelea kuzilinda nafsi [zetu]” kwa njia gani?

12 Sababu ya pili inayotufanya tushirikiane na waangalizi Wakristo ni kwamba “wanaendelea kuzilinda nafsi [zetu].” Wakigundua katika mtazamo au mwenendo wetu jambo fulani ambalo linaweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho, kwa haraka wanatupa shauri linalohitajiwa wakiwa na kusudi la kuturekebisha upya. (Wagalatia 6:1) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kulinda’ linamaanisha kihalisi “kujinyima usingizi.” Msomi mmoja wa Biblia anasema kwamba neno hilo “linadokeza hali ya mchungaji ya kukaa macho daima.” Zaidi ya kukaa macho daima kiroho, huenda wazee wakakosa usingizi wakihangaikia hali yetu ya kiroho. Je, hatupaswi kushirikiana kwa kupenda na wachungaji hao wadogo wenye upendo, ambao wanafanya yote wanayoweza ili kuiga wororo wa Yesu Kristo, yule “mchungaji mkuu wa kondoo”?—Waebrania 13:20.

13. Waangalizi na Wakristo wote watatoa hesabu kwa nani na kwa njia gani?

13 Sababu ya tatu inayotufanya tushirikiane kwa kupenda na waangalizi ni kwamba wanatulinda “kama wale watakaotoa hesabu.” Waangalizi wanakumbuka kwamba wao ni wachungaji wadogo, wanaotumika chini ya Wachungaji wa kimbingu, Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Ezekieli 34:22-24) Yehova ndiye Mmiliki wa kondoo, ambao ‘aliwanunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe,’ Naye atawatoza hesabu waangalizi waliowekwa rasmi kwa sababu ya jinsi wanavyolitendea kundi Lake, ambalo linapaswa kutendewa “kwa wororo.” (Matendo 20:28, 29) Kwa hiyo, sote tutatoa hesabu kwa Yehova kulingana na jinsi tunavyoitikia mwelekezo wake. (Waroma 14:10-12) Kuwatii wazee waliowekwa rasmi kunathibitisha pia kwamba tunamnyenyekea Kristo, Kichwa cha kutaniko.—Wakolosai 2:19.

14. Ni nini kinachoweza kuwafanya waangalizi Wakristo ‘waugue,’ na matokeo yanaweza kuwa nini?

14 Paulo alitaja sababu ya nne inayopaswa kutufanya tujitiishe kwa unyenyekevu chini ya waangalizi Wakristo. Aliandika hivi: “Ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.” (Waebrania 13:17) Wazee Wakristo wana majukumu mazito sana kama vile kufundisha, kufanya uchungaji, kuongoza katika kazi ya kuhubiri, kutunza familia zao, na kushughulikia matatizo kutanikoni. (2 Wakorintho 11:28, 29) Tukikosa kushirikiana nao, tunafanya kazi yao iwe ngumu zaidi. Hilo litawafanya ‘waugue.’ Kuonyesha roho ya kutoshirikiana hakumpendezi Yehova na kunaweza kutudhuru. Lakini, tunapoonyesha heshima na ushirikiano unaofaa, wazee wanaweza kutimiza wajibu wao kwa shangwe, na hilo linachangia umoja na kutuletea sote shangwe tunaposhiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme.—Waroma 15:5, 6.

Kuonyesha Kwamba Tunanyenyekea

15. Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunatii na kunyenyekea?

15 Kuna njia nyingi zinazofaa za kushirikiana na waangalizi waliowekwa rasmi. Kwa sababu ya mabadiliko ya hali katika eneo, je, wazee wamepanga ili mikutano ya utumishi wa shambani ifanywe siku na wakati ambao unatulazimu kubadili ratiba yetu? Na tujitahidi kabisa kuunga mkono mipango hiyo mipya. Huenda tukapata baraka ambazo hatukutazamia. Je, mwangalizi wa utumishi anatembelea Funzo letu la Kitabu la Kutaniko? Na tushiriki kikamili zaidi katika kazi ya kuhubiri juma hilo. Je, tumepokea mgawo katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Tunapaswa kujitahidi kuhudhuria na kutimiza mgawo wetu. Je, mwangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko ametangaza kwamba ni zamu ya kikundi chetu kusafisha Jumba la Ufalme? Na tumuunge mkono kikamili kadiri afya na uwezo wetu unavyoruhusu. Katika njia hizo na nyingine nyingi, tunaonyesha kwamba tunawanyenyekea wanaume ambao Yehova na Mwana wake wameweka rasmi ili walitunze kundi.

16. Ikiwa mzee hafanyi mambo kupatana na mwelekezo, kwa nini hiyo si sababu ya kutufanya tuasi?

16 Nyakati nyingine, huenda mzee akafanya mambo kwa njia ambayo haipatani na mwelekezo wa jamii ya mtumwa mwaminifu na Baraza lake Linaloongoza. Akiendelea kufanya hivyo, atatozwa hesabu na Yehova, “mchungaji na mwangalizi wa nafsi [zetu].” (1 Petro 2:25) Lakini hatupaswi kutumia makosa au kasoro yoyote ya wazee fulani kuwa kisingizio cha kutojitiisha chini yao. Yehova habariki kutotii na uasi.—Hesabu 12:1, 2, 9-11.

Yehova Anawabariki Wale Wanaoshirikiana na Waangalizi kwa Kupenda

17. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea waangalizi?

17 Yehova Mungu anajua kwamba wanaume ambao amewaweka rasmi kuwa waangalizi si wakamilifu. Hata hivyo, anawatumia, na kupitia roho yake, anawachunga watu wake duniani. Wazee pamoja na sisi sote tumeona kwamba “nguvu zinazopita zile za kawaida [ni] za Mungu na si zile za kutoka ndani yetu wenyewe.” (2 Wakorintho 4:7) Kwa hiyo, tunapaswa kumshukuru Yehova kwa ajili ya yale anayotimiza kupitia waangalizi wetu waaminifu, nasi tunapaswa kushirikiana nao kwa kupenda.

18. Tunaponyenyekea waangalizi wetu, kwa kweli tunafanya nini?

18 Waangalizi wanafanya yote wanayoweza ili kuishi kupatana na maelezo ya Yehova kuhusu wachungaji waliowekwa rasmi juu ya kundi lake katika siku za mwisho. Maelezo hayo yako katika Yeremia 3:15: “Nitawapa wachungaji wenye kupatana na moyo wangu, na hakika wao watawalisha ninyi kwa ujuzi na ufahamu.” Bila shaka wazee walio miongoni mwetu wanafanya kazi nzuri ya kufundisha na kuwalinda kondoo wa Yehova. Acheni tuendelee kuonyesha kwamba tunathamini kazi yao ngumu kwa kushirikiana nao kwa kupenda, kuwatii, na kuwanyenyekea. Tukifanya hivyo, tutaonyesha kwamba tunawathamini Wachungaji wetu wa kimbingu, Yehova Mungu na Yesu Kristo.

Kwa Kupitia

• Yehova na Yesu Kristo wameonyesha jinsi gani kwamba wao ni Wachungaji wenye upendo?

• Mbali na kutii, kwa nini kunyenyekea kunahitajiwa?

• Tunaweza kuonyesha kwa njia gani zinazofaa kwamba tunanyenyekea?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Wazee Wakristo wananyenyekea uongozi wa Kristo

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kuna njia nyingi za kuonyesha kwamba tunawanyenyekea wachungaji waliowekwa rasmi na Yehova