Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutafuta Majibu Yanayofaa

Kutafuta Majibu Yanayofaa

Kutafuta Majibu Yanayofaa

Ninaweza kutunza afya yangu jinsi gani?

Ninaweza kufanya nini ili maisha ya familia yangu yawe yenye furaha?

Ninaweza kufanya nini ili nifaulu kudumisha kazi?

JE, UMEWAHI kujiuliza mojawapo ya maswali hayo? Je, ulipata majibu mazuri yaliyofaa hali zako? Kila mwaka, vitabu tofauti-tofauti 2,000 hivi ambavyo vinazungumzia mambo hayo na pia mambo mengine muhimu vinachapishwa. Nchini Uingereza peke yake, kila mwaka watu wanatumia kufikia pauni milioni 80 (karibu dola milioni 150 za Marekani) kununua vitabu vinavyotoa mashauri kuhusu jinsi ya kukabiliana na matatizo ya maisha. Huko Marekani, biashara ya vitabu vyenye mashauri ya kujisaidia kibinafsi inachuma dola milioni 600 hivi kwa mwaka. Bila shaka, si wewe tu unayetafuta mashauri mazuri kuhusu jinsi ya kushughulika na maisha ya kila siku.

Kuhusu mashauri yanayopatikana katika vitabu hivyo vingi, mtungaji mmoja alisema: “Vitabu vingi vipya vinarudia tu yale ambayo tayari yameandikwa.” Kwa kweli, mashauri mengi yaliyo katika vitabu hivyo yanarudia tu mashauri yenye hekima yaliyo katika kimoja kati ya vitabu vya kale zaidi ulimwenguni. Kitabu hicho kimeenezwa zaidi ya vitabu vingine vyote ulimwenguni. Kimetafsiriwa kikiwa kizima au kwa sehemu katika lugha 2,400. Kwa ujumla, nakala zaidi ya bilioni 4.6 za kitabu hicho zimechapishwa duniani pote. Kitabu hicho si kingine ila ni Biblia.

Biblia inasema hivi waziwazi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Timotheo 3:16) Ni kweli kwamba Biblia haikuandikwa ikiwa kitabu cha mwongozo wa kujisaidia kibinafsi. Kusudi lake kuu ni kuwafunulia wanadamu mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, Biblia ina habari nyingi kuhusu jinsi ya kukabiliana na matatizo yanayotupata sote kwa ukawaida, na inaahidi kwamba wale wanaofuata mwongozo wake watajifunza kujifaidi wenyewe. (Isaya 48:17, 18) Mashauri mazuri ya Biblia yanapotumiwa, yanaleta mafanikio sikuzote, haidhuru mtu ana elimu gani, ni wa jamii au utamaduni gani. Mbona usichunguze habari inayofuata na ukate kauli yako mwenyewe ikiwa mashauri ambayo Biblia inatoa kuhusu mambo kama vile afya, familia, na kazi ya kuajiriwa, yanafaa?