Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoa Dhabihu Ambazo Zinampendeza Mungu

Kutoa Dhabihu Ambazo Zinampendeza Mungu

Kutoa Dhabihu Ambazo Zinampendeza Mungu

“UHAI ulitokana na kifo, ndivyo walivyoamini Waazteki ambao waliwadhabihu wanadamu kwa kiwango kisicho na kifani huko Mesoamerika,” kinasema kitabu kimoja (The Mighty Aztecs). Kitabu hicho kinaendelea kusema hivi: “Kadiri milki hiyo ilivyopanuka, ndivyo wanadamu wengi zaidi walivyotolewa dhabihu ili kujenga imani katika milki hiyo.” Kitabu kingine kinasema kwamba Waazteki waliwadhabihu wanadamu 20,000 kwa mwaka.

Katika historia yote, wanadamu wametoa dhabihu tofauti-tofauti kwa miungu yao labda kwa sababu ya woga na wasiwasi au kwa sababu ya hatia na majuto. Kwa upande mwingine, Biblia inaonyesha kwamba dhabihu fulani zilianzishwa na Mungu mweza-yote, Yehova. Kwa hiyo, inafaa kuuliza hivi: Ni dhabihu gani zinazompendeza Mungu? Na je, matoleo na dhabihu zinapaswa kuwa sehemu ya ibada leo?

Matoleo na Dhabihu Katika Ibada ya Kweli

Taifa la Israeli lilipoanzishwa, Yehova alitoa maagizo yaliyo wazi kuhusu njia ambayo alitaka Waisraeli watumie kumwabudu, na ilitia ndani dhabihu na matoleo. (Hesabu, sura ya 28 na 29) Matoleo fulani yalikuwa mazao ya nchi; mengine yalihusu kudhabihu wanyama kama vile, ng’ombe-dume, kondoo, mbuzi, hua, na njiwa-tetere. (Mambo ya Walawi 1:3, 5, 10, 14; 23:10-18; Hesabu 15:1-7; 28:7) Kulikuwa na matoleo mazima ya kuteketezwa ambayo yalipasa kuteketezwa kabisa katika moto. (Kutoka 29:38-42) Kulikuwa pia na dhabihu za ushirika. Wale waliotoa dhabihu hizo walishiriki kwa kula kutokana na kile kilichotolewa dhabihu kwa Mungu.—Mambo ya Walawi 19:5-8.

Matoleo na dhabihu zote ambazo zilitolewa kwa Mungu chini ya Sheria ya Musa zilikuwa njia ya kumwabudu Mungu na kumtambua kuwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. Kupitia dhabihu hizo, Waisraeli walionyesha shukrani zao kwa Yehova kwa sababu ya kuwabariki na kuwalinda, na pia walisamehewa dhambi zao. Walibarikiwa sana kadiri walivyoendelea kufuata kwa uaminifu matakwa ya Yehova ya ibada.—Methali 3:9, 10.

Jambo muhimu zaidi kwa Yehova lilikuwa mtazamo wa wale waliotoa dhabihu. Kupitia nabii wake Hosea, Yehova alisema hivi: “Mimi ninapendezwa na fadhili zenye upendo, na si dhabihu; ninapendezwa na kumjua Mungu kuliko matoleo mazima ya kuteketezwa.” (Hosea 6:6) Kwa hiyo, watu walipoacha ibada ya kweli na kuwa na mwenendo mpotovu na kumwaga damu isiyo na hatia, dhabihu ambazo walikuwa wakitoa kwenye madhabahu ya Yehova hazikuwa na thamani yoyote. Ndiyo sababu Yehova aliliambia hivi taifa la Israeli kupitia Isaya: “Dhabihu zenu nyingi zina faida gani kwangu? . . . Nimetosheka na matoleo mazima ya kuteketezwa ya kondoo-dume na mafuta ya wanyama waliolishwa vizuri; nami sikupendezwa na damu ya ng’ombe-dume wachanga na wana-kondoo na mbuzi-dume.”—Isaya 1:11.

“Jambo Ambalo Sikuamuru”

Tofauti kabisa na Waisraeli, wakaaji wa Kanaani waliwatoa watoto wao kuwa dhabihu kwa miungu yao, kutia ndani mungu wa Waamoni aliyeitwa Moleki, pia aliitwa Milkomu au Moloki. (1 Wafalme 11:5, 7, 33; Matendo 7:43) Kitabu kimoja (Halley’s Bible Handbook) kinasema: “Wakanaani walikuwa na desturi ya kidini ya kuabudu kwa kujihusisha na ukosefu wa adili katika ngono mbele za miungu yao; kisha, waliwaua na kuwatoa watoto wao wazaliwa wa kwanza kuwa dhabihu kwa miungu hiyo.”

Je, mazoea hayo yalimpendeza Yehova Mungu? Bila shaka hapana. Waisraeli walipokuwa karibu kuingia katika nchi ya Kanaani, Yehova aliwapa amri iliyoandikwa katika andiko la Mambo ya Walawi 20:2, 3: “Utawaambia wana wa Israeli, ‘Mtu yeyote wa wana wa Israeli, na mkaaji mgeni yeyote anayekaa akiwa mgeni katika Israeli, anayempa Moleki yeyote kati ya uzao wake, lazima auawe. Watu wa nchi watampiga kwa mawe mpaka afe. Mimi nami, nitauweka uso wangu juu ya mtu huyo, nami nitamkatilia mbali kutoka katikati ya watu wake, kwa sababu amempa Moleki baadhi ya uzao wake kwa kusudi la kupatia unajisi mahali pangu patakatifu na kulitia unajisi jina langu takatifu.’”

Ingawa huenda likaonekana kuwa jambo lisiloaminika, Waisraeli fulani walioacha ibada ya kweli walifuata zoea hilo lililoongozwa na roho waovu la kuwadhabihu watoto wao kwa miungu ya uwongo. Kuhusu hilo, Zaburi 106:35-38 inasema hivi: “Wakachangamana na hayo mataifa na kuanza kujifunza matendo yao. Nao waliendelea kutumikia sanamu zao, nazo zikawa mtego kwao. Nao wakawa wakiwatoa dhabihu wana wao na binti zao kwa roho waovu. Kwa hiyo wakaendelea kumwaga damu isiyo na hatia, damu ya wana wao na binti zao, ambao waliwatoa dhabihu kwa sanamu za Kanaani; na nchi ikachafuliwa na umwagaji wa damu.”

Akionyesha chuki yake kuelekea zoea hilo, Yehova alisema hivi kuhusu wana wa Yuda kupitia nabii wake Yeremia: “Wameyaweka machukizo yao katika nyumba ambayo jina langu limeitwa juu yake, ili kuitia unajisi. Nao wamejenga mahali pa juu pa Tofethi, palipo katika bonde la mwana wa Hinomu, ili kuwateketeza wana wao na binti zao katika moto, jambo ambalo sikuamuru wala halikuingia moyoni mwangu.”—Yeremia 7:30, 31.

Kwa sababu ya kujihusisha na mazoea kama hayo yenye kuchukiza, mwishowe taifa la Israeli lilipoteza kibali cha Mungu. Jiji lake kuu, Yerusalemu, liliharibiwa hatimaye, na watu wakapelekwa utekwani huko Babiloni. (Yeremia 7:32-34) Ni wazi kwamba zoea la kuwatoa wanadamu dhabihu halitokani na Mungu wa kweli wala si sehemu ya ibada safi. Kuwatoa wanadamu kuwa dhabihu kwa njia yoyote ile ni zoea linaloongozwa na roho waovu, na waabudu wa kweli wa Mungu wanakataa kitu chochote ambacho kinahusiana na zoea kama hilo.

Dhabihu ya Fidia ya Kristo Yesu

Hata hivyo, huenda watu fulani wakauliza hivi: ‘Basi, kwa nini Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli ilitia ndani dhabihu za wanyama?’ Mtume Paulo alizungumzia swali hilo naye anatoa jibu: “Basi, kwa nini Sheria? Iliongezwa ili kufanya makosa yawe wazi, mpaka ufike uzao ambao ulikuwa umepewa ahadi . . . Kwa sababu hiyo Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo.” (Wagalatia 3:19-24) Dhabihu za wanyama chini ya Sheria ya Musa zilifananisha dhabihu kubwa zaidi ambayo Yehova Mungu angetoa kwa ajili ya wanadamu, dhabihu ya Mwana wake, Yesu Kristo. Yesu alizungumzia tendo hilo la upendo aliposema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

Akichochewa na upendo kwa Mungu na kwa wanadamu, Yesu alitoa kwa kupenda uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe fidia kwa ajili ya wazao wa Adamu. (Waroma 5:12, 15) Yesu alisema hivi: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Hakuna mtu mwingine yeyote duniani ambaye angeweza kuwakomboa wanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo, ambamo waliuzwa na dhambi ya kwanza ya Adamu. (Zaburi 49:7, 8) Hivyo, Paulo alieleza kwamba Yesu “aliingia, si kwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe-dume wachanga, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote ndani ya mahali patakatifu na kupata ukombozi wa milele kwa ajili yetu.” (Waebrania 9:12) Kwa kukubali damu ya Yesu ya kidhabihu, Mungu ‘aliifuta kabisa ile hati iliyoandikwa kwa mkono kutupinga.’ Yaani, Yehova aliondoa agano la Sheria, pamoja na matakwa yake ya matoleo na dhabihu, hivyo akaleta ‘zawadi ya uzima wa milele.’—Wakolosai 2:14; Waroma 6:23.

Dhabihu na Matoleo ya Kiroho

Kwa kuwa dhabihu na matoleo ya wanyama hayahitajiwi tena katika ibada ya kweli, je, tunahitajiwa kutoa dhabihu zozote leo? Bila shaka. Yesu Kristo aliishi maisha ya kujidhabihu alipomtumikia Mungu na mwishowe kujitoa mwenyewe kwa ajili ya wanadamu. Kwa hiyo, alitangaza hivi: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.” (Mathayo 16:24) Hilo linamaanisha kwamba mtu yeyote anayetaka kuwa mfuasi wa Yesu ni lazima atoe dhabihu fulani. Ni dhabihu gani hizo?

Kwanza, mfuasi wa kweli wa Kristo haishi tena kwa ajili yake mwenyewe bali anaishi akiwa na kusudi la kufanya mapenzi ya Mungu. Anatanguliza mapenzi ya Mungu kabla ya mapenzi na tamaa zake mwenyewe. Ona jinsi mtume Paulo anavyoeleza jambo hilo: “Nawasihi ninyi kwa huruma za Mungu, akina ndugu, mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri. Na acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Waroma 12:1, 2.

Zaidi ya hayo, Biblia inaonyesha kwamba maneno yetu ya sifa yanaweza kuonwa kuwa dhabihu zinazotolewa kwa Yehova. Nabii Hosea alitumia maneno “ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu,” ambayo yanaonyesha kwamba Mungu anaona sifa za midomo yetu kuwa moja kati ya dhabihu bora zaidi. (Hosea 14:2) Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo Waebrania: “Tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.” (Waebrania 13:15) Leo, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kuhubiri kwa bidii sana habari njema na kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Wanamtolea Mungu dhabihu za sifa mchana na usiku duniani pote.—Ufunuo 7:15.

Zaidi ya kuhubiri, kuwatendea wengine mema ni kati ya dhabihu ambazo zinampendeza Mungu. “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine,” akahimiza Paulo, “kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” (Waebrania 13:16) Kwa kweli, ili dhabihu za sifa zimpendeze Mungu, wale wanaozitoa wanapaswa kuwa na mwenendo mzuri. Paulo alishauri hivi: “Jiendesheni kwa namna inayostahili habari njema juu ya Kristo.”—Wafilipi 1:27; Isaya 52:11.

Kama nyakati zilizopita, dhabihu zote ambazo zinatolewa ili kuunga mkono ibada ya kweli zitaleta shangwe kubwa na baraka nyingi kutoka kwa Yehova. Kwa hiyo, acheni tufanye yote tunayoweza ili kutoa dhabihu ambazo zinampendeza Mungu kikweli!

[Picha katika ukurasa wa 18]

“Wana wao na binti zao . . . waliwatoa dhabihu kwa sanamu za Kanaani”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wakristo wa kweli wanatoa dhabihu ambazo zinampendeza Mungu kwa kuhubiri habari njema na kuwasaidia watu kwa njia nyingine