Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mashauri Yanayofaa Maishani!

Mashauri Yanayofaa Maishani!

Mashauri Yanayofaa Maishani!

KUSUDI kuu la mashauri mengi yaliyo katika vitabu vingi vya kujisaidia vinavyopatikana leo ni kuwasaidia watu walio na matatizo maishani. Biblia ni tofauti. Ingawa mashauri yake yanaweza kuwasaidia watu walio na matatizo, Biblia inafanya mengi zaidi. Mashauri yake yanamsaidia mtu kuepuka makosa ambayo yanaweza kuleta matatizo yasiyo ya lazima maishani.

Biblia inaweza “kuwapa werevu wale wasio na uzoefu, kumpa kijana ujuzi na uwezo wa kufikiri.” (Methali 1:4) Ukifuata mashauri ya Biblia, “uwezo wa kufikiri utakutunza, utambuzi utakulinda, ili kukukomboa kutoka katika njia mbaya.” (Methali 2:11, 12) Fikiria mifano hususa inayoonyesha jinsi kufuata mashauri ya Biblia kunavyoweza kuilinda afya yako, kuboresha maisha yako ya familia, na kukufanya uwe mwajiri au mfanyakazi bora.

Epuka Kunywa Vileo Kupita Kiasi

Biblia haikatazi kunywa vileo kwa kiasi. Mtume Paulo alitaja faida za kitiba za kutumia divai alipomshauri hivi kijana Timotheo: “Utumie divai kidogo kwa ajili ya tumbo lako na ugonjwa wako wa mara kwa mara.” (1 Timotheo 5:23) Maandiko mengine ya Biblia yanaonyesha kwamba Mungu hakukusudia divai itumiwe tu kama dawa. Inasemekana kwamba divai “hufanya moyo wa mwanadamu anayeweza kufa ushangilie.” (Zaburi 104:15) Hata hivyo, Biblia inaonya kuhusu kuwa “watumwa wa divai nyingi sana.” (Tito 2:3) Inasema: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno, kati ya watu wanaokula nyama kwa ulafi. Kwa maana mlevi na mlafi watakuwa maskini.” (Methali 23:20, 21) Matokeo yanakuwa nini mtu anapopuuza mashauri hayo yenye usawaziko? Fikiria mambo ya hakika katika nchi chache tu.

Ripoti moja (Global Status Report on Alcohol 2004) ya Shirika la Afya Ulimwenguni inasema hivi: “Matatizo yanayohusiana na vileo yanagharimu watu wa Ireland dola bilioni 3 hivi za Marekani kila mwaka.” Ripoti hiyo inasema kwamba kiasi hicho kikubwa cha fedha kinatia ndani “gharama za matibabu (dola milioni 350), hasara ya misiba ya barabarani (dola milioni 380 ), hasara ya jeuri inayohusiana na vileo (dola milioni 126), na hasara kazini kwa kuwa wafanyakazi wanakosa kufika kazini kwa sababu ya kunywa vileo (dola milioni 1300).”

Hasara kubwa zaidi kuliko hasara ya kifedha inayosababishwa na matumizi mabaya ya vileo ni kuteseka kwa wanadamu. Kwa mfano, nchini Australia, katika muda wa miezi 12 tu, zaidi ya watu nusu milioni walitendewa vibaya na watu waliokuwa wamekunywa vileo. Huko Ufaransa, inasemekana kwamba matumizi mabaya ya vileo yanasababisha asilimia 30 ya visa vya jeuri nyumbani. Unapofikiria hayo, je, huoni kwamba shauri la Biblia kuhusu vileo linafaa?

Epuka Mazoea Yanayochafua Mwili

Muda mrefu uliopita, katika mwaka wa 1942, wakati ambapo zoea la kuvuta sigara lilipendwa na watu wengi, gazeti la Mnara wa Mlinzi liliwasaidia wasomaji wake kutambua kwamba kutumia tumbaku ni kuvunja kanuni za Biblia na kwamba zoea hilo linapaswa kuepukwa. Habari fulani iliyochapishwa mwaka huo ilisema kwamba ni lazima wale wanaotaka kumpendeza Mungu wafuate amri ya Biblia kuhusu ‘kujisafisha wenyewe kila unajisi wa mwili na roho.’ (2 Wakorintho 7:1) Leo, miaka 65 hivi baadaye, je, hatukubali kwamba shauri hilo linalotegemea Biblia lilifaa?

Mnamo mwaka wa 2006, Shirika la Afya Ulimwenguni lilisema kwamba matumizi ya tumbaku ni “kisababishi cha pili kikuu cha vifo ulimwenguni.” Kila mwaka, watu milioni tano hivi wanakufa kwa sababu ya kutumia tumbaku. Kwa kulinganishwa, karibu watu milioni tatu wanakufa kila mwaka kutokana na UKIMWI. Inakadiriwa kwamba katika karne ya 20 watu milioni 100 walikufa kwa sababu ya uvutaji wa sigara. Idadi hiyo inakaribia ile ya watu wote waliouawa katika vita vyote vilivyopiganwa katika karne hiyo. Kwa kweli, shauri lenye hekima la kuepuka tumbaku linakubaliwa na wengi leo.

“Ukimbieni Uasherati”

Watu wengi hawataki kukubali maoni ya Biblia kuhusu masuala ya ngono. Kinyume na yale ambayo wengi wameshawishiwa kuamini, Biblia haisemi kwamba kila tamaa ya ngono ni dhambi. Lakini inatoa mashauri mazuri kuhusu jinsi watu wanavyopaswa kutenda kuhusiana na tamaa yao ya ngono. Biblia inafundisha kwamba mwanamume na mwanamke ambao wamefunga ndoa ndio tu wanaoruhusiwa kufanya ngono. (Mwanzo 2:24; Mathayo 19:4-6; Waebrania 13:4) Mahusiano ya ngono yanawapa wenzi wa ndoa nafasi ya kuonyeshana upendo mwororo. (1 Wakorintho 7:1-5) Watoto wowote wanaozaliwa na wenzi hao wa ndoa wanafaidika kwa sababu wana wazazi wawili wanaopendana.—Wakolosai 3:18-21.

Biblia inaamuru hivi kuhusu upotovu wa kingono: “Ukimbieni uasherati.” (1 Wakorintho 6:18) Tuna sababu gani moja ya kukimbia uasherati? Mstari huo unaendelea kusema hivi: “Kila dhambi nyingine ambayo mtu huenda akafanya iko nje ya mwili wake, lakini yeye aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” Kunakuwa na matokeo gani wakati mashauri ya Biblia kuhusu masuala ya ngono yanapopuuzwa?

Fikiria hali ilivyo nchini Marekani. Kati ya nchi zilizoendelea, Marekani ndiyo nchi iliyo na idadi kubwa zaidi ya matineja wanaopata mimba—karibu matineja 850,000 kila mwaka. Watoto wengi ambao mama zao hawakutoa mimba wanalelewa na akina mama ambao hawajaolewa. Hapana shaka kwamba baadhi ya akina mama hao vijana wanajitahidi wawezavyo kuwalea watoto wao kwa upendo na nidhamu, na baadhi yao wanafanikiwa. Hata hivyo, ukweli unaoumiza ni kwamba inaelekea wana wa akina mama hao matineja watafungwa gerezani na binti zao watapata mimba wakiwa matineja. Baada ya kuchunguza takwimu za makumi kadhaa ya miaka iliyopita, mtafiti Robert Lerman aliandika hivi: “Inaelekea kwamba kuzuka kwa familia za mzazi mmoja kumechangia kuongezeka kwa matatizo mengine ya kijamii kama vile idadi kubwa ya watoto wanaoacha shule, matumizi ya vileo na dawa za kulevya, watoto wanaobalehe kupata mimba na kuzaa, na ujeuri miongoni mwa vijana.”

Wale wanaojihusisha na ukosefu wa adili katika ngono, wanahatarisha afya yao ya kimwili na ya kiakili. Kwa mfano, gazeti moja (Pediatrics) linaripoti hivi: “Takwimu zinaonyesha kwamba vijana wanaobalehe ambao wanajihusisha katika ngono wanakabili hatari kubwa ya kushuka moyo na kujiua.” Shirika la Marekani la Afya ya Jamii linasema hivi kuhusu hatari nyinginezo za afya: “Zaidi ya nusu ya watu wote [nchini Marekani] watapata ugonjwa mmoja wa zinaa wakati fulani maishani mwao.” Fikiria maumivu na mateso mengi ambayo yangeepukwa ikiwa mashauri yanayofaa ya Biblia kuhusu ngono yangefuatwa!

Jenga Vifungo Imara vya Familia

Biblia inasema mengi zaidi ya kutuonya tuepuke mazoea yanayodhuru. Ona mashauri mazuri ya Biblia kuhusu jinsi ya kuboresha maisha ya familia.

Neno la Mungu linasema: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:28) Badala ya kuwapuuza wake zao, waume wanahimizwa wakae nao ‘kulingana na ujuzi, wakiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke.’ (1 Petro 3:7) Kuhusu kutoelewana ambako kunaweza kutokea, waume wanashauriwa hivi: “Endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Wakolosai 3:19) Je, hukubali kwamba mume anayefuata shauri hilo atapendwa na kuheshimiwa na mke wake?

Biblia inawapa wake mwongozo huu: “Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko . . . Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:22, 23, 33) Je, huoni kwamba mke ambaye anafuata shauri hilo anapozungumza na mume wake au anapozungumza kumhusu atapendwa sana na mume wake?

Kuhusu kuwalea watoto, Biblia inawashauri ninyi wazazi mzungumze na watoto wenu ‘mnapoketi katika nyumba yenu na mnapotembea barabarani na mnapolala na mnapoamka.’ (Kumbukumbu la Torati 6:7) Akina baba hasa wanaagizwa wawape watoto wao mwongozo wa kiadili na nidhamu yenye upendo. Neno la Mungu linasema: “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Nao watoto wanaambiwa hivi: “Watiini wazazi wenu,” tena “mheshimu baba yako na mama yako.” *Waefeso 6:1, 2.

Je, huoni kwamba familia zitafaidika zikifuata mashauri hayo? Huenda ukasema ‘Ndiyo, ni mashauri mazuri, lakini je, yanafaa?’ Tunakualika utembelee Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu. Humo utakutana na familia ambazo zinajitahidi kufuata mashauri yenye hekima kutoka katika Biblia. Zungumza na familia hizo. Angalia jinsi washiriki wake wanavyotendeana. Utajionea mwenyewe kwamba kwa kweli kuishi kulingana na kanuni za Biblia kunafanya familia ziwe na furaha!

Mfanyakazi Mwenye Bidii na Mwajiri wa Kazi Mnyoofu

Biblia inasema nini kuhusu tatizo la kawaida la kudumisha kazi? Inasema kwamba inaelekea mfanyakazi aliye stadi katika kazi yake atathaminiwa na kuthawabishwa. “Je, umemwona mtu stadi katika kazi yake?” Mfalme Sulemani mwenye hekima aliuliza. “Yeye atasimama mbele ya wafalme.” (Methali 22:29) Kwa upande mwingine, “mtu mvivu” ni mwenye kuudhi kama “moshi kwenye macho” ya mtu aliyemwajiri kazi. (Methali 10:26) Biblia inawahimiza wafanyakazi wawe wanyoofu na wenye bidii. “Mwizi asiibe tena, bali afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema.” (Waefeso 4:28) Shauri hilo linatumika hata wakati ambapo mwajiri wa kazi hatazami. “Watiini katika kila jambo wale ambao ni mabwana zenu katika maana ya kimwili, si kwa matendo ya utumishi wa macho, kama wenye kupendeza wanadamu, bali kwa unyoofu wa moyo, kwa kumwogopa Yehova.” (Wakolosai 3:22) Ikiwa wewe ni mwajiri wa kazi, je, hungemthamini mfanyakazi anayefuata shauri hilo?

Kwa mfano, Biblia inawakumbusha hivi waajiri wa kazi: “Mfanyakazi anastahili mshahara wake.” (1 Timotheo 5:18) Kulingana na Sheria ya Mungu kwa Waisraeli, waajiri wa kazi walipaswa kuwapa wafanyakazi mshahara wanaostahili bila kukawia. “Usimpunje mwenzako, wala usinyang’anye. Usikae na mshahara wa mfanyakazi wa kukodiwa usiku kucha mpaka asubuhi,” akaandika Musa. (Mambo ya Walawi 19:13) Je, hungefurahi kumfanyia kazi mwajiri ambaye anatii mwelekezo wa Biblia na kukupa mshahara unaostahili bila kukawia?

Chanzo Bora Kabisa cha Hekima

Je, hushangai kuona kitabu cha zamani kama Biblia kikiwa na mashauri yanayofaa sana leo? Biblia imeendelea kuwafaidi watu huku vitabu vingine vikipoteza faida yake kwa sababu Biblia si neno la wanadamu bali ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

Tunakuhimiza utumie wakati ili kulielewa zaidi Neno la Mungu. Ukifanya hivyo, utaanza kusitawisha upendo kumwelekea Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu. Fuata mashauri anayotoa, nawe utaona yakikulinda kutokana na madhara na kukusaidia kuboresha maisha yako. Kwa kufanya hivyo, ‘utamkaribia Mungu, naye atakukaribia wewe.’ (Yakobo 4:8) Hakuna kitabu kingine chochote kinachoweza kukusaidia kufanya hivyo kama Biblia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Ili upate habari zaidi kuhusu kanuni za Biblia zinazoweza kuisaidia familia yako, ona kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Je, unaona maoni ya Biblia kuhusu vileo yanafaa?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Je, unakubaliana na shauri la Biblia kuhusu kuepuka tumbaku?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kufuata mashauri ya Biblia kunaboresha maisha ya familia

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

Globe: Based on NASA photo