Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Paulo anamaanisha nini anaposema kwamba ni lazima mjane awe “mke wa mume mmoja” ili astahili kusaidiwa na kutaniko la Kikristo?—1 Timotheo 5:9.

Kwa kuwa mtume Paulo alikuwa akizungumza kuhusu mjane, ni wazi kwamba maneno “mke wa mume mmoja” yanaonyesha hali yake kabla ya kuwa mjane. Je, hilo linamaanisha kwamba mjane huyo aliolewa mara moja tu? Au huenda maneno ya Paulo yana maana nyingine? *

Watu fulani wamedai kwamba Paulo alikuwa akizungumza kuhusu wajane ambao walikuwa wameolewa mara moja tu. Ni kweli kwamba katika tamaduni na jamii nyingi, mjane ambaye alibaki bila kuolewa alionwa kuwa mwenye sifa nzuri sana. Hata hivyo, maoni hayo yanapingana na mambo ambayo Paulo aliandika katika barua nyingine. Kwa mfano, kwa Wakristo Wakorintho, alieleza wazi kuwa ingawa alionelea kwamba mjane angekuwa na furaha zaidi ikiwa angebaki bila kuolewa, “yuko huru kuolewa na yeyote anayemtaka, katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39, 40; Waroma 7:2, 3) Kwa kuongezea, katika barua yake kwa Timotheo, Paulo alisema: “Natamani wanawake wajane ambao ni vijana waolewe.” (1 Timotheo 5:14) Kwa hiyo, mjane aliyeamua kuolewa tena hangeshutumiwa.

Basi tunapaswa kuelewa namna gani maneno ya Paulo kwa Timotheo? Maneno “mke wa mume mmoja” yanapatikana katika mstari huo peke yake. Katika lugha ya awali, yanamaanisha kihalisi “mwanamke wa mwanamume mmoja.” Kwa wazi, maneno hayo yanalingana na yale ambayo Paulo alitumia mara kadhaa katika barua zake, yaani, “mume wa mke mmoja,” au “mwanamume wa mwanamke mmoja” katika lugha za awali. (1 Timotheo 3:2, 12; Tito 1:6) Paulo alitumia maneno “mume wa mke mmoja” alipotaja sifa za kustahili za waangalizi Wakristo na watumishi wa huduma. Katika maandiko yaliyotajwa, maneno hayo yanamaanisha kwamba ili mwanamume astahili kupata mapendeleo katika kutaniko la Kikristo, ikiwa ameoa, anapaswa kuwa mwaminifu na mshikamanifu kwa mke wake na kuwa bila shtaka lolote la kiadili. * Kupatana na hilo, inaonekana kwamba maneno yaliyo katika 1 Timotheo 5:9 yanakazia jambo hilohilo: Ili mjane astahili kusaidiwa na kutaniko, lazima awe alikuwa mke mshikamanifu na mwenye ujitoaji ambaye alikuwa mwaminifu kwa mume wake alipokuwa hai na hapaswi kuwa na shtaka lolote la kiadili. Sifa nyingine za kustahili ambazo zinatajwa na Paulo zinamhusu mjane wa aina hiyo.—1 Timotheo 5:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Zoea la mke mmoja kuwa na waume wengi wakati uleule, halikukubaliwa huko Ugiriki na Roma nyakati za mitume. Kwa hivyo, haielekei kwamba Paulo alikuwa akimwandikia Timotheo kuhusu zoea hilo wala hakuwa akimshutumu mtu yeyote mwenye zoea hilo.

^ fu. 5 Jambo hili limezungumziwa katika Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1996, (15/10/1996), ukurasa wa 17, na “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo la Aprili 1, 1984, (1/4/1984), ukurasa wa 23.