Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Mshikamanifu kwa Kristo na kwa Mtumwa Wake Mwaminifu

Uwe Mshikamanifu kwa Kristo na kwa Mtumwa Wake Mwaminifu

Uwe Mshikamanifu kwa Kristo na kwa Mtumwa Wake Mwaminifu

“Bwana wake . . . atamweka juu ya mali zake zote.” —MATHAYO 24:45-47.

1, 2. (a) Maandiko yanaonyesha Kiongozi wetu ni nani? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Kristo analiongoza kikweli kutaniko la Kikristo?

“MSIWARUHUSU watu wawaite ‘viongozi’—mna kiongozi mmoja tu, Kristo!” (Mathayo 23:10, The New Testament in Modern English) Kwa maneno hayo Yesu aliwaonyesha wazi wafuasi wake kwamba hawangekuwa na kiongozi yeyote mwanadamu duniani. Wangekuwa na Kiongozi mmoja mbinguni, yaani, Yesu Kristo mwenyewe. Yesu amewekwa rasmi na Mungu awe kiongozi. Yehova ‘alimfufua kutoka kwa wafu na . . . kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko, ambalo ni mwili wake.’—Waefeso 1:20-23.

2 Kwa kuwa Kristo ni “kichwa juu ya vitu vyote” kuhusiana na kutaniko la Kikristo, ana mamlaka juu ya mambo yote yanayotukia kutanikoni. Anaona kila jambo linalotukia katika kutaniko. Anachunguza kwa makini hali ya kiroho ya kila kikundi au kutaniko la Kikristo. Jambo hilo linaonyeshwa wazi katika ufunuo ambao mtume Yohana alipewa mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. Katika ujumbe wake kwa yale makutaniko saba, Yesu alisema mara tano kwamba alijua matendo yao, sifa zao nzuri, na udhaifu wao, naye alitoa mashauri na kitia-moyo kinachofaa. (Ufunuo 2:2, 9, 13, 19; 3:1, 8, 15) Tuna sababu nzuri za kuamini kwamba Kristo alijua pia hali ya kiroho ya makutaniko mengine huko Asia Ndogo, Palestina, Siria, Babilonia, Ugiriki, Italia, na kwingineko. (Matendo 1:8) Namna gani leo?

Mtumwa Mwaminifu

3. Kwa nini inafaa kumlinganisha Kristo na kichwa na kulinganisha kutaniko lake na mwili?

3 Baada ya kufufuliwa na muda mfupi kabla hajapanda mbinguni kwa Baba yake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Alisema hivi pia: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:18-20) Angeendelea kuwa pamoja nao na kuwaongoza akiwa Kichwa chao. Katika barua kwa Wakristo huko Efeso na Kolosai, mtume Paulo alilinganisha kutaniko la Kikristo na “mwili,” ambao Kristo ndiye Kichwa chake. (Waefeso 1:22, 23; Wakolosai 1:18) Kitabu kimoja (The Cambridge Bible for Schools and Colleges) kinasema kwamba ulinganisho huo “haudokezi tu muungano muhimu pamoja na Kichwa bali pia kwamba viungo vinafanya mambo ambayo Kichwa anataka. Viungo hivyo ni vyombo Vyake.” Kristo ametumia kikundi gani kama chombo chake tangu alipopewa mamlaka ya Ufalme mwaka wa 1914?—Danieli 7:13, 14.

4. Kama ilivyotabiriwa katika unabii wa Malaki, Yehova na Kristo Yesu walipata nini walipokuja kukagua hekalu la kiroho?

4 Unabii wa Malaki ulitabiri kwamba Yehova, “Bwana wa kweli,” akiandamana na ‘mjumbe wake wa agano,’ Mwana wake aliyetawazwa karibuni kuwa mfalme, Kristo Yesu, angekuja kuhukumu na kukagua “hekalu” Lake, au nyumba yake ya kiroho ya ibada. Ushuhuda unaonyesha kwamba “wakati uliowekwa” wa kuanza ‘kuhukumu nyumba ya Mungu’ ulifika mwaka wa 1918. * (Malaki 3:1; 1 Petro 4:17) Wale waliodai kumwakilisha Mungu na ibada yake ya kweli hapa duniani walikaguliwa kabisa. Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ambayo kwa karne nyingi yalifundisha mambo yanayomvunjia Mungu heshima na ambayo yalihusika sana katika mauaji ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, yalikataliwa. Mabaki waaminifu ambao ni Wakristo watiwa-mafuta kwa roho walijaribiwa, wakasafishwa kwa moto, na kukubaliwa, na hivyo kwa Yehova wakawa “watu wanaotoa toleo la zawadi katika uadilifu.”—Malaki 3:3.

5. Kulingana na unabii wa Yesu wa “kuwapo” kwake, “mtumwa” mwaminifu alithibitika kuwa nani?

5 Kulingana na unabii wa Malaki, ishara yenye mambo mengi ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake ili waweze kutambua wakati wa ‘kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo,’ inatia ndani kuitambua jamii ya “mtumwa.” Yesu alisema hivi: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa? Mtumwa huyo atakuwa mwenye furaha ikiwa bwana wake atakapofika atamkuta akifanya hivyo. Kwa kweli ninawaambia ninyi, Atamweka juu ya mali zake zote.” (Mathayo 24:3, 45-47) Kristo ‘alipofika’ ili kumkagua “mtumwa” huyo katika mwaka wa 1918, alipata mabaki ya wanafunzi waaminifu waliotiwa mafuta kwa roho, ambao tangu mwaka wa 1879 walikuwa wakitumia Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vinavyotegemea Biblia kuandaa ‘chakula kwa wakati unaofaa.’ Aliwakubali kwa ujumla kuwa chombo chake, au “mtumwa,” na mnamo 1919 akawaweka wasimamie mali zake zote za kidunia.

Kusimamia Mali za Kidunia za Kristo

6, 7. (a) Yesu alizungumza kuhusu “mtumwa” mwaminifu kwa maneno gani mengine? (b) Yesu anamaanisha nini anapotumia neno “msimamizi-nyumba”?

6 Miezi michache kabla ya Yesu kutoa unabii kuhusu ishara ya kuwapo kwake, kutia ndani kuwapo kwa “mtumwa” ambaye angemwakilisha hapa duniani, alizungumza kuhusu “mtumwa” huyo kwa maneno tofauti kidogo ambayo yanafunua wajibu wa mtumwa huyo. Yesu alisema hivi: “Ni nani kwa kweli aliye msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka rasmi juu ya watumishi wake kuendelea kuwapa kipimo chao cha chakula katika wakati unaofaa? Ninawaambia ninyi kwa kweli, Yeye atamweka rasmi juu ya mali zake zote.”—Luka 12:42, 44.

7 Katika andiko hilo mtumwa huyo anaitwa msimamizi-nyumba. Neno hilo linatafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “msimamizi wa shamba au nyumba.” Jamii hiyo ya msimamizi-nyumba haingekuwa tu kikundi cha wasomi wanaoeleza mambo yenye kupendeza kutoka katika Biblia. Mbali na kuandaa chakula kizuri cha kiroho “kwa wakati unaofaa,” “msimamizi-nyumba mwaminifu” angewekwa rasmi juu ya kikundi kizima cha watumishi wa Kristo, naye angepewa mgawo wa kusimamia kutaniko la Kristo na shughuli zake zote duniani, yaani, “mali zake zote.” Mgawo huo ungetia ndani nini?

8, 9. Mtumwa amewekwa rasmi asimamie “mali” gani?

8 Wajibu wa mtumwa huyo unatia ndani kusimamia majengo na vifaa halisi vinavyotumiwa na wafuasi wa Kristo kuendesha shughuli zao za Kikristo, kama vile makao makuu ya ulimwenguni pote na ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova, na pia mahali pao pa kufanyia ibada, yaani, Majumba ya Ufalme na Majumba ya Makusanyiko ulimwenguni pote. Jambo muhimu zaidi ni kwamba mtumwa huyo anasimamia pia programu za kiroho zenye kujenga za kujifunza Biblia katika mikutano ya kila juma na makusanyiko yanayofanywa mara kwa mara. Katika mikutano na makusanyiko hayo, habari kuhusu kutimizwa kwa unabii wa Biblia inazungumziwa, na mwelekezo unatolewa kwa wakati unaofaa ambao unaonyesha jinsi ya kutumia kanuni za Biblia katika maisha ya kila siku.

9 Wajibu wa msimamizi-nyumba huyo unatia ndani pia kusimamia kazi muhimu zaidi ya kuhubiri “habari njema ya ufalme” na ya kufanya “wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” Kazi hiyo inatia ndani kuwafundisha watu kufanya mambo yote ambayo Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko, aliamuru yafanywe katika wakati huu wa mwisho. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Ufunuo 12:17) Kazi hiyo ya kuhubiri na kufundisha imetokeza “umati mkubwa” wa waandamani washikamanifu wa mabaki watiwa-mafuta. Bila shaka, ‘vitu hivyo vyenye kutamanika vya mataifa yote’ ni sehemu ya “mali” za Kristo zenye thamani ambazo mtumwa mwaminifu anasimamia.—Ufunuo 7:9; Hagai 2:7.

Baraza Linaloongoza Ambalo Linamwakilisha Mtumwa

10. Ni baraza gani lililofanya maamuzi katika karne ya kwanza, na jambo hilo lilikuwa na matokeo gani kwa makutaniko?

10 Bila shaka, wajibu mzito wa mtumwa huyo ungehusisha kufanya maamuzi mengi. Katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, mitume na wazee huko Yerusalemu waliwakilisha jamii ya mtumwa, nao walifanya maamuzi kwa ajili ya kutaniko lote la Kikristo. (Matendo 15:1, 2) Makutaniko yalijulishwa maamuzi ya baraza linaloongoza la karne ya kwanza kupitia barua na wawakilishi wanaosafiri. Wakristo wa mapema walifurahi kupokea mwelekezo huo ulio wazi, nao walipata amani na umoja kwa sababu ya kushirikiana kwa kupenda na baraza linaloongoza.—Matendo 15:22-31; 16:4, 5; Wafilipi 2:2.

11. Kristo anatumia nani leo kuelekeza kutaniko lake, nasi tunapaswa kuwa na maoni gani kuelekea kikundi hicho cha Wakristo watiwa-mafuta?

11 Kama ilivyokuwa katika siku za mapema za Ukristo, leo Baraza Linaloongoza la wafuasi wa Kristo walio duniani linafanyizwa na kikundi kidogo cha waangalizi watiwa-mafuta. Kwa “mkono wake wa kuume” ambao unawakilisha nguvu zake, Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko, anaelekeza wanaume hao waaminifu wanaposimamia kazi ya Ufalme. (Ufunuo 1:16, 20) Katika simulizi la maisha yake, Albert Schroeder, mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza ambaye alikufa hivi majuzi akiwa na tumaini la kwenda mbinguni, aliandika hivi: “Baraza Linaloongoza linakutana kila Jumatano (Siku ya Tatu), na linaanza mkutano huo kwa sala na kuomba mwelekezo wa roho ya Yehova. Jitihada kubwa inafanywa ili kuhakikisha kwamba kila jambo linaloshughulikiwa na kila uamuzi unaofanywa unapatana na Neno la Mungu, Biblia.” * Tunaweza kuwatumaini Wakristo hao waaminifu waliotiwa mafuta. Tunapaswa kufuata shauri hili la mtume Paulo hasa kuhusiana na Baraza Linaloongoza: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu.”—Waebrania 13:17.

Kumheshimu Inavyofaa Mtumwa Mwaminifu

12, 13. Tuna sababu gani za Kimaandiko za kuiheshimu jamii ya mtumwa?

12 Sababu kuu ya kuiheshimu inavyofaa jamii ya mtumwa mwaminifu ni kwamba tunapofanya hivyo kwa kweli tunamheshimu Bwana, Yesu Kristo. Paulo aliandika hivi kuhusu watiwa-mafuta: “Yeye aliyeitwa akiwa mtu aliye huru ni mtumwa wa Kristo. Mlinunuliwa kwa bei.” (1 Wakorintho 7:22, 23; Waefeso 6:6) Kwa hiyo, tunapotii kwa ushikamanifu mwelekezo wa mtumwa mwaminifu na Baraza lake Linaloongoza, tunajitiisha chini ya Kristo, Bwana wa mtumwa huyo. Kuheshimu inavyofaa chombo ambacho Kristo anatumia kusimamia mali zake za kidunia ni njia moja ya ‘kukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.’—Wafilipi 2:11.

13 Sababu nyingine ya Kimaandiko ya kumheshimu mtumwa mwaminifu ni kwamba Wakristo watiwa-mafuta wanatajwa kwa njia ya mfano kuwa “hekalu” ambamo Yehova anakaa “kwa njia ya roho.” Kwa hiyo, wao ni ‘watakatifu.’ (1 Wakorintho 3:16, 17; Waefeso 2:19-22) Yesu ameikabidhi jamii hiyo ya hekalu takatifu la kiroho mali zake za kidunia. Hilo linamaanisha kwamba haki na wajibu fulani katika kutaniko la Kikristo ni wa jamii hiyo ya mtumwa peke yake. Kwa sababu hiyo, wote kutanikoni wanahisi kwamba wana wajibu mtakatifu wa kufuata na kuunga mkono mwelekezo kutoka kwa mtumwa mwaminifu na Baraza lake Linaloongoza. Bila shaka, “kondoo wengine” wanaona kuwa ni pendeleo kubwa kuisaidia jamii ya mtumwa katika kushughulikia mambo ya Bwana.—Yohana 10:16.

Kumtegemeza kwa Ushikamanifu

14. Kama ilivyotabiriwa na Isaya, kondoo wengine wanatembea jinsi gani nyuma ya jamii ya mtumwa iliyotiwa mafuta na kutumika wakiwa ‘wafanyakazi wasiolipwa’?

14 Unabii wa Isaya ulitabiri kwamba kondoo wengine wangejitiisha kwa unyenyekevu chini ya washiriki watiwa-mafuta wa Israeli la kiroho: “Yehova amesema hivi: ‘Wafanyakazi wa Misri wasiolipwa na wanabiashara wa Ethiopia na Wasabea, watu warefu, watakujia wewe, nao watakuwa wako. Watatembea nyuma yako; watakuja wamefungwa pingu, nao watakuinamia wewe. Watasali kwako, wakisema, “Kwa kweli Mungu ameungana na wewe, na hakuna mwingine yeyote; hakuna Mungu mwingine.”’” (Isaya 45:14) Leo, kondoo wengine wanatembea kwa njia ya mfano nyuma ya jamii ya mtumwa iliyotiwa mafuta na Baraza lake Linaloongoza na kufuata mwongozo wao. Wakiwa ‘wafanyakazi wasiolipwa,’ kondoo wengine wanatumia kwa kupenda nguvu na mali zao ili kutegemeza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo Kristo aliwapa wafuasi wake watiwa-mafuta walio duniani.—Matendo 1:8; Ufunuo 12:17.

15. Unabii wa Isaya 61:5, 6 unatabiri jinsi gani uhusiano uliopo kati ya kondoo wengine na Israeli la kiroho?

15 Kondoo wengine wanafurahi na wanashukuru kumtumikia Yehova chini ya uangalizi wa jamii ya mtumwa na Baraza lake Linaloongoza. Wanatambua kwamba watiwa-mafuta ni washiriki wa “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16) Wakiwa “wageni” wa mfano na “watu wa nchi nyingine” wanaoshirikiana na Israeli la kiroho, wanatumika kwa shangwe wakiwa “wakulima” na “watunza-mizabibu” chini ya mwelekezo wa watiwa-mafuta, ambao ni “makuhani wa Yehova” na “wahudumu wa Mungu.” (Isaya 61:5, 6) Wanashiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. Wanaisaidia kwa moyo wote jamii ya mtumwa katika kuchunga na kutunza watu wapya walio mfano wa kondoo.

16. Ni nini kinachowachochea kondoo wengine wamuunge mkono kwa ushikamanifu mtumwa mwaminifu na mwenye busara?

16 Kondoo wengine wanatambua kwamba wamefaidika sana kutokana na jitihada kubwa za mtumwa mwaminifu za kuwaandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Wanakubali kwa unyenyekevu kwamba ikiwa hawangekuwa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, hawangejua mengi au hawangejua kamwe kweli zenye thamani za Biblia kama vile, enzi kuu ya Yehova, kutakaswa kwa jina lake, Ufalme, mbingu mpya na dunia mpya, nafsi, hali ya wafu, na ukweli kumhusu Yehova, Mwana wake, na roho takatifu. Kwa sababu ni wenye shukrani na washikamanifu, kondoo wengine wanawaunga mkono kwa upendo “ndugu” watiwa-mafuta wa Kristo walio duniani wakati huu wa mwisho.—Mathayo 25:40.

17. Baraza Linaloongoza linaona umuhimu wa kufanya nini, na ni nini kitakachozungumziwa katika habari inayofuata?

17 Kwa kuwa idadi ya watiwa-mafuta inazidi kupungua, hawawezi kuwapo katika kila kutaniko ili kuhakikisha kwamba mali za Kristo zinasimamiwa vizuri. Kwa hiyo, Baraza Linaloongoza linaweka rasmi wanaume ambao ni washiriki wa kondoo wengine wawe waangalizi katika ofisi za tawi, katika wilaya, mizunguko, na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Je, mtazamo wetu kuwaelekea wachungaji hao wadogo unaonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kwa Kristo na kwa mtumwa wake mwaminifu? Jambo hilo litazungumziwa katika habari inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa habari zaidi kuhusu jambo hili, ona Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 2004 (1/3/2004), ukurasa 13-18, na Desemba 1, 1992 (1/12/1992), ukurasa 13.

^ fu. 11 Lilichapishwa katika Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1988 (1/3/1988), ukurasa wa 10-17.

Kwa Kupitia

• Kiongozi wetu ni nani, na ni nini kinachoonyesha kwamba anajua hali za makutaniko?

• Wakati wa kukagua “hekalu,” ni nani waliopatikana wakiwa mtumwa mwaminifu, nao walikabidhiwa mali gani?

• Tuna sababu gani za Kimaandiko za kumuunga mkono kwa ushikamanifu mtumwa mwaminifu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Mali” zinazosimamiwa na “msimamizi-nyumba” zinatia ndani mali halisi, programu za kiroho, na kazi ya kuhubiri

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kondoo wengine wanaunga mkono jamii ya mtumwa mwaminifu kwa kuhubiri kwa bidii