Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Ukatili Utakwisha?

Je, Kweli Ukatili Utakwisha?

Je, Kweli Ukatili Utakwisha?

WATU wengi wanakubali kwamba uchoyo ndicho chanzo cha ukatili ulimwenguni leo. Mbegu zilizopandwa miaka mingi iliyopita na kizazi cha ubinafsi zimetokeza jamii ambayo ina watu wengi wanaojali tu faida zao wenyewe. Wengi wako tayari kufanya chochote kile ili kupata wanachotaka, na mara nyingi hilo limesababisha matendo ya ukatili. Si watu mmoja-mmoja tu wanaohusika lakini pia mataifa mazima-mazima.

Maisha ya wanadamu wenzao hayaonekani tena kuwa yenye thamani. Watu wengine hata wanafurahia kuwa wakatili. Ukatili unawaburudisha, kama vile wahalifu wanaokiri kwamba wanawaumiza wengine ili kujifurahisha tu. Namna gani kuhusu mamilioni ya watu ambao wanapendelea sinema za ujeuri na ukatili na hivyo kuwaletea watayarishaji wa sinema faida kubwa kutokana na sinema za aina hiyo? Kuendelea kuangalia matendo ya ukatili kupitia burudani na vyombo vya habari kumefanya hisia za watu wengi zife ganzi.

Mara nyingi ukatili unasababisha madhara ya kiakili na kihisia ambayo daima yanaendeleza ukatili. Akizungumzia ujeuri ambao unasababishwa na ukatili, Noemí Díaz Marroquín, anayefundisha katika chuo kimoja (National Autonomous University of Mexico) huko Mexico, anasema hivi: “Watu wanajifunza ujeuri, ni sehemu ya utamaduni wetu . . . Tunajifunza kutenda kwa njia za ujeuri mazingira yetu yanapoturuhusu na kutuchochea kuwa wajeuri.” Kwa hiyo, huenda wale ambao wametendewa vibaya wakawatendea wengine vibaya, labda hata kuwatendea jinsi walivyotendewa.

Katika visa vingine, wale ambao wanatumia vibaya vitu kama vile pombe na dawa za kulevya wanaweza kuwa wakatili. Pia, tusisahau watu ambao hawaridhishwi na serikali zao ambazo zimeshindwa kutosheleza mahitaji ya raia. Wengine wao, wakiwa wameazimia kuonyesha maoni yao, wanatenda kwa ukatili na kuunga mkono ugaidi, jambo ambalo mara nyingi linawaumiza watu wasio na hatia.

Hivyo huenda ukajiuliza: ‘Je, watu wamejifunza wenyewe tu kuwa wakatili? Ni nini kinachosababisha ukatili uliopo leo?’

Ni Nani kwa Kweli Anayesababisha Ukatili?

Biblia inatueleza kwamba Shetani Ibilisi ana uvutano wenye nguvu juu ya ulimwengu huu, nayo inamwita “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4) Yeye ndiye mtu mwenye ubinafsi na ukatili zaidi katika ulimwengu wote. Kwa kufaa, Yesu alisema Shetani ni “muuaji” na “baba ya uwongo.”—Yohana 8:44.

Tangu Adamu na Hawa walipoasi, wanadamu wamekuwa chini ya uvutano wenye nguvu wa Shetani. (Mwanzo 3:1-7, 16-19) Karne 15 hivi baada ya wanadamu wawili wa kwanza kumkataa Yehova, malaika waasi walivaa miili ya kibinadamu na kufanya ngono na wanawake, na wakatokeza jamii isiyo ya kawaida iliyoitwa Wanefili. Ni nini hasa kilichofanya wajulikane? Jina lao linajibu swali hilo. Linamaanisha “Waangushaji,” au “wale wanaowaangusha wengine chini.” Inaelekea kwamba walikuwa watu wajeuri ambao walileta ukatili na ukosefu wa adili ambao ungeweza kukomeshwa tu na gharika iliyoletwa na Mungu. (Mwanzo 6:4, 5, 17) Ingawa Wanefili waliangamizwa na Gharika, baba zao walirudi katika makao ya roho wakiwa roho waovu wasioonekana.—1 Petro 3:19, 20.

Mwelekeo wa ukatili wa malaika hao waasi unaonekana wazi katika kisa cha mvulana mmoja aliyekuwa na roho mwovu katika siku za Yesu. Roho huyo mwovu alikuwa akimfanya mtoto huyo agaegae chini, na kumtupa ndani ya moto na ndani ya maji ili kumwangamiza. (Marko 9:17-22) Kwa wazi, “majeshi ya roho waovu” kama hao yanaonyesha utu usio na huruma wa kiongozi wao mkatili, Shetani Ibilisi.—Waefeso 6:12.

Leo, uvutano wa roho waovu unaendeleza ukatili wa wanadamu, kama Biblia ilivyotabiri: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wenye kujidai, wenye majivuno, . . . wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.”—2 Timotheo 3:1-5.

Unabii wa Biblia unafunua kwamba nyakati zetu ni za hatari hasa kwa sababu baada ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa mwaka wa 1914 mikononi mwa Kristo Yesu, Shetani na majeshi yake ya roho waovu walitupwa kutoka mbinguni. Biblia inatangaza hivi: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:5-9, 12.

Je, hilo linamaanisha kwamba hali haiwezi kuwa bora? Díaz Marroquín, aliyetajwa mapema, anasema kwamba “watu wanaweza kuacha” tabia zisizofaa. Hata hivyo, kwa kuwa uvutano wa Shetani unaenea duniani leo, inaelekea kwamba ni vigumu mtu kuacha tabia hizo asiporuhusu nguvu nyingine, yenye uwezo zaidi iongoze mawazo na matendo yake. Ni nguvu gani hiyo?

Inawezekana Jinsi Gani Kubadilika?

Inapendeza kujua kwamba roho takatifu ya Mungu ndiyo nguvu yenye uwezo zaidi ulimwenguni, nayo inaweza kushinda uvutano wowote wa roho waovu. Inawachochea watu kuonyesha upendo na inaboresha maisha yao. Ili ajazwe na roho ya Mungu, mtu yeyote anayetaka kumpendeza Yehova anapaswa kuepuka mwenendo ambao hata unakaribia kuwa wa kikatili. Hilo linahitaji mtu abadili utu wake ili upatane na mapenzi ya Mungu. Mapenzi ya Mungu ni nini? Ni kwamba tuige njia za Mungu kadiri tunavyoweza. Hilo linatia ndani kuwaona wengine kama Mungu anavyowaona.—Waefeso 5:1, 2; Wakolosai 3:7-10.

Kujifunza njia za Mungu za kushughulikia mambo kutakusadikisha kwamba Yehova hajawahi kamwe kuwapuuza wengine. Hajamtendea mwanadamu yeyote wala hata mnyama yeyote isivyo haki. * (Kumbukumbu la Torati 22:10; Zaburi 36:7; Methali 12:10) Anachukia ukatili na watu wote wakatili. (Methali 3:31, 32) Utu mpya ambao Yehova anataka Wakristo wakuze unawasaidia wawaone wengine kuwa bora na kuwaheshimu. (Wafilipi 2:2-4) Utu huo mpya wa Kikristo unatia ndani “upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.” Hatupaswi kupuuza upendo, “kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:12-14) Je, hukubali kwamba ulimwengu ungekuwa tofauti ikiwa sifa hizo zingeenea?

Hata hivyo, huenda ukajiuliza ikiwa kwa kweli mtu anaweza kubadili kabisa utu wake. Hebu fikiria mfano halisi unaofuata. Martín * alizoea kumfokea mke wake mbele ya watoto wao na kumpiga vibaya. Pindi moja, hali ilikuwa mbaya sana hivi kwamba watoto wakakimbilia kwa majirani ili kuomba msaada. Baada ya miaka mingi, familia hiyo ilianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Martín alijifunza sifa ambazo anapaswa kuonyesha na jinsi anavyopaswa kuwatendea wengine. Je, alibadilika? Mke wake anajibu hivi: “Zamani, mume wangu alikuwa mtu tofauti alipokasirika. Kwa sababu hiyo, maisha yetu yalivurugika kwa muda mrefu. Sijui nimshukuru Yehova jinsi gani kwa sababu ya kumsaidia Martín kubadilika. Sasa yeye ni baba mzuri na mume bora kabisa.”

Hicho ni kisa kimoja tu. Ulimwenguni pote, mamilioni ya watu ambao wamejifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova wameacha ukatili. Ndiyo, inawezekana kubadilika.

Mwisho wa Ukatili Wote Unakaribia

Hivi karibuni, Ufalme wa Mungu, serikali ambayo imesimamishwa mbinguni ikiongozwa na Mtawala mwenye huruma, Kristo Yesu, itatawala dunia yote. Tayari imekwisha kumwondoa Shetani mbinguni, ambaye ndiye chanzo cha ukatili wote, na roho wake waovu. Hivi punde, Ufalme wa Mungu utatosheleza mahitaji ya raia wake duniani ambao wanapenda amani. (Zaburi 37:10, 11; Isaya 11:2-5) Hilo ndilo suluhisho pekee kwa matatizo ya ulimwengu. Lakini, namna gani ukitendewa kikatili unapoendelea kungoja Ufalme huo?

Kulipiza kisasi hakuwezi kusaidia. Ukifanya hivyo utatendewa tu kwa ukatili zaidi. Biblia inatuomba tumtegemee Yehova, ambaye kwa wakati wake ‘atampa kila mmoja kulingana na njia zake, kulingana na matunda ya matendo yake.’ (Yeremia 17:10) (Ona sanduku lenye kichwa, “Jinsi ya Kukabiliana na Ukatili.”) Ni kweli kwamba huenda ukaumia kwa sababu ya kutendewa uhalifu wa kikatili. (Mhubiri 9:11) Hata hivyo, Mungu anaweza kuondoa matokeo ya ukatili wowote ule, hata kifo. Kulingana na ahadi yake, wale walio katika kumbukumbu lake ambao waliuawa kikatili watakuwa hai tena.—Yohana 5:28, 29.

Ingawa kuna uwezekano wa kutendewa kwa ukatili, tunaweza kufarijiwa kwa kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu na kuwa na imani yenye nguvu katika ahadi zake. Fikiria kisa cha Sara ambaye alilea wanawe wawili bila kuwa na mume, naye alihakikisha kwamba walipata elimu nzuri. Alipozeeka, wana hao walimwacha, hawakumsaidia kimwili wala kimatibabu. Hata hivyo, Sara ambaye sasa ni Mkristo anasema hivi: “Ingawa ninahuzunika sana, Yehova hajaniacha. Ninahisi kwamba ananitegemeza kupitia ndugu na dada zangu wa kiroho, ambao sikuzote wananitunza. Ninaamini kabisa kwamba hivi karibuni atatatua matatizo yangu na pia ya wote wanaotegemea nguvu zake na kufanya yale anayoamuru.”

Ni nani ndugu na dada wa kiroho ambao Sara anazungumzia? Ni washiriki wake Wakristo ambao ni Mashahidi wa Yehova. Wao ni undugu wa ulimwenguni pote wa watu wenye huruma ambao wanasadiki kwamba hivi karibuni ukatili utakwisha. (1 Petro 2:17) Shetani Ibilisi, yule anayesababisha ukatili ataondolewa, na pia mtu yeyote anayetenda kama yeye. Hii “enzi ya ukatili,” kama inavyoitwa na mwandishi mmoja, haitakuwapo tena. Mbona usijifunze kuhusu tumaini hilo kwa kuzungumza na Shahidi yeyote wa Yehova?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Ili kujifunza kuhusu utu na sifa za Mungu kwa undani zaidi, ona kitabu Mkaribie Yehova, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 17 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Jinsi ya Kukabiliana na Ukatili

Neno la Mungu linatoa mashauri mazuri kuhusu jinsi ya kukabiliana na ukatili. Fikiria jinsi unavyoweza kufuata maneno yafuatayo ya hekima:

“Usiseme: ‘Nitalipiza uovu!’ Mtumaini Yehova, naye atakuokoa.”—Methali 20:22.

“Ukimwona mtu yeyote maskini akionewa na hukumu na uadilifu zikitwaliwa kijeuri . . . , usishangazwe na jambo hilo, kwa maana aliye juu zaidi kuliko yule aliye juu anaangalia.”—Mhubiri 5:8.

“Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.”—Mathayo 5:5.

“Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

“Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. Fanyeni mambo mema machoni pa watu wote. Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’”—Waroma 12:17-19.

“Hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu. . . . Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.”—1 Petro 2:21-23.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yehova amewafundisha watu wengi kuacha ukatili