Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutaniko na Lijengwe

Kutaniko na Lijengwe

Kutaniko na Lijengwe

“Kutaniko . . . likaingia katika kipindi cha amani, likijengwa.” —MATENDO 9:31.

1. Ni maswali gani yanayoweza kuulizwa kuhusu “kutaniko la Mungu”?

SIKU ya Pentekoste 33 W.K., Yehova alikubali kikundi cha wanafunzi wa Kristo kuwa taifa jipya, “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16) Wakristo hao waliotiwa mafuta kwa roho walikuja pia kuwa lile ambalo Biblia inaliita “kutaniko la Mungu.” (1 Wakorintho 11:22) Lakini, hilo lilitia ndani nini? “Kutaniko la Mungu” lingepangwa jinsi gani? Lingetenda kazi jinsi gani duniani, haidhuru washiriki wake wanaishi wapi? Maisha yetu na furaha yetu inahusika jinsi gani?

2, 3. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba kutaniko lingekuwa na mpangilio?

2 Kama habari iliyotangulia ilivyoonyesha, Yesu alitabiri kuwapo kwa kutaniko hilo la wafuasi wake watiwa-mafuta, alipomwambia mtume Petro hivi: “Juu ya mwamba huu [Yesu Kristo] nitajenga kutaniko langu, na malango ya Kaburi hayatalizidi nguvu.” (Mathayo 16:18) Zaidi ya hilo, Yesu alipokuwa bado na mitume wake alieleza kuhusu utaratibu na utendaji wa kutaniko hilo ambalo lingeanzishwa baada ya muda mfupi.

3 Yesu alifundisha kwa maneno na matendo kwamba washiriki fulani wa kutaniko hilo wangeongoza. Wangefanya hivyo kwa kuwatumikia au kuwahudumia washiriki wengine katika kikundi chao. Kristo alisema: “Mnajua kwamba wale ambao huonekana kuwa wanatawala mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu wao hutumia mamlaka juu yao. Hivyo sivyo ilivyo katikati yenu; bali yeyote yule anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu, na yeyote yule anayetaka kuwa wa kwanza katikati yenu lazima awe mtumwa wa wote.” (Marko 10:42-44) Ni wazi kwamba “kutaniko la Mungu” halingekuwa tu watu mmoja-mmoja waliosambaa na walio peke yao, yaani, kutaniko ambalo halina mpangilio wowote. Badala yake, kungekuwa na mpangilio, na kila mtu katika kutaniko angeshirikiana na mwenzake.

4, 5. Tunajua namna gani kwamba kutaniko lingehitaji kufundishwa mambo ya kiroho?

4 Yesu ambaye angekuwa Kichwa cha ‘kutaniko hilo la Mungu’ alisema kwamba mitume wake na watu wengine ambao walijifunza kutoka kwake wangekuwa na wajibu wa pekee kuelekea washiriki wengine wa kutaniko. Wangefanya nini? Mgawo wao muhimu ungekuwa kuwafundisha washiriki wa kutaniko mambo ya kiroho. Kumbuka kwamba Yesu aliyefufuliwa, alimwambia Petro hivi mbele ya mitume wengine: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda?” Petro akamjibu: “Ndiyo, Bwana, unajua ninakupenda.” Yesu akamwambia hivi: “Lisha wana-kondoo wangu. . . . Chunga kondoo wangu wadogo. . . . Lisha kondoo wangu wadogo.” (Yohana 21:15-17) Huo ulikuwa mgawo mzito kama nini!

5 Kutokana na maneno ya Yesu tunaweza kuona kwamba wale ambao wanakusanywa katika kutaniko wanafananishwa na kondoo walio katika zizi. Kondoo hao, wanaume, wanawake, na watoto Wakristo, wanahitaji kulishwa kiroho na kuchungwa kwa njia inayofaa. Kwa kuongezea, kwa kuwa Yesu aliwaamuru wafuasi wake wote wawafundishe wengine na kufanya wanafunzi, watu wowote wapya ambao wangekuwa kondoo wake wangehitaji kuzoezwa kuhusu jinsi ya kutimiza kazi hiyo waliyopewa na Mungu.—Mathayo 28:19, 20.

6. Ni mipango gani iliyofanywa katika “kutaniko la Mungu” lililokuwa limetoka tu kuanzishwa?

6 Baada ya “kutaniko la Mungu” kuanzishwa, washiriki wake walikutana kwa ukawaida ili kufundishwa na kutiana moyo: “Wakaendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume na kushirikiana, katika kula milo na katika sala.” (Matendo 2:42, 46, 47) Jambo lingine la maana katika masimulizi hayo ya kihistoria ni kwamba wanaume fulani walio na sifa za kustahili walichaguliwa ili wasaidie kutoa huduma fulani zilizohitajiwa. Hawakuchaguliwa kwa sababu walikuwa na elimu nyingi, wala kwa sababu walikuwa na ustadi fulani. Walikuwa wanaume “wenye kujaa roho na hekima.” Mmoja wao alikuwa Stefano, na masimulizi hayo yanataja kwamba alikuwa “mwanamume mwenye kujaa imani na roho takatifu.” Kwa sababu ya mpango huo wa makutaniko, “neno la Mungu likaendelea kukua, na hesabu ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana katika Yerusalemu.”—Matendo 6:1-7.

Wanaume Wanaotumiwa na Mungu

7, 8. (a) Mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu walitumika wakiwa nani kati ya Wakristo wa karne ya kwanza? (b) Matokeo yalikuwa nini wakati maagizo yalipotolewa kupitia makutaniko?

7 Kwa wazi, mitume waliongoza katika mpango wa makutaniko ya karne ya kwanza, lakini hawakuwa peke yao. Wakati fulani, Paulo na wenzake walirudi Antiokia ya Siria. Andiko la Matendo 14:27 linasema hivi: “Walipokuwa wamefika na wakiwa wamelikusanya kutaniko pamoja, wakaeleza mambo mengi ambayo Mungu alikuwa amefanya kupitia kwao.” Walipokuwa wangali na kutaniko hilo, swali lilitokea kuhusu ikiwa waamini wasio Wayahudi walihitaji kutahiriwa. Ili kusuluhisha jambo hilo, Paulo na Barnaba walitumwa “kwa mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu,” ambao kwa wazi walitumika wakiwa baraza linaloongoza.—Matendo 15:1-3.

8 Mzee Mkristo Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu ambaye hakuwa mtume, alisimamia mkutano wakati ‘mitume na wanaume wazee walipokusanyika pamoja ili waliangalie jambo hilo.’ (Matendo 15:6) Baada ya kuzungumzia jambo hilo na kwa msaada wa roho takatifu, walifikia uamuzi uliopatana na Maandiko. Waliyatumia makutaniko barua kuhusu uamuzi huo. (Matendo 15:22-32) Wale waliopokea habari hiyo waliikubali na kuifuata. Matokeo yalikuwa nini? Ndugu na dada walijengwa na kutiwa moyo. Biblia inaripoti hivi: “Kwa hiyo, kwa kweli, makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka hesabu siku baada ya siku.”—Matendo 16:5.

9. Biblia inaorodhesha wajibu gani wa wanaume Wakristo walio na sifa za kustahili?

9 Lakini makutaniko hayo yaliendeshwa namna gani siku baada ya siku? Kwa mfano, fikiria makutaniko ambayo yalikuwa katika kisiwa cha Krete. Ingawa watu wengi walioishi huko walikuwa na sifa mbaya, wengine walibadilika na kuwa Wakristo wa kweli. (Tito 1:10-12; 2:2, 3) Waliishi katika majiji mbalimbali, na wote walikuwa mbali sana na baraza linaloongoza ambalo lilikuwa Yerusalemu. Hata hivyo, hilo halikuwa tatizo kubwa kwa sababu “wanaume wazee” wa kiroho waliwekwa rasmi katika kila kutaniko la Krete, kama ilivyokuwa katika sehemu nyingine. Wanaume hao walitimiza sifa za kustahili ambazo zinatajwa katika Biblia. Waliwekwa rasmi kuwa wazee, au waangalizi, ambao wangeweza “kuhimiza kwa fundisho lenye afya na . . . kuwakaripia wale ambao hulipinga.” (Tito 1:5-9; 1 Timotheo 3:1-7) Wanaume wengine wa kiroho walikuwa na sifa za kustahili kuyahudumia makutaniko wakiwa watumishi wa huduma.—1 Timotheo 3:8-10, 12, 13.

10. Kulingana na Mathayo 18:15-17, matatizo mazito yalipaswa kusuluhishwa kwa njia gani?

10 Yesu alionyesha kwamba mpango huo ungekuwapo. Kumbuka simulizi la Mathayo 18:15-17, ambamo alisema kwamba nyakati fulani tatizo linaweza kutokea kati ya watu wawili wanaomtumikia Mungu, mtu mmoja anapomtendea mwingine dhambi fulani. Yule aliyekosewa angepaswa kumfikia yule mwingine na ‘kufunua kosa lake’ faraghani, wakiwa wawili tu. Ikiwa hatua hiyo haikusuluhisha tatizo hilo, mtu mmoja au wawili ambao walijua mambo yaliyotukia wangeweza kuombwa wasaidie. Namna gani ikiwa wangeshindwa kutatatua tatizo hilo? Yesu alisema: “Asipowasikiliza hao, liambie kutaniko. Ikiwa halisikilizi hata kutaniko, mwache awe kwako kama mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Yesu aliposema hivyo, bado Wayahudi walikuwa “kutaniko la Mungu,” kwa hiyo mwanzoni maneno yake yaliwahusu. * Hata hivyo, mara tu kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, maagizo hayo ya Yesu yangetumika katika kutaniko la Kikristo. Hilo ni jambo lingine linaloonyesha kwamba watu wa Mungu wangekuwa na mpangilio katika kutaniko ili kutoa mwongozo na kumjenga kila Mkristo.

11. Wazee walitimiza wajibu gani katika kusuluhisha matatizo?

11 Kwa kufaa, wanaume wazee, au waangalizi wangewakilisha kutaniko katika kushughulikia au kusuluhisha matatizo au visa vya dhambi. Na hilo linapatana na sifa za kustahili za wazee zinazotajwa katika Tito 1:9. Kwa kweli, wazee hao walikuwa wanaume wasio wakamilifu, kama vile Tito ambaye alitumwa na Paulo ayatembelee makutaniko ili ‘ayarekebishe mambo yaliyokuwa na kasoro.’ (Tito 1:4, 5) Leo, wale wanaofikiriwa kuwekwa rasmi kuwa wazee ni lazima wawe wamethibitisha imani na ujitoaji wao kwa muda fulani. Hivyo, wengine kutanikoni wanakuwa na sababu nzuri ya kutegemea mwelekezo na mwongozo unaotolewa kupitia mpango huu.

12. Wazee wana wajibu gani kuelekea kutaniko?

12 Paulo aliwaambia hivi wazee wa kutaniko la Efeso: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo roho takatifu imewaweka ninyi rasmi kuwa waangalizi kati yake, kulichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Matendo 20:28) Leo pia waangalizi wa kutaniko wanawekwa rasmi “kulichunga kutaniko la Mungu.” Wanapaswa kufanya hivyo kwa upendo, wala si kwa kupiga ubwana juu ya kundi. (1 Petro 5:2, 3) Waangalizi wanapaswa kujitahidi kulijenga na kulisaidia “kundi lote.”

Kushikamana na Kutaniko

13. Ni nini kinachoweza kutokea katika kutaniko nyakati nyingine, na kwa nini?

13 Wazee na washiriki wengine wote kutanikoni si wakamilifu, kwa hiyo, kutoelewana au matatizo yanatokea mara kwa mara, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza mitume fulani walipokuwapo. (Wafilipi 4:2, 3) Huenda mwangalizi au mtu mwingine akasema jambo fulani ambalo halionekani kuwa la adabu, la fadhili, au la kweli kabisa. Au huenda tukafikiri kwamba jambo fulani lisilopatana na Maandiko linafanywa, na inaonekana kwamba ingawa wazee wa kwenu wanalijua, hawalirekebishi. Bila shaka, huenda jambo hilo tayari limeshughulikiwa au linaendelea kushughulikiwa kupatana na Maandiko na hatujui mambo yote yanayohusika. Hata ikiwa hali iko jinsi tunavyofikiri, fikiria wazo hili: Kwa muda fulani, dhambi nzito ilikuwa ikiendelea katika kutaniko la Korintho, kutaniko ambalo Yehova alihangaikia. Baada ya muda, alihakikisha kwamba tatizo hilo linashughulikiwa na kurekebishwa kwa uthabiti. (1 Wakorintho 5:1, 5, 9-11) Tunaweza kujiuliza hivi, ‘Kama ningekuwa ninaishi Korintho wakati huo, ningefanya nini kabla ya tatizo hilo kushughulikiwa?’

14, 15. Kwa nini wengine waliacha kumfuata Yesu, na hilo linatufundisha nini?

14 Fikiria hali nyingine inayoweza kutokea katika kutaniko. Tuseme kwamba mtu anashindwa kuelewa na kukubali fundisho fulani la Kimaandiko. Huenda amefanya utafiti katika Biblia na vichapo vinavyopatikana kupitia kutaniko, na ametafuta msaada wa Wakristo wenzake wakomavu, hata wazee. Lakini bado anashindwa kuelewa au kukubali fundisho hilo. Anaweza kufanya nini? Kulikuwa na hali kama hiyo mwaka mmoja hivi kabla ya Yesu kufa. Yesu alisema kwamba alikuwa “mkate wa uzima” na kwamba ili mtu aishi milele anapaswa ‘kula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake.’ Wengine kati ya wanafunzi wake walishtuka kusikia hivyo. Badala ya kutafuta maelezo zaidi au kungojea tu kwa imani, wanafunzi wengi ‘wakawa hawatembei tena pamoja na Yesu.’ (Yohana 6:35, 41-66) Tujiulize tena, kama tungekuwapo wakati huo tungefanya nini?

15 Katika nyakati za kisasa, watu fulani wameacha kushirikiana na kutaniko lao wakifikiri kwamba wanaweza kumtumikia Mungu wakiwa peke yao. Huenda wakasema kwamba ni kwa sababu waliumizwa hisia, wanafikiri kosa fulani halirekebishwi, au hawawezi kukubali fundisho fulani. Je, wanatenda kwa busara? Ingawa ni kweli kwamba kila Mkristo anapaswa kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu, hatuwezi kupinga kwamba Mungu anatumia kutaniko la ulimwenguni pote, kama alivyofanya katika siku za mitume. Zaidi ya hayo, Yehova aliyatumia makutaniko katika karne ya kwanza na kuyabariki. Aliandaa mpango wa wazee na watumishi wa huduma wenye sifa za kustahili kwa faida ya makutaniko. Ndivyo ilivyo pia leo.

16. Mtu akishawishiwa kujitenga na kutaniko, anapaswa kufikiria nini?

16 Ikiwa Mkristo anafikiri kwamba anaweza kutegemea tu uhusiano wake mwenyewe pamoja na Mungu bila kushirikiana na kutaniko, anakataa mpango ulioanzishwa na Mungu, mpango wa kutaniko la ulimwenguni pote na kutaniko la kwao la watu wa Mungu. Huenda mtu huyo akamwabudu Mungu akiwa peke yake au akashirikiana na watu wengine wachache tu, lakini atafaidika jinsi gani na mpango wa wazee na watumishi wa huduma wa kutaniko? Kwa kweli, Paulo alipoyaandikia makutaniko huko Kolosai na kuagiza barua hiyo isomwe pia huko Laodikia, alizungumza kuhusu ‘kutia mizizi na kujengwa katika Kristo.’ Wale waliokuwa katika makutaniko ndio wangefaidika, wala si watu mmoja-mmoja waliojitenga wenyewe na makutaniko.—Wakolosai 2:6, 7; 4:16.

Nguzo na Tegemezo la Ile Kweli

17. Andiko la 1 Timotheo 3:15 linatufundisha nini kuhusu kutaniko?

17 Katika barua yake ya kwanza kwa mzee Mkristo Timotheo, mtume Paulo alitaja sifa za kustahili za wazee na watumishi wa huduma katika kila kutaniko. Kisha, Paulo alitaja “kutaniko la Mungu aliye hai,” na kusema kwamba kutaniko hilo ni “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Timotheo 3:15) Bila shaka, kutaniko lote la Wakristo watiwa-mafuta lilithibitika kuwa nguzo katika karne ya kwanza. Na ni wazi kwamba kila Mkristo angeweza kupokea kweli hiyo hasa kupitia kutaniko la kwao. Hapo ndipo wangesikia kweli ikifundishwa na kutegemezwa, na ndipo wangejengwa kibinafsi.

18. Kwa nini mikutano ya kutaniko ni ya maana?

18 Vivyo hivyo, kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote ni nyumba ya Mungu, “nguzo na tegemezo la ile kweli.” Njia kuu ya kujenga na kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Mungu na kuzoezwa kufanya mapenzi yake ni kupitia kuhudhuria na kushiriki katika mikutano ya kutaniko. Paulo alipokuwa akiliandikia kutaniko huko Korintho, alikazia mambo yaliyozungumziwa katika mikutano kama hiyo. Aliandika kuwa alitamani mambo yaliyosemwa katika mikutano yawe wazi na yenye kueleweka ili wale wanaohudhuria waweze ‘kujengwa.’ (1 Wakorintho 14:12, 17-19) Leo, tunaweza kujengwa tukitambua kwamba Yehova Mungu ameanzisha mpango wa makutaniko, naye anayategemeza.

19. Kwa nini unahisi kwamba unapaswa kulithamini kutaniko lenu?

19 Kwa kweli, ikiwa tunatamani kujengwa tukiwa Wakristo, tunapaswa kubaki katika kutaniko. Kwa miaka mingi limekuwa ngome ya kutulinda kutokana na mafundisho ya uwongo, na Mungu amekuwa akilitumia kuhubiri habari njema ya Ufalme wake wa Kimasihi duniani pote. Hapana shaka kwamba Mungu ametimiza mengi kupitia kutaniko la Kikristo.—Waefeso 3:9, 10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Msomi wa Biblia Albert Barnes alitambua kwamba agizo la Yesu la ‘kuliambia kutaniko’ lingemaanisha “wale ambao wamepewa mamlaka ya kusikiliza kesi kama hizo, yaani, wawakilishi wa kanisa, au wale wanaotenda kwa ajili yao. Katika sinagogi la Wayahudi kulikuwa na wazee ambao walikuwa waamuzi, na kesi za aina hiyo zililetwa mbele yao.”

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunapaswa kutazamia Mungu atumie makutaniko duniani?

• Ingawa wazee si wakamilifu, wanafanya nini kwa faida ya kutaniko?

• Kutaniko lenu linakujenga kwa njia gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu walitumika wakiwa baraza linaloongoza

[Picha katika ukurasa wa 28]

Wazee na watumishi wa huduma wanafundishwa ili waweze kutimiza wajibu wao kuelekea kutaniko