Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutaniko na Limsifu Yehova

Kutaniko na Limsifu Yehova

Kutaniko na Limsifu Yehova

“Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kutaniko nitakusifu wewe.”—WAEBRANIA 2:12.

1, 2. Kwa nini kutaniko linawafaidi watu sana, na kusudi lake kuu ni nini?

KATIKA historia yote, watu wamepata urafiki na usalama katika familia. Hata hivyo, Biblia inataja mahali pengine ambapo watu wengi sana duniani pote leo wanafurahia usalama na urafiki wa pekee sana. Mahali hapo ni kutaniko la Kikristo. Iwe wewe ni mshiriki wa familia yenye umoja inayotoa utegemezo au hapana, unaweza na unapaswa kuthamini maandalizi ambayo Mungu amefanya kupitia mpango wa kutaniko. Bila shaka, ikiwa tayari unashirikiana na kutaniko la Mashahidi wa Yehova, unaweza kuthibitisha kwamba unafurahia ushirika mchangamfu katika kutaniko na una usalama.

2 Kutaniko si kikundi tu cha kijamii. Si shirika au kikundi cha watu wanaokutana kwa sababu wana malezi au mapendezi yanayofanana kuhusu michezo au utendaji fulani. Badala yake, kusudi kuu la mpango wa kutaniko ni kumsifu Yehova Mungu. Imekuwa hivyo kwa muda mrefu kama kitabu cha Zaburi kinavyokazia. Tunasoma hivi kwenye Zaburi 35:18: “Nitakusifu katika kutaniko kubwa; nitakusifu kati ya kikundi cha watu wengi.” Vivyo hivyo, Zaburi 107:31, 32 inatutia moyo hivi: “Watu na wamtolee Yehova shukrani kwa ajili ya fadhili zake zenye upendo na kwa ajili ya kazi zake za ajabu kwa wana wa binadamu. Na wamtukuze katika kutaniko la watu.”

3. Kulingana na Paulo, kutaniko linafanya nini?

3 Mtume Mkristo Paulo alikazia kusudi lingine muhimu la kutaniko alipotaja “nyumba ya Mungu, ambayo ni kutaniko la Mungu aliye hai, nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Timotheo 3:15) Paulo alikuwa akizungumza kuhusu kutaniko gani? Biblia inatumia neno “kutaniko” katika njia gani? Kutaniko linapaswa kuwa na uvutano gani katika maisha yetu na mambo ambayo tunatarajia? Ili kupata majibu, acheni kwanza tuchunguze jinsi neno “kutaniko” linavyotumiwa katika Neno la Mungu.

4. Mara nyingi neno “kutaniko” linatumiwa jinsi gani katika Maandiko ya Kiebrania?

4 Neno la Kiebrania ambalo mara nyingi linatafsiriwa “kutaniko,” linatokana na mzizi wa neno unaomaanisha “kusanya pamoja” au “kutanisha.” (Kumbukumbu la Torati 4:10; 9:10) Mtunga-zaburi alitumia neno “kutaniko” kuhusiana na malaika mbinguni, nalo linaweza kutumiwa kuhusu kikundi cha watu waovu. (Zaburi 26:5; 89:5-7) Hata hivyo, mara nyingi Maandiko ya Kiebrania yanatumia neno hilo kuwahusu Waisraeli. Mungu alisema kwamba Yakobo angekuwa “kutaniko la vikundi vya watu,” na hilo lilitukia. (Mwanzo 28:3; 35:11; 48:4) Waisraeli walikusanywa au walichaguliwa kuwa “kutaniko la Yehova,” “kutaniko la Mungu wa kweli.”—Hesabu 20:4; Nehemia 13:1; Yoshua 8:35; 1 Samweli 17:47; Mika 2:5.

5. Ni neno gani la Kigiriki ambalo kwa kawaida linatafsiriwa kuwa “kutaniko,” na neno hilo linaweza kutumiwa katika njia gani?

5 Katika Kigiriki neno kutaniko ni ek·kle·siʹa, linalotokana na maneno mawili ya Kigiriki yanayomaanisha “nje” na “ita.” Linaweza kutumiwa kuhusu kikundi kinachokusanyika kwa makusudi yasiyo ya kidini, kama lile “kusanyiko” ambalo Demetrio alichochea limshambulie Paulo huko Efeso. (Matendo 19:32, 39, 41) Lakini kwa ujumla Biblia inatumia neno hilo kuhusu kutaniko la Kikristo. Tafsiri fulani zinatafsiri neno hilo kuwa “kanisa,” lakini kamusi moja (The Imperial Bible-Dictionary) inasema kwamba ‘neno hilo halimaanishi kamwe jengo halisi ambamo Wakristo wanakusanyikia kwa ajili ya ibada ya watu wote.’ Hata hivyo, inapendeza kwamba katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo neno “kutaniko” linatumiwa katika angalau njia nne tofauti.

Kutaniko la Mungu Lililotiwa Mafuta

6. Daudi na Yesu walifanya nini katika kutaniko?

6 Akitumia maneno ya Daudi yaliyo katika Zaburi 22:22 kumhusu Yesu, mtume Paulo aliandika hivi: “‘Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kutaniko nitakusifu wewe kwa wimbo.’ Kwa hiyo, [Yesu] alipaswa kuwa kama ‘ndugu’ zake katika mambo yote, ili awe kuhani mkuu mwenye rehema na mwaminifu katika mambo yanayohusiana na Mungu.” (Waebrania 2:12, 17) Daudi alikuwa amemsifu Mungu katikati ya kutaniko la Israeli la kale. (Zaburi 40:9) Hata hivyo, Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba Yesu alimsifu Mungu “katikati ya kutaniko”? Ni kutaniko gani hilo?

7. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanatumia neno “kutaniko” katika njia gani ya msingi?

7 Maneno tunayosoma katika Waebrania 2:12, 17 ni yenye maana sana. Yanaonyesha kwamba Kristo alikuwa mshiriki wa kutaniko ambamo alitangaza jina la Mungu kwa ndugu zake. Ndugu hao ni nani? Ni wale ambao ni sehemu ya “uzao wa Abrahamu,” ndugu za Kristo waliotiwa mafuta, “washiriki wa mwito wa mbinguni.” (Waebrania 2:16–3:1; Mathayo 25:40) Basi, maana ya msingi ya neno “kutaniko” katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ni kikundi chenye washiriki wengi cha wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo. Watiwa-mafuta hao 144,000 wanafanyiza “kutaniko la wazaliwa wa kwanza ambao wameandikishwa mbinguni.”—Waebrania 12:23.

8. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba kutaniko la Kikristo lingeanzishwa?

8 Yesu alionyesha kwamba “kutaniko” hilo la Kikristo lingeanzishwa. Mwaka mmoja hivi kabla ya kifo chake, Yesu alimwambia hivi mmoja wa mitume wake: “Wewe ni Petro, na juu ya mwamba huu nitajenga kutaniko langu, na malango ya Kaburi hayatalizidi nguvu.” (Mathayo 16:18) Petro na Paulo walielewa kwa usahihi kwamba Yesu mwenyewe ndiye mwamba uliotabiriwa. Petro aliandika kwamba wale ambao wanajengwa kama “mawe yaliyo hai” ya nyumba ya kiroho juu ya mwamba, yaani, Kristo, walikuwa ‘watu wa kuwa mali ya pekee, ili watangaze kotekote sifa bora’ za Yule aliyewaita.—1 Petro 2:4-9; Zaburi 118:22; Isaya 8:14; 1 Wakorintho 10:1-4.

9. Kutaniko la Mungu lilianza kufanyizwa wakati gani?

9 ‘Watu hao waliokuwa mali ya pekee’ walianza kufanyizwa kuwa kutaniko la Kikristo wakati gani? Ni wakati wa Pentekoste 33 W.K., Mungu alipomwaga roho takatifu juu ya wanafunzi waliokusanyika huko Yerusalemu. Baadaye siku hiyo, Petro alitoa hotuba yenye kuchochea sana kwa kikundi cha Wayahudi na watu waliogeuzwa imani. Wengi wao walichomwa moyoni kuhusu kifo cha Yesu; wakatubu na kubatizwa. Simulizi la Biblia linaripoti kwamba watu elfu tatu walifanya hivyo, na muda mfupi baadaye wakawa sehemu ya kutaniko jipya la Mungu ambalo lilikuwa likiongezeka. (Matendo 2:1-4, 14, 37-47) Lilikuwa likiongezeka kwa sababu watu waliogeuzwa imani pamoja na Wayahudi wengi zaidi na zaidi walikubali ukweli wa kwamba taifa la Israeli la asili halikuwa tena kutaniko la Mungu. Badala yake, Wakristo watiwa-mafuta waliokuwa “Israeli wa Mungu” sasa walikuwa kutaniko la kweli la Mungu.—Wagalatia 6:16; Matendo 20:28.

10. Kuna uhusiano gani kati ya Yesu na kutaniko la Mungu?

10 Mara nyingi, Biblia inamtofautisha Yesu na watiwa-mafuta. Kwa mfano, inasema “kwa habari ya Kristo na kutaniko.” Yesu ndiye Kichwa cha kutaniko hilo la Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho. Paulo aliandika kwamba Mungu ‘alimfanya Yesu kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko, ambalo ni mwili wake.’ (Waefeso 1:22, 23; 5:23, 32; Wakolosai 1:18, 24) Leo, ni mabaki wachache tu walio duniani wa washiriki watiwa-mafuta wa kutaniko hilo. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Kichwa chao, Yesu Kristo, anawapenda. Hisia zake kuwaelekea zinaelezwa kwenye Waefeso 5:25: ‘Kristo pia alilipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.’ Analipenda kwa sababu linamtolea Mungu kwa bidii “dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani,” kama Yesu alivyofanya alipokuwa duniani.—Waebrania 13:15.

Maana Nyingine za Neno “Kutaniko”

11. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanatumia neno “kutaniko” katika njia gani ya pili?

11 Nyakati nyingine, Biblia inatumia neno “kutaniko” katika njia ya pekee zaidi ambayo haihusu kikundi kizima cha watiwa-mafuta 144,000 ambao ni “kutaniko la Mungu.” Kwa mfano, Paulo alisema hivi alipoandikia kikundi kimoja cha Wakristo: “Epukeni kuwa vikwazo kwa Wayahudi na vilevile kwa Wagiriki na kwa kutaniko la Mungu.” (1 Wakorintho 10:32) Bila shaka, ikiwa Mkristo fulani katika Korintho la kale angetenda kwa njia isiyofaa, huenda angekwaza wengine. Lakini je, angeweza kuwakwaza Wagiriki, Wayahudi, au watiwa-mafuta wote kuanzia wakati huo mpaka leo? Bila shaka hapana. Kwa hivyo, inaonekana kwamba katika mstari huo maneno “kutaniko la Mungu” yanamaanisha Wakristo wanaoishi katika kipindi fulani. Hivyo basi, mtu anaweza kusema kwamba Mungu analiongoza, analitegemeza, au analibariki kutaniko, kumaanisha Wakristo wote wanaoishi katika kipindi fulani, haidhuru wanaishi wapi. Au tunaweza kusema kwamba furaha na amani inaenea katika kutaniko la Mungu leo, tukimaanisha undugu mzima wa Wakristo.

12. Biblia inatumia neno “kutaniko” katika njia gani ya tatu?

12 Biblia inatumia neno “kutaniko” katika njia ya tatu kuhusu Wakristo wote wanaoishi katika eneo fulani. Tunasoma hivi: “Kutaniko kotekote katika Yudea na Galilaya na Samaria likaingia katika kipindi cha amani.” (Matendo 9:31) Kulikuwa na vikundi vingi vya Kikristo katika eneo hilo kubwa, lakini vikundi hivyo vyote katika Yudea, Galilaya, na Samaria vinaitwa “kutaniko.” Tukifikiria idadi ya watu waliobatizwa siku ya Pentekoste 33 W.K. na muda mfupi baadaye, huenda kulikuwa na vikundi mbalimbali vilivyokusanyika kwa ukawaida katika eneo la Yerusalemu. (Matendo 2:41, 46, 47; 4:4; 6:1, 7) Herode Agripa wa Kwanza alitawala Yudea mpaka alipokufa mwaka wa 44 W.K., na kutokana na andiko la 1 Wathesalonike 2:14, ni wazi kwamba kufikia mwaka wa 50 W.K. hivi kulikuwa na makutaniko kadhaa huko Yudea. Hivyo, tunaposoma kwamba Herode alikuwa ‘akiwatendea vibaya baadhi ya wale wa kutaniko,’ huenda inamaanisha vikundi mbalimbali vilivyokusanyika kwa ukawaida huko Yerusalemu.—Matendo 12:1.

13. Biblia inatumia neno “kutaniko” katika njia gani ya nne ambayo ni ya kawaida?

13 Neno “kutaniko” linatumiwa katika njia ya nne ambayo ni ya kawaida na ya pekee kumaanisha Wakristo wanaofanyiza kutaniko moja linalokutana mahali fulani, kama vile katika nyumba fulani. Paulo alitaja “makutaniko ya Galatia.” Kulikuwa na zaidi ya kutaniko moja kama hilo katika jimbo hilo kubwa la Roma. Mara mbili Paulo alitumia neno “makutaniko” alipotaja Galatia. Yalitia ndani makutaniko yaliyokuwa Antiokia, Derbe, Listra, na Ikoniamu. Wanaume wazee walio na sifa za kustahili, au waangalizi, waliwekwa rasmi katika kila moja ya makutaniko hayo. (1 Wakorintho 16:1; Wagalatia 1:2; Matendo 14:19-23) Kulingana na Maandiko, yote hayo yalikuwa “makutaniko ya Mungu.”—1 Wakorintho 11:16; 2 Wathesalonike 1:4.

14. Tunaweza kukata kauli gani kutokana na jinsi neno “kutaniko” linavyotumiwa katika maandiko machache?

14 Nyakati nyingine, haikosi vikundi vilivyohudhuria mikutano ya Kikristo vilikuwa vidogo, na vilitoshea katika nyumba ya mtu fulani. Hata hivyo, neno “kutaniko” lilitumiwa kuhusu vikundi fulani kama hivyo. Tunajua kwamba kulikuwa na makutaniko katika nyumba ya Akila na Priska, Nimfa, na Filemoni. (Waroma 16:3-5; Wakolosai 4:15; Filemoni 2) Jambo hilo linapaswa kutia moyo makutaniko ya leo ambayo ni madogo sana na ambayo huenda hata yanakutana kwa ukawaida katika nyumba fulani. Yehova alitambua makutaniko kama hayo madogo katika karne ya kwanza, na bila shaka anafanya hivyo leo, naye anayabariki kupitia roho yake.

Makutaniko Yanamsifu Yehova

15. Utendaji wa roho takatifu ulionekana jinsi gani katika makutaniko fulani ya karne ya kwanza?

15 Tuliona kwamba Yesu alitimiza Zaburi 22:22 kwa kumsifu Mungu katikati ya kutaniko. (Waebrania 2:12) Wafuasi wake waaminifu walipaswa kufanya vivyo hivyo. Katika karne ya kwanza, Wakristo wa kweli walipotiwa mafuta kwa roho takatifu ili kuwa wana wa Mungu na ndugu za Kristo, roho ilianza kutenda kazi juu ya wengine wao kwa njia nyingine ya pekee. Walipokea zawadi za kimuujiza za roho. Zawadi hizo zilionekana kwa njia kama vile maneno ya pekee ya hekima au ujuzi, nguvu za kuponya au kutoa unabii, au hata uwezo wa kusema lugha ambazo hawakuzijua.—1 Wakorintho 12:4-11.

16. Taja moja ya makusudi ya zawadi za kimuujiza.

16 Paulo alisema hivi kuhusu kusema kwa lugha: “Nitaimba sifa kwa zawadi ya roho, lakini pia nitaimba sifa kwa akili yangu.” (1 Wakorintho 14:15) Alitambua umuhimu wa wengine kuelewa maneno yake ili wajifunze. Kusudi la Paulo lilikuwa kumsifu Yehova katika kutaniko. Aliwahimiza hivi wengine waliokuwa na zawadi za roho: “Tafuteni kujawa nazo kwa ajili ya kulijenga kutaniko,” yaani, kutaniko ambamo walitumia zawadi hizo. (1 Wakorintho 14:4, 5, 12, 23) Ni wazi kwamba Paulo alipendezwa na makutaniko ya kwao, akijua kwamba katika kila kutaniko Wakristo wangepata nafasi za kumsifu Mungu.

17. Tunaweza kuwa na uhakika gani kuhusu makutaniko yetu leo?

17 Yehova anaendelea kulitumia na kulitegemeza kutaniko lake. Anabariki jamii ya Wakristo watiwa-mafuta walio duniani leo. Hilo linathibitishwa na chakula kingi sana cha kiroho ambacho watu wa Mungu wanapokea. (Luka 12:42) Anabariki undugu mzima wa ulimwenguni pote. Naye anabariki makutaniko yetu, ambamo tunamsifu Muumba wetu kwa matendo yetu na maelezo ya kiroho yenye kujenga. Katika makutaniko hayo tunaelimishwa na kuzoezwa ili tuweze kumsifu Mungu nyakati nyingine ambazo hatuko katikati ya kutaniko letu.

18, 19. Wakristo wenye kujitoa katika kutaniko lolote wanapaswa kufanya nini?

18 Kumbuka kwamba mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wa kutaniko la Filipi huko Makedonia: “Hili ndilo ninaloendelea kusali, kwamba [ninyi] mjazwe matunda ya uadilifu, ambayo ni kupitia Yesu Kristo, kwa utukufu na sifa kwa Mungu.” Hilo lingetia ndani kuwaambia wengine, wale walio nje, kuhusu imani yao katika Yesu na tumaini lao zuri. (Wafilipi 1:9-11; 3:8-11) Kwa hivyo, Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Kupitia [Yesu] sikuzote na tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.”—Waebrania 13:15.

19 Je, unafurahia kumsifu Mungu “katikati ya kutaniko,” kama Yesu alivyofanya, na kutumia midomo yako kumsifu Yehova mbele ya wale ambao sasa hawamjui wala hawamsifu Yehova? (Waebrania 2:12; Waroma 15:9-11) Kwa kadiri fulani, jibu letu binafsi linaweza kutegemea jinsi tunavyohisi kuhusu wajibu wa kutaniko letu katika kusudi la Mungu. Katika habari inayofuata, tutachunguza jinsi Yehova anavyoelekeza na kulitumia kutaniko letu na wajibu wa kutaniko hilo katika maisha yetu leo.

Je, Unakumbuka?

• “Kutaniko la Mungu” ambalo limefanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta lilianza jinsi gani?

• Biblia inatumia neno “kutaniko” katika maana gani nyingine tatu?

• Daudi, Yesu, na Wakristo wa karne ya kwanza walitaka kufanya nini kuhusiana na kutaniko, na hilo linapaswa kuwa na matokeo gani kwetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yesu alikuwa msingi wa kutaniko gani?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Vikundi vya Wakristo vilikutana vikiwa “makutaniko ya Mungu”

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kama Wakristo wa Benin, tunaweza kumsifu Yehova katikati ya makundi yaliyokutanika