Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Mkristo anapaswa kuepuka vinywaji na vyakula ambavyo vina kafeini?

Biblia haimkatazi Mkristo kunywa vinywaji kama vile kahawa, chai, chokoleti, na soda zenye kafeini. Hata hivyo, Maandiko yanatoa kanuni ambazo zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima. Acheni kwanza tuzungumzie kwa nini watu fulani wanaepuka vinywaji na vyakula ambavyo vina kafeini.

Sababu moja kuu ni kwamba kafeini inaweza kuonwa kuwa dawa ya kulevya ambayo inasisimua akili na kuathiri hisia. Inaweza pia kusababisha uraibu au kuzoea. Kitabu kimoja cha madaktari wa madawa kinasema hivi: “Kutumia kafeini nyingi kwa muda mrefu kunaweza kumfanya mtu awe mtumiaji sugu, mzoefu, au mraibu. Mtu anayeacha ghafula kutumia kafeini anapata matatizo kama vile kuumwa na kichwa, kukasirika-kasirika, wasiwasi, mahangaiko, na kizunguzungu.” Matatizo hayo yanayosababishwa na kuacha kafeini yanafikiriwa kuorodheshwa pamoja na matatizo mengine ya kuacha dawa za kulevya katika kitabu kimoja cha magonjwa ya akili (Diagnostic and Statistical Manual of Mental Disorders). Kwa hiyo, inaeleweka kwamba huenda Wakristo fulani wakahisi haifai kutumia kafeini kwa sababu wanataka kuepuka kuzoea au uraibu na wanataka kuonyesha sifa ya kujizuia.—Wagalatia 5:23.

Watu fulani wanaamini kwamba kafeini inaweza kuathiri afya ya mtu au ya mtoto ambaye hajazaliwa. Ni lazima Wakristo wampende Mungu ‘kwa nafsi yao yote,’ kwa hiyo hawafanyi jambo lolote ambalo litafupisha maisha yao. Na kwa kuwa wanaamriwa pia wampende jirani yao, wanaepuka vitu ambavyo vinaweza kumdhuru mtoto ambaye hajazaliwa.—Luka 10:25-27.

Je, ni muhimu kuwa na mahangaiko hayo ya kiafya? Kuna ubishi kuhusu uhusiano kati ya magonjwa mbalimbali na utumiaji wa kafeini. Watafiti fulani hata wanasema kwamba kahawa ni kinywaji kizuri kwa afya. Katika mwaka wa 2006, gazeti moja (Time) liliripoti hivi: “Uchunguzi wa mwanzoni ulionyesha [kwamba kafeini] inaweza kusababisha kansa ya kibofu, shinikizo la juu la damu na magonjwa mengine. Utafiti wa hivi karibuni umepinga mengi ya madai hayo na zaidi ya hilo umetaja faida fulani muhimu. Inaonekana kwamba kafeini inazuia kwa kadiri fulani matatizo ya ini, ugonjwa wa kutetemeka (Parkinson’s disease), ugonjwa wa sukari, ugonjwa wa Alzheimer, vijiwe vya nyongo, kushuka moyo na huenda inazuia pia aina fulani za kansa.” Kuhusu matumizi ya kafeini, gazeti moja liliripoti hivi: “Hapana shaka kwamba siri ni kuitumia kwa kiasi.”

Kila Mkristo anapaswa kufanya uamuzi wake binafsi unaotegemea uelewaji wake wa habari inayopatikana sasa kuhusu kafeini na kuhusu kanuni za Biblia ambazo zinahusika. Kwa mfano, Mkristo ambaye ni mama mjamzito anaweza kuamua kutotumia kafeini akiwa na mimba ikiwa atakata kauli kwamba inaweza kuathiri mtoto wake ambaye hajazaliwa. Ikiwa Mkristo anaona kwamba kutotumia kafeini kwa ukawaida kunamfanya akasirike-kasirike au awe mgonjwa, anaweza kushauriwa aache kutumia kafeini angalau kwa muda fulani. (2 Petro 1:5, 6) Wakristo wengine wanapaswa kuheshimu uamuzi kama huo, bila kumlazimisha afuate maoni yao.

Katika uamuzi wowote unaofanya kuhusu vinywaji na vyakula ambavyo vina kafeini, kumbuka himizo hili la Paulo: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.