Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matarajio Yanapokosa Kutimizwa

Matarajio Yanapokosa Kutimizwa

Matarajio Yanapokosa Kutimizwa

HALI ya kuvunjika moyo inaweza kusitawi katika ndoa yoyote, hata ikiwa wakati wa uchumba ilionekana kwamba mwanamume na mwanamke walikuwa wanapatana sana. Lakini kwa nini watu wawili walioonekana kuwa wanapatana sana kabla ya kuweka nadhiri za ndoa wanabadilika na kuwa tofauti kabisa baadaye?

Biblia inasema kwamba wale wanaofunga ndoa watakuwa na “uchungu na huzuni.” (1 Wakorintho 7:28, The New English Bible) Mara nyingi, dhiki hiyo inasababishwa kwa kiasi fulani na kutokamilika kwa kibinadamu. (Waroma 3:23) Kwa kuongezea, huenda mwenzi mmoja au wote wawili hawafuati kanuni za Biblia. (Isaya 48:17, 18) Hata hivyo, nyakati nyingine mwanamume au mwanamke anaingia katika ndoa akiwa na matarajio yasiyo halisi. Hilo likitukia, kutoelewana kunaweza kusababisha matatizo mazito.

Matarajio Yasiyo Halisi

Ikiwa wewe ni mume au mke, inaelekea kwamba uliingia katika ndoa ukiwa na matarajio fulani; na watu wengi wanakuwa nayo. Tua kidogo na ufikirie aina ya maisha ambayo ulitarajia. Je, ndoa yako imekosa kutimiza matarajio yako? Ikiwa ndivyo, usikate kauli kwamba matatizo hayawezi kutatuliwa. Kufuata kanuni za Biblia kunaweza kukusaidia kunyoosha mambo. * (2 Timotheo 3:16) Kwa sasa, inafaa uchunguze matarajio fulani ambayo ulikuwa nayo kuhusu ndoa.

Kwa mfano, watu fulani wamefikiri kwamba sikuzote wataonyeshana mapenzi katika maisha yao ya ndoa, kama ilivyo katika hadithi nyingi za mapenzi. Au labda ulifikiri kwamba wewe na mwenzi wako mtakuwa kila mara pamoja au nyote wawili mtatatua kila tatizo linalotokea kati yenu kwa njia nzuri na ya ukomavu. Watu wengi waliamini kwamba ndoa ingeondoa kabisa uhitaji wa kujizuia katika ngono. Bila shaka, matarajio hayo yote ya kawaida yanawakatisha tamaa watu fulani kwa sababu kwa njia fulani matarajio hayo si halisi.—Mwanzo 3:16.

Matarajio mengine yasiyo halisi ni kwamba kufunga ndoa tu kunaweza kumfanya mtu awe na furaha. Bila shaka, kuwa na mwenzi maishani kunaweza kuleta shangwe kubwa. (Methali 18:22; 31:10; Mhubiri 4:9) Lakini je, tunaweza kutarajia ndoa isuluhishe kimuujiza matatizo yoyote ya kutoelewana? Kwa kawaida, wale wanaofikiri hivyo wanashtuka wanapogundua kwamba sivyo ilivyo!

Matarajio Yasiyosemwa

Kuna matarajio mengine ambayo ni halisi. Kuna yale ambayo yanahusu tamaa nzuri. Ingawa hivyo, matatizo yanaweza kutokea kwa sababu ya matarajio fulani. Mshauri mmoja wa ndoa anasema hivi: “Ninaona wenzi wa ndoa wakikasirikiana kwa sababu mmoja wao anangoja tamaa fulani aliyonayo itimizwe, lakini mwenzi wake hata hajui kamwe kwamba mwenzake ana tamaa hiyo.” Ili kuelewa jinsi hilo linavyoweza kutukia, fikiria kisa kifuatacho.

Mary anaolewa na David, ambaye anaishi mamia ya kilomita kutoka nyumbani kwa akina Mary. Kabla ya kufunga ndoa, Mary alitambua kwamba angekabili magumu fulani ikiwa angehamia eneo jipya, hasa kwa kuwa kwa kawaida yeye ni mwoga. Hata hivyo, alikuwa na hakika kwamba David angemsaidia kuzoea hali. Kwa mfano, Mary alitarajia kwamba David angekuwa kando yake na kumsaidia kuwafahamu marafiki wake. Hata hivyo, David hafanyi hivyo. David anazungumza sana na marafiki wake wengi, huku akimwacha Mary, ambaye ni mpya, akiwa peke yake. Mary anahisi kwamba David anampuuza, hata anahisi ni kana kwamba ameachwa. Anajiuliza hivi, ‘Mbona David hajali hisia zangu hata kidogo?’

Je, Mary ana matarajio yasiyo halisi? Hapana. Anataka tu mume wake amsaidie kuzoea mazingira hayo mapya. Mary ni mwoga, naye anavurugika kwa sababu ya kukutana na watu wengi sana wapya. Hata hivyo, ukweli ni kwamba Mary hajawahi kamwe kumfunulia David hisia zake. Kwa hiyo, David hajui hali ambayo Mary anakabili. Ni nini kitakachotukia hali hiyo ikiendelea? Uchungu wa Mary unaweza kuongezeka, na baada ya muda, anaweza kufikiri kwamba mume wake anapuuza kabisa hisia zake.

Huenda wewe pia umewahi kuvunjika moyo na kukata tamaa wakati inapoonekana kwamba mwenzi wako wa ndoa anapuuza mahitaji yako. Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini?

Zungumzeni Kuhusu Matarajio Yenu

Matarajio yasiyotimizwa yanaweza kwa kweli kumfadhaisha mtu. (Methali 13:12) Hata hivyo, kuna jambo unaloweza kufanya kuhusu hali hiyo. Methali moja ya Biblia inasema: “Unaweza kuwashawishi wengine ukiwa na hekima na ukizungumza kupatana na akili.” (Methali 16:23, Contemporary English Version) Kwa hiyo, ukihisi kwamba una matarajio mazuri ambayo hayatimizwi, zungumzia jambo hilo na mwenzi wako.

Jaribu kuchagua wakati unaofaa, mahali panapofaa, na maneno yanayofaa ili kueleza mambo yanayokuhangaisha. (Methali 25:11) Zungumza kwa utulivu na heshima. Kumbuka kusudi lako si kumshutumu mwenzi wako bali ni kumjulisha kuhusu matarajio na hisia zako.—Methali 15:1.

Je, una sababu yoyote ya kufanya hivyo? Je, mwenzi mwenye kujali hana uwezo wa kutambua mahitaji yako? Kwa kweli, huenda mwenzi wako ana maoni tofauti lakini angefurahi na kutilia maanani maoni yako ikiwa ungemweleza. Kusema mambo unayotaka au unayohitaji si ishara ya kwamba ndoa yenu haijafaulu wala hakuonyeshi kwamba mwenzi wako hajali.

Kwa hiyo, usisite kuzungumzia mambo pamoja na mwenzi wako. Kwa mfano, katika kisa kilichotajwa mapema, Mary angemwambia David: “Ninakubali kwamba ninaogopa kukutana na watu wengi wapya. Je, unaweza kunisaidia kuwa mtulivu mpaka nitakapowazoea?”

“Mwepesi Kuhusu Kusikia”

Sasa chunguza jambo hilo kwa njia nyingine. Tuseme kwamba mwenzi wako anakufikia, naye amefadhaika kwa sababu hutimizi tarajio fulani zuri. Msikilize mwenzi wako akikufikia! Jitahidi kuepuka kujitetea. Badala yake, ‘uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19; Methali 18:13) Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.

Unaweza kufanya hivyo kwa kujiweka katika hali ya mwenzi wako. Biblia inasema hivi: “Enyi waume, endeleeni kukaa [na wake zenu] vivyo hivyo kulingana na ujuzi,” au, kama tafsiri ya J. B. Philip inavyosema, “ninyi waume mnapaswa kujitahidi kuwaelewa wake mnaoishi nao.” (1 Petro 3:7) Bila shaka, wake wanapaswa pia kujitahidi kufanya vivyo hivyo kuhusu waume zao.

Kumbuka kwamba hata iwe unapatana kadiri gani na mwenzi wako wa ndoa, hamwoni mambo yote kwa njia ileile. (Ona sanduku “Mandhari Ileile, Maoni Tofauti.”) Kwa kweli, kuna faida ya kuona mambo kulingana na maoni ya mtu mwingine. Nyote wawili, yaani, wewe na mwenzi wako mliingia katika ndoa yenu mkiwa na matarajio ya pekee yaliyotegemea mambo kama vile malezi ya familia na utamaduni. Kwa hiyo, mnaweza kupendana sana na bado muwe na matarajio yasiyopatana.

Kwa mfano, huenda wenzi Wakristo wakajua kanuni ya Biblia kuhusu ukichwa. (Waefeso 5:22, 23) Lakini, ukichwa utatumiwa kwa njia gani katika familia yenu, na ujitiisho utaonyeshwa jinsi gani? Je, nyote wawili mnaongozwa na kanuni hiyo ya Biblia, na je, mnajitahidi kikweli kuifuata?

Mnaweza pia kuwa na maoni tofauti kuhusu masuala mengine katika maisha ya kila siku. Ni nani atakayefanya kazi fulani za nyumbani? Ni wakati gani mtakuwa pamoja na watu wa ukoo, na mtakuwa nao kwa muda gani? Wenzi Wakristo wataonyesha jinsi gani kwamba wanatanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao? (Mathayo 6:33) Kuhusu pesa, ni rahisi kuwa na madeni, kwa hiyo ni vizuri kutumia pesa kwa busara na kutafuta njia za kuokoa pesa. Lakini kutumia pesa kwa busara na kuziokoa kunamaanisha nini? Mambo kama hayo yanahitaji kuzungumziwa waziwazi na kwa heshima. Mtafaidika sana mkifanya hivyo.

Mazungumzo kama hayo yanaweza kuwasaidia kupata amani nyingi zaidi katika ndoa yenu, hata ikiwa matarajio fulani hayajatimizwa kufikia sasa. Kwa kweli, mtaweza hata zaidi kufuata himizo hili la mtume Paulo: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”—Wakolosai 3:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kina mashauri mengi mazuri kwa ajili ya wenzi wa ndoa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

MANDHARI ILEILE, MAONI TOFAUTI

“Ebu wazia umati wa watalii ukitazama mandhari yenye kuvutia sana. Ingawa kikundi chote kinatazama mandhari ileile, kila mtu aiona kwa njia tofauti. Kwa nini? Kwa sababu kila mtu mmoja-mmoja anaiona kutoka mahali tofauti. Hakuna watu wawili wanaosimama mahali palepale hasa. Zaidi ya hayo, si kila mtu anayekaza macho kwenye sehemu ileile ya mandhari hiyo. Kila mtu aona sehemu tofauti kuwa yenye kuvutia hasa. Ndivyo ilivyo katika ndoa. Hata wanapopatana sana, hakuna wenzi wawili wanaoshiriki maoni yaleyale hasa juu ya mambo. . . . Uwasiliano unatia ndani juhudi ya kupatanisha tofauti hizo katika uhusiano wa mwili mmoja. Hilo lataka kufanyiza wakati wa kuongea.”—Mnara wa Mlinzi, Agosti 1, 1993, ukurasa wa 4.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

YALE AMBAYO UNAWEZA KUFANYA SASA

• Chunguza tena matarajio yako. Je, ni halisi? Je, unatarajia mengi kutoka kwa mwenzi wako kuliko yale anayoweza kutimiza?Wafilipi 2:4; 4:5.

• Jitahidi kubadili matarajio yoyote yasiyo halisi. Kwa mfano, badala ya kusema, “Hatutakosa kuelewana kamwe,” azimia kujitahidi kutatua matatizo kwa njia ya amani.Waefeso 4:32.

• Zungumzieni matarajio yenu. Kuzungumzia mambo pamoja ni hatua muhimu ya kujifunza kuonyeshana upendo na heshima.Waefeso 5:33.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Uwe “mwepesi kuhusu kusikia” mahangaiko ya mwenzi wako