Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Safiri na Paulo Kwenda Beroya

Safiri na Paulo Kwenda Beroya

Safiri na Paulo Kwenda Beroya

Kazi ya wamishonari fulani wawili ilifanikiwa sana, na watu wengi sana wakawa waamini. Kisha umati ukainuka kuwapinga. Hivyo uamuzi ukafanywa. Kwa faida ya kutaniko jipya na kwa sababu ya usalama wa wamishonari hao, wamishonari hao wawili walipaswa kuondoka mara moja, katikati ya usiku. Hivyo, katika mwaka wa 50 W.K. hivi, Paulo na Sila wakakimbia kutoka katika bandari ya Thesalonike huko Makedonia. Walifunga safari kwenda kuhubiri huko Beroya.

KUTOKA mbali, watu wanaotembelea eneo hilo leo, kama wasafiri wa zamani, wanaweza kuona jiji la Beroya (Véroia) likiwa upande wa mashariki chini ya Mlima Bermios katika eneo lenye mimea mingi. Jiji hilo liko kilomita 65 hivi kusini magharibi ya Thesalonike na kilomita 40 kutoka katika Bahari ya Aegea. Mlima Olympus, unaosemekana kuwa makao ya miungu mikuu ya zamani ya Ugiriki, uko upande wa kusini.

Beroya ni mahali ambapo panawapendeza wanafunzi wa Biblia kwa kuwa Paulo alihubiri katika jiji hilo na kufanya wengi wawe Wakristo. (Matendo 17:10-15) Acheni tusafiri na Paulo na kuchunguza historia ya jiji hilo la kale.

Historia ya Zamani

Hakuna mtu anayejua kwa hakika wakati ambapo jiji la Beroya lilianzishwa. Wakaaji wa kwanza wa jiji hilo labda kutoka katika makabila ya Frigia, walifukuzwa na watu wa Makedonia katika karne ya saba K.W.K. Karne tatu baadaye, Makedonia lilitajirika baada ya ushindi wa Aleksanda Mkuu. Majengo na kuta zenye kuvutia zilijengwa, na pia madhabahu ya Zeu, Artemi, Apolo, Athena, na miungu mingine ya Wagiriki.

Kitabu kimoja cha historia kinasema kwamba kwa karne nyingi Beroya “lilitimiza mengi katika maeneo ya karibu na katika maeneo mengine kaskazini mwa Ugiriki.” Jiji hilo lilikuwa maarufu zaidi hasa wakati wa utawala wa Αntigonid, familia ya mwisho ya wafalme wa Makedonia (306-168 K.W.K.), ambao mwishowe walipinduliwa na Roma.

Wakati Waroma walipomshinda Mfalme Philip wa Tano mwaka wa 197 K.W.K., “mfumo wa zamani wa utawala uliondolewa na Roma ikawa mamlaka yenye nguvu mashariki mwa Mediterania,” kinasema kitabu fulani (Encyclopædia Britannica). Mwaka wa 168 K.W.K., huko Pydna, kilomita kadhaa kusini mwa Beroya, jemadari mmoja Mroma alimshinda Perseus, mfalme wa mwisho wa zamani wa Makedonia. Kama ilivyotabiriwa katika unabii wa Biblia, serikali kuu ya ulimwengu ya Ugiriki ilichukua mahali pa Roma. (Danieli 7:6, 7, 23) Baada ya vita hivyo, Beroya lilikuwa mojawapo ya majiji ya kwanza ya Makedonia kujisalimisha kwa Roma.

Katika karne ya kwanza K.W.K., Makedonia lilikuwa eneo la mapambano wakati wa vita kati ya Pompey na Kaisari Yulio. Kwa hakika, Pompey aliweka makao yake makuu na jeshi lake karibu na jiji la Beroya.

Linasitawi Chini ya Waroma

Wakati wa Pax Romana, au Amani ya Roma, watu waliotembelea Beroya waliona barabara zilizojengwa kwa mawe ambazo zilikuwa na nguzo pembeni. Jiji hilo lilikuwa na vyumba vya kuogea vya watu wote, kumbi, maktaba, na majengo yaliyotumiwa kwa ajili ya michezo yenye jeuri. Maji ya kunywa yalipitishwa kwenye mabomba, na jiji hilo lilikuwa na mfumo wa chini ya ardhi wa kuondoa maji machafu. Beroya lilijulikana sana kuwa kituo cha kibiashara kilichotembelewa na wafanyabiashara, wasanii, wanamichezo, na watu waliokuja kutazama michezo na matukio mengine. Wageni wangeweza kupata mahali pa kuabudu ambapo wangefanyia desturi zao za kidini. Ndiyo, watu wa madhehebu ya milki yote ya Roma walikutana katika jiji hilo.

Maliki wa Roma waliokufa walionwa kuwa miungu nao waliabudiwa huko Beroya. Hilo halikuwa jambo geni kwa Waberoya kwa sababu Aleksanda Mkuu aliabudiwa kama mungu na hivyo kuanzisha ibada ya maliki. Kitabu kimoja cha Kigiriki kinasema hivi: “Kwa kuwa walizoea kuheshimu mfalme kama mungu wakati wa maisha yake, Wagiriki wa Milki ya mashariki walifurahia kuwaabudu na kuwaheshimu maliki wa Roma pia . . . Kwenye sarafu zao maliki alionyeshwa kuwa mungu, akiwa amevaa taji linalong’aa. Walimsifu kama mungu kwa nyimbo.” Madhabahu na mahekalu yalijengwa na dhabihu zilitolewa kwake. Hata maliki walikuja kuhudhuria sherehe za kidini za serikali ambazo zilitia ndani mashindano ya michezo, sanaa, na ya uandishi.

Kwa nini Beroya lilikuwa kituo cha ibada ya kipagani? Ni kwa sababu Koinon ya Makedonia ilikuwa huko. Koinon ilikuwa bunge lenye wajumbe kutoka katika majiji ya Makedonia. Wajumbe hao walikutana kwa ukawaida huko Beroya ili kuzungumzia mambo yanayohusu majiji na jimbo na kuyashughulikia chini ya usimamizi wa Roma. Moja ya kazi kuu za Koinon ilikuwa kusimamia sherehe za kidini za serikali.

Hiyo ndiyo iliyokuwa hali ya jiji ambamo Paulo na Sila walikimbilia walipotoka Thesalonike. Kufikia wakati huo, Beroya lilikuwa chini ya utawala wa Roma kwa karne mbili.

Habari Njema Inafika Beroya

Paulo alianza kazi yake ya kuhubiri huko Beroya katika sinagogi la jiji hilo. Walimpokea namna gani? Simulizi lililoongozwa na roho linasema kwamba Wayahudi wa huko “walikuwa wasikivu kuliko wale wa Thesalonike, kwa maana walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:10, 11) Kwa kuwa “walikuwa wasikivu,” hawakushikilia desturi zao kwa ushupavu. Ingawa walikuwa wakisikia mambo mapya, hawakuwa na maoni mabaya wala hawakukasirika. Badala ya kukataa ujumbe wa Paulo, walimsikiliza kwa makini bila kushikilia tu maoni yao na bila ubaguzi.

Wayahudi hao wangeweza kutambua jinsi gani ukweli katika mafundisho ya Paulo? Walichunguza yale waliyosikia kwa kutumia chanzo chenye kutegemeka zaidi. Walichunguza Maandiko kwa uangalifu na kwa bidii. Msomi wa Biblia, Matthew Henry, alikata kauli hii: “Kwa kuwa Paulo alitumia maandiko kuwasadikisha, na kuwaelekeza kwenye Agano la Kale ili wathibitishe yale aliyosema, waligeukia Biblia zao, wakafungua maandiko aliyowatajia, wakasoma masimulizi yote, wakachunguza kwa undani maana ya masimulizi hayo, wakayalinganisha na maandiko mengine, wakachunguza ikiwa maelezo ya Paulo yalikuwa sahihi na ya kweli na ikiwa sababu alizotoa zilikuwa zenye kusadikisha, na hivyo wakakata kauli yao wenyewe.”

Huo haukuwa uchunguzi wa kijuu-juu tu uliofanywa mara moja. Waberoya walijifunza kwa bidii na bila kuacha, wakitumia wakati fulani kila siku kufanya hivyo, wala si siku ya Sabato tu.

Hebu wazia matokeo ya kufanya hivyo. Wayahudi wengi huko Beroya walikubali ujumbe huo na kuwa waamini. Wagiriki fulani, labda kutia ndani Wayahudi waliogeuzwa imani waliamini pia. Lakini jambo hilo liliwaudhi wengine. Wayahudi kutoka Thesalonike walipopata habari hizo, walienda haraka Beroya “ili kuchochea na kuwafadhaisha watu.”—Matendo 17:4, 12, 13.

Paulo alilazimika kuondoka Beroya, lakini aliendelea na kazi yake ya kuhubiri katika maeneo mengine. Wakati huu alisafiri kwa meli iliyokuwa ikienda Athene. (Matendo 17:14, 15) Hata hivyo, angeweza kushangilia kwamba Ukristo ulitia mizizi huko Beroya kwa sababu ya kazi yake. Na kazi hiyo inazaa matunda leo.

Ndiyo, bado kuna watu huko Beroya (Véroia) ambao wanachunguza Maandiko kwa uangalifu ili ‘wahakikishe mambo yote’ na ‘kushika sana’ mambo ambayo yamethibitishwa kabisa na ya kweli. (1 Wathesalonike 5:21) Makutaniko mawili ya Mashahidi wa Yehova ambayo yanasitawi katika eneo hilo yanahubiri kama Paulo alivyofanya, na kuwapelekea watu ujumbe wa Biblia. Wanawatafuta watu wenye mioyo minyoofu na kujadiliana nao kwa kutumia Maandiko, nao wanaacha nguvu zenye kuchochea za Biblia ziwasaidie wote wanaotaka kumjua Yehova, Mungu wa kweli.—Waebrania 4:12.

[Ramani katika ukurasa wa 13]

 

Sehemu ya safari ya pili ya umishonary ya Paulo

MISIA

Troasi

Neapoli

Filipi

MAKEDONIA

Amfipoli

Thesalonike

Beroya

UGIRIKI

Athene

Korintho

AKAYA

ASIA

Efeso

RODESI

[Picha katika ukurasa wa 13]

Sarafu ya fedha ya Aleksanda Mkuu akiwa amefananishwa na mungu wa Wagiriki

[Hisani]

Coin: Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Lango la makao ya Wayahudi huko Beroya (Véroia)

[Picha katika ukurasa wa 15]

Sinagogi la zamani katika jiji la leo la Beroya (Véroia)