Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tamaa ya Adryana

Tamaa ya Adryana

Tamaa ya Adryana

ADRYANA, msichana mwenye umri wa miaka sita huko Tulsa, Oklahoma, Marekani alitamani sana jambo fulani. Tamaa yake ilikuwa kama ya mtunga-zaburi Daudi, aliyeimba hivi: “Nimemwomba Yehova jambo moja—ndilo nitakalolitafuta, kwamba nipate kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yangu, ili kuuona uzuri wa Yehova na kulitazama kwa uthamini hekalu lake.”—Zaburi 27:4.

Adryana alipokuwa na umri wa miezi sita tu, aligunduliwa kuwa na aina fulani ya kansa (neuroblastoma), uvimbe wenye kuua unaokua katika mfumo wa neva. Ugonjwa huo hatari ulifanya miguu yake ipooze. Madaktari walimtibu kwa kemikali kwa mwaka mzima na kumfanyia upasuaji mara nyingi.

Baba ya Adryana ambaye hafuati dini ya Adryana na mama yake, alienda kwenye shirika fulani na kuomba binti yake atembelee mahali fulani maarufu pa burudani. Kabla ya kukubali ombi hilo, shirika hilo lilimhoji Adryana. Aliwashukuru kwa sababu ya kumfikiria lakini akawaambia kwamba badala yake angependa kutembelea Betheli, makao makuu ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote huko New York. Alipopata habari kuhusu ombi la baba yake, Adryana alimwomba Yehova ampe nafasi ya kutembelea Betheli. Ingawa mwanzoni shirika hilo lilifikiri kwamba Betheli si mahali panapowafaa watoto, lilikubali ombi la Adryana wakati baba yake alipokubali chaguo lake.

Akiwa pamoja na dada, mama, na rafiki yake mmoja, Adryana alisafiri kwenda New York ili kutembelea Betheli kwa mara ya kwanza. Adryana alisema hivi: “Yehova alinijibu. Nilijua kwamba angetukaribisha Betheli. Niliona jinsi vitabu, magazeti, na Biblia zinavyotengenezwa. Betheli ni bora kuliko mahali pa burudani.”

Adryana ‘aliuona uzuri wa Yehova’ na kutazama kwa uthamini jinsi kazi inavyofanywa kwenye makao makuu ya watu wa Yehova leo. Wewe pia unakaribishwa kutembelea Betheli. Zaidi ya makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova huko New York, kuna ofisi za tawi katika sehemu nyingine za ulimwengu.