Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu wa Leo Wenye Ukatili

Ulimwengu wa Leo Wenye Ukatili

Ulimwengu wa Leo Wenye Ukatili

MARÍA alikuwa na umri wa miaka 64, naye aliishi peke yake. Alipatikana akiwa amekufa nyumbani mwake, akiwa amepigwa na kunyongwa kwa waya.

Umati wenye hasira uliwapiga polisi watatu, ukidai kwamba waliwateka nyara watoto wawili. Umati huo uliwamwagia petroli polisi wawili kati yao na kuwasha moto, nao wakaungua kabisa. Yule polisi wa tatu alifaulu kukimbia.

Mtu fulani asiyejulikana alipiga simu ili kuripoti jambo fulani lenye kushtua. Mabaki ya miili ya wanaume wanne watalii ilifukuliwa katika bustani moja. Walikuwa wamefungwa vitambaa machoni, na mikono yao ilikuwa imefungwa. Uchunguzi wa miili yao ulionyesha kwamba walizikwa wakiwa hai.

Matendo hayo ya ukatili si tamasha za kikatili na jeuri zinazoonyeshwa katika sinema za kutisha. Visa hivyo vyote ni vya kweli kabisa na viliripotiwa hivi karibuni na magazeti katika nchi moja ya Amerika Kusini. Hata hivyo, visa kama hivyo havitukii leo katika nchi hiyo peke yake.

Matendo ya ukatili yamekuwa mambo ya kawaida. Ulipuaji wa mabomu, mashambulizi ya kigaidi, mauaji, uvamizi, kupiga watu risasi, na kulala wanawake kinguvu ni machache tu kati ya matendo mengi ya ukatili. Tena na tena, vyombo vya habari vinaripoti visa vyenye kuchukiza sana vya ukatili, na watu wengi hawashtuki tena kuona au kusikia visa vya ukatili kama hivyo.

Huenda ukauliza: ‘Ulimwengu unapatwa na nini leo? Je, watu wameacha kujali hisia za wengine na kuheshimu uhai?’ Kwa nini tunaishi katika ulimwengu kama huu?

Sasa fikiria kisa cha Harry, mwanamume mwenye umri wa miaka 69 ambaye ana ugonjwa wa kansa. Mke wake ana ugonjwa wa neva, lakini majirani na marafiki wake wanajitolea kumsaidia. Harry anasema hivi: “Sijui tungefanya nini kama watu hawa wote hawangetusaidia.” Huko Kanada, ambako anaishi, uchunguzi unaonyesha kwamba zaidi ya asilimia 50 ya watu ambao wanawatunza wazee wanasaidia watu ambao si wa familia zao. Bila shaka, unajua watu fulani wa kawaida ambao siku baada ya siku wanaonyesha fadhili na ujirani. Ndiyo, wanadamu wana uwezo wa kuonyesha huruma na fadhili badala ya kuwa wakatili.

Ikiwa ndivyo ilivyo, kwa nini kuna matendo mengi ya ukatili? Ni nini kinachowafanya watu watende kikatili? Je, wale wanaowatendea wengine kikatili wanaweza kubadilika? Je, kweli ukatili utakwisha? Na ikiwa ndivyo, utakwisha jinsi gani na wakati gani?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

Train: CORDON PRESS