Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitihada Zetu za Kutafuta Hazina Zilituletea Utajiri wa Kudumu

Jitihada Zetu za Kutafuta Hazina Zilituletea Utajiri wa Kudumu

Simulizi la Maisha

Jitihada Zetu za Kutafuta Hazina Zilituletea Utajiri wa Kudumu

Kama lilivyosimuliwa na Dorothea Smith na Dora Ward

Tulikuwa tukitafuta hazina ya aina gani? Tulikuwa wasichana wawili vijana wenye hamu kubwa ya kushiriki kutimiza amri hii ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19) Acheni tueleze jinsi jitihada hizo zilivyotuletea utajiri wa kudumu.

DOROTHEA: Katika mwaka wa 1915, mara tu baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kuanza, nilizaliwa nikiwa mtoto wa tatu katika familia yetu. Tuliishi karibu Howell, Michigan, huko Marekani. Baba yangu hakupendezwa sana na mambo ya kidini, lakini mama yangu alikuwa mwanamke aliyemwogopa Mungu. Mama alijitahidi kutufundisha kufuata zile Amri Kumi, lakini alikuwa na wasiwasi kwa sababu mimi, ndugu yangu, Willis; na dada yangu, Viola; hatukuwa washiriki wa kanisa lolote.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, Mama aliamua kwamba ninapaswa kubatizwa ili niwe mshiriki wa Kanisa la Presbiteri. Ninakumbuka vizuri sana siku niliyobatizwa. Nilibatizwa wakati mmoja na watoto wawili wachanga, kila mmoja wao akiwa amebebwa na mama yake. Niliaibika sana kubatizwa pamoja na watoto wachanga. Kasisi alininyunyizia matone machache ya maji kichwani na kusema kwa sauti ya chini maneno fulani ambayo sikuyaelewa. Kwa kweli, nilikuwa kama watoto hao ambao hawakujua chochote kuhusu ubatizo!

Siku moja mwaka wa 1932, gari fulani lilifika nyumbani kwetu, na mama akaja mlangoni. Vijana wawili walisimama mlangoni na kumwonyesha vitabu vya kidini. Mmoja wao alisema anaitwa Albert Schroeder. Alimwonyesha Mama vitabu fulani vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Mama yangu alichukua vitabu hivyo. Vitabu hivyo vilimsaidia kukubali kweli ya Neno la Mungu.

Ninaanza Kutafuta Hazina

Mwishowe, nilienda kuishi na dada yangu huko Detroit. Nikiwa huko nilikutana na mwanamke fulani mzee ambaye alikuwa akimtembelea dada yangu na kumfundisha Biblia. Mazungumzo hayo yalinikumbusha kipindi fulani cha redio cha kila juma ambacho nilisikiliza nilipokuwa nyumbani pamoja na mama yangu. Kipindi hicho kilitia ndani hotuba ya dakika 15 iliyotegemea habari fulani ya Biblia iliyotolewa na J. F. Rutherford, ambaye alikuwa msimamizi wa Mashahidi wa Yehova wakati huo. Mwaka wa 1937, tulianza kushirikiana na kutaniko la kwanza la Mashahidi wa Yehova huko Detroit. Nilibatizwa mwaka uliofuata.

Mapema katika miaka ya 1940, ilitangazwa kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakianzisha shule ya kuwazoeza wamishonari iliyoitwa Gileadi huko South Lansing, New York. Nilipopata habari kwamba huenda wahitimu fulani wa shule hiyo wakatumwa katika nchi nyingine ili watumike huko, nilijiambia hivi, ‘Ningependa kwenda Gileadi!’ Nilijiwekea mradi wa kuhudhuria shule ya Gileadi. Ningekuwa na pendeleo kubwa kama nini la kutafuta “hazina” katika nchi nyingine, yaani, kuwatafuta watu wanaotaka sana kuwa wanafunzi wa Kristo Yesu!—Hagai 2:6, 7.

Kufikia Mradi Wangu Hatua kwa Hatua

Mnamo Aprili (Mwezi wa 4) 1942, nilijiuzulu kazi yangu na nikawa painia, au mweneza-injili wa wakati wote, huko Findlay, Ohio, pamoja na kikundi cha dada watano Mashahidi. Hakukuwa na kutaniko lililofanya mikutano kwa ukawaida, lakini tulitiana moyo kwa kusoma tukiwa kikundi makala mbalimbali kutoka katika vichapo vya Kikristo. Katika mwezi wangu wa kwanza wa upainia, niliwaachia watu waliopendezwa vitabu 95! Karibu mwaka mmoja na nusu baadaye, nilipokea mgawo wa kuwa painia wa pekee huko Chambersburg, Pennsylvania. Huko, niliungana na kikundi cha mapainia wengine watano, kutia ndani Dora Ward, dada Mkristo kutoka Iowa. Dora alikuwa mwenzi wangu katika upainia. Tulibatizwa mwaka uleule, na tulikuwa na tamaa ya kuhudhuria Shule ya Gileadi na kutumika katika nchi nyingine tukiwa wamishonari.

Mwanzoni mwa mwaka wa 1944, siku muhimu ilifika! Sote wawili tulipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la nne la Gileadi. Tulijiandikisha Agosti (Mwezi wa 8) mwaka huo. Lakini kabla sijaendelea, hebu Dora awaambie jinsi alivyopata kuwa mwenzi wangu wa muda mrefu katika kazi ya kutafuta hazina.

Hamu ya Kuanza Kazi ya Wakati Wote ya Kuhubiri

DORA: Mama yangu alisali ili aelewe Neno la Mungu. Jumapili moja (Siku ya Yenga), nilikuwa pamoja naye wakati tuliposikia hotuba ikitolewa na J. F. Rutherford katika redio. Hotuba ilipokwisha, Mama alisema hivi kwa mshangao, “Huu ndio ukweli!” Muda mfupi baadaye, tulianza kujifunza vichapo vya Mashahidi wa Yehova. Mwaka wa 1935, nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilisikiliza hotuba ya ubatizo iliyotolewa na Shahidi mmoja wa Yehova, nami nikatamani sana kuweka maisha yangu wakfu kwa Yehova. Baada ya miaka mitatu, nilibatizwa. Kujiweka wakfu na kubatizwa kulinisaidia kubaki imara na kukazia fikira miradi yangu katika miaka ya mwisho shuleni. Nilitaka sana kumaliza masomo ili niweze kuanza kutumika nikiwa painia.

Wakati huo, kikundi cha Mashahidi ambao tulishirikiana nao kilikuwa kikikutana kama kutaniko huko Fort Dodge, Iowa. Jitihada nyingi zilihitajiwa ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Zamani hizo, makala za mafunzo ya Mnara wa Mlinzi hazikuwa na maswali ya kutumiwa katika mazungumzo kutanikoni. Kila mhubiri aliombwa ampe ndugu aliyeongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi maswali yaliyotayarishwa. Kila Jumatatu usiku (Siku ya 1), mimi na mama tulitayarisha swali la kila fungu, kisha tukampa kiongozi maswali hayo ili achague maswali ambayo angetumia.

Mara kwa mara, kutaniko letu lilitembelewa na mwangalizi anayesafiri. Mmoja wa ndugu hao, John Booth, alinifundisha kuhubiri nyumba kwa nyumba nilipokuwa na miaka 12. Nikiwa na miaka 17, nilimwomba anionyeshe jinsi ya kujaza fomu ya ombi la utumishi wa upainia, naye akanisaidia. Sikujua kamwe kwamba ningekutana naye tena maishani na kwamba angekuwa rafiki wa muda mrefu!

Nikiwa painia, mara nyingi nilihubiri pamoja na Dada Dorothy Aronson, mweneza-injili wa wakati wote ambaye alikuwa amenizidi umri kwa miaka 15. Tulifanya upainia pamoja mpaka alipoalikwa kuhudhuria darasa la kwanza la Gileadi mwaka wa 1943. Baadaye, niliendelea kufanya upainia nikiwa peke yangu.

Wapinzani Wanashindwa Kutuzuia

Tulikabili hali ngumu sana katika miaka ya 1940 kwa sababu ya roho ya uzalendo iliyochochewa na Vita vya Pili vya Ulimwengu. Tulipohubiri nyumba kwa nyumba, mara nyingi tulitupiwa mayai yaliyooza, nyanya zilizoiva, na nyakati nyingi hata mawe! Tulipata jaribu kali zaidi tulipotoa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Consolation (sasa ni Amkeni!) tukiwa pembeni mwa barabara. Wakichochewa na wapinzani wa kidini, polisi walitufikia na kututisha kwamba wangetukamata ikiwa tungeonekana tukihubiri hadharani tena.

Bila shaka, tulikataa kuacha kutoa ushahidi, na tukapelekwa katika kituo cha polisi ili kuhojiwa. Baada ya kuachiliwa huru, tulirudi kwenye pembe ileile ya barabara na kutoa magazeti yaleyale. Tulitumia andiko la Isaya 61:1, 2 kujitetea kama ndugu wenye mapendeleo walivyotushauri tufanye. Pindi moja nilipofikiwa na askari mmoja kijana, nilisema kwa sauti andiko hilo mbele yake nikiwa na wasiwasi. Inashangaza kwamba aligeuka ghafula na kwenda zake! Niliona kwamba malaika walikuwa wakitulinda.

Siku Isiyosahaulika

Mwaka wa 1941, nilifurahi kuhudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la siku tano huko St. Louis, Missouri. Katika kusanyiko hilo, Ndugu Rutherford aliwaomba watoto wote wenye umri wa kati ya miaka 5 na 18 wakusanyike katika sehemu kuu ya uwanja. Maelfu ya watoto walikusanyika hapo. Ndugu Rutherford alitusalimu kwa kupeperusha kitambaa chake cha mkononi. Sote tulimpungia mikono. Baada ya kutoa hotuba kwa saa moja, alisema: “Watoto ambao wamekubali kufanya mapenzi ya Mungu na wamechukua msimamo upande wa serikali ya kitheokrasi ya Kristo Yesu na hivyo wamekubali kumtii Mungu na Mfalme wake, tafadhali simameni.” Watoto wote 15,000 walisimama pamoja. Nilikuwa kati yao! Msemaji akaongezea hivi: “Ninyi nyote ambao mtafanya yote mnayoweza ili kuwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu na baraka zake, tafadhali semeni Ndiyo.” Tulisema ndiyo, kisha makofi yakapigwa kwa kishindo.

Kisha kitabu Children * kikatolewa, na msururu mrefu wa watoto ulipitia mbele ya jukwaa huku Ndugu Rutherford akimpa kila mmoja wetu nakala ya kitabu hicho kipya. Ilisisimua sana! Leo, idadi kubwa ya wale waliopokea kitabu hicho siku hiyo bado wanamtumikia Yehova kwa bidii ulimwenguni pote, wakitangaza Ufalme wa Mungu na uadilifu wake.—Zaburi 148:12, 13.

Baada ya kufanya upainia kwa miaka mitatu, nilifurahi kama nini kutumwa nikiwa painia wa pekee huko Chambersburg! Huko, nilikutana na Dorothea, na muda si muda tukawa marafiki wakubwa sana. Tulikuwa vijana wenye uchangamfu sana na wenye nguvu nyingi. Tulitaka sana kupanua utumishi wetu katika kazi ya kuhubiri. Tulianza pamoja kutafuta hazina, na tumefanya hivyo maisha yetu yote.—Zaburi 110:3.

Miezi michache baada ya kuanza kutumika tukiwa mapainia wa pekee, tulikutana na mhitimu wa darasa la kwanza la Gileadi, Albert Mann. Alikuwa akijitayarisha kwenda katika mgawo wake katika nchi nyingine. Alitutia moyo kukubali mgawo wowote ambao huenda tungepewa katika nchi nyingine.

Tunahudhuria Shule Pamoja

DORA NA DOROTHEA: Wazia shangwe tuliyokuwa nayo tulipoanza mazoezi yetu ya umishonari! Siku ya kwanza, tuliandikishwa katika shule na Albert Schroeder, ndugu ambaye alikuwa amemwachia mama ya Dorothea kitabu Studies in the Scriptures miaka 12 iliyopita. John Booth alikuwapo pia. Sasa alikuwa msimamizi wa Kingdom Farm, mahali ambapo shule ilikuwa. Baadaye, ndugu hao wawili walitumika wakiwa washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

Katika Shule ya Gileadi, tulijifunza kweli za ndani za Biblia. Yalikuwa mazoezi bora sana. Darasa letu lilikuwa na wanafunzi 104, kutia ndani mwanafunzi wa kwanza asiye Mwamerika. Alitoka Mexico. Alikuwa akijitahidi kuboresha Kiingereza chake nasi tulikuwa tukijitahidi kujifunza Kihispania. Tulisisimuka kama nini siku ambayo Ndugu Nathan H. Knorr alitupatia sisi wanafunzi migawo ya kwenda nchi nyingine! Wengi walitumwa Amerika ya Kati na ya Kusini; mgawo wetu ulikuwa Chile.

Kutafuta Hazina Nchini Chile

Ili kuingia Chile, ilikuwa lazima kwetu kuchukua viza, na muda mrefu ulihitajiwa ili kuipata. Hivyo, baada ya kuhitimu mnamo Januari (Mwezi wa 1), 1945, tulifanya upainia huko Washington, D.C., kwa mwaka mmoja na nusu. Tulipopata viza zetu, tulifunga safari ya kwenda Chile tukiwa wamishonari tisa. Wamishonari saba kati yetu walikuwa wamehudhuria madarasa yaliyotangulia ya Gileadi.

Ndugu kadhaa Wakristo walikuja kutukaribisha tulipofika Santiago, mji mkuu wa Chile. Mmoja wao alikuwa Albert Mann, mhitimu wa Gileadi ambaye alitutia moyo miaka michache mapema. Alikuwa amekuja Chile mwaka uliotangulia, pamoja na Joseph Ferrari wa darasa la pili la Gileadi. Tulipofika nchini Chile idadi ya wahubiri haikuzidi 100. Tulikuwa na hamu kubwa ya kutafuta hazina zaidi, yaani, watu wanyoofu, katika mgawo wetu mpya.

Tulipewa mgawo wa kutumika katika nyumba ya wamishonari huko Santiago. Ilikuwa mara ya kwanza kwetu kuishi na familia kubwa ya wamishonari. Zaidi ya kuhubiri kwa saa fulani hususa, wamishonari wote walikuwa na zamu ya kupikia familia mara moja kila juma. Pindi fulani tulifanya mambo yaliyotuletea aibu. Wakati mmoja, tulioka biskuti moto ambazo familia yetu yenye njaa ingekula wakati wa kiamsha-kinywa, lakini tulipotoa biskuti hizo ndani ya meko, tulipigwa na harufu fulani isiyopendeza. Kumbe tulitumia magadi badala ya hamira! Mtu fulani alitia magadi ndani ya mkebe wa hamira.

Hata hivyo, makosa tuliyofanya tulipokuwa tukijifunza Kihispania yalituletea aibu kubwa zaidi. Familia moja kubwa ambayo tulikuwa tukijifunza Biblia pamoja nayo karibu iache kujifunza kwa sababu haikuelewa tulichokuwa tukisema. Bado walijifunza kweli kwa kusoma maandiko katika Biblia zao wenyewe, na watu watano wa familia hiyo wakawa Mashahidi. Katika miaka hiyo, hakukuwa na programu ya kuwafundisha wamishonari wapya lugha. Tulianza kuhubiri mara moja na kujaribu kujifunza lugha kupitia watu tuliokuwa tukiwahubiria.

Tuliongoza mafunzo mengi ya Biblia, na wengine kati ya wanafunzi wetu walifanya maendeleo haraka. Tulihitaji kuwavumilia sana wanafunzi wengine. Teresa Tello, mwanamke fulani kijana, alisikiliza ujumbe wa kweli, naye akasema, “Tafadhali, mrudi tena ili mniambie mengi.” Tulirudi mara 12 lakini hatukumpata. Miaka mitatu ilipita. Kisha tukahudhuria kusanyiko ambalo lilifanywa katika ukumbi fulani huko Santiago. Tulipokuwa tukiondoka kusanyikoni Jumapili, tulisikia mtu akiita, “Senorita Dora, Senorita Dora!” Tuligeuka, tukamwona Teresa. Alikuwa amemtembelea dada yake aliyeishi ng’ambo ya barabara, basi alikuja kwenye kusanyiko kuona kilichokuwa kikiendelea. Tulifurahi kama nini kukutana naye tena! Tulifanya mipango ya kujifunza Biblia, na baada ya muda mfupi alibatizwa. Baadaye, akawa painia wa pekee. Leo, baada ya miaka 45 kupita, Teresa angali anaendelea na utumishi wa pekee wa wakati wote.—Mhubiri 11:1.

Kupata Hazina Katika “Mchanga”

Mwaka wa 1959, tulipewa mgawo wa kwenda Punta Arenas, jina linalomaanisha “Eneo Lenye Mchanga.” Eneo hilo liko kusini kabisa ya pwani ya Chile yenye umbali wa kilomita 4,300. Punta Arenas ni eneo lisilo la kawaida. Wakati wa kiangazi, siku zinakuwa ndefu na giza linaingia baada ya saa 5:30 usiku. Tuliweza kushiriki katika huduma kwa siku nyingi lakini si bila matatizo, kwa kuwa wakati wa kiangazi kunakuwa na upepo mkali sana kutoka Antaktiki. Miezi fulani ina baridi kali sana, na siku ni fupi.

Hata ingawa kuna hali hizo ngumu, eneo la Punta Arenas lina mambo fulani yanayovutia. Wakati wa kiangazi, mawingu makubwa ya mvua yanaenea katika anga la magharibi. Mara kwa mara mvua inakunyeshea, lakini upepo unavuma na kukukausha. Upinde maridadi wa mvua unaonekana wakati miale ya jua inapopenya mawingu hayo. Nyakati nyingine, pinde hizo za mvua zinakaa kwa saa nyingi, na zinatokea na kupotea miale ya jua inapoonekana kupitia mawingu ya mvua.—Ayubu 37:14.

Wakati huo, kulikuwa na wahubiri wachache huko Punta Arenas. Sisi akina dada tulilazimika kuongoza mikutano katika kutaniko dogo la huko. Yehova alibariki jitihada zetu. Miaka 37 baadaye, tulirudi kutembelea eneo hilo. Tulipata nini? Makutaniko sita makubwa na Majumba matatu maridadi ya Ufalme. Yehova alitufanya tuwe na shangwe kubwa kama nini kwa kutuwezesha kupata hazina za kiroho katika maeneo hayo ya kusini yenye mchanga!—Zekaria 4:10.

Hazina Zaidi Katika “Ufuo Mpana”

Baada ya kutumika kwa miaka mitatu na nusu huko Punta Arenas, tulipewa mgawo wa kwenda kutumika katika mji wenye bandari wa Valparaiso. Mji huo una vilima 41 kuzunguka ghuba inayoelekeana na Bahari ya Pasifiki. Tulihubiri hasa katika kilima kimoja, Playa Ancha, jina linalomaanisha “Ufuo Mpana.” Katika muda wa miaka 16 tuliyokaa huko, tuliona kikundi cha ndugu vijana Wakristo wakikua kiroho hivi kwamba sasa wanatumika wakiwa waangalizi wanaosafiri na wazee Wakristo katika makutaniko mbalimbali nchini Chile.

Mgawo wetu uliofuata wa umishonari ulikuwa Viña del Mar. Tulitumika huko kwa miaka mitatu na nusu mpaka tetemeko la nchi lilipoharibu nyumba yetu ya wamishonari. Tulirudi Santiago, ambako tulianza utumishi wetu wa umishonari miaka 40 iliyopita. Mambo yalikuwa yamebadilika. Majengo mapya ya ofisi ya tawi yalikuwa yamejengwa, na majengo ya zamani ya ofisi yakawa makao ya wamishonari wote waliobaki nchini. Baadaye, makao hayo yalianza kutumiwa kwa ajili ya Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Wakati huo, tulionyeshwa tena fadhili zenye upendo za Yehova. Wamishonari watano kati yetu ambao walikuwa na umri mkubwa walialikwa kuishi Betheli. Wakati ambao tumetumika nchini Chile, tumepata migawo 15. Tumeona kazi ikikua kutoka wahubiri wasiozidi 100 kufikia wahubiri 70,000! Tumekuwa na shangwe kubwa kama nini kutafuta hazina nchini Chile kwa miaka 57!

Tunahisi tumebarikiwa sana kwa sababu Yehova ameturuhusu kupata hazina ya kweli, yaani, watu wengi sana ambao Yehova ameendelea kuwatumia katika tengenezo lake. Katika miaka zaidi ya 60 ambayo tumetumikia Yehova pamoja, tunakubaliana kwa moyo wote na maneno haya yaliyoandikwa na Mfalme Daudi: “Jinsi ulivyo mwingi wema wako, ambao umewawekea hazina wale wanaokuogopa!”—Zaburi 31:19.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 24 Kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Dorothea, mwaka wa 2002 na katika kazi ya kuhubiri mwaka wa 1943

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nikihubiri barabarani huko Fort Dodge, Iowa, mwaka wa 1942

[Picha katika ukurasa wa 10]

Dora, 2002

[Picha katika ukurasa wa 12]

Dorothea na Dora nje ya nyumba yao ya kwanza ya wamishonari nchini Chile, mwaka wa 1946