Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ufufuo Ni Halisi Kwako?

Je, Ufufuo Ni Halisi Kwako?

Je, Ufufuo Ni Halisi Kwako?

“Kutakuwa na ufufuo.” —MATENDO 24:15.

1. Kwa nini inaonekana kwamba kifo ni jambo tusiloweza kuepuka?

“HAKUNA jambo lolote lililo hakika katika ulimwengu huu ila kifo na kodi.” Maneno hayo yaliyoandikwa mwaka wa 1789 na kiongozi wa Marekani Benjamin Franklin, yameonwa na watu wengine kuwa maneno yenye busara. Hata hivyo, watu wengi wasio wanyoofu wanadanganya na hawalipi kodi zao. Inaonekana kifo ni jambo ambalo hatuwezi kuepuka hata kidogo. Pasipo msaada, hakuna hata mmoja wetu anayeweza kuepuka kifo. Kifo kinatufuata sisi sote. Kaburi, ambalo halishibi, linawameza wapendwa wetu. (Methali 27:20) Lakini fikiria wazo hili lenye kufariji.

2, 3. (a) Kwa nini watu wengi leo hawajui kwamba kuna watu ambao hawatakufa kamwe? (b) Tutazungumzia mambo gani katika habari hii?

2 Neno la Yehova linatupa tumaini hakika la ufufuo, yaani, kuamshwa ili kuishi tena. Tumaini hilo si ndoto tu, na hakuna nguvu zozote katika ulimwengu ambazo zinaweza kumzuia Yehova kufanya tumaini hilo liwe hakika. Hata hivyo, watu wengi leo hawajui kwamba kuna watu ambao hawatakufa kamwe. Kwa nini hawatakufa kamwe? Kwa sababu “umati mkubwa” ambao hauna hesabu utaokoka “dhiki kuu,” inayokaribia sana. (Ufunuo 7:9, 10, 14) Baada ya kuokoka wataendelea kuishi wakiwa na tarajio la uzima wa milele. Hivyo, hawatakufa kamwe. Zaidi ya hayo, ‘kifo kitaangamizwa.’—1 Wakorintho 15:26.

3 Tunapaswa kuwa na uhakika juu ya ufufuo kama mtume Paulo aliyesema hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Acheni tuchunguze maswali matatu kuhusu ufufuo. Kwanza, ni nini kinachofanya tumaini hilo liwe hakika? Pili, wewe binafsi unaweza kupata faraja gani kutokana na tumaini la ufufuo? Tatu, tumaini hilo linaweza kuwa na uvutano gani juu ya maisha yako sasa?

Ufufuo Ni Jambo Hakika

4. Ufufuo ni wa maana jinsi gani katika kusudi la Yehova?

4 Kuna mambo fulani yanayofanya ufufuo uwe jambo hakika. Kwanza, ni muhimu kwa kusudi la Yehova. Kumbuka, Shetani aliwaingiza wanadamu katika dhambi, kutia ndani matokeo yake yasiyoepukika, yaani, kifo. Hivyo, Yesu alisema hivi kumhusu Shetani: “Huyo alikuwa muuaji alipoanza.” (Yohana 8:44) Lakini Yehova aliahidi kwamba “mwanamke” wake, yaani, tengenezo lililo kama mke huko mbinguni lingetokeza “uzao” ambao ungemponda kichwa na kumharibu kabisa Shetani, yule “nyoka wa zamani.” (Mwanzo 3:1-6, 15; Ufunuo 12:9, 10; 20:10) Kadiri Yehova alivyofunua hatua kwa hatua kusudi lake kuhusiana na Uzao wa Kimasihi, ilikuwa wazi kwamba Uzao huo ungefanya mengi zaidi ya kumharibu Shetani. Neno la Mungu linasema: “Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alifunuliwa, yaani, ili azivunje kazi za Ibilisi.” (1 Yohana 3:8) Kifo ambacho kinatokana na dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu ni mojawapo ya kazi kuu za Shetani ambazo Yehova anakusudia kuziharibu au kuzivunja kupitia Yesu Kristo. Kuhusiana na hilo, dhabihu ya fidia ya Yesu na ufufuo wake ni mambo ya maana sana.—Matendo 2:22-24; Waroma 6:23.

5. Kwa nini ufufuo utatukuza jina la Yehova?

5 Yehova ameazimia kulitukuza jina lake takatifu. Shetani amechafua jina la Mungu na kueneza uwongo. Alidanganya kwamba Adamu na Hawa ‘hakika hawangekufa’ ikiwa wangekula matunda waliyokatazwa na Mungu. (Mwanzo 2:16, 17; 3:4) Tangu wakati huo, Shetani amekuwa akieneza uwongo kama huo, kama vile fundisho la uwongo la kwamba nafsi inaendelea kuishi mwili unapokufa. Hata hivyo, kupitia ufufuo, Yehova atafunua kabisa uwongo huo wote. Atathibitisha kabisa kwamba yeye peke yake ndiye Anayelinda na Anayerudisha uhai.

6, 7. Yehova anahisi namna gani kuhusu kuwafufua watu, na tunajua jinsi gani kwamba ana hisia hizo?

6 Yehova anatamani kuwafufua watu. Biblia inaonyesha wazi hisia za Yehova kuhusu jambo hilo. Kwa mfano, fikiria maneno haya ya mwanamume mwaminifu Ayubu yaliyoongozwa na roho: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena? Mimi nitangojea siku zote za kazi yangu ya kulazimishwa, mpaka kitulizo changu kije. Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Maneno hayo yanamaanisha nini?

7 Ayubu alijua kwamba baada ya kufa, angepaswa kungoja kwa kipindi fulani cha wakati akiwa amelala katika kifo. Aliona kipindi hicho kuwa wakati wa ‘kazi ya kulazimishwa,’ kipindi ambacho angelazimishwa kungoja ili aachiliwe huru. Aliona kuachiliwa huko kuwa jambo hakika. Ayubu alitambua kwamba kitulizo chake kingekuja. Kwa nini? Kwa sababu alijua hisia za Yehova. Yehova ‘angetamani sana’ kumwona tena mtumishi wake mwaminifu. Ndiyo, Mungu anatamani sana kuwafufua watu wote waadilifu. Pia, Yehova atawapa wengine nafasi ya kuishi milele katika Paradiso duniani. (Luka 23:43; Yohana 5:28, 29) Kwa kuwa ni mapenzi ya Mungu kutimiza kusudi hilo, ni nani anayeweza kumzuia?

8. Yehova “ametoa uhakikisho kamili” wa tumaini letu la wakati ujao jinsi gani?

8 Ufufuo wa Yesu unatoa uhakikisho kamili wa tumaini letu la wakati ujao. Paulo alipotoa hotuba huko Athene, alitangaza hivi: “[Mungu] ameweka siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” (Matendo 17:31) Watu fulani waliomsikiliza Paulo walimdhihaki alipowaambia kuhusu ufufuo. Hata hivyo, wachache wakawa waamini. Labda walivutiwa na wazo la kwamba uhakikisho kamili umetolewa kuhusu tumaini hilo. Yehova alipomfufua Yesu, Alifanya muujiza mkubwa kuliko yote. Alimfufua Mwana wake kutoka katika kifo kuja kwenye uhai akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu. (1 Petro 3:18) Yesu aliyefufuliwa alikuwa mkuu zaidi kuliko hata jinsi alivyokuwa kabla ya kuwa mwanadamu. Akiwa asiyeweza kufa na wa pili kwa cheo baada ya Yehova, sasa Yesu anaweza kutimiza migawo mizito anayopewa na Baba yake. Yehova anamtumia Yesu kuwafufua watu wengine wote kwenye uhai wa kimbingu au wa kidunia. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yohana 5:25; 11:25) Kwa kumfufua Mwana wake, Yehova aliwatolea waaminifu wote uhakikisho kamili wa matumaini kama hayo.

9. Masimulizi ya Biblia yanaonyesha jinsi gani kwamba ufufuo ni jambo hakika?

9 Ufufuo umefanywa mbele ya mashahidi wa kujionea nao umeandikwa katika Neno la Mungu. Masimulizi ya Biblia yanazungumzia matukio manane ya watu ambao walifufuliwa kwenye uhai wa kibinadamu hapa duniani. Miujiza hiyo haikufanywa kisiri-siri, ilifanywa waziwazi na mara nyingi mbele ya watu. Yesu alimfufua Lazaro aliyekuwa mfu kwa siku nne. Yesu alifanya hivyo mbele ya umati uliokuwa ukiomboleza ambao bila shaka ulitia ndani watu wa familia, marafiki, na majirani. Uthibitisho huo ambao ulionyesha kwamba Yesu alitumwa na Mungu ulikuwa wenye nguvu sana hivi kwamba maadui wa kidini wa Yesu hawakupinga kwamba alimfufua Lazaro. Badala yake, walipanga njama, si ya kumuua Yesu tu, bali pia Lazaro! (Yohana 11:17-44, 53; 12:9-11) Ndiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba ufufuo ni jambo hakika. Mungu ametupa masimulizi ya matukio yaliyopita ya ufufuo ili kutufariji na kujenga imani yetu.

Kufarijiwa na Tumaini la Ufufuo

10. Ni nini kitakachotusaidia kupata faraja kutokana na masimulizi ya Biblia kuhusu ufufuo?

10 Je, unatamani kufarijiwa unapokabili kifo? Chanzo kimoja hakika cha faraja ni masimulizi ya Biblia kuhusu ufufuo. Kusoma, kutafakari, na kufikiria masimulizi hayo kunaweza kufanya tumaini la ufufuo liwe halisi zaidi kwako. (Waroma 15:4) Masimulizi hayo si hadithi tu. Yalitukia kikweli kwa watu halisi kama sisi, walioishi wakati halisi na mahali halisi. Acheni tuzungumzie kwa ufupi mfano mmoja, yaani, ufufuo wa kwanza unaotajwa katika Biblia.

11, 12. (a) Mjane wa Sarefathi alipata msiba gani, naye alifanya nini mwanzoni? (b) Eleza kile ambacho Yehova alimwezesha nabii wake Eliya kumfanyia mjane huyo.

11 Hebu wazia tukio lifuatalo. Kwa majuma machache, nabii Eliya amekuwa mgeni wa mjane mmoja huko Sarefathi. Eliya amekuwa akiishi katika chumba cha juu cha nyumba ya mjane huyo. Ni wakati wa huzuni. Eneo hilo limekumbwa na ukame na njaa kali. Watu wengi wanakufa. Tayari Yehova amemtumia Eliya kufanya muujiza kwa muda mrefu ili kuthawabisha imani ya mjane huyo mnyenyekevu. Mjane huyo na mwana wake mdogo walikuwa karibu kufa kwa njaa, walikuwa wamebaki na chakula cha mwisho wakati Mungu alipomwezesha Eliya kufanya muujiza ili mafuta na unga wa mjane huyo usipungue. Hata hivyo, mjane huyo anapata msiba. Kwa ghafula, mtoto huyo anakuwa mgonjwa naye anakufa. Mjane huyo anafadhaika sana! Tayari ni vigumu kwake kuishi bila msaada na utegemezo wa mume, lakini sasa amefiwa na mwana wake wa pekee. Kwa sababu ya huzuni yake, hata anamlaumu Eliya na Mungu wake, Yehova! Nabii huyo atafanya nini?

12 Eliya hamkemei mjane huyo kwa sababu ya shtaka lake la uwongo. Badala yake, anasema hivi: “Nipe mwana wako.” Eliya anamchukua mtoto huyo aliyekufa na kumpeleka katika chumba cha juu, kisha anasali tena na tena ili uhai wa mtoto huyo urudishwe. Mwishowe, Yehova anatenda! Wazia jinsi uso wa Eliya unavyong’aa kwa shangwe anapoona kifua cha mtoto huyo kikiinuka anapovuta hewa. Macho ya mtoto huyo yanafunguka, nayo yanang’aa kwa uhai. Eliya anamleta mvulana huyo chini kwa mama yake na kusema hivi: “Tazama, mwana wako yuko hai.” Mama huyo ana shangwe isiyoelezeka, naye anasema hivi: “Kwa kweli sasa najua kwamba wewe ni mtu wa Mungu na kwamba neno la Yehova kinywani mwako ni la kweli.” (1 Wafalme 17:8-24) Imani yake katika Yehova na mwakilishi wake inakuwa yenye nguvu hata zaidi.

13. Kwa nini simulizi la Eliya kumfufua mwana wa mjane linatufariji leo?

13 Bila shaka, utapata faraja kubwa ukitafakari kuhusu simulizi kama hilo. Ni wazi kabisa kwamba Yehova anaweza kumshinda adui yetu kifo! Hebu wazia siku ambayo maelfu ya watu duniani watakuwa na shangwe kama ya mjane huyo katika ufufuo wa wafu! Pia, kutakuwa na shangwe kubwa mbinguni kwa kuwa Yehova anapendezwa kumwongoza Mwana wake afufue wafu duniani pote. (Yohana 5:28, 29) Je, umefiwa na mtu fulani unayempenda? Inafurahisha kama nini kujua kwamba Yehova anaweza na atawafufua wafu!

Tumaini Lako na Maisha Yako Sasa

14. Tumaini la ufufuo linaweza kuwa na matokeo gani katika maisha yako?

14 Tumaini la ufufuo linaweza kuwa na matokeo gani katika maisha yako sasa? Tumaini hilo linaweza kukutia nguvu unapopatwa na hali ngumu, matatizo, mateso, au hatari. Shetani anataka uogope kifo sana ili uvunje utimilifu wako kwa sababu ya ahadi fulani ya uwongo ya usalama. Kumbuka kwamba Shetani alimwambia Yehova hivi: “Kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.” (Ayubu 2:4) Aliposema hivyo, Shetani alituchongea sisi sote, kutia ndani wewe. Je, ni kweli kwamba utaacha kumtumikia Mungu ukikabili hatari? Kwa kutafakari tumaini la ufufuo, unaweza kutia nguvu azimio lako la kuendelea kufanya mapenzi ya Baba yako wa mbinguni.

15. Maneno ya Yesu yaliyo katika Mathayo 10:28 yanaweza kutufariji jinsi gani tunapokabili hatari?

15 Yesu alisema: “Msiwaogope wale ambao wanaua mwili lakini hawawezi kuiua nafsi; lakini badala ya hivyo mwogopeni yeye anayeweza kuangamiza vyote viwili nafsi na mwili katika Gehena.” (Mathayo 10:28) Hatuhitaji kumwogopa Shetani au wanadamu wanaomtumikia. Ni kweli kwamba wengine wao wana nguvu za kusababisha madhara, hata kifo. Hata hivyo, jambo baya zaidi ambalo wanaweza kufanya ni la muda tu. Yehova anaweza na ataondoa kabisa madhara ambayo yamewapata watumishi wake waaminifu, na hata atawafufua. Yehova peke yake ndiye tunayestahili kuogopa, kuhofu, na kuheshimu. Yehova peke yake ndiye aliye na uwezo wa kuondoa uhai na matumaini yoyote ya uhai wa wakati ujao, na kuharibu mwili na nafsi katika Gehena. Inafurahisha kwamba Yehova hataki jambo kama hilo likupate. (2 Petro 3:9) Kwa sababu ya tumaini la ufufuo, sisi tukiwa watumishi wa Mungu, tunaweza sikuzote kuwa na uhakika kwamba tuko salama. Tutapata uzima wa milele tukiendelea kuwa waaminifu, na Shetani na watumishi wake hawawezi kamwe kutuzuia kuupata.—Zaburi 118:6; Waebrania 13:6.

16. Mtazamo wetu una matokeo gani juu ya mambo tunayotanguliza?

16 Ikiwa tumaini la ufufuo ni jambo halisi kwetu, linaweza kubadili mtazamo wetu kuhusu maisha. Tunatambua kwamba “tukiishi na tukifa, sisi ni wa Yehova.” (Waroma 14:7, 8) Basi, tunapofikiria mambo ya kutanguliza, tunafuata shauri hili la Paulo: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Watu wengi wako katika hekaheka za kutimiza kila tamaa waliyo nayo, iwe tamaa ya makuu au msukumo wowote wa moyo wao. Kwa kuwa wanaona maisha ni mafupi, ni kana kwamba wanafanya kila wawezalo kufuatia raha, na ikiwa wana namna fulani ya ibada, bila shaka haipatani na ‘mapenzi ya Mungu yaliyo makamilifu.’

17, 18. (a) Neno la Yehova linaonyesha jinsi gani kwamba maisha ya wanadamu ni mafupi, lakini Mungu anatutakia nini? (b) Kwa nini tunachochewa kumsifu Yehova kila siku?

17 Ni kweli kwamba maisha ni mafupi. ‘Lazima yapite upesi, nasi huruka na kwenda zetu,’ labda baada ya miaka 70 au 80 hivi. (Zaburi 90:10) Wanadamu wanatokea na kutoweka kama majani mabichi, kama kivuli kinachopita, kama pumzi. (Zaburi 103:15; 144:3, 4) Lakini Mungu hakukusudia tukue kwa makumi machache ya miaka, tupate hekima na uzoefu, kisha tutumie makumi machache ya miaka inayofuata tukidhoofika, kuwa wagonjwa, na kufa. Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuishi milele. Biblia inatuambia hivi: “Wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao.” (Mhubiri 3:11) Je, Mungu ni mkatili hivi kwamba atuumbe tukiwa na tamaa hiyo kisha akose kuitimiza? Bila shaka hapana, kwa kuwa “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Kupitia ufufuo, atawawezesha wafu wapate uzima wa milele.

18 Kwa sababu ya tumaini la ufufuo, tunaweza kuwa na wakati ujao ulio salama. Hatuhitaji kujitahidi sana kutimiza sasa mambo yote tunayoweza. Hatuhitaji kuutumia “kwa ukamili” ulimwengu huu unaoangamia. (1 Wakorintho 7:29-31; 1 Yohana 2:17) Tofauti na watu wasio na tumaini halisi, sisi tuna zawadi nzuri sana ya kujua kwamba tukiendelea kuwa waaminifu kwa Yehova Mungu, tutamsifu na kufurahia maisha kwa umilele wote. Basi, kwa vyovyote vile, na tumsifu Yehova kila siku, yeye ambaye amefanya tumaini la ufufuo liwe hakika!

Ungetoa Jibu Gani?

• Tunapaswa kuhisi namna gani kuhusu ufufuo?

• Ni mambo gani yanayofanya tumaini la ufufuo liwe jambo hakika?

• Unaweza kupata faraja kwa njia gani kutokana na tumaini la ufufuo?

• Tumaini la ufufuo linaweza kuwa na matokeo gani katika maisha yako?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ayubu alijua kwamba Yehova anatamani kuwafufua waadilifu

[Picha katika ukurasa wa 29]

“Tazama, mwana wako yuko hai”