Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Unaogopa Wakati Ujao?

Je, Wewe Unaogopa Wakati Ujao?

Je, Wewe Unaogopa Wakati Ujao?

KUNA sababu nyingi zinazowafanya watu wawe na woga. Kwa mfano, watu fulani wanaogopa mambo ambayo yataipata dunia wakati ujao. Gazeti moja (Time) la Aprili 3, 2006 (3/4/2006) linasema hivi: “Mambo kama vile mawimbi yenye joto, dhoruba, mafuriko, mioto, barafu nzito sana inayoyeyuka, yote hayo yanaonyesha kwamba hali ya hewa ulimwenguni imebadilika sana.”

Mnamo Mei (Mwezi wa 5) 2002, Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa lilitoa ripoti yenye kichwa “Hali ya Wakati Ujao ya Mazingira Duniani-3.” Ripoti hiyo ilitayarishwa na watu zaidi ya 1,000. Kulingana na ripoti fulani ya habari, ripoti hiyo ilisema hivi: “Sayari yetu iko katika hali hatari kwa kuwa maamuzi mazito yanayofanywa leo kuhusu misitu, bahari, mito, milima, wanyama, na vitu vingine vinavyotegemeza uhai yana uvutano mkubwa juu ya vizazi vya sasa na vile vinavyokuja.”

Hali ya mazingira ulimwenguni leo ni mojawapo ya mambo yanayoogopesha. Watu ulimwenguni pote wanaishi sasa wakiwa na woga wa mashambulizi ya kigaidi. Naibu mkurugenzi wa shirika kuu la usalama nchini Kanada alisema hivi: “Tunakosa usingizi kwa sababu ya kuogopa vitisho ambavyo hatujui vitatekelezwa wakati gani na jinsi gani.” Kwa kweli, hata kuangalia habari za jioni kwenye televisheni kunaogopesha!

Watu wazima wengi ambao ni wafanyakazi wenye bidii wanaogopa kupoteza kazi zao. Kufutwa kazi, kufungwa kwa viwanda, mashindano mahali pa kazi, na kudaiwa mengi na waajiri wa kazi ni mambo yanayoweza kuwafanya watu waogope kupoteza kazi. Vijana wanaogopa kukataliwa na wenzao. Huenda watoto wakaogopa kwamba wazazi wao hawawapendi kwelikweli. Lakini watoto hao wanahisi namna gani kuhusu hali za ulimwengu unaowazunguka? Mama mmoja mwenye wasiwasi anasema hivi: “Watoto na wale wasio na uzoefu, wanaona ulimwengu nje ya nyumbani kwao kuwa kama mahali pakubwa penye kutisha nyakati fulani.” Na wazazi wengi wana wasiwasi kuhusu matokeo ambayo wapendwa wao, na hasa watoto wao watapata kwa sababu ya upotovu wa maadili katika ulimwengu.

Mara nyingi, watu waliozeeka wanaogopa kuanguka kwenye ngazi au kushambuliwa mitaani. Ndiyo, ‘wanaogopa chochote kilicho juu, na kuna vitisho njiani.’ (Mhubiri 12:5) Pia, watu wanaogopa kupatwa na ugonjwa hatari. Ripoti za virusi hatari vya mafua, kansa, na magonjwa yanayoambukiza zinaweza kutufanya tuogope kupata ugonjwa mpya na usio wa kawaida ambao unaweza kutulemaza au kutuua sisi na familia yetu. Kwa kweli, tunapoona watu wenye afya na nguvu wakiwa wagonjwa na kudhoofika, ni kawaida kuwa na wasiwasi kwamba hali kama hiyo inaweza kutupata sisi au wapendwa wetu. Na inahuzunisha kama nini kutazama macho ya mtu aliye mgonjwa na kuona kwamba hana tumaini lolote!

Kwa kuwa tuna sababu nyingi za kuogopa, je, tuna sababu yoyote nzuri ya kuwa na matumaini mazuri ya wakati ujao? Je, kuna chochote kinachoweza kutusaidia kuendelea kuwa na mtazamo mzuri? Habari inayofuata itajibu maswali hayo.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

© Jeroen Oerlemans/Panos Pictures