Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Tumaini Katika Ulimwengu Uliojaa Taabu

Kupata Tumaini Katika Ulimwengu Uliojaa Taabu

Kupata Tumaini Katika Ulimwengu Uliojaa Taabu

“WATU wa kawaida wana uwezo zaidi wa kufanya mema na kutatua matatizo ya kawaida kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya wanadamu.” Aliyekuwa raisi wa Marekani Bill Clinton alisema maneno hayo katika mkutano uliofanywa huko Ottawa, Kanada, mnamo Machi (Mwezi wa 3) 2006. Alisema kwamba roho ya kusaidia imekuwa ikisitawi ulimwenguni pote tangu tsunami ya mwaka wa 2004. Alisema hayo akiwa na matumaini mazuri kwamba sasa ulimwengu una “ushirikiano ambao haujapata kuwapo.”

Je, tunaweza kutarajia misiba ya kiasili iwafanye watu kila mahali washirikiane na kuleta wakati ujao ulio mzuri zaidi? Je, ‘ushirikiano huo ambao haujapata kuwapo’ ni msingi unaotegemeka wa kutumaini wakati ujao wenye amani ya kweli na usalama wa kudumu?

Chanzo cha Tumaini la Kweli

Jitihada za wanadamu kwa muda wa zaidi ya miaka elfu sita zinaonyesha kwamba wanadamu wamewakatisha tamaa wanadamu wenzao. Hivyo, kuna sababu nzuri kwa nini Maandiko yaliyoongozwa na roho yanatushauri hivi: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.” (Zaburi 146:3) Kuweka tumaini letu katika mashirika ya ulimwengu huu, mali zake, na miradi yake kutatukatisha tu tamaa. Kwa nini? Kwa sababu “ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake.”—1 Yohana 2:17.

Hata hivyo, kwa karne nyingi, Mungu amekuwa tumaini lenye kutegemeka la wanadamu waadilifu. Biblia inamwita “tumaini la Israeli [la kale]” na “tumaini la mababu [wa Israeli],” na ina maneno mengi yanayohusiana na tumaini, tegemeo, na uhakika katika yeye. (Yeremia 14:8; 17:13; 50:7) Kwa kweli, Maandiko yanatutia moyo ‘tumtumaini Yehova.’—Zaburi 27:14.

Andiko la Methali 3:5, 6 linatuhimiza hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” Una kila sababu ya kuwa na uhakika kabisa katika ahadi kama hiyo kwa sababu Yehova Mungu habadiliki, ni mwenye kutegemeka, na sikuzote anatimiza neno lake. (Malaki 3:6; Yakobo 1:17) Anakutakia mema, na ikiwa sikuzote utatii yale yaliyo katika Neno lake Biblia, itakuongoza kwa mafanikio katika nyakati hizi zenye kuogopesha.—Isaya 48:17, 18.

Mtu ambaye anafuata kwa moyo wote mwongozo wa Mungu anaweza kutegemea ahadi hii: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” (Isaya 41:10) Kusali kwa bidii na kutafakari kuhusu uhakikisho huo ni jambo linalowafariji sana wale wanaompenda kikweli Yehova Mungu, kwa kuwa linawasaidia kupambana na hali ngumu na mahangaiko.

Mfikirie Andrea, Shahidi wa Yehova ambaye ni mama mwenye watoto wawili. Anasema hivi: “Ninapata nguvu za kupambana na nyakati ngumu katika maisha yangu kwa sababu tu ninasali na kutafakari kuhusu ahadi za Yehova. Nikiendelea kumwona Yehova kuwa mtu asiyebadilika katika maisha yangu, ni rahisi zaidi kubaki imara.”

Tia Nguvu Tumaini Lako Katika Yehova

Akionyesha umuhimu wa kumtumaini Yehova, mtunga-zaburi mmoja alisema hivi: “Wale wanaoipenda sheria yako wana amani nyingi, na hakuna kitu cha kuwakwaza.” (Zaburi 119:165) Kujifunza Neno la Mungu kwa unyoofu kunaweza kukusaidia sana kujaza katika akili na moyo wako mambo ya kiroho yanayojenga, yaani, ‘mambo yaliyo ya kweli, yaliyo ya hangaiko zito, yaliyo ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, yaliyo ya kupendeka, yanayosemwa vema, na yaliyo yenye kustahili sifa.’ Ikiwa unajitahidi sana kusikiliza, kujifunza, kukubali, na kutenda mambo hayo, ‘Mungu wa amani atakuwa pamoja nawe.’—Wafilipi 4:8, 9.

Akizungumza kutokana na mambo ambayo amejionea kwa makumi ya miaka, John anasema hivi: “Ili nibadili maoni yangu kuhusu wakati ujao, ilinibidi kujifunza kwamba nilihitaji kubadili kabisa utu na mawazo yangu ili niweze kujenga uhusiano pamoja na Mungu mkamilifu asiyeonekana. Njia ya pekee ambayo ningeweza kujenga uhusiano huo ni kuwa mtu wa kiroho. Hilo lilihusisha kubadilika na kuwa na maoni kama ya Mungu kwa kusoma na kulitafakari Neno lake lililoongozwa na roho.”

Ukinywa maji ya kweli yenye kuburudisha ya uzima yaliyo katika Maandiko yaliyoongozwa na roho, utakuwa ukitumia njia ya kweli na iliyojaribiwa ya kupambana na mambo mengi mabaya yanayoenezwa kila siku na vyombo vya habari. Kufuata yale yanayosemwa katika Biblia kunaweza pia kutia nguvu uhusiano wa familia yako na kusaidia kupunguza mahangaiko. Zaidi ya hayo, Mungu anaahidi kwamba yuko tayari ‘kuonyesha nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.’ (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Atashughulikia mambo kwa njia ambayo itakufanya uache kabisa kuogopa.

Phinehas, ambaye ameona vita na mauaji ya watu wengi, anasema hivi: “Nimejifunza kuweka maisha yangu katika mikono ya Yehova ambaye anajali. Kufuata kabisa kanuni za Biblia kumenisaidia kuepuka matatizo mengi.” Ukimtegemea kabisa Yehova Mungu, anaweza kukusaidia kushinda tatizo lolote lililo kama ukuta. (Zaburi 18:29) Mtoto mdogo aliye na uhusiano mzuri pamoja na wazazi wake anawatumaini kabisa na kujihisi salama wanapomtunza hata anapokuwa mgonjwa au anapokuwa na tatizo lingine. Wewe pia unaweza kuhisi vivyo hivyo ukijitahidi na kukubali mwaliko wa kumtumaini Yehova.—Zaburi 37:34.

Msingi Hakika wa Tumaini

Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake hivi: “Ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.’” (Mathayo 6:9, 10) Mungu ataonyesha haki yake ya kutawala dunia akiwa mwenye enzi kuu kupitia Ufalme huo wa mbinguni ambao ni serikali iliyo mikononi mwa Yesu Kristo.—Zaburi 2:7-12; Danieli 7:13, 14.

Mambo mengi yanayowaogopesha wanadamu katika kila sehemu ya maisha yao leo yanaonyesha kwamba tunahitaji msaada wa Mungu. Inafurahisha kujua kwamba msaada huo uko karibu! Sasa akiwa Mfalme wa Kimasihi aliyewekwa na Mungu, Yesu Kristo amepewa mamlaka ya kutetea enzi kuu ya Yehova na kulitakasa jina la Mungu. (Mathayo 28:18) Hivi karibuni, utawala wa Ufalme utaelekezwa duniani ili kuondoa kabisa mambo yote yanayowafanya wanadamu waogope na kuhangaika. Andiko la Isaya 9:6 linataja sifa ambazo zinaonyesha kwamba Yesu ni Mtawala anayestahili ambaye anaweza kuondoa mambo yote yanayotuogopesha. Kwa mfano, Yesu anaitwa “Baba wa Milele,” “Mshauri wa Ajabu,” na “Mkuu wa Amani.”

Fikiria maneno “Baba wa Milele” ambayo yanagusa moyo. Akiwa “Baba wa Milele,” Yesu ana uwezo na mamlaka na pia tamaa ya kuwapa wanadamu watiifu tumaini la uzima wa milele duniani kwa msingi wa dhabihu yake ya fidia. Hilo linamaanisha kwamba mwishowe watawekwa huru kutokana na dhambi na kutokamilika ambako walirithi kutoka kwa mwanadamu wa kwanza aliyetenda dhambi, Adamu. (Mathayo 20:28; Waroma 5:12; 6:23) Pia, Kristo atatumia mamlaka yake aliyopewa na Mungu kuwafufua watu wengi waliokufa.—Yohana 11:25, 26.

Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kwamba yeye ni “Mshauri wa Ajabu.” Kwa sababu ya ujuzi wake wa Neno la Mungu na kwa kuwa anajua sana hali ya wanadamu, Yesu alijua jinsi ya kutatua matatizo ya maisha ya kila siku. Tangu alipowekwa kuwa mfalme mbinguni, Kristo anaendelea kuwa “Mshauri wa Ajabu,” akitumiwa na Yehova kutimiza wajibu muhimu sana katika kuwapasha wanadamu habari. Nyakati zote, mashauri ya Yesu yaliyoandikwa katika Biblia ni yenye hekima na hayana kasoro. Kujua na kuamini jambo hilo kunaweza kukusaidia kuishi maisha yasiyo na wasiwasi na woga mwingi.

Pia, andiko la Isaya 9:6 linamtambulisha Yesu kuwa “Mkuu wa Amani.” Akiwa na daraka hilo, hivi karibuni Kristo atatumia nguvu zake kuondoa tofauti zote za kisiasa, kijamii, na kiuchumi. Jinsi gani? Kwa kuwaleta wanadamu chini ya utawala mmoja wenye amani wa Ufalme wa Kimasihi.—Danieli 2:44.

Chini ya utawala wa Ufalme, amani ya kudumu itaenea duniani pote. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika huo? Sababu inaonyeshwa katika Isaya 11:9, ambapo tunasoma hivi: “[Raia wa Ufalme] hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote katika mlima wangu wote mtakatifu; kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Mwishowe, kila mwanadamu duniani atakuwa na ujuzi sahihi juu ya Mungu na atamtii yeye. Je, jambo hilo linachangamsha moyo wako? Ikiwa ndivyo, usichelewe kupata ‘ujuzi juu ya Yehova’ ambao ni wenye thamani.

Unaweza kufaidika kutokana na ujuzi juu Mungu unaojenga imani na kuongoza kwenye uzima kwa kuchunguza yale ambayo Biblia inafundisha hasa kuhusu matukio ya siku zetu na wakati ujao mzuri sana unaoahidiwa katika Biblia. Kwa hiyo, tunakuhimiza ufaidike na mpango wa kujifunza Biblia bila malipo unaotolewa na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu. Hiyo ni njia moja ya kushinda woga na kupata tumaini la kweli katika ulimwengu uliojaa taabu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Kwa Nini Tunapaswa Kuitumainia Serikali ya Ufalme

Yesu Kristo, akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, amepewa mamlaka na haki ya kutawala mbinguni na duniani. (Mathayo 28:18) Atafanya viumbe na mazingira ya dunia yawe tena na usawaziko kamili. Pia, ana uwezo wa kuondoa magonjwa yote. Miujiza ambayo Yesu alifanya alipokuwa duniani ilionyesha kimbele baraka kubwa zaidi ambazo ataleta chini ya utawala wake akiwa Mfalme mkamilifu na mwenye kutegemeka. Ni sifa gani hasa kati ya sifa zinazoorodheshwa hapa chini za Mfalme huyo wa Kimasihi ambazo zinakuvutia?

Mwenye urafiki.Marko 10:13-16.

Mwenye usawaziko na asiye na ubaguzi. Marko 10:35-45.

Mwenye Kutegemeka na asiye na uchoyo. Mathayo 4:5-7; Luka 6:19.

Mwadilifu na mwenye haki.Isaya 11:3-5; Yohana 5:30; 8:16.

Mwenye ufikirio, mwenye kujali, na mnyenyekevu.Yohana 13:3-15.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kusoma Biblia na kutafakari kunaweza kutuchochea tumtumaini Yehova