Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tukutanike Pamoja?

Kwa Nini Tukutanike Pamoja?

Kwa Nini Tukutanike Pamoja?

MUME wa Christine alimwacha ghafula baada ya kuishi naye kwa miaka 20 katika ndoa. Christine alijikuta peke yake na kulazimika kuwalea wana saba na binti mmoja. Umri wa watoto hao ulikuwa kati ya miaka 7 na 18. “Sasa ilinibidi kufanya maamuzi yote mazito nikiwa peke yangu,” anasema. “Nilihisi nimelemewa na daraka hilo na nikatamani kupata utegemezo na mwongozo.” Alipata wapi msaada aliohitaji?

“Mikutano ya Kikristo iliniokoa mimi na familia yangu,” Christine anasema. “Katika mikutano, tulipata utegemezo wa marafiki wetu na mwongozo kutoka kwa Neno la Mungu. Kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kulitusaidia katika kila jambo muhimu la maisha yetu ya familia.”

Katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” ni lazima sisi sote tukabili majaribu mbalimbali. (2 Timotheo 3:1) Kama Christine, huenda ukaiona mikutano ya Mashahidi wa Yehova kuwa msaada mkubwa wa kiroho na sehemu muhimu ya ibada unayomtolea Yehova. Inaelekea sana kwamba mikutano mitano inayofanywa kila juma inakuchochea kumpenda Mungu, inatia nguvu tumaini lako la wakati ujao, na kukupa mwongozo unaotegemea Biblia kuhusu njia ya kukabiliana na majaribu.

Hata hivyo, inakuwa vigumu kwa wengine kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Wanakuwa wachovu sana mwishoni mwa siku, na huenda wazo la kuvaa inavyofaa na kwenda mikutanoni likawalemea. Mpangilio wa kazi unawazuia wengine kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Ili wahudhurie mikutano yote, watalazimika kupata mshahara mdogo au huenda wakapoteza kazi. Huenda wachache wakakosa mikutano kwa sababu wanahisi kwamba aina fulani ya tafrija itawaburudisha kuliko kushirikiana na kutaniko.

Hivyo, tuna sababu gani nzuri za kuhudhuria mikutano ya Kikristo? Unaweza jinsi gani kufanya pindi hizo zikuburudishe? Ili kujibu maswali hayo, acheni tuchunguze mwaliko wa Yesu wenye uchangamfu ulioandikwa katika Mathayo 11:28-30. Alisema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.”

“Njooni Kwangu”

Yesu alisema: “Njooni kwangu.” Njia moja ya kuitikia mwaliko huo ni kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Kuna sababu nzuri ya kuwapo mikutanoni, kwa kuwa Yesu alisema hivi pindi fulani: “Palipo na wawili au watatu wakiwa wamekusanyika pamoja katika jina langu, hapo mimi nipo katikati yao.”—Mathayo 18:20.

Katika karne ya kwanza, Yesu mwenyewe aliwaalika watu mbalimbali wamfuate. Kwa njia hiyo, aliwapa nafasi ya kufurahia ushirika wa karibu pamoja naye. Wengine kati yao walikubali mwaliko huo mara moja. (Mathayo 4:18-22) Wengine waliacha mambo kama vile mambo ya kimwili yawazuie wasikubali mwaliko huo. (Marko 10:21, 22; Luka 9:57-62) Yesu aliwapa wale waliomfuata uhakikisho huu: “Ninyi hamkunichagua mimi, bali mimi niliwachagua.”—Yohana 15:16.

Baada ya kufa na kufufuliwa, Kristo hakuendelea kuwa na wanafunzi wake kihalisi. Lakini alikuwa nao katika maana ya kwamba aliendelea kuongoza kazi yao na kuangalia jinsi walivyoitikia mashauri yake. Kwa mfano, miaka 70 baada ya ufufuo wake, Yesu aliyashauri na kuyatia moyo makutaniko saba ya Asia Ndogo. Maelezo yake yalionyesha kwamba alijua vizuri uwezo na udhaifu wa watu mmoja-mmoja katika makutaniko hayo.—Ufunuo 2:1–3:22.

Bado Yesu anamjali sana kila mmoja wa wanafunzi wake. Anaahidi hivi: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20) Sasa tunaishi katika siku za mwisho, na hivyo tunapaswa kukubali mwaliko wa Yesu wa kumfuata yeye. Kwa kadiri fulani, kufanya hivyo kunamaanisha kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Yesu anataka tumsikilize na ‘tufundishwe kupitia yeye’ kwa njia ya vichapo na hotuba zinazotegemea Biblia ambazo zinatolewa kwa ukawaida kwenye mikutano. (Waefeso 4:20, 21) Je, unaitikia mwaliko huu wa Yesu: “Njooni kwangu”?

“Nyote Mnaotaabika na Kulemewa na Mizigo”

Sababu muhimu ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni kutiwa moyo. (Waebrania 10:24, 25) Bila shaka, wengi wetu ‘wanataabika na kulemewa’ kwa njia mbalimbali. Huenda unalemewa na mahangaiko ya kibinafsi, kama vile matatizo ya afya. Katika mikutano ya Kikristo, unaweza kupata badilishano la kitia-moyo. (Waroma 1:11, 12) Kwa mfano, utasikia majibu yenye kujenga kiroho, utakumbushwa kuhusu tumaini lako linalotegemea Biblia, na kuona imani ya wengine wanaovumilia majaribu. Yote hayo yanaweza kukusaidia kukabiliana na matatizo yako na kuwa na maoni yanayofaa kuyahusu.

Fikiria maelezo haya ya mwanamke mmoja Mkristo aliye na ugonjwa wa kudumu. “Kwa sababu ya ugonjwa wangu ninalazimika kukaa hospitalini kwa muda fulani,” anasema. “Kwenda mikutanoni baada ya kukaa hospitalini kwa muda fulani si rahisi, lakini mahali panaponifaa ni katika mikutano. Uchangamfu na upendo wa akina ndugu na dada unachochea shangwe yangu, na mafundisho na mwongozo ambao Yehova na Yesu wanatoa unanifanya niwe na kusudi maishani.”

“Nira Yangu Ni Laini na Mzigo Wangu Ni Mwepesi”

Ona kwamba katika mistari tunayochanganua, Yesu alisema: “Mjifunze kutoka kwangu.” Kwa kujifunza kutoka kwa Yesu, tunakuwa wanafunzi wake, na tunachukua nira yake wakati tunapojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa. (Mathayo 28:19, 20) Ili tuendelee kuwa wanafunzi wa Yesu ni muhimu tushiriki kwa ukawaida katika mikutano. Kwa nini? Kwa sababu, katika mikutano ya Kikristo tunafundishwa kumhusu Yesu, mafundisho yake, na njia zake.

Kristo anataka tubebe mzigo gani? Ni mzigo uleule ambao yeye anabeba, yaani, pendeleo la kufanya mapenzi ya Mungu. (Yohana 4:34; 15:8) Jitihada inahitajiwa ili kutii amri za Mungu, lakini mzigo huo si mzito sana hivi kwamba hatuwezi kuubeba. Huenda ukaonekana kuwa mzito ikiwa tunajaribu kuubeba kwa nguvu zetu wenyewe. Hata hivyo, tukisali tupewe roho ya Mungu na tukila chakula cha kiroho kinachoandaliwa mikutanoni, tutapata “nguvu zinazopita zile za kawaida” ambazo zinatoka kwa Mungu. (2 Wakorintho 4:7) Kwa kujitayarisha kwa ajili ya mikutano na kushiriki katika mikutano, upendo wetu kwa Yehova unakuwa wenye nguvu hata zaidi. Na tunapochochewa na upendo, amri za Mungu haziwi “mzigo mzito.”—1 Yohana 5:3.

Watu kwa ujumla wana matatizo mbalimbali kama vile matatizo ya kutafuta riziki, ya kiafya, na ya kibinafsi. Hata hivyo, hatutegemei hekima ya wanadamu tunapopambana na matatizo hayo. Mikutano ya kutaniko inatusaidia ‘kuacha kuhangaika,’ kwa kuwa Yehova anatosheleza mahitaji yetu naye anatusaidia kupambana na matatizo. (Mathayo 6:25-33) Bila shaka, mikutano ya Kikristo inaonyesha kwamba Mungu anatupenda.

“Mimi Ni Mwenye Tabia-Pole na Mnyenyekevu Moyoni”

Yesu alikuwa na desturi ya kwenda kwenye masinagogi, mahali ambapo Neno la Mungu lilizungumziwa. Pindi moja alipokuwa hekaluni, Yesu alichukua kitabu cha kukunjwa cha Isaya na kusoma hivi: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema, alinituma kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka na kupata kuona tena kwa vipofu, kuacha waliopondeka waende zao wakiwa wameachiliwa huru, kuhubiri mwaka wa Yehova wenye kukubalika.” (Luka 4:16, 18, 19) Ingekuwa shangwe kama nini kumsikia Yesu akionyesha jinsi maneno hayo yalivyotimia aliposema: “Leo andiko hili ambalo mmesikia sasa hivi limetimizwa”!—Luka 4:21.

Bado Yesu, “mchungaji mkuu” mwenye tabia-pole, anasimamia uchungaji wa kiroho wa wafuasi wake. (1 Petro 5:1-4) Chini ya mwelekezo wake, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameweka rasmi wanaume wawe wachungaji katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. (Mathayo 24:45-47; Tito 1:5-9) Wanaume hao ‘wanalichunga kundi la Mungu’ kwa upole, nao wanaweka mfano mzuri kwa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Unaweza kuonyesha kwamba unawathamini wanaume hao walio “zawadi katika wanadamu,” kwa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Utawatia moyo wengine kwa kuwapo katika mikutano na kwa kushiriki.—Matendo 15:30-33; 20:28; Waefeso 4:8, 11, 12.

“Mtapata Burudisho kwa Ajili ya Nafsi Zenu”

Unapohudhuria mikutano ya Kikristo, unaweza kufanya nini ili pindi hizo ziwe zenye kuburudisha kwelikweli? Njia moja ni kufuata shauri hili la Yesu: ‘Kazia uangalifu jinsi unavyosikiliza.’ (Luka 8:18) Watu ambao kwa kweli walitaka kujifunza walimsikiliza Yesu kwa makini. Walimwomba afafanue mifano aliyotoa na, kwa sababu hiyo, walithawabishwa kwa kupewa uelewaji wenye kina zaidi.—Mathayo 13:10-16.

Unaweza kuwaiga watu hao waliokuwa na njaa ya kiroho kwa kusikiliza kwa makini hotuba zinazotolewa katika mikutano yetu. (Mathayo 5:3, 6) Ili akili zako zisitange-tange, jitahidi kufuata hoja mbalimbali za msemaji. Jiulize maswali kama haya akilini mwako: ‘Ninaweza kutumia habari hii jinsi gani maishani mwangu? Ninaweza kuitumia kwa njia gani kuwasaidia wengine? Ninaweza kueleza jambo hili namna gani?’ Kwa kuongezea, fungua maandiko ambayo msemaji anatumia kuunga mkono mambo makuu. Kadiri unavyosikiliza ndivyo mikutano itakavyokuwa yenye kuburudisha zaidi.

Baada ya mkutano, zungumza pamoja na wengine mambo yaliyozungumziwa mikutanoni. Fikiria habari hiyo na jinsi inavyoweza kutumiwa. Mazungumzo yenye kujenga yanafanya mikutano iwe yenye kuburudisha sana.

Bila shaka, tuna sababu nzuri za kukutanika pamoja. Baada ya kufikiria faida ambazo zimezungumziwa, mbona usijiulize hivi, ‘Ninaitikia namna gani mwaliko wa Yesu: “Njooni kwangu”?’

[Picha katika ukurasa wa 11]

Je, shughuli nyingine zinakuzuia usihudhurie mikutano?