Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mipango Yako Itafanywa Imara”

“Mipango Yako Itafanywa Imara”

“Mipango Yako Itafanywa Imara”

KATIKA wimbo aliotunga, mtunga-zaburi Daudi alisali hivi: “Uumbe moyo safi ndani yangu, Ee Mungu, na kuweka ndani yangu roho mpya, iliyo imara. Unirudishie shangwe ya wokovu wako, nawe unitegemeze kwa roho ya kupenda.” (Zaburi 51:10, 12) Baada ya dhambi yake na Bath-sheba, Daudi aliyetubu alimsihi Yehova Mungu ausafishe moyo wake na kuweka ndani yake roho au mwelekeo wa akilini wa kufanya yaliyo sawa.

Je, kweli Yehova anaumba ndani yetu moyo mpya, na hata kuweka ndani yetu roho mpya ya kupenda? Au moyo safi ni kitu tunachopaswa kujitahidi kupata na kulinda? “Yehova ndiye mchunguzaji wa mioyo,” lakini anajihusisha kwa kadiri gani na mambo yaliyo moyoni mwetu? (Methali 17:3; Yeremia 17:10) Ana uvutano mkubwa kadiri gani juu ya maisha, nia, na matendo yetu?

Mistari ya kwanza tisa ya Methali sura ya 16 inatumia jina la Mungu mara nane, nayo inatuonyesha jinsi tunavyoweza kumwacha Mungu aongoze maisha yetu ili ‘mipango yetu ifanywe imara.’ (Methali 16:3) Mstari wa 10 mpaka wa 15 unazungumzia daraka la mfalme au mtawala.

Ni Nani ‘Anayefanya Mipango ya Moyo’?

“Mipango ya moyo ni ya mtu wa udongo,” inasema Methali 16:1a. Kwa wazi, ni daraka letu kufanya “mipango ya moyo.” Yehova hatayarishi mioyo yetu kimuujiza au kutupa roho ya kupenda. Tunahitaji kujitahidi kupata ujuzi sahihi wa Neno lake, Biblia, kutafakari kuhusu yale tunayojifunza, na kupatanisha mawazo yetu na mawazo yake.—Methali 2:10, 11.

Hata hivyo, ombi la Daudi la kupewa “moyo safi” na “roho mpya,” linaonyesha kwamba alitambua mwelekeo wake wenye dhambi na alihitaji Mungu amsaidie kusafisha moyo wake. Kwa kuwa hatujakamilika, tunaweza kushawishiwa tutende “kazi za mwili.” (Wagalatia 5:19-21) Tunahitaji msaada wa Yehova ili tuweze ‘kuua viungo vya mwili wetu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.’ (Wakolosai 3:5) Ni muhimu sana kwamba tusali ili tusishindwe na vishawishi na kuondoa mioyoni mwetu mielekeo yenye dhambi!

Je, tunaweza kuwasaidia wengine “kupanga” mioyo yao? “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma,” Biblia inasema, “lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Methali 12:18) Ulimi wetu unaponya wakati gani? Wakati tu ‘jibu la ulimi linapotoka kwa Yehova,’ ndipo tunaposema maneno ya kweli yaliyo sahihi kiroho.—Methali 16:1b.

“Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari,” Biblia inasema. (Yeremia 17:9) Moyo wetu wa mfano una mwelekeo wa kujitetea na kujidanganya. Akionya juu ya hatari hiyo, Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alisema: “Njia zote za mwanadamu ni safi machoni pake mwenyewe, lakini Yehova anazipima roho.”Methali 16:2.

Kujipenda wenyewe kunaweza kutufanya tutetee kasoro zetu, tufunike sifa zetu mbaya, na tufumbie macho makosa yetu. Hata hivyo, Yehova hawezi kudanganywa. Yeye anazipima roho. Roho ya mtu ni mwelekeo wake mkuu wa akilini na unahusiana na moyo. Kwa kadiri kubwa, kusitawi kwa roho ya mtu kunategemea utendaji wa moyo wa mfano, ambao unahusisha mambo kama vile mawazo, hisia, na nia ya mtu. “Mchunguzaji wa mioyo” anapima roho, na hukumu zake si zenye upendeleo wala ubaguzi. Ni jambo la hekima kwetu kulinda roho yetu.

‘Mkabidhi Yehova Kazi Zako’

Kufanya mipango kunahusisha kufikiri, jambo linalofanywa na moyo wetu. Kwa kawaida matendo yanafuata mipango. Je, mipango yetu itafaulu? Sulemani anasema: “Mkabidhi Yehova mwenyewe kazi zako nayo mipango yako itafanywa imara.” (Methali 16:3) Kumkabidhi Yehova kazi zetu kunamaanisha kumtumaini, kumtegemea yeye, kujitiisha kwake, kuacha kubeba mzigo wetu na badala yake kumkabidhi Yehova mzigo huo. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Mkabidhi Yehova njia yako, na kumtegemea, naye mwenyewe atatenda.”—Zaburi 37:5.

Hata hivyo, ili mipango yetu ifanywe imara, ni lazima ipatane na Neno la Mungu na ichochewe na nia nzuri. Zaidi ya hilo, tunapaswa kumwomba Yehova atusaidie na kututegemeza kisha tujitahidi tuwezavyo kufuata mashauri ya Biblia. Ni muhimu hasa ‘tumtupie Yehova mzigo wetu’ tunapopatwa na majaribu na matatizo, kwa kuwa ‘atatutegemeza sisi.’ Bila shaka, Yehova “hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”—Zaburi 55:22.

“Yehova Amefanya Kila Kitu kwa Kusudi Lake”

Tutapata matokeo gani mengine tukimkabidhi Yehova kazi zetu? “Yehova amefanya kila kitu kwa kusudi lake,” anasema mfalme Sulemani mwenye hekima. (Methali 16:4a) Muumba wa ulimwengu mzima ni Mungu mwenye kusudi. Tunapomkabidhi kazi zetu, maisha yetu yanajaa utendaji wa maana na wenye kusudi, na ambao si wa ubatili. Na kusudi la Yehova kuelekea dunia na mwanadamu ni la milele. (Waefeso 3:11) Aliifanya dunia na kuiumba ili “ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Zaidi ya hilo, kusudi lake la mwanzoni kuelekea wanadamu hapa duniani litatimizwa. (Mwanzo 1:28) Maisha ya mtu anayejitoa kwa Mungu wa kweli hayatakuwa na mwisho nayo yatakuwa na kusudi milele.

Yehova amemfanya “hata mwovu kwa ajili ya siku ya uovu.” (Methali 16:4b) Yehova hakuwaumba waovu, kwa kuwa “kazi zake ni kamilifu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hata hivyo, amewaacha waovu wawepo na waendelee kuishi mpaka atakapoona inafaa kutekeleza hukumu yake kali. Kwa mfano, Yehova alimwambia Farao wa Misri hivi: “Kwa sababu hii nimekuacha uendelee kuwako, ili kukuonyesha nguvu zangu na ili nifanye jina langu litangazwe katika dunia yote.” (Kutoka 9:16) Yale Mapigo Kumi na kuharibiwa kwa Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu kulionyesha kwa njia isiyoweza kusahauliwa nguvu za Mungu ambazo hazina kifani.

Yehova anaweza pia kuelekeza mambo kwa njia ambayo itawafanya waovu watimize kusudi lake bila kujua. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Ghadhabu ya mwanadamu itakusifu; [Yehova] utajifunga ghadhabu iliyobaki.” (Zaburi 76:10) Yehova anaweza kuacha maadui wake waonyeshe hasira yao kuwaelekea watumishi wake, lakini anaacha wafanye hivyo kwa kadiri tu inayotosha kuwatia nidhamu na kuwazoeza watumishi wake. Mungu anashughulikia jambo lolote linalozidi hilo.

Yehova anawaunga mkono watumishi wake wanyenyekevu, hata hivyo, wenye kiburi na majivuno watapatwa na nini? “Kila mtu mwenye kiburi moyoni ni chukizo kwa Yehova,” anasema mfalme wa Israeli. “Mkono unaweza kuungana na mkono, hata hivyo mtu hatakosa adhabu.” (Methali 16:5) Wale “wenye kiburi moyoni” wanaweza kuungana na kutegemezana, lakini hawataepuka adhabu. Basi, ni hekima kwetu tusitawishe roho ya unyenyekevu hata kama tuna ujuzi au uwezo mwingi kadiri gani au tuna mapendeleo gani ya utumishi.

“Kwa Kumwogopa Yehova”

Tuna mwelekeo wa kukosea kwa kuwa tumezaliwa katika dhambi. (Waroma 3:23; 5:12) Ni nini kitakachotusaidia kuepuka kufanya mipango itakayoongoza kwenye dhambi? Methali 16:6 inasema: “Kosa hufanyiwa upatanisho kwa fadhili zenye upendo na ukweli, na mtu huepuka uovu kwa kumwogopa Yehova.” Ingawa kwa fadhili zake zenye upendo na ukweli Yehova anafanya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu, kumwogopa Yehova kunatuzuia tusitende dhambi. Mbali na kumpenda Mungu na kuthamini fadhili zake zenye upendo, ni muhimu sana tusitawishe woga wa kutompendeza yeye!

Woga wa kimungu unaingia moyoni mwetu tunapoheshimu sana nguvu za ajabu za Mungu. Hebu wazia nguvu zake ambazo zinafunuliwa kupitia uumbaji! Kukumbushwa kuhusu nguvu zinazofunuliwa kupitia kazi za uumbaji za Mungu kulimsaidia mzee wa ukoo, Ayubu, kurekebisha maoni yake. (Ayubu 42:1-6) Je, hatusaidiwi vivyo hivyo kurekebisha maoni yetu tunaposoma na kutafakari masimulizi ya Biblia yanayoonyesha jinsi Yehova alivyoshughulika na watu wake? Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Njooni mwone matendo ya Mungu. Kushughulika kwake na wana wa binadamu kunaogopesha.” (Zaburi 66:5) Fadhili zenye upendo za Yehova hazipaswi kuchezewa. Waisraeli ‘walipoasi na kuihuzunisha roho yake takatifu, Yehova alibadilika akawa adui yao; yeye mwenyewe alipiga vita juu yao.’ (Isaya 63:10) Kwa upande mwingine, “Yehova anapofurahia njia za mtu, huwafanya hata adui zake wawe na amani naye.” (Methali 16:7) Kumwogopa Yehova ni ulinzi mkubwa kama nini!

“Afadhali kuwa na kidogo pamoja na uadilifu kuliko kuwa na wingi pasipo haki,” anasema mfalme huyo mwenye hekima. (Methali 16:8) Methali 15:16 inasema: “Afadhali kuwa na vitu vichache pamoja na kumwogopa Yehova kuliko kuwa na vitu vingi pamoja na mvurugo.” Ili kuendelea kufuatia uadilifu, ni muhimu kumwogopa na kumheshimu Mungu.

“Huenda Moyo wa Mtu wa Udongo Ukaifikiria Njia Yake”

Mwanadamu aliumbwa akiwa na uhuru wa kujiamulia, uwezo wa kuchagua mema au mabaya. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Moyo wetu wa mfano una uwezo wa kuchunguza mambo mbalimbali na kufuatia jambo moja au zaidi. Akionyesha kwamba daraka la kufanya uamuzi ni letu sisi, Sulemani anasema: “Huenda moyo wa mtu wa udongo ukaifikiria njia yake.” Baada ya hilo, “Yehova ndiye huzielekeza hatua zake.” (Methali 16:9) Kwa kuwa Yehova anaweza kuongoza hatua zetu, tunatenda kwa hekima tunapomwomba atusaidie ‘kufanya mipango yetu iwe imara.’

Kama tulivyoona, moyo ni mdanganyifu na unaweza kuwa na mawazo yasiyo ya kweli. Kwa mfano, huenda mtu akafanya dhambi na moyo wake ukaanza kumtetea. Badala ya kuacha mwendo wake wenye dhambi, huenda akasema Mungu ni mwenye upendo, fadhili, rehema, na mwenye kusamehe. Mtu kama huyo amesema moyoni mwake: “Mungu amesahau. Ameuficha uso wake. Hakika hatauona kamwe.” (Zaburi 10:11) Hata hivyo, ni jambo lisilofaa na la hatari kuchezea rehema za Mungu.

“Kitu cha Kupimia cha Haki na Mizani Ni vya Yehova”

Akiachana na moyo na matendo ya mtu wa udongo na kuanza kuzungumza kuhusu mfalme, Sulemani anasema hivi: “Uamuzi ulioongozwa na roho unapaswa kuwa katika midomo ya mfalme; kinywa chake hakipasi kukosa uaminifu katika hukumu.” (Methali 16:10) Bila shaka, hivyo ndivyo itakavyokuwa kumhusu Mfalme Yesu Kristo aliyetawazwa. Utawala wake juu ya dunia utapatana na mapenzi ya Mungu.

Akionyesha ni nini chanzo cha haki na uadilifu, mfalme huyo mwenye hekima anasema: “Kitu cha kupimia cha haki na mizani ni vya Yehova; mawe yote ya mizani ya mfuko ni kazi yake.” (Methali 16:11) Kitu cha kupimia cha haki na mizani imetoka kwa Yehova. Mfalme hana haki ya kuweka viwango hivyo kulingana na mapendezi yake mwenyewe. Yesu alisema hivi alipokuwa duniani: “Mimi siwezi kufanya lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; kama vile ninavyosikia, ndivyo ninavyohukumu; na hukumu ninayotoa ni ya uadilifu, kwa sababu ninatafuta, si mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi yake aliyenituma.” Tunaweza kutazamia haki kamilifu kutoka kwa Mwana ambaye Baba ‘amemkabidhi kazi yote ya kuhukumu.’—Yohana 5:22, 30.

Unaweza kutazamia nini kingine kutoka kwa mfalme anayemwakilisha Yehova? “Kufanya uovu ni chukizo kwa wafalme,” anasema mfalme wa Israeli, “kwa maana kiti cha ufalme hufanywa imara kwa uadilifu.” (Methali 16:12) Ufalme wa Kimasihi unaongozwa na kanuni za uadilifu za Mungu. Hauna mapatano yoyote na “kiti cha ufalme kinachosababisha shida.”—Zaburi 94:20; Yohana 18:36; 1 Yohana 5:19.

Kupata Nia Njema ya Mfalme

Raia wa mfalme mtukufu wanapaswa kutenda kwa njia gani? Sulemani anasema: “Midomo ya uadilifu ni furaha ya mfalme mkuu; naye humpenda mtu anayesema mambo ya unyoofu. Ghadhabu ya mfalme ni kama wajumbe wa kifo, lakini mwenye hekima huigeuza.(Methali 16:13, 14) Waabudu wa Yehova leo wanatii maneno hayo na wanafanya kwa bidii kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Wanajua kwamba kutumia midomo yao kwa njia hiyo kunamletea furaha Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo. Bila shaka, lilikuwa jambo la hekima kuepuka hasira ya mfalme wa kibinadamu mwenye nguvu na kutafuta kibali chake. Ni jambo la hekima hata zaidi kutafuta kibali cha Mfalme wa Kimasihi!

“Katika nuru ya uso wa mfalme kuna uzima,” Sulemani anaendelea, “nayo nia yake njema ni kama wingu la majira ya mvua ya masika.” (Methali 16:15) “Nuru ya uso wa mfalme” inamaanisha kibali cha mfalme, kama vile ‘nuru ya uso wa Yehova’ inavyofananisha kibali cha Yehova. (Zaburi 44:3; 89:15) Kama vile mawingu ya mvua yanavyothibitisha kwamba mvua itanyesha na mazao yatakuwapo, nia njema ya mfalme inathibitisha kwamba kuna mema yanayotarajiwa. Maisha chini ya utawala wa Mfalme wa Kimasihi yatakuwa yenye shangwe, furaha, na ufanisi mkubwa, kama tu ilivyokuwa kwa kadiri ndogo chini ya utawala wa Mfalme Sulemani.—Zaburi 72:1-17.

Tunapongojea Ufalme wa Mungu uanze kuongoza shughuli zote chini ya jua, acheni tumwombe atusaidie kusafisha mioyo yetu. Acheni pia tumtegemee Yehova na kusitawisha woga wa kimungu. Kisha tunaweza kuwa na hakika kabisa kuwa ‘mipango yetu itafanywa imara.’—Methali 16:3.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yehova amemfanya “mwovu kwa ajili ya siku ya uovu” katika maana gani?