Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kuwasaidia Jinsi Gani Watoto Wangu Waelimike Kikweli?

Ninaweza Kuwasaidia Jinsi Gani Watoto Wangu Waelimike Kikweli?

Ninaweza Kuwasaidia Jinsi Gani Watoto Wangu Waelimike Kikweli?

KUMWELIMISHA mtoto kunaweza kufananishwa na kufunga safari ngumu na yenye kusisimua. Ni safari ambayo unafunga pamoja na watoto wako. Unawatia moyo na kuwaongoza kwa upendo, huku ukiwasaidia kufanya maendeleo maishani. Wana mengi sana ya kujifunza!

Ili watoto wafanikiwe na kuwa wenye furaha kikweli, wanapaswa kusitawisha sifa zinazotegemea maadili mema na uhusiano wao pamoja na Mungu, na kujifunza kutofautisha mema na mabaya. Wakimjua na kumpenda Yehova, elimu yao itawafaidi sana na mafundisho watakayopata yatadumu milele. Ukiwa mzazi, unatimiza daraka muhimu kuhusiana na yale ambayo watoto wako wanajifunza, jinsi wanavyoyachanganua, na kuyaelewa.

Kuna matatizo fulani ambayo wazazi watakabili. Watoto wanaweza kuvutiwa kwa urahisi, na wanaweza kujifunza mambo mengi mabaya kutoka kwa watu wengine. Tunaishi katika ulimwengu unaotawaliwa na Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Shetani anapendezwa na elimu ya watoto wako, lakini kwa kusudi tofauti kabisa. Shetani ni mwalimu stadi na mwenye uzoefu mwingi, lakini ni mwalimu mwovu sana. Ingawa anajifanya kuwa “malaika wa nuru,” nuru anayotoa ni yenye kupotosha na inapingana na Neno la Yehova na mapenzi yake. (2 Wakorintho 4:4; 11:14; Yeremia 8:9) Ibilisi na roho wake waovu ni wadanganyifu wenye ustadi ambao wanaendeleza ubinafsi, ukosefu wa unyoofu, na upotovu wa maadili.—1 Timotheo 4:1.

Unaweza kufanya nini ili kuwalinda watoto wako wasipotoshwe? Unaweza kuwafundisha jinsi gani kukubali mambo yaliyo ya kweli na yanayofaa? Hatua muhimu ni kujichunguza wewe mwenyewe. Unahitaji kuweka mfano mzuri. Pia ni muhimu ukubali daraka lako la kuwazoeza watoto wako na kutenga wakati wa kuwazoeza. Hata hivyo, kabla ya kuzungumzia mambo hayo, acheni tuzungumzie msingi wa elimu inayofaa.

Msingi wa Elimu ya Kweli

Tunaweza kujifunza kutokana na Mfalme Sulemani wa Israeli ambaye ni mmoja wa watu wenye hekima zaidi. Biblia inatuambia hivi: “Mungu akaendelea kumpa Sulemani hekima na uelewaji kwa wingi sana na ukunjufu wa moyo, kama mchanga ulio kando ya bahari. Na hekima ya Sulemani ilikuwa pana zaidi kuliko hekima ya watu wengine wote wa Mashariki na kuliko hekima yote ya Misri.” Sulemani “alikuwa na uwezo wa kusema methali elfu tatu, na nyimbo zake zikawa elfu moja na tano.” Alikuwa na ujuzi mwingi kuhusu mimea na wanyama. (1 Wafalme 4:29-34) Pia, Mfalme Sulemani alisimamia miradi ya ujenzi katika Israeli, kutia ndani ujenzi wa hekalu tukufu la Yehova huko Yerusalemu.

Maandishi ya Sulemani, kama yale yaliyo katika kitabu cha Mhubiri, yanafunua kwamba alielewa vizuri utu wa mwanadamu. Aliongozwa na roho ya Mungu kutaja msingi wa elimu ya kweli. Sulemani alisema: “Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa ujuzi.” Mfalme huyo mwenye hekima alisema hivi pia: “Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima, na kumjua aliye Mtakatifu Zaidi ni uelewaji.”—Methali 1:7; 9:10.

Ikiwa tunamwogopa Mungu, tunamheshimu sana na kuwa waangalifu tusikose kumpendeza. Tunatambua kwamba yeye ndiye Aliye Mkuu Zaidi nasi tunawajibika kwake. Huenda wale wanaompuuza yule ambaye uhai wetu unamtegemea wakaonekana kuwa wenye hekima machoni pa watu, lakini hekima hiyo ni “upumbavu kwa Mungu.” (1 Wakorintho 3:19) Watoto wenu wanahitaji elimu inayotegemea “hekima inayotoka juu.”—Yakobo 3:15, 17.

Kuogopa kutompendeza Yehova kunahusiana sana na kumpenda. Yehova anataka watumishi wake wamwogope na kumpenda. Musa alisema: “Ee Israeli, Yehova Mungu wako anataka nini kutoka kwako ila kumwogopa Yehova Mungu wako, ili kutembea katika njia zake zote na kumpenda yeye na kumtumikia Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote; kuzishika amri za Yehova na sheria zake ninazokuamuru wewe leo, kwa faida yako?”—Kumbukumbu la Torati 10:12, 13.

Tukiwafundisha watoto wetu kumwogopa na kumheshimu Yehova, tutakuwa tukiweka msingi kwa ajili ya elimu itakayowafanya wawe wenye hekima kikweli. Wakiendelea kujenga juu ya msingi huo, watazidi kumthamini Muumba wao, aliye Chanzo cha ujuzi wote wa kweli. Hilo litawasaidia watoto wetu kufahamu vizuri yale wanayojifunza, na kuwazuia wasikate kauli zenye kasoro. Watasitawisha uwezo wa “kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Msingi kama huo utawasaidia kuendelea kuwa wanyenyekevu na kuepuka kufanya mabaya.—Methali 8:13; 16:6.

Watoto Wenu Wanawatazama!

Lakini, tunaweza kuwasaidia jinsi gani watoto wetu wampende na kumwogopa Yehova? Jibu la swali hilo limo katika Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli kupitia nabii Musa. Wazazi Waisraeli waliambiwa hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.”—Kumbukumbu la Torati 6:5-7.

Mistari hiyo inawafundisha wazazi mambo muhimu. Jambo moja ni hili: Ukiwa mzazi unapaswa kuweka mfano mzuri. Ili kuwafundisha watoto wako kumpenda Yehova, wewe mwenyewe unapaswa kumpenda Mungu, na maneno yake yanapaswa kuwa moyoni mwako. Kwa nini jambo hilo ni la maana sana? Kwa sababu wewe hasa ndiye mwalimu wa watoto wako. Yale wanayojifunza kutokana na mfano wako yatakuwa na uvutano mkubwa juu yao. Na hakuna jambo lingine linaloweza kuwa na uvutano mkubwa katika maisha ya mtoto kuliko mfano wa wazazi wake.

Tamaa, viwango, kanuni, na mapendezi yako hayapaswi kuonekana kupitia maneno yako tu bali pia kupitia matendo yako. (Waroma 2:21, 22) Tangu wakiwa wachanga, watoto wanajifunza kwa kuwatazama wazazi wao kwa uangalifu. Watoto wanatambua mambo yaliyo ya maana kwa wazazi wao, na kwa kawaida hayo ndiyo mambo yanayokuwa ya maana kwa watoto. Ikiwa unampenda Yehova kikweli, watoto wako watatambua jambo hilo. Kwa mfano, wataona kwamba kusoma na kujifunza Biblia ni mambo muhimu kwako. Watatambua kwamba unatanguliza mambo ya Ufalme katika maisha yako. (Mathayo 6:33) Ukihudhuria mikutano kwa ukawaida na kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme utawaonyesha kwamba kumtolea Yehova utumishi mtakatifu ni jambo la maana sana kwako.—Mathayo 28:19, 20; Waebrania 10:24, 25.

Timiza Daraka Lako

Jambo lingine ambalo wazazi wanaweza kujifunza katika Kumbukumbu la Torati 6:5-7 ni hili: Mna daraka la kuwazoeza watoto wenu. Kati ya watu wa Yehova wa nyakati za zamani, wazazi ndio waliokuwa na daraka la kuwaelimisha watoto wao. Kati ya Wakristo wa karne ya kwanza, wazazi waliendelea kutimiza daraka hilo muhimu la kuwaelimisha watoto wao. (2 Timotheo 1:5; 3:14, 15) Akiwaandikia Wakristo wenzake, mtume Paulo alionyesha kwamba akina baba hasa, walipaswa ‘kuendelea kuwalea [watoto wao] katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.’—Waefeso 6:4.

Kwa sababu ya kazi na shughuli nyingine nyingi za siku hizi ambazo zinachukua wakati na nguvu nyingi, wazazi wanaweza kushawishiwa kuwaacha watoto wao waelimishwe na watu wengine kama vile walimu na watu wanaowatunza watoto. Hata hivyo, hakuna mtu anayeweza kuchukua mahali pa mzazi mwenye upendo anayejali. Usipuuze hata kidogo umuhimu na uvutano wako kwa watoto wako. Ikiwa unahitaji msaada, utafute kwa hekima, lakini usimpe kamwe mtu mwingine wajibu wako mtakatifu.

Tumia Wakati Kuwazoeza Watoto Wako

Jambo lingine tena ambalo wazazi wanajifunza katika Kumbukumbu la Torati 6:5-7 ni hili: Wakati na jitihada zinahitajiwa ili kuwazoeza watoto. Wazazi Waisraeli walipaswa ‘kukazia’ kweli ya Mungu ndani ya watoto wao. Katika Kiebrania cha awali, neno ‘kazia’ linamaanisha “kurudia,” “kusema tena na tena.” Wazazi walipaswa kufanya hivyo siku nzima, ndiyo, kuanzia asubuhi mpaka jioni, ‘katika nyumba zao’ na “barabarani.” Wakati na jitihada zinahitajiwa ili kuwafundisha watoto na kufinyanga mitazamo na tabia yao ili wampendeze Mungu.

Basi, unaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wako waelimike kikweli? Kuna mengi unayoweza kufanya. Wafundishe kumpenda na kumwogopa Yehova. Wawekee mfano mzuri. Timiza daraka lako la kuwafundisha watoto wako, na utenge wakati ili kuwazoeza. Wewe si mkamilifu, na hivyo utakosea mara kwa mara unapojaribu kuwasaidia. Lakini ukijitahidi kikweli kufanya mapenzi ya Mungu, inaelekea sana kwamba watoto wako watathamini na kufaidika na jitihada zako. “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa,” inasema Methali 22:6. “Hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” Kanuni hiyohiyo inatumika kuwahusu wasichana pia.

Kupata elimu ni kama kufunga safari inayoendelea kwa maisha yote. Ikiwa wewe na watoto wako mnampenda Mungu, mtafurahia safari hiyo milele na milele. Hiyo ni kwa sababu nyakati zote tutakuwa na mengi ya kujifunza kumhusu Yehova na jinsi tunavyoweza kutimiza kusudi lake.—Mhubiri 3:10, 11.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, unawasomea watoto wako Biblia?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Tenga wakati wa kuwafundisha watoto wako kumhusu Muumba