Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu Kwa Nini Mateso Yote Yatakwisha Karibuni

Sababu Kwa Nini Mateso Yote Yatakwisha Karibuni

Sababu Kwa Nini Mateso Yote Yatakwisha Karibuni

“Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 32:4.

1, 2. (a) Kwa nini unathamini tumaini la kuishi milele? (b) Ni nini kinachowazuia watu wengi wasiamini kwamba kuna Mungu ambaye anatoa ahadi nzuri sana za wakati ujao?

JE, UNAFURAHIA kuwazia jinsi maisha yatakavyokuwa katika Paradiso? Pengine unajiwazia ukichunguza dunia hii maridadi na kujifunza juu ya jamii nyingi sana za vitu vilivyo hai ambavyo viko duniani. Au labda unatafakari kuhusu uradhi ambao utapata unapofanya na wengine kazi ya kuitunza dunia na kuigeuza yote iwe bustani. Au huenda unawazia ustadi ambao unaweza kusitawisha katika sanaa, ujenzi, muziki, au mambo mengine ambayo huna wakati wa kuyafanya katika ulimwengu wa leo wenye hekaheka nyingi. Kwa vyovyote vile, unathamini tumaini la kuishi milele ambalo Biblia inaita “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima ambao Yehova alikusudia tuwe nao, uzima wa milele.—1 Timotheo 6:19.

2 Kuwahubiria wengine kuhusu tumaini hilo linalotegemea Biblia ni pendeleo lenye thamani na lenye kufurahisha, sivyo? Hata hivyo, wengi wanakataa tumaini hilo. Wanapinga kwamba ni ndoto isiyoweza kutimizwa ambayo inaaminiwa na watu wanaodanganyika kwa urahisi. Huenda hata ikawa vigumu kwao kuamini kwamba kuna Mungu ambaye anaahidi uzima wa milele katika Paradiso. Kwa nini? Watu fulani wanatatanishwa na kuwepo kwa uovu. Wanasema kwamba ikiwa kuna Mungu ambaye ni mweza-yote na mwenye upendo, haieleweki ni kwa nini kuna uovu na mateso ulimwenguni. Wanasema kwamba hakuna Mungu ambaye anaweza kuacha uovu uwepo, na ikiwa kuna mungu wa aina hiyo, basi si mungu mweza-yote au hatujali sisi. Watu fulani wanaona maoni hayo kuwa yenye kusadikisha. Kwa kweli, Shetani amekuwa bingwa katika kupofusha akili za wanadamu.—2 Wakorintho 4:4.

3. Tunaweza kuwasaidia watu kujibu swali gani gumu, na kwa nini tuna nafasi ya pekee ya kufanya hivyo?

3 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuna nafasi ya pekee ya kuwasaidia watu ambao wanadanganywa na Shetani na hekima ya ulimwengu huu. (1 Wakorintho 1:20; 3:19) Tunaelewa kwa nini watu wengi hawaamini ahadi za Biblia. Ni kwa sababu hawamjui Yehova. Labda hawajui jina lake au maana ya jina hilo, na inaelekea kwamba wanajua machache au hawajui jambo lolote kuhusu sifa zake au uwezo wake wa kutimiza ahadi zake. Ni pendeleo kwetu kujua mambo hayo. Mara kwa mara, ni vizuri kwetu kufikiria jinsi tunavyoweza kuwasaidia watu ambao ‘wako katika giza kiakili’ wapate jibu la moja ya maswali magumu zaidi ambayo yanaulizwa na wanadamu, “Kwa nini Mungu anaacha uovu na mateso yawepo?” (Waefeso 4:18) Kwanza, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kujibu swali hilo kwa njia yenye kuridhisha. Kisha, tutazungumzia jinsi sifa za Yehova zinavyofunuliwa kupitia njia ambayo ameshughulikia suala la uovu.

Njia Nzuri ya Kujibu Swali Hilo

4, 5. Huenda tukahitaji kufanya nini kwanza mtu anapouliza kwa nini Mungu ameacha mateso yawepo? Eleza.

4 Mtu anapouliza kwa nini Mungu anaacha mateso yawepo, tunamjibu namna gani? Huenda tukataka kumpa maelezo mengi papo hapo, kuanzia yale yaliyotukia katika bustani ya Edeni. Nyakati nyingine, huenda ikafaa kufanya hivyo. Hata hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu. Pengine tunahitaji kwanza kuweka msingi fulani. (Methali 25:11; Wakolosai 4:6) Acheni tuchunguze mambo matatu yanayoweza kutusaidia kumsaidia mtu kabla ya kuanza kujibu swali hilo.

5 Kwanza, ikiwa mtu amevurugika sana kwa sababu ya kuenea kwa uovu ulimwenguni, inaelekea kwamba yeye binafsi au wapendwa wake wameumizwa na uovu. Hivyo, huenda likawa jambo la hekima kuonyesha kwamba unamhurumia kikweli. Mtume Paulo aliwashauri hivi Wakristo: “Lieni pamoja na watu wanaolia.” (Waroma 12:15) Kumhurumia, au kumwonyesha “hisia-mwenzi,” kunaweza kumgusa moyo mtu huyo. (1 Petro 3:8) Akielewa kwamba tunamjali, inaelekea sana atasikiliza yale tutakayomwambia.

6, 7. Kwa nini inafaa tumpongeze mtu mnyoofu anayeuliza swali la Kimaandiko linalotatanisha?

6 Pili, tunaweza kumpongeza mtu mnyoofu kwa sababu ya kuuliza swali hilo. Watu fulani wanakata kauli kwamba kwa sababu wanatatanishwa na maswali kama hayo, hawana imani au hawamheshimu Mungu. Huenda hata wameambiwa hivyo na kiongozi fulani wa kidini. Hata hivyo, si lazima iwe hivyo. Kwa kweli, watu waaminifu katika nyakati za Biblia waliuliza maswali kama hayo. Kwa mfano, mtunga-zaburi Daudi aliuliza hivi: “Ee Yehova, kwa nini unaendelea kusimama mbali? Kwa nini unaendelea kujificha nyakati za taabu?” (Zaburi 10:1) Pia, nabii Habakuki aliuliza hivi: “Ee Yehova, nililie msaada mpaka wakati gani, nawe usisikie? Nitakuomba msaada kutokana na jeuri mpaka wakati gani, nawe usiokoe? Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu, kwa nini kugombana hutokea, kwa nini mzozo huendelezwa?”—Habakuki 1:2, 3.

7 Hao walikuwa wanaume waaminifu ambao walimheshimu sana Mungu. Je, walilaumiwa kwa sababu ya kuuliza maswali hayo yaliyowasumbua? Badala ya kuwalaumu, Yehova aliona kwamba inafaa maswali yao ya unyoofu yaandikwe katika Neno lake. Leo, huenda mtu anayevurugika kwa sababu ya kuenea kwa uovu akawa na njaa ya kiroho. Pengine anatamani kupata majibu ambayo yanaweza kupatikana tu katika Biblia. Kumbuka, Yesu aliwasifu wale ambao wana njaa ya kiroho, au wale “wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Ni pendeleo kubwa sana kuwasaidia watu kama hao wapate furaha ambayo Yesu aliahidi!

8. Ni mafundisho gani yenye kuvuruga ambayo yamewafanya watu wengi waamini kwamba Mungu ndiye anayesababisha mateso, na tunaweza kuwasaidia jinsi gani?

8 Tatu, huenda tukahitaji kumsaidia mtu huyo kuelewa kwamba Mungu hasababishi uovu ambao umeenea sana ulimwenguni. Watu wengi wanafundishwa kwamba Mungu anatawala ulimwengu huu tunamoishi, kwamba zamani za kale Mungu alipanga mambo yote yanayotupata, na kwamba ana sababu zisizoeleweka na zisizochunguzika za kuwatesa wanadamu. Mafundisho hayo ni ya uwongo. Yanamvunjia Mungu heshima na yanaonyesha kwamba Mungu ndiye anayesababisha uovu na mateso ulimwenguni. Kwa hiyo, huenda tukahitaji kutumia Neno la Mungu kunyoosha mambo kama hayo. (2 Timotheo 3:16) Si Yehova anayeutawala mfumo huu wa mambo uliopotoka; Shetani Ibilisi ndiye anayeutawala. (1 Yohana 5:19) Yehova hapangi mapema mambo yatakayowapata viumbe wake wenye akili; anampa kila mmoja uhuru na nafasi ya kuchagua kati ya mema na mabaya, lililo sawa na lililo kosa. (Kumbukumbu la Torati 30:19) Na Yehova si chanzo cha uovu; anachukia uovu na anawajali wale wanaoteseka isivyo haki.—Ayubu 34:10; Methali 6:16-19; 1 Petro 5:7.

9. Taja vifaa fulani ambavyo “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametayarisha ili kuwasaidia watu waelewe kwa nini Yehova Mungu ameacha mateso yawepo?

9 Baada ya kuweka msingi kama huo, huenda msikilizaji wako akawa tayari kujifunza kwa nini Mungu anaacha mateso yaendelee. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametayarisha vifaa vingi vya kukusaidia. (Mathayo 24:45-47) Kwa mfano, katika Kusanyiko la Wilaya la “Utii wa Kimungu” la 2005/06, trakti yenye kichwa Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni! ilitolewa. Ikiwa trakti hiyo inapatikana katika lugha yenu, kwa nini usifahamu mambo yaliyomo? Pia, kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, ambacho kinapatikana sasa katika lugha 157, kina sura nzima inayozungumzia swali hilo muhimu. Tumia vizuri kabisa vifaa hivyo. Vinaeleza waziwazi matukio ya Kimaandiko kuhusu suala la enzi kuu ambalo lilitokezwa katika Edeni na kwa nini Yehova alishughulikia suala hilo kama alivyofanya. Pia, kumbuka kwamba unapozungumzia jambo hilo, unampa msikilizaji wako nafasi ya kupata ujuzi muhimu sana. Ni ujuzi kumhusu Yehova na sifa zake nzuri sana.

Kazia Sifa za Yehova

10. Kwa nini ni vigumu kwa watu wengi kuelewa sababu ambayo imemfanya Mungu aache uovu uwepo, na ni ujuzi gani unaoweza kuwasaidia?

10 Unapowasaidia watu waelewe kwa nini Yehova ameacha wanadamu wajitawale chini ya uvutano wa Shetani, jaribu kukazia sifa nzuri sana za Yehova. Watu wengi wanajua kwamba Mungu ni mwenye nguvu; wamezoea kusikia akiitwa Mungu Mweza-Yote. Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kwao kuelewa kwa nini hatumii nguvu zake nyingi ili kukomesha mara moja ukosefu wa haki na mateso. Pengine hawaelewi sifa nyingine za Yehova, kama vile utakatifu, haki, hekima, na upendo wake. Yehova anaonyesha sifa hizo kwa njia kamilifu na yenye usawaziko. Hivyo, Biblia inasema hivi: “Kazi zake ni kamilifu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Unaweza kukazia sifa hizo jinsi gani unapojibu maswali ambayo yanaulizwa mara nyingi kuhusu suala hilo? Acheni tuchunguze mifano michache.

11, 12. (a) Kwa nini Adamu na Hawa walipotenda dhambi hawangeweza kusamehewa? (b) Kwa nini Yehova hataacha dhambi iendelee milele?

11 Je, Yehova angeweza tu kuwasamehe Adamu na Hawa? Katika kisa hiki hangeweza kamwe kuwasamehe. Wakiwa wanadamu wakamilifu, Adamu na Hawa walichagua kimakusudi kukataa enzi kuu ya Yehova na badala yake wakakubali mwongozo wa Shetani. Haishangazi kwamba waasi hao hawakuonyesha ishara yoyote ya kutubu. Hata hivyo, watu wanapouliza kwa nini Yehova hakuwasamehe, huenda wakawa wanauliza kwa nini Yehova hakushusha matakwa yake na hivyo kuruhusu dhambi na uasi uwepo. Jibu la swali hilo linahusiana sana na sifa muhimu ya utu wa Yehova, yaani, utakatifu wake.—Kutoka 28:36; 39:30.

12 Biblia inakazia utakatifu wa Yehova mara nyingi sana. Hata hivyo, inasikitisha kwamba watu wachache katika ulimwengu huu mpotovu wanaelewa sifa hiyo. Yehova ni safi, ametakata, na amejitenga na dhambi yote. (Isaya 6:3; 59:2) Amefanya mipango ya upatanisho kwa ajili ya dhambi ili kuifutilia mbali, lakini hataiacha iendelee milele. Kama Yehova angeacha dhambi iendelee milele, hatungekuwa na tumaini la wakati ujao. (Methali 14:12) Wakati wake uliowekwa utakapofika, Yehova atarudisha uumbaji wote katika hali ya utakatifu. Hilo ni jambo hakika, kwa kuwa ni mapenzi ya Yule Mtakatifu.

13, 14. Kwa nini Yehova aliamua kutowaharibu wale waasi katika Edeni?

13 Je, Yehova angewaharibu tu waasi hao katika Edeni na kuanza mambo upya? Bila shaka alikuwa na nguvu za kufanya hivyo. Hivi karibuni atatumia nguvu zake kuwaharibu waovu wote. Huenda watu fulani wakauliza, ‘Kwa nini hakufanya hivyo wakati kulipokuwa na watenda-dhambi watatu tu katika ulimwengu mzima? Je, dhambi na mateso yote tunayoona ulimwenguni hayangezuiwa?’ Kwa nini Yehova hakuamua kufanya hivyo? Andiko la Kumbukumbu la Torati 32:4 linasema hivi: “Njia zake zote ni haki.” Yehova anathamini sana haki. Kwa kweli, “Yehova ni mpenda-haki.” (Zaburi 37:28) Kwa sababu anapenda haki, Yehova alijizuia kutowafagilia mbali waasi hao katika Edeni. Kwa nini?

14 Uasi wa Shetani ulitokeza suala linalohusu haki ya Mungu ya kuwa mwenye enzi kuu. Kupatana na sifa ya Yehova ya haki, dai la Shetani lilihitaji kujibiwa kwa njia ya haki. Ingawa waasi hao walistahili kuangamizwa mara moja, kufanya hivyo hakungejibu dai hilo kwa njia ya haki. Kufanya hivyo kungethibitisha zaidi kwamba Yehova ni mkuu katika nguvu, lakini suala lililotokezwa halikuhusu nguvu zake. Kwa kuongezea, Yehova alikuwa amewaambia Adamu na Hawa kusudi lake. Walipaswa kuzaa na kuijaza dunia, kuitiisha, na kutawala viumbe vyote duniani. (Mwanzo 1:28) Ikiwa Yehova angewaharibu mara moja Adamu na Hawa, kusudi alilotangaza kuhusu wanadamu halingekuwa na maana yoyote. Sifa ya Yehova ya haki haingeruhusu hata kidogo jambo hilo litukie, kwa kuwa nyakati zote kusudi lake linatimia.—Isaya 55:10, 11.

15, 16. Tunaweza kuwasaidia namna gani watu wanapopendekeza njia tofauti za “kutatua” suala lililotokezwa Edeni?

15 Je, kuna mtu yeyote katika ulimwengu mzima ambaye angeweza kushughulikia uasi huo kwa njia ya hekima kuliko Yehova? Watu fulani wanaweza kupendekeza njia zao wenyewe za “kutatua” uasi uliotokea Edeni. Hata hivyo, je, kufanya hivyo hakungeonyesha kwamba wanafikiri wanaweza kushughulikia suala hilo kwa njia bora zaidi? Huenda wasifanye hivyo kwa nia mbaya, lakini hawamwelewi Yehova na hawaelewi hekima yake yenye kustaajabisha. Akiwaandikia Wakristo huko Roma, mtume Paulo alizungumzia kwa undani hekima ya Mungu, kutia ndani ‘siri takatifu’ kuhusu kusudi la Yehova la kutumia Ufalme wa Kimasihi kuwakomboa wanadamu waaminifu na kulitakasa jina Lake takatifu. Paulo alihisi namna gani kuhusu hekima ya Mungu mwenye kusudi hilo? Mtume huyo alimalizia barua yake kwa maneno haya: “Kwa Mungu, mwenye hekima peke yake, kuwe na utukufu kupitia Yesu Kristo milele. Amina.”—Waroma 11:25; 16:25-27.

16 Paulo alielewa kwamba Yehova ni “mwenye hekima peke yake.” Yeye ndiye mwenye hekima yote katika ulimwengu mzima. Ni mwanadamu gani asiye mkamilifu ambaye angefikiri kwamba yeye ana njia bora zaidi ya kutatua tatizo lolote, bila kutaja suala gumu zaidi lililohitaji kushughulikiwa kwa hekima ya kimungu? Basi tunahitaji kuwasaidia watu wamheshimu na kumwogopa Mungu “mwenye hekima moyoni” kama sisi tunavyofanya. (Ayubu 9:4) Kadiri tunavyozidi kuelewa vizuri hekima ya Yehova, ndivyo tutakavyozidi kutumaini kwamba njia yake ya kushughulikia mambo ndiyo njia bora zaidi.—Methali 3:5, 6.

Kuthamini Sifa Kuu ya Yehova

17. Kuelewa zaidi upendo wa Yehova kunaweza kuwasaidia namna gani wale wanaotaabika kwa sababu Mungu ameacha mateso yawepo?

17 “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Kwa maneno hayo ya pekee, Biblia inafunua sifa kuu ya Yehova, sifa inayovutia zaidi kuliko sifa zote na inayowafariji zaidi watu wanaotaabika kwa sababu ya kuenea kwa uovu. Yehova ameonyesha upendo katika njia zote ambazo ameshughulikia matokeo mabaya sana ambayo yameletwa na dhambi juu ya uumbaji wake. Upendo ulimchochea Yehova kuwapa wazao wenye dhambi wa Adamu na Hawa tumaini, na kuwafungulia njia ya kumfikia Yeye na kuwa na uhusiano mzuri pamoja Naye. Upendo ulimchochea Mungu kuandaa fidia ambayo ingewawezesha kusamehewa kabisa dhambi na kupata tena uzima wa milele ulio mkamilifu. (Yohana 3:16) Na upendo umemchochea Mungu awaonyeshe wanadamu subira, na kuwapa wengi iwezekanavyo nafasi ya kumkataa Shetani na kumchagua Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu wao.—2 Petro 3:9.

18. Tunafurahi kuwa na ufahamu gani, na tutazungumzia jambo gani katika habari inayofuata?

18 Kasisi mmoja alipohutubia umati uliokuwa umekusanyika ili kukumbuka shambulizi baya sana la kigaidi, alisema hivi: “Hatujui kwa nini Mungu anaacha uovu na mateso yaendelee.” Maneno hayo yanasikitisha sana! Je, hatufurahi kwamba tuna ufahamu kuhusu habari hiyo? (Kumbukumbu la Torati 29:29) Na kwa kuwa Yehova ni mwenye hekima, haki, na upendo, tunajua kwamba hivi karibuni atakomesha mateso yote. Kwa kweli, ameahidi kwamba atafanya hivyo. (Ufunuo 21:3, 4) Lakini namna gani wote ambao wamekufa kwa muda wa karne nyingi? Je, njia ya Yehova ya kushughulikia lile suala la Edeni imewaacha bila tumaini? Hapana. Upendo umemchochea Mungu kuwafaidi kupitia ufufuo. Jambo hilo litazungumziwa katika habari inayofuata.

Ungetoa Jibu Gani?

• Tunaweza kumwambia nini mtu anayeuliza kwa nini Mungu ameacha mateso yawepo?

• Sifa ya Yehova ya utakatifu na ya haki zinaonekana jinsi gani kutokana na njia aliyotumia kushughulika na wale waasi huko Edeni?

• Kwa nini tunapaswa kuwasaidia watu waelewe zaidi upendo wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Jitahidi kuwasaidia wale wanaotaabishwa na mateso yaliyo ulimwenguni

[Picha katika ukurasa wa 23]

Daudi na Habakuki waliokuwa waaminifu walimuuliza Mungu maswali manyoofu