Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yeftha Anatimiza Nadhiri Yake Kwa Yehova

Yeftha Anatimiza Nadhiri Yake Kwa Yehova

Yeftha Anatimiza Nadhiri Yake Kwa Yehova

SHUJAA mmoja aliyeshinda vitani anarudi nyumbani baada ya kuweka huru taifa lake kutokana na uonevu. Binti yake anakimbia kumpokea, akicheza dansi kwa furaha na kupiga tari. Shujaa huyo anapomwona, anararua mavazi yake badala ya kushangilia. Kwa nini? Je, hafurahi kama binti yake kwamba amerudi salama? Ameshinda vita gani? Huyo ni nani?

Mwanamume huyo ni Yeftha, mmoja wa waamuzi wa Israeli la kale. Lakini ili kujibu yale maswali mengine na kuona jinsi simulizi hilo linavyotuhusu, tunahitaji kuchunguza mambo yaliyotukia kabla hajakutana na binti yake.

Hali Mbaya Sana Katika Israeli

Yeftha anaishi wakati ambapo hali ni mbaya sana. Waisraeli wenzake wameacha ibada safi na wanatumikia miungu ya Sidoni, Moabu, Amoni, na Filistia. Kwa hiyo, Yehova anawaacha watu wake mikononi mwa Waamoni na Wafilisti, ambao wanawakandamiza kwa miaka 18. Wakaaji wa Gileadi, mashariki ya Mto Yordani, wanateseka sana. * Mwishowe, Waisraeli wanarudiwa na akili, wanatubu na kutafuta msaada wa Yehova, wanaanza kumtumikia, na wanaondoa miungu ya kigeni iliyokuwa katikati yao.—Waamuzi 10:6-16.

Waamoni wanapiga kambi huko Gileadi, na Waisraeli wanajikusanya ili kukutana nao. Lakini Waisraeli hawana kiongozi. (Waamuzi 10:17, 18) Wakati huo, Yeftha ana matatizo yake mwenyewe. Ndugu zake wa kambo wenye pupa wamemfukuza ili wachukue urithi wake. Kwa hiyo, Yeftha anahamia Tobu, eneo lililo mashariki ya Gileadi na ambalo linaweza kuvamiwa kwa urahisi na maadui wa Israeli. “Watu wanaozurura-zurura,” ambao inaelekea walikuwa watu walioachishwa kazi na wakandamizaji au watu ambao waliasi kwa sababu ya kutumikishwa, wanajikusanya kwa Yeftha. ‘Wanaenda nje pamoja naye,’ labda kumaanisha kwamba wanafuatana na Yeftha anapovamia majirani wenye uadui. Inaelekea kwamba Maandiko yanamwita Yeftha “mwanamume mwenye nguvu na shujaa” kwa sababu ya uwezo wake mkubwa na ujasiri akiwa mpiganaji. (Waamuzi 11:1-3) Basi ni nani atakayeongoza Israeli kupigana na Waamoni?

“Njoo Uwe Kiongozi Wetu”

Wanaume wazee wa Gileadi wanamsihi Yeftha hivi: “Njoo uwe kiongozi wetu.” Ikiwa wanamtazamia akubali haraka nafasi hiyo ya kurudi nyumbani kwao, wamekosea. “Je, si ninyi mlionichukia, mkanifukuza kutoka nyumbani kwa baba yangu?” anawajibu. “Kwa nini basi mmenijia hivi sasa mkiwa katika taabu?” Ni jambo lilisofaa kama nini kwamba wanaume hao wazee wanamkataa Yeftha kwanza kisha wanamwomba awasaidie!—Waamuzi 11:4-7.

Yeftha atakuwa kiongozi huko Gileadi ikiwa tu watakubali takwa moja. Anasema hivi: ‘Yehova akimtia Amoni mkononi mwangu, mimi mwenyewe nitakuwa kichwa chenu!’ Ushindi utathibitisha kwamba Mungu anamuunga mkono, lakini Yeftha anataka pia kuhakikisha kwamba utawala wa Mungu haupuuzwi punde tu baada ya hali hiyo mbaya kupita.—Waamuzi 11:8-11.

Kushughulika na Amoni

Yeftha anajaribu kufanya mapatano na Waamoni. Anatuma wajumbe kwa mfalme wao ili wajue kwa nini Waamoni wamewashambulia. Waamoni wanawajibu kwa kutoa shtaka hili: Waisraeli walipotoka Misri walichukua eneo la Waamoni, na eneo hilo linapaswa kurudishwa.—Waamuzi 11:12, 13.

Kwa sababu anaelewa sana historia ya Israeli, Yeftha anapinga kwa busara madai hayo ya Waamoni. Anawaambia kwamba Waisraeli hawakuwasumbua Waamoni, Wamoabu, au Waedomu walipotoka Misri; wala Waisraeli walipotoka Misri Waamoni hawakuwa wakimiliki nchi hiyo iliyokuwa ikibishaniwa. Wakati huo, Waamori ndio waliokuwa wakiimiliki, lakini Mungu akamtia mfalme wao, Sihoni, mikononi mwa Israeli. Zaidi ya hayo, Waisraeli walikuwa wameishi katika eneo hilo kwa miaka 300. Kwa nini Waamoni wanadai eneo hilo wakati huu hasa?—Waamuzi 11:14-22, 26.

Yeftha anazungumzia pia suala muhimu linalowafanya Waisraeli wateseke: Mungu wa kweli ni nani? Je, ni Yehova au ni miungu ya nchi ambayo Waisraeli wamemiliki? Ikiwa Kemoshi alikuwa na nguvu zozote, je, hangezitumia kulinda nchi ya watu wake? Hayo ni mapambano kati ya dini ya uwongo, inayoongozwa na Waamoni, na ibada ya kweli. Hivyo, Yeftha anakata kauli hii inayopatana na akili: “Yehova aliye Mwamuzi na ahukumu leo kati ya wana wa Israeli na wana wa Amoni.”—Waamuzi 11:23-27.

Mfalme wa Amoni hasikilizi ujumbe wa Yeftha wa moja kwa moja. “Sasa roho ya Yehova [inakuja] juu ya Yeftha, naye [anapitia] katika Gileadi na Manase,” inaelekea akiwakusanya wanaume wenye nguvu kwa ajili ya vita.—Waamuzi 11:28, 29.

Nadhiri ya Yeftha

Akitafuta sana mwongozo wa Mungu, Yeftha anaweka nadhiri hii kwa Mungu: “Hakika ukiwatia wana wa Amoni mkononi mwangu, itatukia pia kwamba yule atakayetoka nje, atakayetoka nje ya milango ya nyumba yangu kuja kunipokea nitakaporudi kwa amani kutoka kwa wana wa Amoni, lazima atakuwa wa Yehova, nami nitamtoa huyo kuwa toleo la kuteketezwa.” Mungu anamjibu kwa kumbariki Yeftha. Anamwezesha kupiga majiji 20 ya Waamoni kwa “mauaji makubwa,” hivyo anawatiisha maadui wa Israeli.—Waamuzi 11:30-33.

Yeftha anaporudi kutoka vitani, hakuna anayempokea ila binti yake mpendwa, ambaye ni mtoto wake wa pekee! Simulizi hilo linasema hivi: “Alipomwona, akaanza kuyararua mavazi yake na kusema: ‘Ole, binti yangu! Kwa kweli umenifanya niiname chini, nawe mwenyewe umekuwa ndiye yule ambaye nilikuwa nikitenga. Mimi nimemfungulia Yehova kinywa changu, nami siwezi kurudi nyuma.’”—Waamuzi 11:34, 35.

Je, kweli Yeftha atamtoa binti yake kuwa dhabihu? Hapana. Yeftha hangewazia kufanya hivyo. Yehova anachukia kuwadhabihu wanadamu kihalisi, ambalo ni mojawapo ya mazoea maovu ya Wakanaani. (Mambo ya Walawi 18:21; Kumbukumbu la Torati 12:31) Roho ya Mungu ilikuwa ikitenda juu ya Yeftha alipoweka nadhiri hiyo, na pia Yehova alibariki jitihada zake. Maandiko yanamsifu Yeftha kwa sababu ya imani yake na kwa yale aliyofanya kuhusiana na kusudi la Mungu. (1 Samweli 12:11; Waebrania 11:32-34) Kwa hiyo, hangefikiria hata kidogo kumtoa mwanadamu awe dhabihu. Kufanya hivyo ni uuaji. Hivyo basi, Yeftha alikuwa akifikiria nini alipoweka nadhiri ya kumtoa mtu kwa Yehova?

Ni wazi kwamba Yeftha alimaanisha kuwa angemtoa yule ambaye angekuja kumpokea ili amtumikie Mungu kikamili. Chini ya Sheria ya Musa watu waliruhusiwa kuweka nadhiri ya nafsi kwa Yehova. Kwa mfano, wanawake walifanya kazi katika maskani, labda kwa kuchota maji. (Kutoka 38:8; 1 Samweli 2:22) Hatujui mengi kuhusu utumishi huo au hata ikiwa ulikuwa wa kudumu. Inaonekana Yeftha alikuwa akifikiria ujitoaji huo wa pekee alipoweka nadhiri yake, na inaonekana kwamba ahadi yake ilihusu utumishi wa kudumu.

Binti ya Yeftha na baadaye mvulana Samweli walikubali kutimiza nadhiri za wazazi wao waliomwogopa Mungu. (1 Samweli 1:11) Akiwa mwabudu mshikamanifu wa Yehova, binti ya Yeftha alisadiki mwenyewe kama baba yake kwamba nadhiri iliyowekwa na baba yake ilipaswa kutimizwa. Ilikuwa dhabihu kubwa, kwa sababu ilimaanisha kwamba hangeolewa kamwe. Aliulilia ubikira wake kwa sababu kila Mwisraeli alitamani kupata watoto ili kuendeleza jina na urithi wa familia. Kwa Yeftha, kutimiza nadhiri hiyo kulimaanisha kutoshirikiana tena na mtoto wake mpendwa na wa pekee.—Waamuzi 11:36-39.

Maisha ya mwanamwali huyo mwaminifu hayakupotea. Utumishi wa wakati wote katika nyumba ya Yehova ulikuwa mzuri sana, wenye kuridhisha, na njia yenye kusifika ya kumheshimu Mungu. Hivyo, “mwaka baada ya mwaka binti za Israeli wakawa wakienda kumpongeza binti ya Yeftha Mgileadi.” (Waamuzi 11:40) Na kwa kweli Yeftha alifurahia utumishi wa binti yake kwa Yehova.

Leo, watu wengi wa Mungu wanachagua maisha ya utumishi wa wakati wote wakiwa mapainia, wamishonari, wahudumu wanaosafiri, au washiriki wa familia ya Betheli. Huenda hilo likamaanisha kutowaona washiriki wa familia zao mara nyingi kama ambavyo wangependa. Hata hivyo, wote wanaohusika wanaweza kufurahia utumishi mtakatifu kama huo unaotolewa kwa Yehova.—Zaburi 110:3; Waebrania 13:15, 16.

Kuasi Mwongozo wa Mungu

Tunapofikiria siku za Yeftha, tunaona kwamba Waisraeli wengi wanakataa mwongozo wa Yehova. Ingawa kuna uthibitisho wa kwamba Mungu anambariki Yeftha, Waefraimu wanagombana naye. Wanataka kujua kwa nini hakuwaita waende vitani. Hata wanakusudia kuiteketeza nyumba ya Yeftha ‘juu yake’ kwa moto!—Waamuzi 12:1.

Yeftha anasema kwamba aliwaita Waefraimu lakini hawakuja. Kwa vyovyote vile, Mungu alishinda vita hivyo. Je, sasa wamekasirika kwa sababu Wagileadi hawakushauriana nao kabla ya kumchagua Yeftha awe kiongozi? Kwa kweli, upinzani wa Waefraimu unaonyesha kwamba wanamwasi Yehova, na hivyo lazima wapigwe. Katika vita vinavyotokea, Waefraimu wanashindwa. Kwa sababu ya kushindwa kutamka vizuri neno “Shibolethi,” wanaume Waefraimu waliokuwa wakikimbia wanatambuliwa kwa urahisi. Kwa ujumla, Waefraimu 42,000 wanauawa katika mapambano hayo.—Waamuzi 12:2-6.

Ulikuwa wakati wenye kuhuzunisha kama nini katika historia ya Israeli! Kulikuwa na amani baada ya Waamuzi Othnieli, Ehudi, Baraka, na Gideoni kushinda vita. Wakati huu amani haitajwi. Simulizi hilo linamalizia hivi tu: “Yeftha akaendelea kuhukumu Israeli kwa miaka sita, kisha Yeftha Mgileadi akafa, akazikwa katika jiji lake kule Gileadi.”—Waamuzi 3:11, 30; 5:31; 8:28; 12:7.

Tunajifunza nini kutokana na yote haya? Kwamba ingawa maisha ya Yeftha yalijaa matatizo, alikuwa mwaminifu kwa Mungu. Mwanamume huyo shujaa alimtaja Yehova alipokuwa akizungumza na wanaume wazee wa Gileadi, Waamoni, binti yake, na Waefraimu, na bila shaka, wakati alipoweka nadhiri yake. (Waamuzi 11:9, 23, 27, 30, 31, 35; 12:3) Mungu alimbariki Yeftha kwa sababu ya ujitoaji wake, naye alimtumia yeye pamoja na binti yake kuendeleza ibada safi. Wakati ambapo watu wengine waliacha viwango vya Mungu, Yeftha alishikamana navyo. Je, siku zote utamtii Yehova kama Yeftha?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Waamoni walikuwa wakatili sana. Baada ya miaka isiyozidi 60, walitisha kwamba wangeng’oa jicho la kuume la kila mkaaji wa jiji moja la Gileadi ambalo walishambulia. Nabii Amosi alitaja kwamba wakati fulani waliwapasua wanawake wenye mimba wa Gileadi.—1 Samweli 11:2; Amosi 1:13.