Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kutahiriwa Ni Ishara ya Kuwa Mtu Mzima?

Je, Kutahiriwa Ni Ishara ya Kuwa Mtu Mzima?

Je, Kutahiriwa Ni Ishara ya Kuwa Mtu Mzima?

KATIKA sehemu nyingi za ulimwengu, watoto wa kiume wanatahiriwa kwa sababu za kiafya. Katika sehemu nyingine za ulimwengu, ni kawaida kwa wanaume kutotahiriwa kamwe. Watu fulani, kama vile Wayahudi na Waislamu, wanatahiriwa kwa sababu tofauti na za kiafya. Wanaona kutahiriwa kuwa jambo lenye maana ya kidini.

Hata hivyo, katika mataifa mengine, sherehe ya kutahiriwa inafanywa mtoto wa kiume anapokuwa mtu mzima. Kwa kawaida, hilo linatia ndani kumpeleka jandoni, yaani, shule ya kitamaduni, ambako anatahiriwa na kutengwa na jamii kwa majuma fulani mpaka apone. Wakati huo, mtoto huyo anapaswa kufuata desturi fulani naye anafundishwa kuwa mwanamume. Je, ni lazima mtoto wa kiume atahiriwe hivyo ili kuthibitisha kwamba sasa yeye ni mtu mzima? Acheni tuchunguze yale ambayo Biblia inasema kuhusu maoni ya Mungu kuelekea jambo hilo.—Methali 3:5, 6.

Maoni ya Mungu Kuhusu Kutahiriwa

Watu fulani katika nyakati za zamani, kama vile Wamisri, walitahiriwa, yaani, walikatwa magovi ya kiungo chao cha kiume. Hata hivyo, Abrahamu hakuzaliwa katika jamii yenye utamaduni kama huo. Kwa kweli, Abrahamu aliishi muda mrefu bila kutahiriwa. Lakini, Abrahamu alikuwa mwanamume shujaa ingawa hakuwa ametahiriwa. Akiwa na kikundi kidogo cha wanaume, aliyafuata na kuyashinda majeshi ya wafalme wanne waliokuwa wamemteka mpwa wake, Loti. (Mwanzo 14:8-16) Miaka 14 hivi baadaye, Mungu alimwamuru Abrahamu atahiriwe na awatahiri wanaume wote wa nyumba yake. Kwa nini Mungu aliamuru hivyo?

Bila shaka, kutahiriwa hakukuonyesha kwamba Abrahamu hakuwa mtoto tena bali sasa alikuwa mtu mzima. Alikuwa na umri wa miaka 99! (Mwanzo 17:1, 26, 27) Mungu alitaja sababu ya kumpa amri hiyo: “Mnapaswa kutahiriwa nyama ya magovi yenu, nayo iwe ishara ya agano kati yangu mimi na ninyi.” (Mwanzo 17:11) Agano hilo la Kiabrahamu lilitia ndani ahadi ya Mungu ya kwamba kupitia Abrahamu, “familia zote za nchi” zingepata baraka nyingi mwishowe. (Mwanzo 12:2, 3) Kwa hiyo, machoni pa Mungu, kutahiriwa hakukuwa kamwe ishara ya kuwa mtu mzima. Kulifanywa ili kuonyesha kwamba mtu alitokana na ukoo wa Waisraeli ambao walikuwa wazao wa Abrahamu, waliopewa pendeleo la ‘kukabidhiwa maneno matakatifu ya Mungu.’—Waroma 3:1, 2.

Baada ya muda, taifa la Israeli halikustahili pendeleo hilo kwa sababu lilimkataa Mzao wa kweli wa Abrahamu, Yesu Kristo. Hivyo, walikataliwa na Mungu, na hivyo kutahiriwa kwao hakukuwa tena na maana yoyote machoni pa Mungu. Hata hivyo, Wakristo fulani katika karne ya kwanza W.K. walisisitiza kwamba bado Mungu alitaka watu watahiriwe. (Matendo 11:2, 3; 15:5) Kwa sababu hiyo, mtume Paulo alimtuma Tito ili ‘ayarekebishe mambo yaliyokuwa na kasoro’ katika makutaniko mbalimbali. Paulo alimwandikia Tito kuhusu kasoro moja: “Kuna watu wengi watundu, wanaoongea maneno yasiyo na faida, na wanaodanganya akili za watu, hasa watu wale ambao hushikamana na tohara. Ni jambo la lazima kuvifunga vinywa vya watu hao, kwa kuwa watu hao wanaendelea kuharibu nyumba nzima-nzima kwa kufundisha mambo ambayo hawapaswi kufundisha, ili kupata pato lisilo la haki.”—Tito 1:5, 10, 11.

Shauri hilo la Paulo bado linafaa. Bila shaka, Mkristo wa kweli angekuwa anafanya kinyume na Maandiko ikiwa angehimiza kwamba mtoto wa mtu fulani atahiriwe. Badala ya “kujiingiza katika mambo ya watu wengine,” Mkristo anaacha wazazi wafanye maamuzi kama hayo ya kibinafsi. (1 Petro 4:15) Kwa kuongezea, Paulo aliongozwa na roho kuandika kuhusu kutahiriwa kulingana na Sheria ya Musa: “Je, mtu yeyote aliitwa akiwa ametahiriwa? Acheni asiwe asiyetahiriwa. Je, mtu yeyote ameitwa akiwa katika kutotahiriwa? Acheni asitahiriwe. Kutahiriwa hakumaanishi kitu, na kutotahiriwa hakumaanishi kitu, lakini kushika amri za Mungu kuna maana. Katika hali yoyote ile ambayo kila mmoja aliitwa, acheni abaki katika hiyo.”—1 Wakorintho 7:18-20.

Namna Gani “Elimu ya Jando”?

Namna gani wazazi Wakristo wakiamua watoto wao wa kiume watahiriwe? Je, wangekuwa wakitenda kupatana na Biblia ikiwa wangeamua kuwapeleka wana wao kwa ile inayoitwa eti elimu ya jando iliyotajwa mapema? Kwenda jandoni kunatia ndani mambo mengi zaidi ya kukata tu magovi. Kwa majuma kadhaa, yule anayeenda jandoni ataishi na kushirikiana kwa ukaribu na vijana na walimu ambao hawamwabudu Yehova. Mambo mengi yanayofundishwa katika jando yanapingana na viwango vya juu vya maadili vya Biblia. Biblia inaonya hivi: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”—1 Wakorintho 15:33.

Pia, hatari za kimwili zinazoweza kumpata mtu anayeenda jandoni zinazidi kuongezeka. Mwaka wa 2003, gazeti moja (South African Medical Journal) lilionya hivi: “Matokeo yenye kutisha ya kutahiriwa yameonekana tena mwaka huu. Ripoti nyingi za vifo na madhara mengine ya kukatwa vibaya viungo vya uzazi zinatangazwa ulimwenguni pote na mashirika makubwa ya habari. . . . Kwa ufupi, nyingi kati ya zile zinazoitwa eti ‘shule za kutahiri’ au jando, leo ni bandia na hatari.”

Zaidi ya hatari ya kijana kuumizwa vibaya kimwili, kuna hatari kubwa hata zaidi ya kiroho. Mafundisho na mambo yanayofanywa jandoni yanahusiana sana na kuwasiliana na pepo na ibada ya mababu waliokufa. Kwa mfano, badala ya kukubali kwamba madaktari wasio waangalifu na hali zisizo safi kiafya zinasababisha madhara, wengi wanaamini kwamba misiba hiyo inasababishwa na ulozi au hasira ya mababu waliokufa. Biblia inatoa amri hii kuhusu kushirikiana na dini ya uwongo: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. Kwa maana kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria? Au nuru ina ushirika gani na giza? . . . ‘Kwa hiyo tokeni katikati yao, na mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kilicho najisi’; ‘nami nitawakaribisha ndani.’” (2 Wakorintho 6:14-17) Kulingana na shauri hilo, halingekuwa jambo la hekima kwa wazazi Wakristo kuwapeleka watoto wao wa kiume katika jando.

Ni Nini Kinachomfanya Mkristo Awe Mtu Mzima?

Iwe mwanamume Mkristo ametahiriwa au hajatahiriwa hilo halionyeshi kwamba yeye ni mtu mzima. Hangaiko kuu la Wakristo wa kweli ni kumpendeza Mungu, wala si “kuwa na sura ya kupendeza katika mwili.”—Wagalatia 6:12.

Hata hivyo, ili kumpendeza Mungu, ni lazima Mkristo ‘autahiri moyo’ wake. (Kumbukumbu la Torati 10:16; 30:6; Mathayo 5:8) Hilo halifanywi kwa kuukata moyo kwa kisu, bali kwa kukataa tamaa mbaya na mawazo ya kiburi, kama ile imani ya kwamba kutahiriwa katika mwili kunamfanya mtu awe bora kuliko wengine. Kwa kuvumilia majaribu na kusimama “imara katika imani,” Mkristo anaweza kuonyesha kwamba yeye ni mtu mzima iwe ametahiriwa au hajatahiriwa.—1 Wakorintho 16:13; Yakobo 1:12.