Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uovu Hauwezi Kushindwa?

Je, Uovu Hauwezi Kushindwa?

Je, Uovu Hauwezi Kushindwa?

Mvulana mdogo aliye na hamu ya kujua mambo, anaokota kitu fulani uwanjani. Kumbe ni bomu la kutegwa ardhini. Linalipuka na kumpofusha, naye anapata madhara mabaya ya kudumu. Mama fulani ambaye ametoka tu kuzaa, anamficha mtoto wake katika takataka kando ya barabara na kumwacha. Mtu mmoja aliyefutwa kazi anarudi mahali alipokuwa akifanya kazi, anawafyatulia risasi watu wote waliopo, kisha anajiua. Mtu fulani anayeheshimiwa katika jamii anawatendea vibaya kingono watoto wasioweza kujilinda.

KWA kusikitisha, ripoti za matendo maovu kama hayo zimekuwa za kawaida katika siku zetu. Inasikitisha hata zaidi kwamba mara nyingi ripoti hizo si kitu zikilinganishwa na habari kuhusu mauaji ya kikabila, maangamizi ya jamii nzima-nzima, na ugaidi. “Kwa sababu ya uovu wake, hii imekuwa karne ya Shetani,” inasema habari fulani iliyochapishwa mwaka wa 1995. “Hakuna wakati mwingine wowote uliopita ambapo watu wameonyesha uwezo au tamaa kubwa ya kuua mamilioni ya watu kwa sababu za kijamii, kidini, au kitabaka.”

Wakati huohuo, wanadamu wanachafua hewa, wanachafua dunia, wanamaliza mali za asili, na kuhatarisha kuwapo kwa jamii nyingi sana za viumbe. Je, mwanadamu anaweza kushinda uovu wote huo na kufanya ulimwengu uwe mahali pazuri na salama zaidi? Au je, kujaribu kufanya hivyo ni jambo la ubatili kama vile kujaribu kuzuia kwa ufagio mawimbi ya bahari yenye nguvu? Profesa ambaye ameandika habari nyingi kuhusu suala la uovu alisema hivi: “Nimeona uhitaji mkubwa sana wa kuleta mabadiliko makubwa ulimwenguni, kuboresha ulimwengu. Lakini inaonekana kwamba ulimwengu haubadiliki.” Huenda wewe pia unahisi vivyo hivyo.

Hali ya ulimwengu inaweza kulinganishwa na meli inayosafiri kuelekea sehemu fulani ya bahari inayozidi kuchafuka na kuzidi kuwa hatari siku kwa siku. Ingawa hakuna anayetaka kuelekea sehemu hiyo ya bahari, jitihada zote za kuelekeza meli hiyo upande tofauti hazifanikiwi. Meli hiyo isiyoweza kusimamishwa inazidi kusonga mbele na kuingia katika sehemu yenye dhoruba kali.

Kwa kadiri fulani, ulimwengu unakabili hali hiyo inayozidi kuwa mbaya kwa sababu ya kutokamilika kwa mwanadamu. (Waroma 3:23) Hata hivyo, inaonekana kwamba kiwango cha uovu, kuenea kwa uovu, na kuendelea kwa uovu hakulingani hata kidogo na chuki ya mwanadamu. Je, kuna uwezekano kwamba mwanadamu anaongozwa na nguvu fulani ya uovu isiyoonekana na iliyo na uwezo mkubwa zaidi? Ikiwa ndivyo, ni nguvu gani hiyo, na tunaweza kujilinda jinsi gani? Habari inayofuata itajibu maswali hayo.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

© Heldur Netocny/Panos Pictures