Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusitawi Kiroho Wakati wa Kuwa na Kichwa Chenye Mvi

Kusitawi Kiroho Wakati wa Kuwa na Kichwa Chenye Mvi

Kusitawi Kiroho Wakati wa Kuwa na Kichwa Chenye Mvi

“Wale ambao wamepandwa katika nyumba ya Yehova . . . wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi.”—ZABURI 92:13, 14.

1, 2. (a) Mara nyingi uzee unafafanuliwa jinsi gani? (b) Maandiko yanaahidi nini kuhusu matokeo ya dhambi ya Adamu?

UZEE—neno hilo linakukumbusha nini? Ngozi yenye makunyanzi? Matatizo ya kusikia? Viungo dhaifu? Au matatizo mengine yanayohusiana na “siku zenye msiba” ambayo yanaelezwa kwa undani zaidi katika Mhubiri 12:1-7? Ikiwa ndivyo, ni jambo la maana kukumbuka kwamba ufafanuzi huo wa kitabu cha Mhubiri sura ya 12 hauonyeshi kuzeeka kuwa kusudi la mwanzoni la Muumba, Yehova Mungu, lakini unaonyesha matokeo ya dhambi ya Adamu juu ya mwili wa mwanadamu.—Waroma 5:12.

2 Kuzeeka kwenyewe si laana, kwa kuwa kadiri tunavyoendelea kuishi ndivyo miaka inavyopita. Kwa kweli, kukua na kukomaa ni sifa zenye kupendeza za vitu vyote vilivyo hai. Hivi karibuni, madhara ya miaka elfu sita ya dhambi na kutokamilika ambayo tunaona leo yatakuwa mambo ya zamani, na wanadamu wote watiifu watafurahia uhai bila maumivu ya uzee na kifo, kama ilivyokuwa imekusudiwa. (Mwanzo 1:28; Ufunuo 21:4, 5) Wakati huo, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Wazee watakuwa tena na ‘nguvu zao za ujana,’ na nyama yao ‘itakuwa laini kuliko wakati wa ujana.’ (Ayubu 33:25) Lakini kwa sasa, sisi sote tunalazimika kupambana na dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu. Hata hivyo, watumishi wa Yehova wanabarikiwa kwa njia za pekee wanapoendelea kuzeeka.

3. Ni katika njia gani Wakristo wanaweza ‘kuendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi’?

3 Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba “wale ambao wamepandwa katika nyumba ya Yehova . . . wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi.” (Zaburi 92:13, 14) Kwa njia ya mfano, mtunga-zaburi anaeleza kweli yenye maana ya kwamba watumishi waaminifu wa Mungu wanaweza kuendelea kufanya maendeleo na kusitawi kiroho, hata ikiwa mwili wao unazidi kudhoofika. Mifano mingi ya nyakati za Biblia na ya siku hizi inaonyesha kwamba jambo hilo ni la kweli.

“Hakosi Kamwe”

4. Ana, nabii wa kike aliyezeeka, alionyesha jinsi gani kwamba alijitoa kwa Mungu, naye alipata thawabu gani?

4 Fikiria nabii wa kike, Ana, aliyeishi katika karne ya kwanza. Akiwa na umri wa miaka 84, Ana “alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana kwa kufunga na dua.” Mwanamke huyo hangeweza kuishi katika hekalu kwa kuwa baba yake hakuwa Mlawi bali alikuwa wa “kabila la Asheri.” Fikiria jinsi alivyojitahidi kufika hekaluni kila siku, tangu wakati wa utumishi wa asubuhi mpaka utumishi wa jioni! Hata hivyo, Ana alithawabishwa sana kwa sababu alijitoa. Alipata pendeleo la kuwepo wakati Yosefu na Maria walipomleta mtoto Yesu hekaluni ili aonyeshwe kwa Yehova kulingana na Sheria. Alipomwona Yesu, Ana ‘alianza kumshukuru Mungu akisema juu ya mtoto huyo kwa wale wote waliokuwa wakiungojea ukombozi wa Yerusalemu.’—Luka 2:22-24, 36-38; Hesabu 18:6, 7.

5, 6. Leo watu wengi waliozeeka wanaonyesha kwa njia gani roho kama ya Ana?

5 Watu wengi waliozeeka ambao wamo kati yetu leo wako kama Ana kwa kuwa wanahudhuria mikutano kwa ukawaida, wanaomba dua kwa bidii ili kuendeleza ibada ya kweli, na wana hamu kubwa ya kuhubiri habari njema. Ndugu mmoja mwenye umri wa miaka 80 na kitu ambaye anahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida pamoja na mke wake, alisema hivi: “Tumesitawisha zoea la kwenda kwenye mikutano. Hatutaki kuwa mahali pengine. Tunataka kuwa mahali ambapo watu wa Mungu wapo. Hapo ndipo tunapojihisi salama.” Ni mfano mzuri wenye kutia moyo kama nini!—Waebrania 10:24, 25.

6 “Ikiwa kuna jambo lolote ambalo linahusu ibada ya kweli na ambalo ninaweza kushiriki, ninataka kufanya hivyo.” Hilo ndilo azimio la Jean, mjane mmoja Mkristo mwenye umri wa miaka 80 na kitu. Anaendelea kusema hivi: “Bila shaka, nyakati nyingine ninahuzunika, lakini kwa nini kila mtu kando yangu awe mwenye huzuni wakati ninapokuwa na huzuni?” Akiwa mwenye macho yanayong’aa, Jean alieleza shangwe anayopata anapotembelea nchi nyingine kwa ajili ya matukio yenye kujenga kiroho. Katika safari ya hivi karibuni, Jean aliwaambia hivi wenzake, “Sitaki tena kusafiri ili kufurahia mazingira; ninataka kwenda kuhubiri!” Ingawa hakujua lugha ya eneo hilo, Jean aliweza kuwachochea watu wapendezwe na ujumbe wa Biblia. Zaidi ya hilo, kwa miaka fulani, alitumika na kutaniko moja ambalo lilihitaji msaada, hata ingawa ilimbidi kujifunza lugha mpya na kusafiri muda wa saa moja kwenda na saa moja kurudi kutoka kwenye mikutano.

Endelea Kutumia Akili Zako

7. Wakati wa uzee wake, Musa alionyesha jinsi gani tamaa yake ya kukuza uhusiano wake pamoja na Mungu?

7 Uzoefu katika maisha unakuja kadiri miaka inavyopita. (Ayubu 12:12) Kwa upande mwingine, maendeleo ya kiroho, hayaji tu kwa sababu ya kuwa na umri mkubwa. Kwa hiyo, badala ya kutegemea tu akiba ya ujuzi waliopata wakati uliopita, watumishi washikamanifu wa Mungu wanajitahidi ‘kuzidi kujifunza,’ kadiri miaka inavyopita. (Methali 9:9) Musa alikuwa na umri wa miaka 80 alipotumwa na Yehova. (Kutoka 7:7) Katika siku zake, inaelekea kuishi mpaka kufikia umri huo kulionwa kuwa jambo lisilo la kawaida, kwa kuwa Musa aliandika hivi: “Kwa maana siku za miaka yetu ni miaka 70; na . . . kwa sababu ya nguvu za pekee ni miaka 80.” (Zaburi 90:10) Hata hivyo, Musa hakujiona kamwe kuwa mzee sana asiweze kujifunza mambo. Baada ya kumtumikia Mungu kwa makumi ya miaka, kuwa na mapendeleo mengi, na kutimiza madaraka mazito, Musa alimsihi Yehova hivi: “Nijulishe, tafadhali, njia zako, nipate kukujua.” (Kutoka 33:13) Sikuzote Musa alitamani sana kukuza uhusiano wake pamoja na Yehova.

8. Danieli aliendelea kutumia akili zake jinsi gani alipokuwa na umri wa miaka 90 na kitu, na matokeo yalikuwa nini?

8 Nabii Danieli, ambaye inaelekea alikuwa na umri wa miaka 90 na kitu, bado aliendelea kuchunguza kwa uangalifu maandishi matakatifu. Yale aliyotambua kwa kujifunza “vitabu,” labda kutia ndani kitabu cha Mambo ya Walawi, Isaya, Yeremia, Hosea, na Amosi, yalimchochea kumtafuta Yehova kwa bidii katika sala. (Danieli 9:1, 2) Sala hiyo ilijibiwa alipopewa habari iliyoongozwa na roho kuhusu kuja kwa Masihi na wakati ujao wa ibada safi.—Danieli 9:20-27.

9, 10. Watu fulani wamefanya nini ili kuendelea kutumia akili zao?

9 Kama Musa na Danieli, tunaweza kujitahidi kuendelea kutumia akili zetu kwa kukazia fikira mambo ya kiroho kadiri tunavyoweza. Wengi wanafanya vivyo hivyo. Worth, mzee Mkristo mwenye umri wa miaka 80 na kitu, anajitahidi kwenda sambamba na programu ya chakula cha kiroho kinachotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Anasema hivi: “Ninapenda sana kweli, na ninasisimka kuona jinsi nuru ya kweli inavyozidi kuongezeka.” (Methali 4:18) Vivyo hivyo, Fred, ambaye amefanya huduma ya wakati wote kwa zaidi ya miaka 60, anaona kuanzisha mazungumzo ya Biblia pamoja na waamini wenzake kuwa jambo lenye kusisimua kiroho. Anasema hivi: “Ninapaswa kuendelea kuifanya Biblia iwe wazi katika akili yangu. Ikiwa unaweza kuifanya Biblia iwe hai, yaani, kuifanya iwe na uvutano juu ya maisha yako, na ikiwa unaweza kupatanisha yale unayojifunza na ‘kielelezo cha maneno yenye afya,’ basi utaelewa kikamili ujumbe wake. Unaweza kuona jinsi kila jambo linavyovutia katika kielelezo hicho.”—2 Timotheo 1:13.

10 Kuwa na umri mkubwa hakumaanishi kwamba mtu hawezi kujifunza mambo mapya na yaliyo magumu. Watu walio na umri wa miaka 60, 70, na hata 80 na kitu wamefaulu kujifunza kusoma na kuandika au wamejifunza lugha mpya. Mashahidi fulani wa Yehova wamefanya hivyo kwa kusudi la kuwahubiria watu wa mataifa mbalimbali habari njema. (Marko 13:10) Harry na mke wake walikuwa na umri wa karibu miaka 70 walipoamua kusaidia kuhubiri katika eneo la watu wanaozungumza Kireno. Harry anasema hivi: “Ni kweli kwamba mtu anapokuwa na umri mkubwa, kazi yoyote maishani inakuwa ngumu zaidi.” Hata hivyo, kwa kuendelea kujitahidi kwa bidii, waliweza kuongoza mafunzo ya Biblia katika Kireno. Kwa miaka mingi sasa, Harry amekuwa pia akitoa hotuba mbalimbali kwenye makusanyiko ya wilaya katika lugha hiyo mpya.

11. Kwa nini ni vizuri kuchunguza yale ambayo watu waaminifu wenye umri mkubwa wametimiza?

11 Bila shaka, si kila mtu aliye na afya au hali zinazomruhusu kufanya hivyo. Basi, kwa nini, tuchunguze yale ambayo wazee fulani wametimiza? Bila shaka, hatupendekezi watu wote wajitahidi kutimiza mambo yaleyale. Badala yake, hilo linapatana na yale ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania kuhusu wazee waaminifu katika kutaniko: “Mnapotafakari jinsi mwisho wa mwenendo wao unavyokuwa, igeni imani yao.” (Waebrania 13:7) Tunapotafakari mifano hiyo ya bidii, tunaweza kutiwa moyo kuiga imani yao yenye nguvu ambayo inawachochea watu hao wenye umri mkubwa katika utumishi wao kwa Mungu. Harry, ambaye sasa ana umri wa miaka 87, anasema hivi kuhusu kile kinachomchochea: “Ningependa kutumia kwa hekima miaka yangu ya maisha inayobaki na kusaidia kadiri iwezekanavyo katika utumishi wa Yehova.” Fred, aliyetajwa mapema, anapata uradhi mkubwa kwa kutimiza mgawo wake wa Betheli. Anasema hivi: “Unahitaji kutafuta njia ya kumtumikia Yehova vizuri zaidi na ushikamane nayo.”

Wanajitoa Ingawa Hali Zinabadilika Maishani

12, 13. Ingawa hali zake maishani zilikuwa zimebadilika, Barzilai alionyesha ujitoaji-kimungu jinsi gani?

12 Inaweza kuwa vigumu kukubali na kukabiliana na mabadiliko ya kimwili. Hata hivyo, mtu anaweza kuonyesha ujitoaji-kimungu hata hali zikibadilika. Barzilai Mgileadi, ni mfano mzuri katika jambo hilo. Akiwa na umri wa miaka 80, Barzilai alimwonyesha Daudi na jeshi lake ukarimu mkubwa sana, kwa kuwapa chakula na mahali pa kulala wakati wa uasi wa Absalomu. Daudi alipokuwa akirudi Yerusalemu, Barzilai aliwasindikiza mpaka kwenye Mto Yordani. Daudi alipendekeza kwamba Barzilai awe mmoja wa watu waliokuwa katika makao yake ya kifalme. Barzilai alisema nini? “Mimi leo nina umri wa miaka 80. . . . Je, mtumishi wako anaweza kuonja ladha ya kile ninachokula na kile ninachokunywa, au je, ninaweza kusikiliza tena sauti za waimbaji wa kiume na wa kike? . . . Lakini, tazama, mtumishi wako Kimhamu. Acha avuke pamoja na bwana wangu mfalme; nawe umfanyie yaliyo mema machoni pako.”—2 Samweli 17:27-29; 19:31-40.

13 Ingawa hali zake maishani zilikuwa zimebadilika, Barzilai alijitahidi alivyoweza kumtegemeza mfalme mtiwa-mafuta wa Yehova. Ijapokuwa alitambua kwamba uwezo wake wa kuonja ladha ya chakula na kinywaji na uwezo wake wa kusikia ulikuwa umepungua, hakuwa mwenye uchungu moyoni. Badala yake, kwa kupendekeza bila uchoyo kwamba Kimhamu afaidike na mapendeleo yaliyotolewa, Barzilai alifunua utu wake wa ndani. Kama Barzilai, leo watu wengi waliozeeka wanaonyesha roho ya ukarimu na isiyo na uchoyo. Wanafanya yale wanayoweza ili kutegemeza ibada ya kweli, wakijua kwamba “Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” Ni baraka kama nini kuwa na watu washikamanifu kati yetu!—Waebrania 13:16.

14. Uzee wa Daudi uliongeza jinsi gani uzito wa maneno ya Zaburi 37:23-25?

14 Ingawa kwa miaka mingi hali za Daudi zilibadilika mara nyingi, bado alisadiki kwamba Yehova haachi kamwe kuwatunza watumishi wake washikamanifu. Mwishoni mwa maisha yake, Daudi alitunga wimbo unaojulikana leo kuwa Zaburi ya 37. Hebu wazia Daudi akitafakari, huku akipiga kinubi chake na kuimba maneno yafuatayo: “Hatua za mwanamume zimetayarishwa na Yehova, na Yeye hupendezwa na njia yake. Ijapokuwa huenda akaanguka, yeye hatatupwa chini, kwa maana Yehova anautegemeza mkono wake. Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.” (Zaburi 37:23-25) Yehova aliona kwamba inafaa kutaja uzee wa Daudi katika zaburi hiyo iliyoongozwa na roho. Jambo hilo linafanya maneno hayo yawe yenye kugusa moyo kama nini!

15. Mtume Yohana aliweka jinsi gani mfano mzuri wa uaminifu ingawa alikuwa amezeeka na hali zake zilikuwa zimebadilika?

15 Mtume Yohana ni mfano mwingine mzuri wa uaminifu ingawa alikuwa amezeeka na hali zake zilikuwa zimebadilika. Baada ya kumtumikia Mungu kwa karibu miaka 70, Yohana alipelekwa uhamishoni katika kisiwa cha Patmo “kwa sababu ya kusema juu ya Mungu na kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 1:9) Hata hivyo, hakuwa amemaliza kazi yake. Kwa kweli, maandishi yote ya Yohana yaliyo katika Biblia aliyaandika katika miaka ya mwisho ya maisha yake. Akiwa Patmo, Yohana alionyeshwa maono yenye kuogopesha sana ya Ufunuo ambayo aliandika kwa makini sana. (Ufunuo 1:1, 2) Kwa ujumla, inafikiriwa kwamba aliachiliwa huru kutoka uhamishoni wakati wa utawala wa Maliki Mroma aliyeitwa Nerva. Baadaye, kufikia mwaka wa 98 W.K. hivi, alipokuwa na umri wa miaka 90 au 100 hivi, Yohana aliandika kitabu cha Injili na barua tatu zinazoitwa kwa jina lake.

Rekodi Isiyoharibika ya Uvumilivu

16. Wale ambao wamepoteza uwezo wao wa kuzungumza wanaweza kuonyesha jinsi gani ujitoaji wao kwa Yehova?

16 Udhaifu unaweza kuwa wa aina nyingi na wa viwango tofauti. Kwa mfano, watu fulani wamepoteza hata uwezo wao wa kuzungumza. Hata hivyo, bado wanathamini na kukumbuka upendo wa Mungu na fadhili zake zisizostahiliwa. Ingawa hawawezi kuzungumza kwa kinywa chao, katika mioyo yao wanamwambia Yehova hivi: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.” (Zaburi 119:97) Yehova, kwa upande wake, anawajua wale “wanaolifikiria jina lake,” naye anathamini jinsi watu hao walivyo tofauti na wanadamu walio wengi, ambao hawajali njia zake. (Malaki 3:16; Zaburi 10:4) Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova anapendezwa na kutafakari kwa mioyo yetu!—1 Mambo ya Nyakati 28:9; Zaburi 19:14.

17. Wale ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi wametimiza jambo gani la pekee sana?

17 Hatupaswi kupuuza uhakika wa kwamba wale ambao wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa makumi ya miaka, wameweka rekodi isiyoharibika ya uvumilivu ambayo ni ya pekee sana na haiwezi kupatikana kwa njia nyingine yoyote. Yesu alisema: “Nanyi kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.” (Luka 21:19) Uvumilivu ni muhimu ili kupata uzima wa milele. Ninyi ambao ‘mmefanya mapenzi ya Mungu’ na mmethibitisha ushikamanifu wenu kupitia maisha yenu mnaweza kutazamia kupokea “utimizo wa ile ahadi.”—Waebrania 10:36.

18. (a) Yehova anapendezwa kuona nini kuhusiana na watu wazee? (b) Tutachunguza nini katika habari inayofuata?

18 Yehova anathamini utumishi wako wa nafsi yote iwe unaweza kufanya mengi au machache. Haidhuru ni mambo gani ambayo huenda yakampata ‘mtu wetu wa nje’ kadiri tunavyozeeka, ‘mtu wetu wa ndani’ anaweza kufanywa upya siku baada ya siku. (2 Wakorintho 4:16) Hapana shaka kwamba Yehova anathamini yale ambayo ulitimiza wakati uliopita, lakini ni wazi sana kwamba anathamini pia yale ambayo unatimiza sasa kwa ajili ya jina lake. (Waebrania 6:10) Katika habari inayofuata, tutachunguza matokeo yenye kudumu ya uaminifu huo.

Ungetoa Jibu Gani?

• Ana aliwawekea Wakristo waliozeeka leo mfano gani mzuri?

• Kwa nini si lazima umri umzuie mtu kutimiza yale anayoweza?

• Watu waliozeeka wanaweza kuendelea kuonyesha ujitoaji-kimungu jinsi gani?

• Yehova ana maoni gani kuhusu utumishi ambao watu waliozeeka wanamtolea?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Danieli aliyezeeka alitambua kupitia “vitabu” muda ambao watu wa Yuda wangekaa uhamishoni

[Picha katika ukurasa wa 25]

Watu wengi waliozeeka ni mifano mizuri katika kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, kuhubiri kwa bidii, na kuwa na hamu ya kujifunza