Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka Kitabu Cha Kukunjwa hadi Kodeksi—Jinsi Ambavyo Biblia Ilifanywa Kuwa Kitabu

Kutoka Kitabu Cha Kukunjwa hadi Kodeksi—Jinsi Ambavyo Biblia Ilifanywa Kuwa Kitabu

Kutoka Kitabu Cha Kukunjwa hadi Kodeksi—Jinsi Ambavyo Biblia Ilifanywa Kuwa Kitabu

KWA karne nyingi, watu wamehifadhi habari katika njia nyingi. Nyakati zilizopita, waandikaji waliandika maneno yao kwenye minara ya ukumbusho, mabamba ya mawe au mbao, hati za ngozi, na vifaa vingine. Kufikia karne ya kwanza, njia iliyokubaliwa na iliyotumiwa huko Mashariki ya Kati ilikuwa kuandika habari katika vitabu vya kukunjwa. Kisha, kodeksi ikaanza kutumiwa, na baadaye ilichukua mahali pa vitabu vya kukunjwa na ikawa njia iliyotumiwa ulimwenguni pote ya kuhifadhi habari. Pia, ilisaidia sana katika kuenea kwa Biblia. Lakini kodeksi ilikuwa nini, na ilianza kutumiwa jinsi gani?

Vitabu vya kwanza kabisa viliitwa kodeksi. Kodeksi ilikuwa na kurasa zilizokunjwa, kukusanywa, na kuunganishwa pamoja. Habari iliandikwa upande wa mbele na wa nyuma wa kurasa hizo nazo zilitiwa jalada. Kodeksi ya kwanza haikuwa kama vitabu vya leo, lakini kama vitu vingine vingi vilivyotengenezwa, kodeksi pia ilirekebishwa na kuboreshwa kulingana na mahitaji na mapendezi ya wale walioitumia.

Mbao, Nta, na Ngozi

Mwanzoni, mara nyingi kodeksi zilitengenezwa kwa mabamba ya mbao yaliyofunikwa kwa nta. Mabamba yenye habari yaliyokunjwa na kuunganishwa pamoja kwenye upande mrefu, na ambayo yalifunikwa kwa nta yalipatikana huko Herculaneum. Mji huo uliharibika pamoja na Pompeii wakati Mlima Vesuvius ulipolipuka mwaka wa 79 W.K. Mwishowe, watu walianza kutumia vifaa vyenye kukunjika badala ya mabamba yasiyoweza kukunjwa. Katika Kilatini, kodeksi au vitabu hivyo, viliitwa membranae, au ngozi, kwa sababu kwa kawaida kurasa zake zilitengenezwa kwa ngozi.

Kodeksi fulani ambazo zimedumu zilitengenezwa kutokana na mafunjo. Kodeksi za Kikristo zinazoonwa kuwa za zamani zaidi ni za mafunjo. Kodeksi hizo zilihifadhiwa katika sehemu fulani zilizo kavu huko Misri. *

Je, Walitumia Kitabu cha Kukunjwa au Kodeksi?

Inaonekana kwamba Wakristo walitumia hasa kitabu cha kukunjwa, angalau mpaka karibu mwisho wa karne ya kwanza W.K. Kuanzia mwisho wa karne ya kwanza mpaka mwanzo wa karne ya tatu W.K. kulikuwa na ubishi kati ya watu waliopendelea kodeksi na wale waliopendelea kitabu cha kukunjwa. Watu wenye kushikilia utamaduni ambao walizoea kutumia kitabu cha kukunjwa, hawakutaka kuacha desturi na mazoea ya zamani. Hata hivyo, fikiria mambo yaliyohusika katika kusoma kitabu cha kukunjwa. Kwa kawaida, kitabu cha kukunjwa kilikuwa na hesabu fulani ya kurasa za mafunjo au ngozi ambazo ziliunganishwa na kufanyiza ukurasa mmoja mrefu ambao ulikunjwa. Maandishi yaliandikwa katika safu upande wa mbele wa kitabu hicho. Ili kukisoma, mtu alikikunjua kitabu hicho na kutafuta fungu ambalo alitaka. Baada ya kukisoma, alikikunja tena. (Luka 4:16-20) Mara nyingi habari moja iliandikwa katika vitabu kadhaa vya kukunjwa, na hivyo ilikuwa vigumu hata zaidi kutumia vitabu hivyo. Ingawa inaonekana kwamba Wakristo walioishi kuanzia karne ya pili na kuendelea walipendelea kufanya nakala za Maandiko katika vitabu vya kodeksi, bado vitabu vya kukunjwa viliendelea kutumiwa kwa karne nyingi. Hata hivyo, wataalamu wanaamini kwamba kodeksi ilianza kupendwa na watu wengi kwa sababu Wakristo waliitumia.

Ni wazi kwamba kodeksi ilikuwa na faida nyingi kama vile, kuhifadhi habari nyingi, na pia ingeweza kutumiwa na kubebwa kwa urahisi. Hata ingawa watu fulani katika siku za zamani waliona faida hizo, wengi hawakuacha mara moja kutumia vitabu vya kukunjwa. Hata hivyo, kwa karne kadhaa, mambo mbalimbali yalichangia kupendwa kwa kodeksi hatua kwa hatua.

Kodeksi haikugharimu pesa nyingi kama kitabu cha kukunjwa. Maandishi yangeweza kuandikwa upande wa mbele na wa nyuma wa ukurasa, na vitabu kadhaa vingeweza kuunganishwa pamoja na kuwa buku moja. Watu fulani wanasema kwamba kodeksi ilikuja kupendwa na Wakristo na wataalamu kama vile wanasheria hasa kwa sababu ilikuwa rahisi kupata mafungu ndani yake. Wakristo walifaidika kwa sababu orodha fupi ya maandiko ya Biblia au kitabu kidogo kilifaa sana katika kazi ya kueneza injili. Zaidi ya hayo, kodeksi ilikuwa na jalada ambalo kwa kawaida lilitengenezwa kwa mbao, kwa hiyo ilidumu kuliko kitabu cha kukunjwa.

Vitabu vya kodeksi pia vilifaa sana katika usomaji wa kibinafsi. Kufikia mwishoni mwa karne ya tatu, vitabu vidogo vya ngozi vya Injili vilikuwa vikienezwa na watu waliodai kuwa Wakristo. Kuanzia wakati huo, mabilioni ya nakala za Biblia nzima au sehemu yake zimetengenezwa kama kodeksi.

Leo, vifaa vingi vimefanya iwe rahisi sana kusoma na kupata hekima ya Mungu iliyo katika Biblia. Inaweza kupatikana katika kompyuta, rekodi za sauti, na katika maandishi. Haidhuru unapendelea Biblia ya aina gani, itumie kukuza upendo kwa ajili ya Neno la Mungu, na ulihangaikie kila siku.—Zaburi 119:97, 167.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona makala “Kodeksi ya Zamani ya Kikristo,” katika toleo la gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1962 (8/15/1962), ukurasa wa 501-505, la Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kodeksi ilisaidia sana katika kuenea kwa Biblia